TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN12%

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN
  • Anza
  • Iliyopita
  • 29 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 42552 / Pakua: 4762
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

Mwandishi:
Swahili

1

2

3

4

5

6

7

19

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA INSHIRAAH (UKUNJUFU) (NA. 94)

INA AYA 8

Kwa jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwenya kurehemu

أَلَمْ نَشْرَحْ لَكَ صَدْرَكَ ﴿١﴾

1. Je, hatukukunjulia moyo wako?

وَوَضَعْنَا عَنكَ وِزْرَكَ ﴿٢﴾

2. Tukakuondolea uzito wako.

الَّذِي أَنقَضَ ظَهْرَكَ ﴿٣﴾

3. Ambao uliuelemea mgongo wako?

وَرَفَعْنَا لَكَ ذِكْرَكَ ﴿٤﴾

4. Tukakutukuzia utajo wako?

فَإِنَّ مَعَ الْعُسْرِ يُسْرًا ﴿٥﴾

5. Hakika pamoja na uzito kuna wepesi.

إِنَّ مَعَ الْعُسْرِ يُسْرًا ﴿٦﴾

6. Hakika pamoja na uzito kuna wepesi.

فَإِذَا فَرَغْتَ فَانصَبْ ﴿٧﴾

7. Basi ukishamaliza (amali yako) jitaabishe kwa ibada.

وَإِلَىٰ رَبِّكَ فَارْغَب ﴿٨﴾

8. Na Mola wako (peke yake) mtake haja.

UBAINIFU

Ni amri ya kujitaabisha kwa ibada kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na kujipendekeza kwa kumtaka haja. Sura hii inawezekana kuwa imeshuka Makka au Madina, na mpangilio wa aya zake unawafikiana zaidi na Madina. Katika baadhi ya riwaya za Maimamu wa Ahlul Bait(a.s) zinasema kuwa Sura ya Adh-dhuha na Al-Inshiraah ni Sura moja. Na yamepokewa hayo vile vile kutoka kwa Twaaus na Umar bin Abdul-Aziz.

Amesema Arrazi katika Tafsiri Kabir baada ya kuwanakili hao wawili: Jambo lililofanya Twaaus na Umar kusema kuwa hizo ni Sura moja ni kuwa kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t): "Je hatukukukunjulia moyo wako ?" Nikama linaungana na neno; "Je hakukukuta ni yatima akakuhifadhi?" Lakini sababu hiyo siyo, kwani neno la kwanza kushuka kwake, lilikuwa ni katika hali ya kuwa Mtume(s.a.w.w) yuko kwenye ghamu kutokana na maudhi ya makafiri, akawa katika hali ya misukosuko na dhiki ya moyo. Na neno la pili linahukumilia kuwa liliposhuka, Mtume alikuwa katika hali ya kukunjuka na kutulia moyo, basi yataungana vipi haya?

Katika hiyo hiyo Tafsiri Kabir imesemwa makusudio ya kuukunjua moyo wake Mtume(s.a.w.w) ni kufanywa Mtume anakunjukiwa na hakika zote anazopewa wala hapati dhiki yoyote kutokana na maarifa yanayomshukia na wala hapati dhiki kutokana na adha ya watu katika kuyafikisha hAya Na nayomshukia. Na wala sio kutulia moyo na furaha, kama yatakavyokuja maelezo zaidi (Inshallah). Yanafahamisha hayo yale yaliyopokewa na Ibn Abu Hatim kutoka kwa Said bin Jubayr naye kutoka kwa Ibn Abbas amesema: Amesema Mtume(s.a.w.w) : "Nilimuuliza Mola wangu masuala ambayo nilitamani nisingemuuliza. Nilimwambia "Ewe Mola wangu Mitume waliokuwa kabla yangu kuna katika wao waliofanyiwa upepo uwatii na waliokuwa wakiwafufua wafu. Ndio akasema Mwenyezi Mungu: "Je sikukuta ni yatima nikakuhifadhi?" Nikasema: "Kwa nini?" Akasema: "Je sikukuta umedangana nikakuongoza?" Nikasema: "Bila shaka ewe Mola wangu." Akasema: "Je sikukukunjulia Moyo wako na nikakuondolea uzito wako?" Nikasema "Bila shaka ewe Mola wangu." Maelezo zaidi yako katika Tafsiri ya Sura Quraish (Liiylafi Quraish).

Aya Na 1

Asili ya neno Nashrah ni kuichangua nyama na mfano wake, na miongoni mwa maana yake ni kukunjua moyo yaani kuukunjua kwa nuru ya Mungu na utuvu unaotokana upande wa Mwenyezi Mungu na Roho inayotoka kwake. Qur'an inasema: "Ewe Allah nikunjulie moyo wangu ." (20:25).

"Je hatukukunjulia moyo wako?" "Je ambaye amekunjuliwa moyo wake na Allah " (39:22).

Kuzifuatisha aya tatu za mwanzo katika madhumuni yake kisha kuzibainisha kwa kauli "Hakika pamoja na uzito kuna wepesi", kwa dhahiri inaonyesha kufungika hali yake Mtume katika mwanzo wa mlingano wake, katikati yake na mwisho wake. Kisha kukaririka kuthibitisha ila na kuzifanya aya mbili za mwisho kuwa ni sehemu yake. Yote hayo yanashuhudia kuwa makusudio ya kukunjua moyo wake Mtume(s.a.w.w) ni kuukunjua kiasi ambacho yatakunjuka yale yanayomfikia miongoni mwa wahyi, yale anayoamrishwa kuyafikisha na yale yanayompata katika maudhi na adha kwa ajili ya Mwenyezi Mungu. Kwa maneno mengine tunaweza kusema ni kuifanya nafsi yake tukufu ni yenye kujiandaa kwa ukamilifu kwa kukubali yale yanayoifikia hiyo nafsi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Aya Na 2-3

Makusudio ya kuondoa uzito wake kutokana na unavyofahamisha mpangilio wa maneno ni kutekeleza mlingano wake na kupitisha juhudi zake kwa ajili ya Mwenyezi Mungu kwa kuwafiki sababu. Kwani hakika ujumbe (Utume), na mlingano ndio uzito aliochukua mara tu! Baada ya kukunjuliwa moyo wake. Inasemekana kuwa kuondoa uzito kunaonyesha kunaelekeana na yale yaliyopokewa kwamba Malaika wawili walimshukia Mtume wakakipasua kifua chake na wakautoa moyo wake wakautoharisha, kisha wakaurudisha mahali pake. Maelezo zaidi yatakuja baadae.

Inasemekana makusudio ya uzito ni yale yaliyomtokea kabla ya kupewa utume, pia imesemwa ni kupatwa kwake na mshangao katika baadhi ya mambo kama kutekeleza haki ya ujumbe na imesemwa kuwa ni uadui wa watu wake na maudhi yao mengi. Pia imesemwa ni huzuni yake kwa kufiwa na ami yake Abu Twalib na mkewe Khadija. Na ikasemwa uzito ni maasi na kuondolewa uzito ni isma (kuhifadhiwa na dhambi) yake na imesemwa kuwa uzito ni dhambi za uma wake na kuondolewa uzito huo ni kusamehewa. Njia hizi baadhi yake ni za kipuuzi na baadhi yake ni dhaifu zisizoafikiana na mpangilio wa maneno. Nazo ziko kati ya imesemekana na inawezekana tu! Hazina uhakika wowote.

Aya Na 4

Kuutukuza utajo maana yake ni kutajwa sana jina lake kuliko mtu mwengine. Miongoni mwa kuutukuza utajo wake ni kukutanisha Mwenyezi Mungu jina lake pamoja na jina la Mtume. Kwani jina la Mtume liko pamoja na la Mola wake katika shahada mbili ambazo ndizo msingi wa dini na ni wajibu kwa kila muislamu kumtaja Mtume pamoja na Mola wake katika swala tano za wajibu kila siku. Ni katika wema kutokea kutukuzwa utajo baada ya kuondolewa uzito.

Aya Na 5

Siyo mbali kuwa ni sababu ya yale yaliyotangulia (kuondoa uzito na kulitukuza jina). Yale aliyobebeshwa na Mwenyezi Mungu na akaamrishwa kuyalingania - ambayo ni mazito kwa mtu kuyachukua - yalikuwa yamezidi. Vile vile watu wake walizidi kumfanya mwongo kwa mwito wake, kumdharau na kujitahidi kuuzima utajo wake (jina lake). Kwa hivyo Mwenyezi Mungu akamwondolea uzito wake ambao ameuchukua kwa kuwafanya watu kumwitikia mwito wake na akautukuza utajo wake ambao walikuwa wanataka kuuzima.

Hayo yanayotokana na desturi yake Mwenyezi Mungu katika ulimwengu kuleta wepesi baada ya uzito, kwa hiyo huenda kumwondolea shida kulikotajwa ni katika desturi yake. Basi kwa hali hii herufi lam katika neno Usri ni ya Jinsiya yaani jinsi ya uzito baadhi yake na wala sio kila uzito. Na huenda desturi na desturi ya kubadilisha matukio na hali isibakie milele.

Amesema Zamakh-Shari katika Kash-Shaff: Washirikishaji Mwenyezi Mungu walikuwa wakimkashifu Mtume(s.a.w.w) kwa ufukara na dhiki mpaka akatambua Mtume kuwa wao wanajiepusha na uislamu kwa sababu ya ufakiri wa watu wake. Kwa hiyo Mwenyezi Mungu anamkumbusha yale aliyomneemesha miongoni mwa neema nyingi kisha akasema: "Hakika pamoja na uzito kuna wepesi". Kana kwamba amesema: "Tumekufadhili yale tuliyokufadhili basi usikate tamaa na fadhila za Mwenyezi Mungu, kwani uzito ulio nao uko pamoja na wepesi." Kwa dhahiri herufi lam ni ya Ahdiyya na wala sio Jinsiyya yaani uzito maalum uliokusudiwa na kwamba makusudio ya wepesi ni ghanima nyingi walizoruzukiwa waumini na Mwenyezi Mungu.

Lakini hayo ni yenye kupingika kwani utambuzi wake Mtume (SAWW) ni mkubwa zaidi kuliko kuogopea hali zao. Kuwa wanajiepusha na usilamu kwa sababu ya ufakiri wa watu wake. Isipokuwa wao walikuwa wakiukataa mwito wake kwa kiburi tu! Na Mwenyezi Mungu alikwishamkatisha tamaa Mtume wake kuwa wengi wao hawataamini aliposema: "Hakika imehakikika kauli juu ya wengi katika wao; kwa hivyo hawaatamini " (36: 7-10).

Na aya hizo zilishuka Makka. Na aya nyengine iliyoshuka Madina inayosema: "Hakika wale ambao wamekufuru ni sawa kwao ukiwaonya au usiwaonye hawataamini ". (1:6).

Lau inachukuliwa kuwa wepesi baada ya uzito ni nguvu ya kiislamu na kuinuka kwake baada ya kuwa chini pamoja na kuchukulia kuwa Sura imeshuka Makka, basi kusingekuwa na ubaya sana.

Aya Na 6

Ni kutilia mkazo na kusisitiza. Imesemekana kuwa ni kuanza upya na wametaja kwamba katika aya mbili hizo (5 na 6) kuna ufahamisho kuwa pamoja na hali nzito moja pana nyepesi mbili. Kwa kawaida jina lenye herufi lam likirudishwa mara ya pili katika maneno, linakuwa kama lile la kwanza kinyume cha jina lisilokuwa na lam. Lakini kawaida hii sio ya lazima, huwa ikabadilika.

Aya Na 7-8

Inatokana na yote yaliyobainishwa mwanzo, miongoni mwa kuchukua ujumbe na kumneemesha kwake Mwenyezi Mungu kwa kuukunjuwa moyo na kuondoa uzito na kuunyanyua utajo na yote hayo ni wepesi baada ya uzito. Kwa hiyo maana inakuwa, ikiwa uzito unafuatiwa na wepesi na mambo yote yanatokana na Mwenyezi Mungu tu! Basi ukimaliza yale uliyofaradhiwa, itaabishe nafsi yako kwa ajili ya Mwenyezi Mungu kwa ibada zake na dua zake na umtake kukuneemesha raha baada ya taabu hii na wepese baada ya uzito huu.

Imesemwa makusudio yake ni ukiishamaliza faradhi, jitaabishe katika suna na pia imesemwa ukishaswali jitaabishe na dua. Na madhumuni ya kauli mbili hizi ni baadhi ya yanayokubalika. Imesemwa maana yake ni ukishamaliza vita, jitahidi katika ibada. Na pia imesemwa makusudio yake, ukisha maliza yale ya duniani jitaabishe katika akhera yako. Na yemesemwa zaidi na hayo, lakini zote hizo ni njia dhaifu.

Utafiti Wa Hadith Katika Durril Manthur ametoa Abdalla bin Ahmad katika Rawaid ez-zuhd kutoka kwa Ubayya bin Kaab kuwa Abu Hurayra alisema kumuuliza Mtume(s.a.w.w) : "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu ni jambo gani uliloona kwanza kuhusu utume?" Mtume(s.a.w.w) akakaa vizuri akasema: "Umeuliza swali ewe Abu Huraira. Mimi nilipokuwa na umri wa miaka ishirini na miezi kadhaa siku moja nilisikia maneno juu ya kichwa changu mara tu mmoja akawa anamwambia mwenzake ndiye huyu? Wakanikabili na sura ambazo sijaziona kwa kiumbe yoyote na roho ambao sijazipata kwa mtu yoyote na nguo sijaziona kwa mtu yoyote kabisa. Wakaja kila mmoja akanishika mkono.

Mmoja wao akamwambia mwenzake mlaze, akanilaza bila kuchelewa, mmoja akasema mpasue kifua chake, akashika kifua changu na kukipasua katika hali ambayo sikuona damu wala maumivu. Akamwambia mwenzake na mfundo wa hasadi, akatoa kitu mfano wa pande la damu kisha akikitupilia mbali akamwambia tia upole na huruma. Mara akatia kitu mfano wa kile kilichotolewa, lakini kikiwa mfano wa fedha, kisha akatingisha kidole gumba cha mguu wangu wa kulia na akasema: "Ondoka uko salama". Basi nikarudi nikawa nina mfanyia upole mdogo na kumuhurumia mkubwa."

Baadhi yao kama katika Rauhilmaani wamesema kwamba alikuwa na umri wa miaka kumi. Na katika baadhi ya riwaya kimenukuliwa kisa wakati wa kushuka Sura ya Alaq (96).

Na wengine kama katika Sahih ya Bukhari, Muslim, Tirmidhi na Nasai, kimenukuliwa kisa wakati wa Israi wa Mtume. Kisa hiki kwa hali yoyote ni cha kufananisha tu! Sio tukio la kweli na wamefanya upekuzi mrefu kwa madhumuni ya kuonyesha kuwa tukio la kweli wakautia nguvu hup upekuzi wao kwa njia ambazo hazina faida kujishughulisha nazo.

Katika hiyo Durril Manthur ametoa Abu Yaala, Jariyr, Ibn Mundhir, Ibn Hatim, Ibn Habban, Ibn Murdawayh na Abu Naim katika Dalail wamepokea kutoka kwa Abu Said El-Khudri naye kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) amesema: "Alinijia Jibril akasema: Hakika Mola wako akasema: "Je, unajua vipi alivyotukuza utajo wako?" Nikasema, "Mwenyezi Mungu ndiye anayejua zaidi ". Akasema: "Nikitajwa, unatajwa pamoja nami." Katika hiyo hiyo Durril Manthur ametoa Abdurrazzaq, Ibn Jariyr, Hakim na Bayhaqi, kutoka kwa Hassan amesema: Siku moja alitoka Mtume(s.a.w.w) akiwa na furaha na kucheka huku akisema: "Nzito moja haiwezi kushinda nyepesi mbili".

"Hakika pamoja na uzito kuna wepesi, hakika pamoja na uzito kuna wepesi." Katika Majmau kuhusu Aya Na 7 na 8 maana yake ukimaliza kuswali swala ya faradhi jitaabishe kwa Mola wako kwa dua na umtake haja. Na hayo pia yamepokewa kutoka kwa Abu Jaffar na Abu Abdiallah(a.s) .

20

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA TIN (TIN) (NA. 95)

INA AYA 8

Kwa jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwenye Kurehemu.

وَالتِّينِ وَالزَّيْتُونِ ﴿١﴾

1. Naapa kwa tini na zaituni.

وَطُورِ سِينِينَ ﴿٢﴾

2. Na kwa Mlima Sinai.

وَهَـٰذَا الْبَلَدِ الْأَمِينِ ﴿٣﴾

3. Na kwa mji huu wenye amani.

لَقَدْ خَلَقْنَا الْإِنسَانَ فِي أَحْسَنِ تَقْوِيمٍ ﴿٤﴾

4. Hakika tumemuumba mwanadamu katika hali nzuri mno.

ثُمَّ رَدَدْنَاهُ أَسْفَلَ سَافِلِينَ ﴿٥﴾

5. Kisha tukamrudisha chini ya walio chini.

إِلَّا الَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ فَلَهُمْ أَجْرٌ غَيْرُ مَمْنُونٍ ﴿٦﴾

6. Ila wale walioamini wakatenda mema; wao wana malipo mema yasiyokoma.

فَمَا يُكَذِّبُكَ بَعْدُ بِالدِّينِ ﴿٧﴾

7. Basi ni lipi baada ya hayo, linalokufanya ukadhibishe malipo?

أَلَيْسَ اللَّـهُ بِأَحْكَمِ الْحَاكِمِينَ ﴿٨﴾

2. Je, Allah si bora ya mahakimu?

UBAINIFU

Sura hii inataja kufufuliwa na malipo, na inaeleza hayo kwa kufuata njia ya kueleza kuumbwa mtu katika hali nzuri, kisha kukhitalifiana watu; Wengine wakatoka na kuanguka chini ya waliochini. Pia inaeleza wajibu wa kihekima wa kupambanua kati ya hayo makundi mawili katika malipo. Sura hii imeshuka Makka, lakini inawezekana kuwa imeshuka Madina. Hata hivyo aya inayosema: "Na kwa mji huu wenye kuaminika," inatilia nguvu kuwa Sura hii imeshuka Makka.

Aya Na 1-3

Inasemekana makusudio ya Tini na Zaituni ni matunda maarufu na Mwenyezi Mungu ameapa kwa matunda hayo kwa sababu ya faida zake nyingi na majani yake yenye manufaa. Pia imesemwa makusudio yake ni mti wa Tini na wa Zaituni. Imesemwa makusudio ya Tini ni jabali iliyoko Damascus na Zaituni ni jabali liliyoko Al-Baytul Muqaddas (Palestina), na kwamba huenda makusudio ya hayo matunda mawili yaliyopo juu ya hayo majabali ni kwa vile hayo matunda yanaota katika majabali hayo na kwamba Mwenyezi Mungu ameapa kwa sehemu hizo kwa vile Mitume wengu wamepewa utume sehemu hizo. Na yamesemwa zaidi ya yaho.

Makusudio ya Turisinin ni jabali ambalo Mwenyezi Mungu Mtukufu alizungumza na Musa bin Imran(a.s) . Vile vile linaitwa Mlima Sinai. Makusudio ya mji huu wenye kuaminika, ni Makka kwa sababu Haram imepewa amani mahsus, ni kama alivyosema Mwenyezi Mungu (s.w.t): "Je, hawaoni ya kwamba tumeifanya ni nchi takatifu (Haram) na ya amani ." (29:67).

Na katika dua ya Ibrahim(a.s) , aliyoizungumzia Mwenyezi Mungu katika Qur'an tukufu: "Ewe Mola wangu, ufanye mji huu wa Makka uwe wa salama ". (2:126).

Kutumia tamko 'mji huu' ni kuthibitisha utukufu wake kwa kuuhusisha huo mji tu. Na kuusifu kwa neno amani inaweza kuwa ni kwa maana ya mji wenye amani au ni kwa maana ya mji wenye kuaminiwa, haohofiwi na shari.

Aya Na 4

Ni jawabu la kiapo. Makusudio ya kuwa mwanadamu ameumbwa katika hali nzuri, ni kuwa hali nzuri na bora katika mambo yake yote. Maana kwa ujumla ni kuwa mtu ameumbwa katika hali nzuri ya maumbile. Maana ya hali nzuri ya kimaumbile kutokana na ufahamisho wa aya inayofuatia (kisha tukamrudisha chini ya waliochini) ni kutengemaa kimaumbile kwa kupanda daraja ya juu na kufuzu kwa maisha ya milele mbele ya Mola wake, yaliyo mema na yasiyokuwa na uovu wowote. Hayo yametokana na vile alivyoandaliwa na Mwenyezi Mungu, pamoja na elimu yenye manufaa na kummakinisha kutokana na elimu hiyo katika amali njema; Mwenyezi Mungu anasema: "Na kwa nafsi na aliyeilingamanisha, akaifahamisha maasia yake na twaa yake ." (92:7-8).

Kwa hiyo akiamini lile alilolijua akaingilia kufanya amali njema Mwenyezi Mungu humnyanyua, kama alivyosema Mwenyezi Mungu:

"Kwake hupanda maneno mazuri na amali njema huyapandisha (hayo maneno mazuri) " (35:10). "na lakini inamfikia twaa yenu " (22:37).

"Allah atawainua wale walioamini miongoni mwenu; na waliopewa elimu katika daraja ." (58:11).

Kuna aya nyengine zisizokuwa hizo zinazofahamisha kuwa kuinuka kwa mtu kufikia daraja ya juu ya kufikilia kwake imani na matendo mema ni zawadi isiyokatika. Na Mwenyezi Mungu ameiita 'malipo' kama alivyosema katika Sura hii. "Wana malipo mema yasiyokatika."

Aya Na 5

Makusudio ya chini ya waliochini ni mahali palipo chini kabisa pa watu waovu na wa hasara; yaani "kisha tukamrudisha chini ya walio chini" katika watu wa adhabu. Inawezekana kuwa maana ya kurudisha ni kufanya yaani kisha tukamfanya chini ya waliochini, au inaweza kuwa kwa maana ya kubadilisha yaani kisha tukambadilisha. Makusudio ya chini kwa hali yote ni ouvu na adhabu.

Imesemwa makusudio ya hali nzuri ni ujana, nguvu ukamilifu wa Sura na uzuri wa umbo. Na kwamba kurudishwa chini wa waliochini ni kurudishwa kwenye uzee kwa kudhoofika nguvu za binadamu za dhahiri za batini na kurudishwa nyuma umbo lake; kwa hiyo aya inakuwa sawa katika maana na aya inayosema: "Na tunaempa umri tunamrejeza nyuma katika umbo ". (36:68).

Lakini hayo hayakubaliani na aya inayofuatia "Ila wale waliomaini na wakatenda amali njema." Kwa sababu kusema kuwa waumini hawawi wazee ni upuuzi tu. Vile vile kusema kuwa makusudio ya mtu ni kafiri na kwamba kurudishwa ni kwa maana ya kurudishwa katika Jahannam au kubadilishwa umbo hakukubaliana na aya inayofuatia.

Aya Na 6

Hapo inavuliwa jinsi ya mtu. Neno "malipo yasiyokatika" linatilia nguvu kuwa makusudio ya chini ya waliochini ni kumrudisha kwenye uovu na adhabu.

Aya Na 7

Hapa anaulizwa mtu kwa kuzingatia jinsi ya mtu yeyote. Imesemwa ni Mtume(s.a.w.w) . Neno dini hapa limekuja kwa maana ya malipo. Na maana yake - kutokana na yale yaliyosemwa - ni, nilipi lilokufanya ukadhibishe malipo ya siku ya Kiyama baada ya kuwa tumewafanya watu makundi mawili: kundi lenya kurudishwa chini yawaliochini na kundi lenye kulipwa malipo yasiyokatika?

Aya Na 8

Kuhusu "Je Allah si hakimu bora wa mahakimu (wote)?" ni swali la kutaka kuthibitisha. Kuwa Mwenyezi Mungu ni hakimu bora na kwamba Yeye yuko juu ya mahakimu wote katika kuzingatia hukumu na haki yake na kuipitisha bila kutokea mgongano wowote au makosa yoyote. Kwa hiyo Yeye Mwenyezi Mungu (s.w.t) anahukumu katika viumbe vyake kwani hekima inawajibisha kuhukumu kwa uzuri na kutekeleza hiyo hukumu. Ikiwa Mwenyezi Mungu ni hakimu bora wa mahakimu wote na watu wakiwa ni makundi mawili tofauti kwa kiitikadi na kimatendo, basi ni katika wajibu kihekima kupambanua kati ya hayo makundi mawili kwa malipo katika maisha yao yatakayobakia, ambayo ni ufufuo.

Kwa hivyo ikiwa watu wote wameumbwa katika hali nzuri (iliyo sawasawa); halafu wakatofautina, likapatikana kundi lililojitoa katika hali yake ya usawa ya umbile lake la kwanza, na kama Mwenyezi Mungu mwenye kuzingatia mambo yao ni hakimu bora wa mahakimu wote, na vile vile ikiwa ni lazima makundi hayo yatofautiane kimalipo, basi iko siku ambayo litalipwa kila kundi kutokana na yale liliyoyafanya, na hili ni jambo lisilokatalika. Aya hizi - kama unavyoziona - ziko katika maana ya aya zinazosema: "Je tuwajaalie wale walioamini na kutenda mema kuwa sawa na wale wafanyao uharibifu katika ardhi? Au tuwajaalie kuwa sawa na waovu? " (38:28).

"Je, wanafikiri wale ambao wamefanya maovu kuwa tutawafanya kama wale walioamini ." (45:21).

Baadhi ya wale wanaosema kuwa Mtume ndiye anaembiwa katika Aya Na "7" wameifanya Maa kuwa na maana na Man (nani), na neno Ahkam kwa maana ya kadhi (mwamuzi). Kwa hiyo maana kwa ujumla itakuwa: Ikiwa watu wanatofautiana, na hilo likalazimisha kutofautiana malipo yao katika siku ya malipo, basi ni nani anayekunasibishia uongo kwa malipo? Je, hakuwa Mwenyezi Mungu ni kadhi bora wa makadhi wote. Basi Yeye ataamua kati yako na ya wale wanaokadhibishia malipo." Lakini kama unavyoona, tafsiri hii ina taklifa isiyokuwa na lazima yeyote.

Utafiti Wa Hadith Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu Aya Na 1-3: Tini ni Madina, Zaituni ni Baytul Muqadas, Turisinin ni Kuffa na mji wenye kuaminika ni Makka. Imepokewa hadith katika maana hayo hayo katika baadhi ya riwaya za Musa bin Jaffar kutokana na mababu zake(a.s) nao kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) . Na katika baadhi ya riwaya nyengine ni kwamba Tini na Zaituni ni Hassan na Hussein Tur ni Ali na mji wenye kuaminika ni Mtume(s.a.w.w) , lakini hayo hayamo katika tafsiri. Katika Durril-Manthur ametoa Ibn Murdawayh kutoka kwa Khuzayma bin Thabit (siye Ansari) alimuuliza Mtume(s.a.w.w) kuhusu mji wenye kuaminika akasema ni Makka.

21

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA ALAQ (PANDE LA DAMU) (NA. 96)

INA AYA 19

Kwa jina la Allah Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu.

اقْرَأْ بِاسْمِ رَبِّكَ الَّذِي خَلَقَ ﴿١﴾

1. Soma kwa jina la Mola wako aliyeumba

خَلَقَ الْإِنسَانَ مِنْ عَلَقٍ ﴿٢﴾

2. Ameuumba mwanadamu katika pande la damu!

قْرَأْ وَرَبُّكَ الْأَكْرَمُ ﴿٣﴾

3. Soma na Mola wako ni Mkarimu mno.

الَّذِي عَلَّمَ بِالْقَلَمِ ﴿٤﴾

4. Ambaye amefunza (kuandika) kwa kalamu.

عَلَّمَ الْإِنسَانَ مَا لَمْ يَعْلَمْ ﴿٥﴾

5. Amefunza mwanadamu asilolijua.

كَلَّا إِنَّ الْإِنسَانَ لَيَطْغَىٰ ﴿٦﴾

6. Si hivyo! Hakika mwanadamu hupetuka mipaka.

أَن رَّآهُ اسْتَغْنَىٰ ﴿٧﴾

7. Kwa kujiona amejitosha

إِنَّ إِلَىٰ رَبِّكَ الرُّجْعَىٰ ﴿٨﴾

8. Hakika marejeo ni kwa Mola wako.

أَرَأَيْتَ الَّذِي يَنْهَىٰ ﴿٩﴾

9. Je, umemwona ambaye humkataza.

عَبْدًا إِذَا صَلَّىٰ ﴿١٠﴾

10. Mmja, ( wa Mungu) anaposwali?

أَرَأَيْتَ إِن كَانَ عَلَى الْهُدَىٰ ﴿١١﴾

11. Je, inaonaje! Ikiwa yuko katika uongofu.

أَوْ أَمَرَ بِالتَّقْوَىٰ ﴿١٢﴾

12. Au akawa anaamrisha wema?

أَرَأَيْتَ إِن كَذَّبَ وَتَوَلَّىٰ ﴿١٣﴾

13. Je, unaonaje! Akikadhi bisha na akaipa mgongo.

أَلَمْ يَعْلَم بِأَنَّ اللَّـهَ يَرَىٰ ﴿١٤﴾

14. Je, hajui kwamba Allah anaona?

كَلَّا لَئِن لَّمْ يَنتَهِ لَنَسْفَعًا بِالنَّاصِيَةِ ﴿١٥﴾

15. Naakome! Naapa asipokoma, tutamkokota kwa nywele za utosi.

نَاصِيَةٍ كَاذِبَةٍ خَاطِئَةٍ ﴿١٦﴾

16. Utosi wenye kusema uongo, wenye kufanya makosa.

فَلْيَدْعُ نَادِيَهُ ﴿١٧﴾

17. Haya na awaite wanachama wenzake.

سَنَدْعُ الزَّبَانِيَةَ ﴿١٨﴾

18. Na sisi tutawaita Malaika wa adhabu.

كَلَّا لَا تُطِعْهُ وَاسْجُدْ وَاقْتَرِب ﴿١٩﴾

19. Naakome! Usimtii (bali) sujudu (swali) na ujikurubishe ( kwa Mola wako).

UBAINIFU

Amri kwa Mtume kupokea Qur'an kwa Wahyi utokao kwake Mwenyezi Mungu (s.w.t) Hii ni ndio Sura ya kwanza kushuka katika Qur'an na mpangilio wake wa maneno haukatai kwa imeshuka kwa mpigo (mkupuo mmoja) kama tutakavyoeleza - Nayo imeshuka Makka , bila ya shaka yoyote.

Aya Na 1

Amesema Raghib kusoma ni kukusanya herufi na matamko, lakini sio mkusanyiko wowote ni kusoma. Haiwezekani kusema umewasomesha watu kwa kuwa umewakusanya. Kwa vyovyote iwavyo husemwa umesoma kitabu kama ukizikusanya herufi na matamko na kuyachunguza katika bongo hata kama hukuyatamka. Na husemwa umesomea mtu kama ukimkusanyia herufi na matamko katika usikizi wake; vile vile hutumiwa neno Tilawa kwa maana ya kisomo kama alivyolitumia Mwenyezi Mungu neno hilo katika Sura ya (98:2): Naye (ni) Mtume aliyetoka kwa Allah anayewasomea madaftari yenye kutakasika.

Kwa dhahiri maana ya neno Soma ni amri ya kupokea yale anayopewa wahyi na Malaika. Kwa ujuma ni amri ya kusoma kitabu ambayo inatokana na kitabu hichi hicho; kama alivyosema msemaji mmoja katika mwanzo wa kitabu chake kwa yule aliyempeleka "Soma kitabu changu hiki na ukifanyie kazi" kwa hivyo hiyo amri ya kusoma kitabu, imetokana na kitabu chenyewe. Mpangilio huu wa maneno:

Kwanza : unatilia nguvu yale yaliyopokewa kwamba Sura hii ni ya kwanza kayika Qur'an kwa Mtume(s.a.w.w) .

Pili : Kwamba makusudio yake ni kusoma Qur'an au yaliyo katika maana yake, na sio makusudio ya kusoma chochote au kuwasomea watu ijapokuwa hilo ni miongoni mwa lengo la kushuka kwake, kama alivyosema Mwenyezi Mungu: "Na Quran tumeigawanya sehemu mbali mbali. Ili uwasomee watu kwa kituo ".(17:106)

Na pia sio makusudio yakuwa lisome jina la Mola wako. Makusudio hasa ni kwamba jumla ya "kwa jina la Moa wako" inafungamana na kitu kilichoondolewa; kukadiriwa kwake ni hali ya kuanza na hali ya kufungua. Hilo halipingi Bismillahi inayoanza katika Sura hiyo, kuwa ni fungu katika Sura, kwani hayo ni katika maneno ya Mwenyezi Mungu aliyoanzia na kuamrisha kuanzia nayo. Kuhusu "Mola wako ambaye ameumba; inaonyesha milki ya Mwenyezi Mungu kwa viumbe vyote, kwani wanaoamshirikisha Mungu walikuwa wakisema Mwenyezi Mungu kazi yake ni kuumba na kupatisha vitu tu! Lakini hana ufalme wowote juu yake. Mwenyezi Mungu analipinga hilo kwa kusema 'Mola wako ambaye ameumba' kwa kutumia neno Rabb ambalo limaana ya kumiliki na kukiangalia vizuri kile kinachimilikiwa kwa hiyo kuumba na kumiliki ni kwake Yeye peke yake.

Aya Na 2

Neno Alaq lina maana ya damu iliyoganda na makusudio yake ni ile inayogeuka kutoka tone la manii katika mfuko wa uzazi. Hiyo inaonyesha vile Mwenyezi Mungu anavyoangalia vizuri na kupanga mambo ya mtu, tangu anapokuwa pande la damu mpaka anapokuwa mtu kamili kwa namna ya kiajabuajabu kiasi ambacho akili zinakwama kujua hilo. Hivyo mtu hatimii wala hakamiliki ila kwa mipangilio inayotokana na Mungu ambayo ni kutoka umbo moja baada ya jingine. Kwa hiyo mtu hana budi kumfanya Mungu pekee ndiye mlezi. Na maneno haya ni hoja ya kuwa Mmoja Mlezi (Mungu).

Aya Na 3

Amri ya kusoma hapa ni ya kusisitiza ile amri ya kwanza. Imesemwa makusudio yake hapo ni kuamrisha kisomo kwa watu yaani kuwafikishia (Tabligh) kama ilivyosemwa kwamba amri ya kwanza ya kusoma na hii ya pili zote ni kwa ajili ya kuwasomea watu. Lakini njia zote mbili hizi haziko wazi

Aya Na 4-5

Herufi Ba ni yakusababisha, kwa maana ya amemfundisha mtu kusoma au kuandika kupitia kalamu. Maneno haya ni kwa ajili ya kuitia nguvu nafsi ya Mtume(s.a.w.w) na kumwondoa kiherehere; kwa kuamrisha kusoma na hali ya kuwa yeye ni ummiy haandiki wala hasomi. Kama vile ameambiwa; soma kitabu cha Mola wako anachokufunulia wala usipogope na hali ya kuwa Mola wako ni Mtukufu ambaye amefundisha mtu kusoma kupitia kalamu, kwa hiyo yeye anaweza kukufundisha kusoma maandishi yake na hali ya kuwa wewe ni ummiy (usiyejua kusoma wala kuandika).

Kisha akaeneza Mwenyezi Mungu (s.w.t) neema, akataja kumfundisha kwke mtu asilolijua akasema: Amemefundisha mtu asilolijua. Hilo ni kuzidisha kuutia nguvu moyo wa Mtume(s.a.w.w) .

Makusudio ya mtu kwa dhahiri ni jinsi ya mtu yoyote. Imesemwa makusudio yake ni Mtume(s.a.w.w) . Na imesemwa ni Mtume Idris(a.s) kwa sababu yeye ndiye mtu wa kwanza kuandika kwa kalamu; Pia imesemwa ni kila Mtume aliyekuwa akiandika. Lakini njia zote ni dhaifu zilizo mbali na ufahamu.

Aya Na 6-7

Makatazo ya kukufuru neema, baada ya Mwenyezi Mungu kumneemesha mtu kwa neema kubwakubwa; mfano kumfundisha kwa kalamu na mengineyo. Ni juu ya mtu kumshukuru juu ya hilo, lakini mtu hukufuru neema zake Mwenyezi Mungu Mtukufu na kupetuka mpaka. Na hiyo ni kutokana na kwamba yeye anajishughulisha na sababu za kidhahir ambazo zinamfikisha kwenye makusudio yake. Kwa hiyo anaghafilika na Mola wake na kuona kuwa hana haja na kumkumbuka na kumshukuru juu ya neema yake, ndipo anamsahau na kupetuka mpaka.

Aya Na 8

Kwa dhahiri maana ya neno marejeo hapa ni kiaga cha mauti na kufufuliwa. Hapa anaambiwa Mtume(s.a.w.w) na imesemwa anaambiwa mtu. Kauli ya kwanza ndiyo iliyodhahiri zaidi.

Aya Na 9-13

Yanatajwa baadhi ya mambo ya mtu mwenye kupetuka mpaka. Makusudio ya mja anayeswali hapa ni Mtume(s.a.w.w) kutokana na unavyofahamisha mwisho wa aya za mwisho wakati Mwenyezi Mungu anapomwamrisha Mtume(s.a.w.w) kusujudu na kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu na kumkataza kumtii huyo anayekataza. Mpangilio wa aya hizi kwa kukadiri kuwa Sura ni ya kwanza kushuka na kushuka kwake mara moja, basi unafahamisha kuwa Mtume alikuwa akiswali kabla ya kushuka Qur'an na pia unafahamisha utume wake kabla ya risala yake ya Qu'an. Ama yale waliyoyataja baadhi yao kwamba swala haikufaradhiwa mwanzo wa utume isipokuwa ilifaradhiwa usiku wa Miraj kwa kusema kwake Mwenyezi Mungu: "Simamisha swala jua linapopinduka mpaka giza la usiku na Qur'an ya Alfajiri "(17:78).

Hiyo inafahamisha kuwa swala tano za kila siku zilifaradhiwa kwa namna yake hasa rakaa mbili mbili, katika usiku wa Miraji, lakini hakuna linalofahamisha kuwa haikuweko kabla yake. Na zimeshuka Sura nyingi kuwa haikuweko kabla yake. Na zimeshuka Sura nyingi kabla ya sura ya 17 (Israi) zinazotaja swala kama Al- Muddathtir, Al-Muzammil nk. kwa ibara tofauti ijapokuwa namna ya swala yenyewe haikudhihirishwa, isipokua ilikuwa ni namna ya kusoma Qur'an na kusujudu, vile vile zimepokewa baadhi ya riwaya za swala ya Mtume(s.a.w.w) pamoja na Khadija bin Ali katika mwanzo wa utume, ingawaje haikutajwa namna ya swala yenyewe. Kwa ujumla maana ya aya ni kumfahamisha yule ambaye anamkataza mja anaposwali na huyo anayekataza anajua kuwa Mwenyezi Mungu anamwona yale anayoyafanya. Nifahamishe huyo anaemkataza mja anayeswali aliye juu ya uongofu au anayeamrisha kumcha Mwenyezi Mungu anamwona?, Je, hastahiki adhabu?

Aya Na 14

Kuhusu "Hivi hajui kuwa Mwenyezi Mungu anamwona ". Makusudio ya kujua hapa yamekuja kwa njia ya kulazimsha kujua. Kwa sababu kuitakidi kuwa Mwenyezi Mungu ni Muumba wa kila kitu kunalizimisha kuitakidi kuwa Yeye (Mwenyezi Mungu) ana ujuzi wa kila kitu. Na huyo mkatazaji alikuwa ni mshirikishaji Mungu anayeabudu masananmu, na wanaobudu masanamu wanakubali kuwa Mwenyezi Mungu ndiye muumba wa kila kitu na wanamtakasa na sifa za upuungufu, kwa hiyo wanaona kuwa Mwenyezi Mungu hapitwi na kitu wala kushindwa na kitu chochote.

Aya Na 15 - 16

Kuusifu utosi wenye kusema uongo ni kwa njia ya fumbo kwa maana ya uongo wa mwenye utosi huo. Maana ya aya kwa jumla ni makemeo na utisho; nikuwa mambo hayako kama anavyotaka yeye. Ninaapa kama hatajizuia na makatazo yake, tutamchukua kidhalili na kumkokota mwenye adhabu ya utosi ambao mwenye utosi huo ni mwongo kwa anayosema na mkosaji kwa anayofanya. Imesemwa maana yake ni tutautia kovu utosi wake kwa moto na kuufanya mweusi.

Aya Na 17-18

Anaeleza Mwenyezi Mungu udhaifu ya huyo mwenye kukataza mja kuswali, kwa kusema: Haya na awaite hao watu wa baraza lake (wanachama wenzake) na sisi tutawaita Malaika wa motoni, wakali wenye nguvu, ambao hawana wa kuwazuyiwa.

Aya Na 19

Ni kusisitiza makemeo. Makusudio ya "Usimtii " ni usimtii anayekukataza swala. Hii inafahamisha kuwa makusudio ya kusujudu ni swala. Huenda swala aliyokuwa akiiswali Mtume(s.a.w.w) wakati huo ni tasbih na kumsujudia Mwenyezi Mungu. Imesemwa makusudio yake ni kusujudu kwa ajili ya kisomo cha Sura hi ambayo ni moja ya Sura nne za Azaim ( zenye sijda za wajib). Na kujikurubisha ni kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu. Imesemwa ni kujikurubisha kutokana na thawabu za Mwenyezi Mungu.

Utafiti Wa Hadithi Katika Durril-Manthur ametoa Abdurrazzaq, Ahmad, Abdu bin Hamid, Bukhari, Muslim, Ibn Jariyr na Ibn Ambari katika Masahif. Vile vile Ibn Murdawayh na Bayhaqi katika njia ya Ibn Shihab kutoka kwa Urwa bin Zubeir naye kutoka kwa Aisha mama wa waumin amesema "mwanzo wa kudhihirikiwa Mtume(s.a.w.w) na wahyi ni ndoto njema katika usingizi. Na alikuwa haoti ndoto ila itadhihiri mfano wa Falaq (nyota ya asubuhi).

Kisha akawa anapendelea kukaa mbali na alikuwa akipendelea kwenda Jabal Hiraa na kuabudu huko kwa idadi ya nyusiku kadhaa akiwa amechukua chakula, kisha hurudi kwa Bibi Khadija kuchukua chakula. Alikuwa akifanya hivyo mpaka ilipomjia haki naye akiwa huko Jabal Hiraa. Akamjia Malaika akasema: "Soma" akamwambia "Mimi si msomaji". Mtume anasema: Akanishika na kunikamua mpaka nikafikiwa na kughumiwa, kisha akaniacha, akasema "Soma" nikasema "mimi si msomaji" akanishika tena na kunikamua kama kwanza kisha akaniacha akaniambia "Soma" nikamwambia "mimi si msomaji". Akanishika tena mara ya tatu kisha akaniwacha akaniambia: "Soma kwa jina la Mola wako ambaye ameumba (kila kitu). Amemuumba Mtu kutokana na pande la damu. Soma na hali yakuwa Mola wako ni Mkarimu. Ambaye amemfundisha (mtu) kuandika kwa kalamu".

Akarudi Mtume(s.a.w.w) kwa Bibi Khadija akiwa anatetemeka moyo wake, akasema: "Nifunikeni, nifunikeni" wakamfunika mpaka ilipomwondokea fazaa, akamuhadithia Khadija habari hiyo na akamwambia 'ninaogopa juu ya nafsi yangu' Khadija akamwambia 'Hapana Mwenyezi Mungu hakukufedhehesha kabisa. Hakika wewe utaunga udugu, utachukua taabu, utawakaribisha wageni na utasaidia upande wa haki'.

Akaondoka Khadija mpaka kwa binamu yake anayeitwa Waraqah bin Naufal bin Asad bin Abdulaziz naye alikuwa ni mkristo katika zama za ujahili na alikuwa akiandika Kiibrania, akawa anaandika Injili kwa Kiibrania; wakati huo alikuwa mzee sana na kipofu. Khadija akamwambia "Ewe binamu nisikilize". Akamwambia "umeona nini?". Akamfahamisha yale aliyoyaona Mtume(s.a.w.w) . Akamwambia "huyo ni msiri ambaye alimshukia Musa! Natamani ningelikuwa kijana, natamani niwe hai wakati watakapokutoa watu wako!" Akasema Mtume(s.a.w.w) "hivi watanitoa?" Akasema, "ndio hakuna mtu yeyote aliyekuja na mfano wa uliyokuja nayo wewe ila hupingwa na nikiwahi siku yako hiyo nitakusaidia." Lakini hakuendelea kuishi Waraqah na akafa katika kipindi cha wahyi.

Amesema Ibn Shihab: "Amenifahamisha Abu Salama bin Abdurrahman kwamba Jabir bin Abdillahi El-Ansari amesema: "Amesema Mtume(s.a.w.w) - akiwa anazungumzia kipindi cha wahyi akasema katika mazungumzo yake mbiguni, nikanyanyua macho yangu, nikamwoma Malaika yule aliyenijia katika Jabal Hiraa kwenye kiti kati ya mbingu na ardhi, nikamwogopa na kurudi nyumbani, nikasema nifunikeni nguo! Nifunikeni! Ndipo Mwenyezi Mungu akateremsha aya: "Ewe mwenye kujifunika maguo, simama uonye (watu) na Mola wako umtukuze. Na nguo zako uzisafishe na mabAya Na puuze ." (74:1-5).

Katika hiyo hiyo Durril-Manthur ametoa Ibn Abu Shaybah, Ibn Jariyr nna Abu Naim kutoka kwa Abdalla bin Shaddad amesema: "Jibril alimjia Muhammad(s.a.w.w) akasema: "Ewe Muhammad "Soma". Akasema "Nisome nini?" Akamshika kisha akasema ewe Muhammad "Soma". Akasema "nisome nini?" Akasema : "Soma kwa jina la Mola wako ambaye ameumba (kila kitu) mpaka akafikia amemfunza mwanadamu asilolijuwa."

Mtume akaja kwa Khadija akamwambia, "Ewe Khadija naona amenidhuru." Akasema Khadija: "Hapana Mola wako hawezi kukufanya hivyo na wala kukufanyia ubaya wowote". Basi Khadija akamwendea Waraqh bin Naufal, akampa habari hiyo akasema. "Ukiwa unasema kweli, basi mumeo ni Mtume na atapata tabu kutokana na umati wake nakama nikimuwahi nitamwamini."

Kisha akachelewa Jibril kumjia, akasema Khadija naona Mola wako amechukia ndio Mwenyezi Mungu akateremsha: "Naapa kwa mwanzo wa mchana. Na kwa usiku unapotulia hakukuacha Mola wako wala hakukukasirikia ". (93:1-3).

Lakini kisa chote hiki hakiwezi kuepukana na shaka. Miongoni mwa shaka yake ni vile kutia shaka Mtume(s.a.w.w) kuwa yule aliyoyaona ni wahyi wa Mwenyezi Mungu kutoka kwa Malaika wa Mbinguni, bali hata kudhani kuwa ameshikwa na shetani aliyemtia wazimu. Na shaka zaidi ni vile kumtegemea Mkristo Mtawa kuwa ndiye atakayemtuliza nafsi yake kwa kumfahamisha kuwa yeye ni Mtume, na hali Mwenyezi Mungu amesema: "Sema hii ni njia yangu ninailingania kwa Allah kwa ujuzi wa kweli, mimi na wanaonifuata. (12:108). "Sasa je, ujuzi wa kweli ndio huko kutulizwa moyo na neno la Waraqah? Na amesema Mwenyezi Mungu:

"Sema mimi ninayodalili wazi itokayo kwa Mola wangu ". (6:57)

Sasa dalili gani iliyo wazi katika neno la Waraqah? Na amesema tena Mwenyezi Mungu: "Hakika sisi tumekuletea wahyi kama tulivyowapelekea Nuh na Manabii (wengine) baada yake ." (4:163). Je hao Mitume wengine walikuwa wakitegemea kupata utume wao mfano wa kisa hiki?

Ilivyo ni kwamba wahyi wa utume unalazimisha kuwepo yakini kutoka kwa Mtume mwenyewe kuwa umetokana na Mwenyezi Mungu Mtukufu. Hayo ndio yaliyopokewa kutokana na Maimamu wa Ahlul Bait. Katika Majmau kuhusu Aya Na tisa; ni kuwa Abu Jahl alisema; "Je Muhammad anaweka uso wake mchangani (anaswali) mbele yenu?" Wakasema "ndio". Akasema "Ninaapa kwa yule anayeapiwa, nikimwona nitaikanyaga shingo yake". Akaambiwa "huyo anaswali". Akawa anakwenda kumkanyaga mara akawa anarudi nyuma huku akijikinga kwa mikono yake wakasema: "Unanini ewe Abul Hakam?" Akasema: "Hakika kati yangu na yake kuna handaki la moto na hawa wenye mbawa". Akasema Mtume: "Naapa kwa yule ambaye nafsi yangu iko katika uweza wake, lau angelinikurubia tu! Wangelimchanachana Malaika. Ndipo akateremsha Mwenyezi Mungu Aya Na tisa mpaka mwisho wa Sura. Hayo ameyapokea Muslim katika Sahih.

Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu aya hiyo hiyo nikuwa ilishuka juu ya Walid bin El-Mughira aliyekuwa akiwakataza watu kuswali na kutiiwa Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Ufahamisho wa hayo haupingi kuwa mwenye kuswali ni Mtume(s.a.w.w) .

Katika Majmau kwenye hadith ya Abdallah bin Masud kwamba Mtume(s.a.w.w) amesema: "Mja anakuwa karibu zaidi na Mwenyezi Mungu anapokuwa amesujudu". Katika Kafi kwa isnadi wa Wash-shai amesema: "Nimemsikia Arridhaa(a.s) akisema: "Karibu zaidi anapokuwa mja na Mwenyezi Mungu ni anaposujudu, ndio maana akasema Mwenyezi Mungu "Sujudu na ujikurubishe (kwa Mola wako)".

Katika Majmau amepokea Abdulla bin Sinan kutoka kwa Abu Abdillahi amesema: Al - Azaim (Sura Sajda za wajibu) ni nne (Sura ya 32, 41, 52 na 96), zisizokua hizo katika Qur'an ni sunna tu, kusujudu!.

14

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA AL-FAJR (ALFAJIRI) (NA. 89)

INA AYA 30

Kwa jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu

وَالْفَجْرِ ﴿١﴾

1. Naapa kwa Alfajiri.

وَلَيَالٍ عَشْرٍ ﴿٢﴾

2. Na (kwa) masiku kumi.

وَالشَّفْعِ وَالْوَتْرِ ﴿٣﴾

3. Na (kwa) shufwa na witiri.

وَاللَّيْلِ إِذَا يَسْرِ ﴿٤﴾

4. Na (kwa) usiku unapopita.

هَلْ فِي ذَٰلِكَ قَسَمٌ لِّذِي حِجْرٍ ﴿٥﴾

5. Katika hayo mna kiapo kwa mwenye akili.

أَلَمْ تَرَ كَيْفَ فَعَلَ رَبُّكَ بِعَادٍ ﴿٦﴾

6. Je, hujui jinsi Mola alivyoifanya (kabila) ya Aad.

إِرَمَ ذَاتِ الْعِمَادِ ﴿٧﴾

7. Iram wenye nguzo ndefu?

الَّتِي لَمْ يُخْلَقْ مِثْلُهَا فِي الْبِلَادِ ﴿٨﴾

8. Ambayo haikuumbwa mfano wake katika miji.

وَثَمُودَ الَّذِينَ جَابُوا الصَّخْرَ بِالْوَادِ ﴿٩﴾

9. Na (kabila) ya Thamud ambao walikua wakipasua majabali katika (mji wa) waad.

وَفِرْعَوْنَ ذِي الْأَوْتَادِ ﴿١٠﴾

10. Na Firaun mwenye vigingi.

الَّذِينَ طَغَوْا فِي الْبِلَادِ ﴿١١﴾

11. Ambao walipetuka mipaka katika miji.

فَأَكْثَرُوا فِيهَا الْفَسَادَ ﴿١٢﴾

12. Wakazidisha humo mambo maovu.

فَصَبَّ عَلَيْهِمْ رَبُّكَ سَوْطَ عَذَابٍ ﴿١٣﴾

13. Akawateremshia Mola wako namna za adhabu.

إِنَّ رَبَّكَ لَبِالْمِرْصَادِ ﴿١٤﴾

14. Hakika Mola wako ni Mwenye kuotea.

فَأَمَّا الْإِنسَانُ إِذَا مَا ابْتَلَاهُ رَبُّهُ فَأَكْرَمَهُ وَنَعَّمَهُ فَيَقُولُ رَبِّي أَكْرَمَنِ ﴿١٥﴾

15. Ama mwanadamu - Mola wake anapomjaribu, akamtukuza, akamneemesha, husema: Mola wangu amenitukuza.

وَأَمَّا إِذَا مَا ابْتَلَاهُ فَقَدَرَ عَلَيْهِ رِزْقَهُ فَيَقُولُ رَبِّي أَهَانَنِ ﴿١٦﴾

16. Ama anapomjaribu akampunguzia riziki yake husema Mola wangu amenitweza.

كَلَّا بَل لَّا تُكْرِمُونَ الْيَتِيمَ ﴿١٧﴾

17. La, si hayo tu! Bali nyinyi humumtukuzi yatima.

وَلَا تَحَاضُّونَ عَلَىٰ طَعَامِ الْمِسْكِينِ ﴿١٨﴾

18. Wala hamhimizani katika kumlisha maskini.

وَتَأْكُلُونَ التُّرَاثَ أَكْلًا لَّمًّا ﴿١٩﴾

19.Na mnakula mirathi kula kwa pupa.

وَتُحِبُّونَ الْمَالَ حُبًّا جَمًّا ﴿٢٠﴾

20. Na mnapenda mali mapenzi makubwa.

كَلَّا إِذَا دُكَّتِ الْأَرْضُ دَكًّا دَكًّا ﴿٢١﴾

21. Si hivyo! Ardhi itakapo pondwa pondwa!

وَجَاءَ رَبُّكَ وَالْمَلَكُ صَفًّا صَفًّا ﴿٢٢﴾

22. Akaja Mola wako na Malaika (wamejipanga) safu kwa safu.

وَجِيءَ يَوْمَئِذٍ بِجَهَنَّمَ ۚ يَوْمَئِذٍ يَتَذَكَّرُ الْإِنسَانُ وَأَنَّىٰ لَهُ الذِّكْرَىٰ ﴿٢٣﴾

23. Ikaletwa siku hiyo Jahannam! Siku hiyo ndipo mwanadamu atakapokumbuka, lakini kutamfaa nini kukumbuka (kwake)?!

يَقُولُ يَا لَيْتَنِي قَدَّمْتُ لِحَيَاتِي ﴿٢٤﴾

24. Atasema laiti niliyatangulizia (wema) maisha yangu.

فَيَوْمَئِذٍ لَّا يُعَذِّبُ عَذَابَهُ أَحَدٌ ﴿٢٥﴾

25. Basi siku hiyo hapana yoyote atakayeadhibu kama adhabu yake (Mwenyezi Mungu).

وَلَا يُوثِقُ وَثَاقَهُ أَحَدٌ ﴿٢٦﴾

26. Wala hapana yoyote atakayefunga kama kufunga kwake.

يَا أَيَّتُهَا النَّفْسُ الْمُطْمَئِنَّةُ ﴿٢٧﴾

27. Ewe nafsi iliyotua!

ارْجِعِي إِلَىٰ رَبِّكِ رَاضِيَةً مَّرْضِيَّةً ﴿٢٨﴾

28. Rejea kwa Mola wako hali yakuwa uradhi (na) mwenye kuridhiwa.

فَادْخُلِي فِي عِبَادِي ﴿٢٩﴾

29. Kisha ingia katika waja wangu (wema).

وَادْخُلِي جَنَّتِي ﴿٣٠﴾

30. Na uingie katika pepo yangu.

UBAINIFU

Katika Sura hii kuna makemeo juu ya kufungamana na dunia kwenye kufuatiwa na kupetuka mpaka na ukafiri, na kuwaogopesha watu wenye mambo hayo na ukali wa adhabu ya Mwenyezi Mungu katika dunia na akhera. Kwa hiyo Sura inabainisha kuwa mtu kwa ufupi wa mtazamo wake na ubaya wa fikra yake anaona kuwa anayoletewa na Mwenyezi Mungu miongoni mwa neema yake ni katika ukarimu wake Mwenyezi Mungu, na yale anayovaana nayo miongoni mwa ufakiri ni utwezo. Kwa hiyo anapetuka mpaka na kuwa mfisadi katika ardhi anapopata na anakufuru anapokosa. Basi yanayompata katika cheo na utajiri na katika ufakiri na dhiki ya maisha, ni mitihani na balaa za Mungu ili adhihirishe kwayo yale atakayoyatanguliza akhera yake kutoka katika dunia yake.

Basi mambo hayako kama vile anavyofikiri mtu na anavyosema, bali mambo yalivyo kama atakavyoyakumbuka itakapotuka hisabu na kuletwa adhabu, kwamba yaliyompata miongoni mwa ufakiri au utajiri na nguvu au unyonge yalikuwa ni mitihani ya Mungu. Ilikuwa inamuwezekania yeye kutangulizia kesho yake kutokana na leo yake, lakini hakufanya na akaathirika na mateso kuliko thawabu. Basi haitapata maisha mema katika akhera isipokuwa nafsi iliyotua kwa Mola wke, isiyoyumba kwa vimbunga vya balaa wala kupetuka mpaka kwa kipato au kukufuru kwa kukosa. Sura hii imeshuka Makka kwa ushahidi wa mpangilio wa aya zake.

Aya Na 1-4

Aya hizo zote ni kiapo. Huenda dhahiri ya neno Alfajiri, Alfajiri yoyote, lakini sio mbali kuwa makusudio yake ni Alfajiri ya usiku wa Ijumaa. Imesemwa ni swala ya Alfajiri na imesemwa ni mchana wote na imesemwa ni kupasuka chemchem katika miamba na mengineyo. Njia zote hizi ziko mbali. Kuhusu masiku kumi huenda makusudio ni masiku kumi ya mwanzo katika mwezi wa Dhulhijja. Imesemwa makusudio ni siku za mwisho za mwezi wa Ramadhan, na ikasemwa ni za mwanzo wake. Pia imesemwa ni siku kumi za mwanzo za mwezi wa Muharram na ikasemwa kuwa ni ibada ya masiku kumi kuchukulia kuwa makusudio ya Alfajiri ni swala ya Alfajiri. Kuhusu Shufwa wa Witiri maana yanakubali kufungamana na kuwa ni siku wa Tarwiya (tarehe 8 Dhul-hijja) na siku ya Arafa (tarehe 9 Dhul-hijja). Imesemwa kuwa makusudio yake ni swala mbili ( rakaa mbilimbili na rakaa moja) katika mwisho wa usiku. Na imesemwa ni swala yoyote, ziko mbili mbili na moja.

Pia imesemwa kuwa Shufwa ni siku ya Idd ya Dhul-hijja wa Witiri ni siku ya Arafa, na imesemwa Shufwa ni viumbe vyote, kwa sababu Mwenyezi Mungu anasema: "Na tukawaumba wanawake na wanaume " (78:8).

Na Witiri ni Mwenyezi Mungu (s.w.t) Kuna riwaya nyingi zitakazokuja juu ya kauli hizi katika utafiti wa hadith 8 Vile Vile imesemwa makusudio yake ni hisabu ya viwiliviwili na kimojakimoja na kwamba kuapa kwa hisabu, ni kuwa kudhibiti idadi katika kiasi ni katika nema kubwa itokayo kwa Mwenyezi Mungu. Imesemwa kuwa ni viumbe vyote, kwa sababu vitu vyote ama vitakuwa ni jozi au kimoja. Imesemwa kuwa makusudio ya Witiri ni Adam na Shufwa ni kuwa pamoja na mkewe Hawa.

Na imesemwa Shufwa ni mchana, na usiku, na Witiri ni mchana ambao, hauna usiku nao ni siku ya Kiyama. Imesemwa Shufwa ni Safa na Marwa na Witiri ni Al-Ka'aba, na imesemwa ni siku za kabila la Ad na Witiri ni nyusiku zake. Na imesemwa Shufwa ni milango ya motoni saba. Na zaidi ya hayo mengi yaliyosemwa zaidi ya kauli thelethini na sita (36). Kuhusu kauli yake; Na (kwa) usiku unapopita ni kama Aya Na 33, Sura ya 74 inayosoma: "Na (kwa) usiku unapokucha".

Kwa dhahiri herufi Lam ni ya jinsi yaani usiku wowote, lakini wengine wamesema ni usiku wa Muzdalifa (usiku wa kuamkia Idd) ambao mahujaji wanapita kutoka Arafa mpaka Muzdalifa wanakusanyika Mahujaji kwa kumtii Mwenyezi Mungu kisha wanaamkia kwenda Mina kwa hiyo kama unavyoona itakuwa makusudio ya usiku kumi ni usiku kumi za mwanzo katika mwezi wa Hijja (Dhul-Hijja).

Aya Na 5

Ni ishara ya yaliyotangulia katika kiapo na ni swali la kuthibitisha, maana yake kwa ujumla, ni kwamba, katika hayo tuliyoyatanguliza kuyaapia yanatosha kwa mwenye akili ya utambuzi wa maneno inayopambanua haki na batili. Na Mwenyezi Mungu akiapa naye haapi isipokuwa lile lenye utukufu na daraja linakuwa ni neno la haki lenye kutiliwa mkazo ambalo halina shaka katika ukweli wake. Jawabu la kiapo limeondolewa linafahamika kutokana na yatakayotajwa katika adhabu ya watu waliopetuka mipaka na ukafiri katika dunia na akhera na thawabu ya nafsi yenye kutulia na kwamba kuneemesha kwake Mwenyezi Mungu (s.w.t) juu ya aliyomneemesha na kumzuilia, hakika hayo ni majaribio na mitihani. Kuondoa jawabu la kiapo na kulileta kwa njia ya fumbo, ni kutilia mkazo zaidi katika hali ya kuonya na kutoa biashara.

Aya Na 6

Ni kabila la Aad wa kwanza nao ni kaumu ya Mtume Hud(a.s) . Vimekaririka visa vyao katika Qur'an tukufu na imeonyesha kwa wao walikuwa watu wa nchi yenye machunguu ya michanga. Yameelezwa yale yanayopatikana katika visa vyao katika Sur ya Hud (11).

Aya Na 7-8

Neno Imad ni nguzo za nyumba. Kwa dhahiri ya aya mbili hizi, ni kuwa Iram ulikua ni mji uliokuwa wa aina yake wenye majumba marefu na maguzo marefu. Hakika habari zao zimekatika na athari zao zimefutika, kwa hiyo hakuna njia ya ufafanuzi itakayoeleza hali zao kiasi cha kuituliza nafsi isipokuwa yale tu, yaliyohadithiwa na Qur'an tukufu kwa ujumla juu ya kisa chao; kwamba wao walikuwa baada ya kaumu ya Nuh, wakazi wa nchi yenye machuguu ya mchanga, na walikuwa ni wenye umbo kubwa na nguvu kubwa zaidi na walikuwa na maendeleo, miji yenye majengo mengi ardhi za rutuba zenye mabustani ya mitende na mimea na mahali pazuri. Kimeelezewa zaidi kisa chao katika Sura ya Nuh.

Imesemwa kuwa makusudi ya neno Iram ni hao kaumu ya Aad - na sili na neno hilo ni jina la baba yao kwa hiyo wakaitwa kwa jina la baba yao, kama inavyosemwa Quraish kwa kukusudia wanawe au Israil kwa kukusudia wana Israil. Makusudio ya kusema wenye maguzo marefu ni kuwa wao ni watu wenye nguvu, na maana yake ni Je, hujui jinsi Mola wako alivyoifanya (kabila) ya Aad Iram wenye nguvu ambao haukumbwa mfano wao katika miji, au katika dunia nzima, lakini hayo hayaepukani na kuwa mbali na dhahiri ya tamko. Ya umbali zaidi ya yaliyosemwa kwamba makusudio ya kuwa wao ni wenye maguzo marefu, ni vile kuwa wao walikuwa ni watu wa kuazimia kusafiri katika wakati wa maleleji na mimea inaponyauka basi hurudi majumbani mwao. Kisa cha bustani ya Iram kilichopokewa kutoka kwa Wahb bin Manbih na Kaabulahbar, ni katika ngano za watu wakale tu!

Aya Na 9

Yaani walipasua miamba ya milima kwa kuichonga kuwa nyumba. Aya hii iko katika maana ya aya inayosema: "Na mnachonga milimani majumba mkastarehe tu! " (26:149)

Aya Na 11

Huyo ni Firaun wa Musa, ameitwa mwenye vigingi- kutokana na yaliyo katika baadhi ya riwaya - kwamba yeye alikuwa akitaka kumuadhibu mtu humnyoosha juu ya ardhi na kuipingilia mikono yake na miguu yake kwa vigingi vine katika ardhi, au humnyoosha juu ya ubao na kumfanyia hivyo. Hayo yanatiliwa nguvu na yale aliyoyasimulia Mwenyezi Mungu kuhusu kauli yake Firaun akiwatisha wachawi walipomwamini Musa kwa kusema: "Nitawasulubu katika mashina ya mitende ." (20:71).

Hakika wao walikuwa wakiwamba mikono ya msulubiwa na miguu yake juu ya ubao wa kusulubu.

Aya Na 12

Ni sifa wa waliotajwa, Ad, Thamud na Firaun, maana yako wazi.

Aya Na 13

Ametaja kumimina kwa njia ya fumbo kwa maana ya kufuatana, maana yake ni kuwa Mwenyezi Mungu aliteremsha kwa mataghut wote hawa wenye kukithirisha uharibifu mara tu, baada ya kupetuka kwao mipaka na ufisadi wao, adhabu kali ya aina yake yenye kufuatana mfululizo.

Aya Na 14

Kuwa Mwenyezi Mungu yuko katika kuotea, ni istiara ya kufananisha Mwenyezi Mungu anavyochunga matendo ya waja wake na mtu anayeotea mtu apite amchukue, bila ya kutambua. Basi Mwenyezi Mungu anachunga matendo ya waja wake, wakipetuka mipaka na kukithirisha ufisadi tu, huwaadhibu kwa adhabu kali. Aya hiyo ni sababu ya yaliyotangulia katika mazungumzo ya kuadhibu wanaopetuka mipaka wenye kukithirisha ufisadi. Kuongeza dhamira katika neno Mola na kuwa "mola wako", ni kuonyesha kuwa desturi hiyo ya adhabu ilikuwa ni yenye kupita katika umma wake Mtume(s.a.w.w) kama ilivyopita katika umati zilizotangulia.

Aya Na 15

Ni mtiririko wa yaliyotangulia, ndani yake mna ufafanuzi kuhusu hali ya mtu anapopewa neema ya dunia au anapozuiliwa, ni kama vile imesemwa: Hakika mtu yuko chini ya ulinzi wa Mungu, anaotewa na Mola wake kuwa je, atatengenea au ataharibika?. Kwa hiyo anamjaribu na kumtahini katika yale atakayompa katika neema yake au kunyima kwake. Ama mtu yeye akineemeshwa huhisabu kwamba huo ni utukuzo wa Mungu kwa hiyo anaweza kufanya vile anavyotaka. Hivyo anapetuka mipaka na kukithirisha ufisadi. Na akimzuilia na kuifanya chache riziki yake, huhisabu kuwa ametwezwa na Mungu, basi hukufuru na kulalamika Makusudio ya mtu ni jinsi ya mtu. Kusema kwake: akamtukuza akamneemesha ni tafsiri ya majarabio yaani Mwenyezi Mungu (s.w.t) amemtukuza na akampa nema iliamshukuru na amuabudu, lakini yeye mtu mwenyewe anajaalia ni mateso juu ya nafsi yake yanayofuatiwa na adhabu. Kuhusu neno "husema Mola wangu amenitukuza" yaani amenijaalia juu ya ukarimu unaotokana naye kwa neema ambazo amenipa, kwa hiyo ninaweza kufanya lile ninalo taka.

Kusema "Mola wangu amenitukuza" kuko katika mnasaba wa kumzingatia Mungu - hayo hayasemwi na waabudu masanamu na wanaomkanusha Mungu - na ni kwenye kujengwa juu ya kumkubali Mungu kwa kiasi cha maumbile yalivyo ijapokuwa ulimi unajizuia na hilo, vile vile aya inayofuatia.

Aya Na 16

Yaani akifanya mtihani ikawa dhiki riziki yake, basi husema Mola wangu amenidhalilisha. Kutokana na aya hizi (15 na 16) yanadhihirika mambo yafuatayo:

Kwanza : Kukaririka majaribio na kuthibitika katika sura mbili za neema na kuzuiliwa, ni kwamba kupewa neema na kuzuiliwa vyote ni katika majaribio na mitihani ya Mungu kama alivyosema: "Tutawajaribu kwa (mambo) ya shari na heri " (21:35).

Pili : Kupewa neema kwa kuwa ni fadhila na rehema, ni utukufu iwapo wanadamu hawakukubadilisha kuwa adhabu. Tatu: Mtu anaona wema wake katika maisha ya dunia ni kuneemeshwa katika dunia ka neema za Mwenyezi Mungu, hivyo anaona ndio utukufu na kunyima kunakotokana na Mwenyezi Mungu anakuona kuwa ni uovu. Ilivyo nikuwa, utukufu uko katika kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu kwa imani na amali njema, ni mamoja iwe ni utajiri au ufakiri, kupata au kukosa, yote hayo ni mitihani. Wanayo maana nyengine kuhusu aya hizi mbili lakini tumeacha kuyaonyesha kwa kutokuwa na umuhimu wowote.

Aya Na 17

Na makemeo kwa yale wanayoyasema kwamba utukufu uko katika utajiri na kwamba ufakiri na kukosa ni madhila. Basi si hivyo isipokuwa kutoa kwake Mwenyezi Mungu (s.w.t) neema, na kuizuia yote hayo ni mitihani anayojaribiwa mtu. Kusema kwake Mwenyezi Mungu: Bali nyinyi hamumtukuzi yatima, ni kutilia mkazo makemeo kwa kutaja baadhi ya neema ambayo haikusanyi utukufu kabisa, kama kukosa kumtukuza yatima kwa kula urathi wake na kumzuilia nao na kukosa kuhimizana juu ya kumlisha maskini kwa ajili ya kupenda mali. Kuacha kumtukuza yatima ni kumzuilia na urathi wa mzazi wake kama walivyokuwa wakiwazuilia watoto wadogo na kurithi, kama inavyotia nguvu aya inayofuatia.

Aya Na 18

Yaani hamuhimizani kutoa sadaka. Hayo yanatokana na kupenda mali sana kama ilivyo katika aya inayofuatia.

Aya Na 19

Maana ya neno Lamma ni mtu kula fungu lake na la mwengine, na kula chochote anachokipata kiwe kibaya au kizuri. Aya hii ni tafsiri ya kukosa kumtukuza yatima kama iliyotangulia.

Aya Na 20

Aya hiyo nayo inafasiri kukosa kuhimizana katika kumlisha maskini kama ilivyotangulia.

Aya Na 21

Makusudio yake ni kufika siku ya Kiyama. Hilo ni kemeo la pili kutokana na yale anayoyasema mtu katika hali mbili za utajiri na ufakiri. Aya hii inasimamia sababu za makemeo kwa maana ya kuwa, sio kama anavyosema mtu, kwani yeye atakumbuka kitakaposimama Kiyama kwamba maisha ya dunia na vilivyomo ndani yake miongoni mwa utajiri na ufakiri sio makusudio kwa dhati, bali yamekuwa ni majaribio na mitihani kutoka kwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) Anapambanua kutokana na mitihani hiyo mwema na mwovu na inamuandalia mtu yale atakayoishi kwayo katika akhera. Hakika mtu ametatizika akadhania kuwa utukufu ndio makusudio kwa dhati akajishughulisha nao na wala asitangulize chochote kwa maisha yake ya Akhera. Kwa hiyo wakati huo atatamani huku akisema: Laiti mimi niliyatanguliza (wema) maisha yangu, lakini matamani hayatatoshelezea lolote na adhabu.

Aya Na 22

Kunasibisha kuja Mungu ni katika mikanganyo ambayo inahukumuliwa na kauli yake Mwenyezi Mungu (s.w.t) "Hakuna chochote mfano wake " (42:11). Na yaliyokuja katika alama za Kiyama, ni katika upambanuzi wa kuondoa sababu na mapazia yaliyowaziba na kushihiri kwamba Mwenyezi Mungu ni haki iliyo wazi. Kwa hiyo yale yaliyopokewa katika hadith yanalirudia hilo kwamba makusudio ya kuja kwake Mwenyezi Mungu (s.w.t) ni kuja amri yake kama alivyosema Mwenyezi Mungu: "Na amri siku hiyo ni ya Allah " (82:19).

Kunatilia nguvu njia hii kusema kwake Mwenyezi Mungu: "Je, kuna jengine wanalongojea ila kuwafikia Allah katika vivuli vya mawingu na kuwafikia malaika na imekwishapitishwa amri ". (2:210).

Kama tukikikutanisha na kusema kwake. "Je, wanangoja jengine (hawa makafiri) ila wawafikie Malaika? Au iwafikie amri ya Mola wako? " (16:33). Kwa hiyo basi kuna neno lililondolewa, kukadiria kwake ni: ikaja amri ya Mola wako. Au kunasibisha kuja Mungu ni kwa majazi (fumbo) ya kiakili.

Aya Na 23

Sio mbali kuwa makusudio ya kuletwa Jahannam ni kudhihirishwa, kama ilivyo katika kauli yake. "Basi tumekuondolea pazia yako kuona kwako leo kumekuwa kukali " (50:22).

Kusema kwake "Siku hiyo atakumbuka mtu" yaani atakumbuka kwa uwazi zaidi kwamba yale yaliyokuwa yakimjia katika maisha ya dunia miongoni mwa heri au shari yalikuwa ni majaribio ya Mwenyezi Mungu na mitihani yake na yeye akapuuza. Hivyo ndivyo unavyofahamisha mpangilio wa maneno. Kusema kwake "wapi kutamfaa kukumbuka" ni fumbo la kukosa kunufaika na kukumbuka isipokuwa kukumbuka kungefaa kama angekuunganisha na kutubia na kutenda amali njema kwa yale aliyoyapuuza, na leo ni siku ya malipo sio siku ya kutubia na kufanya amali.

Aya Na 24

Maisha hapa ni ya akhera au ni maisha ya kihakika ambayo ndiyo hayo maisha ya akhera, kama kulivyozindua kusema kwake: "Na hayakuwa haya maisha ya dunia ila ni upuzi na mchezo; na nyumba ya akhera ndio maisha hasa: Laiti wangalijua ". (29:64) Makusudio ya kuyatanguliza maisha ni kuyatangulizia amali njema.

Aya Na 25-26

Dhamir katika neno adhabu na kufunga inamrudia Mwenyezi Mungu. Yaani siku hiyo hakika adhabu yake na kufunga kwake kutakuwa zaidi ya adhabu ya kiumbe chochote. Wengine wamesoma kwa Fat'ha ya Dhali na Thau. Dhamir kwa kisomo hiki itakuwa inamrudia mtu, yaani hataadhibishwa yoyote siku hiyo mfano wa adhabu ya mtu wala hatafungwa yoyote siku hiyo mfano wa kufunga kwa mtu.

Aya Na 27

Mpangilio wa maneno uonaokubaliana na 'nafsi' hii kutokana na yale yaliyotajwa kabla yake katika sifa zinazofungamana na dunia, upitukaji mipaka, ufisadi na ukafiri na yale yaliyoahidiwa katika mwisho mbaya, unaonyesha kuwa nafsi yenye kutulia ni ile inayotulizana kwa Mola wake na kurudhia kile kinachoridhiwa na Mola wake, inajiona kuwa ni mtumwa asiyejimiliki na chochote katika kheri na inaiona dunia ni nyumba ya kupita, na inayoyakabili katika hiyo dunia miongoni mwa utajiri au ufakiri, manufaa au madhara, ni majaribio na mitihani ya Mungu. Kwa hiyo mtiririko wa neema haumpelekei kupetuka mipaka, kufanya ufisadi mwingi au kujifanya mkubwa wala ufakiri na kukosa kitu hakumuingizi katika ukafiri na kuwacha kushukuru, bali yeye ni mwenye kutulizana, hakosei njia yake yenye kunyooka kwa kupetuka mipaka au kuwapitusha mipaka wengine.

Aya Na 28

Kuisifu nafsi kwa hali yakuwa radhi ni kwamba kutulizana kwale kwa Mola wake kunalazimisha kuridhia kwake yale yaliyokadiriwa na kuhukumiliwa na wala hayamchukizi. Mtu akimridhia Mola wake naye humridhia, kwani Mwenyezi Mungu S.W.T. huchukia sana kutoka mja katika kipambo chake. Basi akilazimiana na njia ya kuwa mja wa Mwenyezi Mungu, litawajibisha hilo radhi ya Mola wake, kwa hiyo ndio maana hali ya kuridhia imefuatishwa na kuridhiwa.

Aya Na 29

Inaungana na aua iliyotangulia inafahamisha kuwa mwenye nafsi yenye kutulia yuko katika kundi la waja wa Mwenyezi Mungu. Hilo ni kwamba alipotulia kwa Mola wake alijiondoa kujiona huru, na akaridhia ile iliyohaki kwa Mola wake, akaona dhati yake, sifa zake na vitendo vyake ni miliki ya Mola wake. Hakupita katika yaliyokadiriwa kuhukumiliwa wala katika yaliyo amrishwa na kukatazwa isipokuwa yale anayoyataka Mola wake. Huko ndiko kudhihiri uja wenye kutimia. Kwa hiyo kusema kwake "ingia katika waja wangu" ni ikrari ya mahali pa uja wake hiyo nafsi. Neno lake "na ingia katika pepo yangu" ni kubainisha kituo chake. Kuitegemeza pepo kwa dhamiri ya mwenye kusema (pepo yangu) ni utukuzo mahsusi wala halipatikani hilo katika maneno yake Mwenyezi Mungu (s.w.t) isipokuwa katika aya hii tu!.

Utafiti Wa Hadithi Katika Majmau kuhusu kusema kwake "na (kwa) Shufwa na Witiri, imesemwa kuwa Shufwa ni kuumba kwa sababu Mwenyezi Mungu amesema: "Na tukawaumba nyinyi wanaume na wanawake (jozi) " (78:8). na Witiri ni Mwenyezi Mungu Mtukufu. Hadithi hiyo imeyoka kwa Atiyal-Aufiy, Abu Saleh, Ibn Abbs na Mujahid, hiyo ni riwAya Na Abu Saad El-Khudriy naye amepokea kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) .

Imesemekana kuwa Shufwa na Witiri ni swala: kuna katika hiyo swala ya Shufwa na ya Witiri. Hiyo ni riwAya Na Ibn Haswin naye amepokea kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) .

Imesemwa kuwa Shufwa ni siku ya kuchinja na Witiri ni siku ya Arafa, kutoka kwa Ibn Abbas Akrama na Adh-Dhah-hak nayo ni riwAya Na Jabir kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) .

Imesemwa kuwa Shufwa ni siku ya Tarwiya (siku ya nane ya mwezi Dhul-Hijja) na Witiri ni siku ya Arafa (siku ya tisa ya Dhul-Hijja), hayo yamepokewa kutoka kwa Abu Jaffar na Abu Abdillah.

Riwaya hizo tatu zimepokewa kwa njia ya Ahli Sunnah. Inawezekana kukusanya kati ya hizo riwaya kwamba makusudio ni Shufwa na Witiri yoyote. Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu "Masiku kumi" amesema ni ya mwezi wa Dhul-Hijja na "Shufwa na Witiri" amesema ni rakaa mbili na moja. Katika hadith Shufwa ni Hassan na Hussein na Witiri ni Amiirul Muuminiin(a.s) . Katika riwAya Na Abu Jarud, kutoka kwa Abu Jaffar kuhusu Aya Na tano anasema ni "Mwenye akili". Katika ulal kwa isnadi yake kwa Abana Al-Ahmar amesema: "Nilimuuliza Abu Abdillahi kuhusu kusema kwake Mwenyezi Mungu. Na Firaun mwenye vigingi, kwanini ameitwa hivyo?" Akasema : "Kwa sababu alikuwa anapomwadhibu mtu humtandaza juu ya ardhi na kumnyoosha mikono yake na miguu yake kisha humwamba kwa vigingi vinne. Mara nyengine humtandaza juu ya ubao na kumwamba miguu yake na mikono yake kwa vigingi vine, kisha humwacha mpaka afe, ndio Mwenyezi Mungu akamwita mwenye vigingi."

Katika Majmau kuhusu "Hakika Mola wako ni mwenye kuotea" imepokewa kutoka kwa Ali(a.s) kwamba yeye amesema: Hakika maana yake ni kwamba Mola wako ni muweza wa kuwalipa waasi malipo yao. Katika hiyo hiyo Majmau imepokewa kwa Swadiq amesema maana ya neno Mirswad ni korongo kwenye Swirat halipiti korongo hilo mja ambaye hakujiweka kimja. Kutoka kwa Ghawali naye kutoka kwa Aswadiq(a.s) katika hadithi ya kutafsiri kauli ya Mwenyezi Mungu (s.w.t): "Na dhun-nun (Yunusi) alipoondoka hali amechukiwa na akadhani ya kwamba hatutamdhikisha." (21:87) Amesema: Husikii kauli yake Mwenyezi Mungu. "Ama amjaribupo, akamdhikisha riziki yake, husema: Mola wangu amenitweza"? Katika Tafsiri ya Qummi katika riwAya Na Abu Jarud, kutoka kwa Abu Jaffar(a.s) kuhusu kauli yake "si hivyo ardhi itakapopondwa pondwa' Amesema hilo ni tetemeko.

Katika Durril-Manthur ametoa Ibn Murduwayh kutoka kwa Ali bin Abu Twalib amesema: "Amesema Mtume(s.a.w.w) he, mnajua nini tafsiri ya aya hii! "Si hivyo ardhi Takapondwa pondwa ikaleta siku hiyo Jahannam" akasema: Kitakapokuwa Kiyama Jahannam itaongozwa kwa hatamu elfu sabini kwa mikono ya Malaika elfu sabini itachomoza mchomozo mmoja, lau Mwenyezi Mungu sikuifunga ingeliunguza mbingu na ardhi. Hadith hii pia ni yenye kupokewa kutoka cha Amali Sheikh kwa isnadi yake kutoka kwa Arridha naye kutoka kwa baba yake naye kutoka kwa Ali(a.s) naye kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) .

Katika Uyun katika mlango wa yaliyokuja kutoka kwa Arridha katika Akhbaru Tawhid kwa isnadi yake kutoka kwa Ali bin Fadh-dhal naye kutoka kwa baba yake amesema: Nilimuuliza Arridha(a.s) kuhusu kusema kwake Mwenyezi Mungu "Na akaja Mola wako na Malaika (wamejipanga) safu kwa safu" Akasema: "Hakika Mwenyezi Mungu Mtukufu hasifiwi na kuja na kwenda isipokuwa maana ni, na ikaja amri ya Mola wako."

Katika Kafi kwa isnadi yake kutoka kwa Sadiyr Asswayrafiy amesema: "Nilimwambia Abu Abdillah(a.s) niwe mkombozi wako ewe mtoto wa Mtume wa Mwenyezi Mungu, Je, muumin anachukia anapotolewa roho yake akasema: Hapana, hakika yeye anapojiwa na Malaika wa Mauti kuchukua roho yake hufadhaika, Malaika wa Mauti huwambia: Ewe walii wa Mwenyezi Mungu usifadhaike, ninaapa kwa ambaye amempa utume Muhammad, hakika mimi nitakufanyia wema na upole kuliko mzazi, fungua macho uone.

Hapo atafanishiwa Mtume(s.a.w.w) , Amirul Muminiin, Fatima, Hassan and Hussein na Maimamu katika kizazi chao(a.s) ataambiwa hawa ni marafiki zako. Atafungua macho yake na atanadi mnadi kutoka mbele ya Mwenyezi Mungu atasema; Ewe nafsi iliyotua! Kwa Muhammad na Ahlul Bait wake rudi kwa Mola wako hali ya kuridhia wilaya na hali ya kuridhiwa thawabu, ingia katika waja wangu yaani Muhammad na Ahlul Bait wake na ingia katika pepo yangu. Litakua ni jambo la kupendeza kwake kutolewa roho yake na kumsikia mnadi. Amepokea Qummi riwaya kwa maana haya katika Tafsiri yake na Al-Barqi katika Mahasin.

15

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA BALAD (MJI) (NA. 90)

INA AYA 20

Kwa jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu

لَا أُقْسِمُ بِهَـٰذَا الْبَلَدِ ﴿١﴾

1. Naapa ka mji huu.

وَأَنتَ حِلٌّ بِهَـٰذَا الْبَلَدِ ﴿٢﴾

2. Na hali yakuwa wewe ni mkazi wa mji huu.

وَوَالِدٍ وَمَا وَلَدَ ﴿٣﴾

3. Na (kwa) mzazi na alichokizaa.

لَقَدْ خَلَقْنَا الْإِنسَانَ فِي كَبَدٍ ﴿٤﴾

4. Hakika tumemuumba mwanadamu, katika mateso.

أَيَحْسَبُ أَن لَّن يَقْدِرَ عَلَيْهِ أَحَدٌ ﴿٥﴾

5.Je anadhani kwamba hatawezekana na yeyote?

يَقُولُ أَهْلَكْتُ مَالًا لُّبَدًا ﴿٦﴾

6. Anasema: Nimepoteza mali mengi!

أَيَحْسَبُ أَن لَّمْ يَرَهُ أَحَدٌ ﴿٧﴾

7. Anadhani kwamba hakuonekana na yeyote?

أَلَمْ نَجْعَل لَّهُ عَيْنَيْنِ ﴿٨﴾

8. Ja hatukumpa macho mawili?

وَلِسَانًا وَشَفَتَيْنِ ﴿٩﴾

9. Na ulimi na midomo miwili?

وَهَدَيْنَاهُ النَّجْدَيْنِ ﴿١٠﴾

10. Tukamuonyesha njia mbili?

فَلَا اقْتَحَمَ الْعَقَبَةَ ﴿١١﴾

11. Basi mbona hakupita njia nzito?

وَمَا أَدْرَاكَ مَا الْعَقَبَةُ ﴿١٢﴾

12. Na umejuaje, ni ipi njia nzito?

فَكُّ رَقَبَةٍ ﴿١٣﴾

13. Ni kumwacha huru mtumwa.

أَوْ إِطْعَامٌ فِي يَوْمٍ ذِي مَسْغَبَةٍ ﴿١٤﴾

14. Au kumlisha siku ya njaa.

يَتِيمًا ذَا مَقْرَبَةٍ ﴿١٥﴾

15. Yatima aliye jamaa.

أَوْ مِسْكِينًا ذَا مَتْرَبَةٍ ﴿١٦﴾

16. Au maskini mwenye haja.

ثُمَّ كَانَ مِنَ الَّذِينَ آمَنُوا وَتَوَاصَوْا بِالصَّبْرِ وَتَوَاصَوْا بِالْمَرْحَمَةِ ﴿١٧﴾

17. Kisha akawa ni katika ambao wameamini, wakausiana kusubiri na wakausiana kuoneana huruma.

أُولَـٰئِكَ أَصْحَابُ الْمَيْمَنَةِ ﴿١٨﴾

18. Hao ndio watu wa heri.

وَالَّذِينَ كَفَرُوا بِآيَاتِنَا هُمْ أَصْحَابُ الْمَشْأَمَةِ ﴿١٩﴾

19. Na ambao wamezikanusha alama zetu, hao ndio wa shari.

عَلَيْهِمْ نَارٌ مُّؤْصَدَةٌ ﴿٢٠﴾

20. Juu yao ni moto uliokomewa.

UBAINIFU

Sura inataja kwamba umbo la mtu ni lenye kujengwa juu ya tabu na mashaka. Huwezi kukuta jambo lolote katika mambo ya maisha isipokuwa litakuwa limekutanishwa na matatizo na tabu, tangu roho inapoingia katika kiwiliwili chake mpaka anapokufa. Hana raha inayoepukana na tabu na mashaka, wala furaha isiyoandamana na misukusuko au huzuni isipokuwa katika nyumba ya akhera tu, mbele ya Mwenyezi Mungu. Basi mtu na avumulie uzito wa taklifa za Mwenyezi Mungu kwa kusubiri juu ya kufanya twaa na kuepukana na maasia. Na ajitahidi kueneza huruma juu ya wale waliopatwa na majaribio na balaa za dunia kama uyatima, ufakiri na maradhi ili awe ni katika watu wa heri. Kama si hivyo, basi akhera yake itakuwa kama dunia yake na atakuwa katika watu waovu juu yao ni moto uliofungiwa.

Mpangilio wa Aya Na Sura nii unafanana na wa Makka, kwa hiyo unatilia nguvu kuwa Sura imeshuka Makka. Baadhi wamedai kuwa hilo (la kushuka Makka) ni kwa Ijmai (mkusanyiko wa makubaliano ya wanazuoni). Imesemekana kwamba Sura hii imeshuka Madina na kwamba mpangilio wa aya za mwanzo hausaidii kusema kuwa imeshula Makka. Na pia imesemwa imeshuka Madina isipokuwa aya nne za mwanzo. Utakuja ufafanuzi katika utafiti wa hadith (Inshallah).

Aya Na 1

Wametaja kuwa makusudio ya mji huu ni Makka na hilo linatilia nguvu kuwa Sura imeshuka Makka.

Aya Na 2

Kuliweka jina dhahiri mahali pa dhamir ni kwa ajili ya kuadhimisha (mji huo) na kushughulika nao ambao ni mji mtukufu. Neno Hillun ni masdar kiarifa chenye kutumika kama jina kwa maana ya kukaa na kuthibiti mahali. Masdar hapa imekuja kwa maana ya (fail) Mtendaji maana yake kwa ujumal: ninaapa kwa mji huu na hali ya kuwa wewe ni mkazi wake. Na hilo uzindushi juu ya utukufu wa Makka kwa sababu ya kukaa kwake Mtume(s.a.w.w) na kuwa ni mahali pake pa kuzaliwa.

Inasemekana jumla hiyo imeingia kati tu; kati ya kiapo na chenye kuapiwa na makusudio yake ni kuhalalishwa. Anasema katika Kash-shaf "Na ameingilia kati ya kiapo na chenye kuapiwa kwa Kusema: "Na hali yakuwa wewe ni mwenye kuhalalishwa katika mji huu" yaani ni katika mateso kwamba mfano wako wewe juu ya ukubwa na utukufu wako unahalalishwa katika mji huu mtukufu, kama linavyohalalishwa windo nje ya haram. Wanaharamishwa kuua windo na kupukusa majani, lakini wanahalalisha kukutoa wewe na kukuua. Hadith hiyo imepokewa katuka kwa Sharhabil. Katika hilo ni uthabiti kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu na uwezekano na mateso aliyokuwa akiyapata kutoka kwa watu kustajaabu kutokana na hali yao ya uadui. Kisha akasema: "au alimfariji Mtume kwa kuapa kwa mji wake kwamba mtu haepukani na shida kisha akaingilia kati kwa kusema kuwa kiaga chake cha ushindi wa Makka kitatimu ili kumpa faraja, kwa hiyo akasema: na hali ya kuwa wewe ni mwenye kuhalalishiwa (yaliyoharamu) katika mji huu yaani na hali wewe utahalilishiwa hapo mbeleni utafanya ndani ya mji huu yale utakayoyataka maka kuua na kuteka".

Kwa hiyo inakuwa tafsiri ya neno Hillum ni kwa maana ya mwenye kuhalilishiwa kinyume chake ni mwenye kuharamishiwa; yaani tutakuhalalishia siku ya ushindi wa kuichukua Makka kwa muda utapigana na utamuua unayemtaka.

Aya Na 3

Ni kulazimisha namna ya kunasibika na kufungamana kati ya kiapo na chenye kuapiwa, kunapelekea kuwa makusudio ya mzazi na alichokizaa, kwamba kuna mnasaba iliowazi kati yake na mji wenye kuapiwa. Hilo linakubaliana na Ibrahim na mtoto wake Ismail(a.s) . Wao ndio chanzo cha kujengwa mji wa Makka na ndio wajenzi wa Al-Ka'aba tukufu: Mwenyezi Mungu anasema; "Na (kumbukeni) alipoinua Ibrahim kuta za nyumba (Al-Ka'aba) na Ismail (pia); (wakaomba wakasema) Ewe Mola wetu tutakabalie (amali yetu). Hakika wewe ndio mwenye kusikia, na mwenye kujua ." (2:127).

Kuleta herufi "Maa" yenye maana ya ambacho badala ya kuleta Man yenye maana ya ambaye, ni kwa ajili ya kulikuza jambo na kulistaajabia jambo lenyewe; kama alivyosema; "na Allah anajua zaidi alichokizaa ." (3:36).

Maana kwa ujumla ni naapa kwa mzazi mwenye jambo kubwa ambaye ni Ibrahim na alichokizaa ambacho ni mtoto wa ajabu wa jambo lake mwenye kubarikiwa; naye ni Ismail. Na wao wawili ndio waliojenga Al-Ka'aba. Ufahamisho wa aya tatu ni kuapa kwa mji mtukufu Makka kwa Mtume ambae amekaa katika mji huo na kwa Ibrahim na Ismail ambao wameujenga. Inasemekana kuwa makusudio ya mzazi ni Ibrahim na alichokizaa ni watoto wake wote Waarabu. Lakini ni umbali kwa Mwenyezi Mungu kuwa Mtume (SAWW) na Nabii Ibrahim(a.s) awakutanishe na watu kama akina Abu Lahab, Abu Jahal na wengineo katika viongozi wa ukafiri na awaapie wote. Na Ibrahim(a.s) alijiepusha na kila asiyemfuata katika watoto wake juu ya Tawhid wakati aliposema: "Na uniepushe mimi na wanangu na kuabudu masanamu. Mola wangu! Hakika (masanamu) hawa wamepoteza watu wengi. Basi aliyenifuata ni wangu mimi na aliyeniasi (unaweza kumsamehe) kwani wewe ni mwingi wa msamaha na Mwingi wa rehema ". (14:35-36).

Basi mwenye kufasiri alichokizaa kuwa ni watoto wa Ibrahim, ni juu yake kuwahusisha waislamu tu, katika kizazi chake, kama ilivyo katika dua ya Ibrahim. "Ewe Mola wetu! Utufanye tuwe wenyenyekevu kwako. Na miongoni mwa kizazi chetu (pia ufanye) umma mnyenyekevu kwako na utuonyeshe njia ya ibada yetu na utusameha ." (2:128).

Inasemekana kuwa makusudio ya mzazi na alichokizaa na Adma(a.s) na kizazi chake chote kwa kuzingatia kuwa kilichoapiwa viapo hivi ni kule kuumbwa mwanadamu katika mateso. Na Mwenyezi Mungu ameweka utaratibu wa kuzaliana ili kuhifadhi jinsi hii. Kwa hiyo ameapia katika aya hizi kwa kupitia utaratibu huu na matokeo yake - nayo ni mzazi na alichokizaa - kuwa mtu yuko katika tabu na mateso kulingana na namna ya kuumbwa kwake kuanzia anapopata uhai mpaka kufa.

Maelezo haya hayana ubaya, lakini kunabakia kubainisha mnasaba uliopo kati ya mji wa Makka na mzazi na kila mwenye kuzaliwa katika kuwakusanya kwenye viapo. Pia imesemwa kuwa makusudio ni Adam na watu wema katika kizazi chake. Maelezo haya ni kama yanamtakasa Mwenyezi Mungu kuapia kwa maadui wake wenye kupetuka mipaka na wafisadi katika makafiri.

Imesemwa kuwa makusudio ni kila mzazi na kila mwenye kuzaliwa na pia imesemwa kuwa ni mwenye kuzaa na asiyezaa kwa kuchukulia herufi Maa kuwa ni ya kukanusha. Vile vile imesemwa makusudio ya mzazi ni Mtume na alichokizaa ni umati wake kwa sababu yeye yuko katika daraja ya baba kwa umati wake; lakini hayo yote ni maelezo yaliyo mbali.

Aya Na 4

Jumla hiyo ni jawabu ya kiapo. Mateso katika umbile la binadamu na tabu katika mambo yake yote ya uhai ni jambo lisilofichika kwa kila mwenye roho. Mwanadamu hakusudii neema yoyote katika neema ya dunia ila huwa na matatizo katika dunia uzuri wako. Wala hawezi kupata kitu chochote katika dunia ila kitakuwa kimechanganyika na usumbufu pamoja na matatizo na mateso kuongozea misiba ya balaa za dunia na matukio ya ghafla.

Aya Na 5

Katika natija ya hoja iliyotangulia, uthibitisho wake ni kuwa; kwa kuwa mtu umbile lake limejengewa tabu, hapati kitu chochote katika anavyovitaka ila hupata asivyotaka, basi yeye ni mwenye kuzungukwa katika umbile lake, mwenye kushindwa katika matakwa yake na ni mwenye kushindwa nguvu katika analoliweza. Anayemshinda katika matakwa yake na kumshinda nguvu kufanya mambo anayoyaweza ni Mwenyezi Mungu (s.w.t) naye ni muweza katika kila upande, yeye anaweza kumfanyia mtu lolote analolitaka na kumchukua wakati anapomtaka.

Kwa hiyo mtu asifikirie kuwa hawezwi na yeyote, kwani fikra hiyo itampelekea kujifanya mkubwa mbele ya Mwenyezi Mungu na kutakabari katika kumwabudu. Au akitoa katika baadhi ya aliyoamrishwa, na kutoa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, basi anajiona ni mwingi wa mali, na husimbulia baada ya kufanya ria, kwa kusema: "Nimepoteza mali mengi!'.

Aya Na 6

Mpangilio wa aya na nyengine zinazofuatia mpaka mwisho wa Sura unaonyesha kuwa kulikuwa na baadhi ya wenye kudhihirisha Uislamu; akitoa baadhi ya mali yake anajifaharisha kuwa ametoa sana kwa kusema: nimepoteza mali mengi! Ndio ikashuka aya kumjibu, kwamba kufuzu kwa kheri za uhai hakutimu ila kwa kupita njia nzito ya kutoa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu na kuingia katika kundi la wale ambao wameamini wakausiana kusubiri na kuoneana huruma. Yatatilia nguvu hilo yale yatakayokuja katika utafiti wa hadith (Inshallah).

Aya Na 7

Ni kukanusha hilo neno la mtu kwa njia ya fumbo. Maana yanayopatikana ni kwamba vile mtu anavyolazimika kusema kuwa amepoteza mali mengi, akafikiria kuwa mimi nimeghafilika na sijui, yale aliyotoa? Basi amekosea katika hilo na Mwenyezi Mungu ni mwenye kuona aliyoyatoa, lakini kiasi hicho hakitoshi kumfanya awe ni mwenye kufuzu kwa maisha ya kheri bali hana budi kuvumilia zaidi ya hayo katika mashaka ya kimja, apite njia nzito na awe pamoja na waumini katika yote waliyonayo.

Aya Na 8-10

Yaani tumemtayarisha katika mwili wake kwa yale anayoonea ili apate elimu ya vinavyoonwa kwa kadri ya upana wa elimu hiyo Na je, hatukumpa ulimi na midomo miwili vitakavyomsaidia kutamka yaliyo katika dhamir yake miongoni mwa elimu na aongoke kwa hilo mwenzake kwa kujua mambo yaliyofichika na macho? Na tumemfahamisha njia ya heri na ya shari kwa ilhamu itokayo kwetu, hivyo yeye anujua heri na anapambanua shari. Na aya hii ya tisa iko katika maana ya Aya Na nane ya Sura Shams Na. (91).

Aya hizo tatu ni hoja juu ya kauli yake Mwenyezi Mungu "Anadhani kwamba hakuonekana na yeyote" Yaani Yeye Mwenyezi Mungu anaona matendo ya waja wake na anajua yaliyo katika dhamiri yao kwa njia ya matendo na anapambanua kheri na shari na mema na mabaya. Kwa ujumla ni kuwa hakika Mwenyezi Mungu S.W.T. ndiye ambaye anamfahamisha yenye kuonekana kupitia macho yake mawili na namna anavyoweza kupiga picha kumfahamisha jambo asilolijua, na ni Yeye ambaye anamfahamisha yaliyo katika dhamiri kupitia kusema Je, inaingilika akilini kuwa Mwenyezi Mungu amfunulie mtu mambo ambayo Yeye mwenyewe hayajui?

Na yeye ndiye ambaye anampambanulia mtu heri na shari kwa ilhamu, Je, inawezekana kuwa Yeye hawezi kujua wala kupambanua? Yeye Mwenyezi Mungu anaona aliyoyafanya mtu na najua anayonuia kuyafanya na kuyapambanua kuwa ni kheri au shari.

Aya Na 11

Maana ya neno Iqtahama ni kuingia kwa haraka na kwa shida kujigagamiza na neno Aqaba ni njia nzito yenye vikwazo vya kupanda majabali. Kujigagamiza kuparamia njia nzito ni ishara ya kutoa (mali) ambako kunakuwa vigumu kwa mtoaji, kama itakavyoelezwa. Inasemekana kuwa jumla yote ni dua dhidi ya mtu anayesema nimepoteza mali mengi lakini si hivyo.

Aya Na 12

Ni kulikuza jambo lenyewe, kama ilivyopita katika mtazamo wake.

Aya Na 13

Yaani njia nzito ni kumwachia hutu mtumwa. Makusudio ya njia nzito ndiyo huko kuacha huru ambako ni kitendo chenyewe, na kujigagamiza kunaamanisha kukitenda. Kwa hiyo basi inaharabika kauli ya baadhi ya wanaosema kwa kumwachia huru mtumwa ndiko kupita njia nzito lakini sio njia nzito yenyewe, kwamba kuna mudhafu (neno lenye kutegemezwa) uliondolewa kukisia kwake ni: Na umejuaje ni nini kupita njia nzito, kupita njia nzito ni kumwacha huru mtumwa. Hayo yaliyotajwa katika kubainisha njia nzito ambayo ni kumwacha huru mtumwa au kulisha siku ya njaa, katika kueneza huruma yamehusishwa kutajwa kutokana na umuhimu wake. Na kumetangulizwa kuacha huru mtumwa kwa sababu dini imeshughulikia sana suala hilo.

Aya Na 14-16

Neno Matraba linatoka katika neno Turab (mchanga) na maana yake ni kushikwa na mchanga (vumbi) kutokana na shida ya ufakiri. Maana yake kwa ujumla ni, au kumlisha siku ya njaa. Yatima mwenye udugu au maskini mwenye ufakiri sana.

Aya Na 17

Kuusiana kusubiri ni kuusiana kusubiri juu ya kumtii Mwenyezi Mungu na kuusiana kuoneana huruma ni kuusiana kuwaonea huruma wenye ufakiri na umaskini. Jumla nzima inaungana na jumla ya kupita njia nzito.

Aya Na 18

Neno Maymana limekuja kwa maana ya heri kinyume chake na Mash'ama uovu. Kuleta ishara ya neno (hao) kwa unavyofahamisha mpangilio wa maneno uliotangulia, ni kuwa: Wale ambao wamepita njia nzito na wakawa katika wale ambao wameamini, na wakausiana kusubiri na wakausiana kuoneana huruma ni watu wa heri. Walilolifanya katika imani na amali yao ni njema wataliona ni jambo lenye kubarikiwa, zuri na lenye kurudhiwa. Imesemekana kuwa makusudio ya Maymana ni Yamin upande wa kuume na watu wa upande ya kuume ndio ambao watapewa vitabu vyao kwa upande wao wa kuume, lakini hilo halifuatani na neno Mash'ama (uovu).

Aya Na 19

Alama zetu ni alama za mbinguni na za kinafsi nazo zinafahamisha juu ya umoja katika uungu na kuzikanusha ndio kumkanusha Mwenyezi Mungu, vile vile ni kukanusha Qur'an tukufu na aya zake na yote yaliyoshuka na kufikishwa kwa njia ya ujumbe.

Utafiti Wa Hadith Katika Majmau Aya Na 2 imesemwa kuwa maana yake ni na hali ya kuwa ni halali kwako kumuua unayemwona anastahiki kuuliwa katika makafiri. Hilo ni wakati alipoamrishwa kupigana siku wa kuichukua Makka; Mwenyezi Mungu akamhalalishia hata akaweza kupigana na kuua. AmesemaMtume(s.a.w.w) haikuhalalishiwa kwa yoyote kabla yangu wala haitakuwa halali baada yangu kwa yoyote, na mimi sikuhalalishiwa isipokuwa saa moja katika mchana. Hadith hiyo imepokewa kutoka kwa Ibn Abbas, Mujahid na Ata.

Imepokewa kutoka kwa Abu Abdillah amesema: "Maquraish walikuwa wakiuadhimisha mji na kumuhalalisha Muhammad(s.a.w.w) katika mji huo, akasema: Naapa kwa mji na halo ya kuwa wewe ni mwenye kuhalalishwa katika mji huu anakusudia kusema kuwa wao wamehalalisha kukuudhi kukuadhibisha na kukutukana. Na wao walikuwa hawamwadhibu hata mtu aliyeua baba wa mmoja wao. Na walikuwa wakivaa majani wa mti kumpa amani, lakini wakahalalisha kwa Mtume(s.a.w.w) yale ambayo hawakumuhalalishia mwengine. Katika hiyo Majmau kuhusu Aya Na tatu imesemwa kuwa ni Adam an alichokizaa katika Mitume, mawalii na wafuasi wao. Hadith hiyo imepokewa kutoka kwa Abu Abdillahi.

Maana yaliyotangulia pia yamepokewa katika njia ya Ahli Sunna. Pia amepokea Qummi katika Tafsiri yake. Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu Aya Na sita amesema maana ya neno Lubada ni mkusanyiko. Na katika Majmau kuhusu aya hiyo hiyo imesemwa huyo aliyesema hivyo ni Harith bin Naufal bin Abdul Manaf, wakati alipofanya dhambi fulani, akataka fatuwa kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) akamwamrisha kutoa kafara, akasema: Tangu nilipoingia dini ya Muhammad mali yangu imeisha katika makafara na kulisha. Hadith hiyo imepokewa na Muqatil. Katika hiyo hiyo Majmau, imesemwa kuwa, aliulizwa Amirul-Miminin Ali(a.s) kwamba watu wanasema kuhusu neno ya Mwenyezi Mungu "Na tukamuongoza njia mbili" kwamba hizo njia mbili ni matiti? Akasema hapana njia mbili hizo ni heri na shari.

Katika Kafi kwa isnadi yake kutoka kwa Hamza bin Muhammad naye kutoka kwa Abu Abdillahi(a.s) amesema nilimuuliza kuhusu kauli ya Mwenyezi Mungu tukamwongoza njia mbili akasema ni njia ya heri na shari. Imepokewa riwaya hii katika Durril Manthur kwa njia ya Ali(a.s) Anas, Abu Amama na wengineo kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) .

Katika Kafi kutoka kwa Jaffar bin Khilad amesema: Alikuwa Abul-Hassan Ridha(a.s) anapokula, huletewa chano karibu na chakula chake, anaangalia chakula kizuri katika vyakula alivyoletewa na kukiweka katika chano, kisha anaamrisha kipewe masikini kisha anasoma ayah ii: 'Haya naapite hiyo njia nzito 'kisha anasema: "Mungu anajua kuwa sio kila mtu anaweza kuacha huru mtumwa kwa hiyo amewafanyia njia nyengine ya kwenda peponi".

Katika Majmau imepokewa hadith Marfuu kutoka kwa Baraa bin Azib amesema: "Alikuja bedui kwa Mtume(s.a.w.w) akasema: "Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu nijulishe amali itakayonitia peponi" Mtume akasema: "Ukiwa umefupisha hotuba basi umerefusha masuala; muache huru mtu, na uifungulie shingo." Akasema yule bedui "kwani yote hayo sio kitu kimoja?" Akasema Mtume: La! Kuacha huruni kumuacha aende zake na kuifungulia shingo ni kumsaidia katika thamani yake. Kama si hivyo, basi mlishe mwenye njaa, na mnyweshe mwenye kiu na uamrishe mema na ukataze maovu na uzuiye ulimi isipokuwa katika jambo la kheri tu. Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu kauli yale Mwenyezi Mungu : "Au maskini mwenye shida" ni yule asiyeweza kujikinga na mchanga (vumbi).


10

11

12

13

14

15

16