TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN12%

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN
  • Anza
  • Iliyopita
  • 29 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 42572 / Pakua: 4763
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

Mwandishi:
Swahili

1

2

3

7

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA INFITAR (KUPASUKA) (NA. 82)

INA AYA 19

Kwa jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu.

إِذَا السَّمَاءُ انفَطَرَتْ ﴿١﴾

1. Mbingu zitakapopasuka.

وَإِذَا الْكَوَاكِبُ انتَثَرَتْ ﴿٢﴾

2. Na nyota zitakapoputika.

وَإِذَا الْبِحَارُ فُجِّرَتْ ﴿٣﴾

3. Na bahari zitakapofunguliwa na kuchanganyika.

وَإِذَا الْقُبُورُ بُعْثِرَتْ ﴿٤﴾

4. Na makaburi yatakapopinduliwa.

عَلِمَتْ نَفْسٌ مَّا قَدَّمَتْ وَأَخَّرَتْ ﴿٥﴾

5. Nafsi wakati huo itajua ilichokitanguliza na ilichobakisha nyumba.

يَا أَيُّهَا الْإِنسَانُ مَا غَرَّكَ بِرَبِّكَ الْكَرِيمِ ﴿٦﴾

6. Ewe mwanadamu! Ni nini kinachokughuri kwa Mola wako Mtukufu.

الَّذِي خَلَقَكَ فَسَوَّاكَ فَعَدَلَكَ ﴿٧﴾

7. Ambaye amekuumba, akakukamilisha, akakulinganisha?

فِي أَيِّ صُورَةٍ مَّا شَاءَ رَكَّبَكَ ﴿٨﴾

8. Akakufanya kwa Sura aliyoipenda.

كَلَّا بَلْ تُكَذِّبُونَ بِالدِّينِ ﴿٩﴾

9. Hapana sio hivyo! Bali mnayakadhibisha malipo.

وَإِنَّ عَلَيْكُمْ لَحَافِظِينَ ﴿١٠﴾

10. Na hakika mna wenye kuwatunza.

كِرَامًا كَاتِبِينَ ﴿١١﴾

11. Watukufu wenye kuandika.

يَعْلَمُونَ مَا تَفْعَلُونَ ﴿١٢﴾

12. Wanajua mnayoyatenda.

يَعْلَمُونَ مَا تَفْعَلُونَ ﴿١٢﴾

13. Hakika watu wema watakuwa katika neema.

وَإِنَّ الْفُجَّارَ لَفِي جَحِيمٍ ﴿١٤﴾

14. Na hakika watu waovu watakuwa katika moto.

يَصْلَوْنَهَا يَوْمَ الدِّينِ ﴿١٥﴾

15. Watauingia siku ya malipo.

وَمَا هُمْ عَنْهَا بِغَائِبِينَ ﴿١٦﴾

16. Wala hawatakuwa mbali nao.

وَمَا أَدْرَاكَ مَا يَوْمُ الدِّينِ ﴿١٧﴾

17. Ni lipi la kukujulisha ni ipi siku ya malipo.

ثُمَّ مَا أَدْرَاكَ مَا يَوْمُ الدِّينِ ﴿١٨﴾

18. Kisha ni lipi la kukujulisha ni ipi siku ya malipo?

يَوْمَ لَا تَمْلِكُ نَفْسٌ لِّنَفْسٍ شَيْئًا وَالْأَمْرُ يَوْمَئِذٍ لِّلَّـهِ ﴿١٩﴾

19. Ni siku ambayo nafsi haitamilikia chochote nafsi nyengine , na amri siku hiyo ni ya Allah (peke yake).

UBAINIFU

Sura inajulisha siku ya Kiyama kwa kutaja baadhi ya alama zake zenye kulazimiana nayo na zenye kuambatana nayo. Inakisifu hicho Kiyama kwa yale yatakayotukia ndani ya siku hiyo; ambayo ni kukumbuka mtu alilolitanguliza na aliloliacha nyuma katika amali zake njema na mbaya - ambayo yamehifadhiwa na malaika wanaohusika nayo - na kulipwa amali yake. Akiwa ni mwema, basi atalipwa wema na akiwa ni mwovu mwenye kukadhibisha siku ya malipo, basi atalipwa moto atakaouingia hali ya kudumu humo. Kisha inaanzia tena kusifu hiyo siku; kwamba ni siku ambayo nafsi haitamilikia nafsi nyengine kwa chochote na amri siku hiyo ni ya Mwenyezi Mungu. Sura hii imeshuka Makka bila ya ubishi wowote.

Aya Ya 1

Aya hii iko kama aya inayosema: "na mbingu zitapasuka, basi siku hiyo zitakuwa dhaifu kabisa ." (69:16).

Aya Ya 2

Kupukutika nyota yaani kutawanyika kwa kuondoka sehemu zake zilipowekwa. Zimefananishwa nyota na lulu zilizotungwa ushanga, kisha ukakatika uzi wake, zikapukutika na kutawanyika.

Aya Ya 3

Yaani nahari zitafunguliwa kwa kuondoka kizuizi na yachanganyike maji ya tamu na ya chumvi na kuwa bahari moja. Haya ndiyo maana yanayosabiana na tafsiri ya kauli yake Mwenyezi Mungu. "Na bahari zitakapofurika " (82:6).

Aya Ya 4

Katika Majmau amesema neno Buuthirat lina maana ya kupindua chini juu. Kwa hivyo maana yake ni utakapogeuzwa mchanga wa makaburi na kugeuzwa ndani nje ili kuwatoa wafu na kufufuliwa kwa ajili ya malipo.

Aya Ya 5

Makusudio ya kujua hapa ni kujua kwa upambunuzi matendo yake aliyoyatenda duniani. Na haya sio kuwa yanapatikana kwa kupewa kitabu la! Mwenyezi Mungu anasema: "Bali mtu ni shahidi juu ya nafsi yake ingawa anatoa nyudhuru zake " (78:15).

"Siku atakayokumbuka mtu alichokitenda ". (79:35).

"Siku ambayo kila nafsi itakuta mema iiyoyafanya yamedhuhurishwa na pia ubaya ilioufanya ". (3:30).

Makusudio ya nafsi ni jinsi ya nafsi yoyote, na makusudio ya ilichokitanguliza, ni kile ilichokifanya katika uhai wake. Na kile ilichokibakisha nyuma ni kile ilichokianzia ikiwa kheri au shari na kikafanywa baada ya kufa kwake huandikwa katika karatasi ya amali yake. Mwenyezi Mungu anasema: "..na tunaliandikia kile walichokitanguliza (bila ya kuacha athari) na (kile walichokifnya kikaacha) athari zao ". (36:12) Inasemekana kuwa makusudio ya aya ni kile ilicho kifanya mwanzo wa umri wake na kile ilichokifanya mwisho wa umri wake. Kwa hiyo inakuwa ni fumbo la uchunguzi zimesemwa maana nyengine ambazo hazihitaji kutajwa hapa. Mwenye kuzitaka na ajipatie vitabu vilivyorefushwa tafsiri.

Aya Ya 6-8

Ni lawama na kumkemea mtu. Makusudio ya mtu hapa ni yule mwenye kukadhibisha siku ya malipo kama unavyofahamisha mzunguuko mzima wa maneno unaokusanya "Bali nyinyi mnakadhibisha malipo". Na kuikadhibisha siku ya malipo ni kufuru na kukanusha sheria ya malipo, na kuikanusha kwake ndio kukanusha ubwana wa Mwenyezi Mungu S.W.T. Msemo umeelekezwa kwa mtu kwa kuwa yeye ni mtu ili iwe ni hoja kwa kuthibiti mambo yaliyotajwa ya neema zinazohusikana naye kama mtu. Amefungamanisha kuhadaika na sifa mbili za ulezi wake na ukarimu wake Mwenyezi Mungu (s.w.t), ili iwe ni hoja katika kuelekeza lawama. Kwani hakika mwenye kulewa, akimwasi mlezi wake ambaye anaangalia mambo yake na kumfunika na neema zake ndani na nje, ni ukafiri usiokuwa na shaka katika ubaya wake na katika kustahiki kwake adhabu, hasa akiwa mlezi ni karimu asiyetaka kulipwa chochote katika neema yake na anachokitoa, anayesamehe makosa yanayotukia kwa kutojua. Basi ikiwa hivyo ukafiri wakati huo utakuwa mbaya zaidi, na shutuma na lawama zitakuwa kali zaidi. Kwa hivyo aya ya (6) ni swali la kukemea analokemewa mtu kwa sababu ya ukafiri, hasa usiokuwa na udhuru, nao ni ukafiri wa kukufuru neema ya Mola wake aliyekarimu.

Hawezi mtu kujibu kwa kusoma "Ewe Mola wangu umenihadaa ukarimu wako" kwani Mwenyezi Mungu amekwishayapitisha aliyoyahukumulia na kumfikishia mtu kupitia kwa ulimi wa Mitume yake; kama alivyosema; "Kama mkishukuru nitawazidishieni, na kama mkikufuru, (jueni) kuwa adhabu yangu ni kali sana." (14:7).

"Ama aliyepetuka mipaka. Akapendelea zaidi maisha ya dunia. Basi moto ndio makazi yake ." (79:39).

Zaidi ya hizo kuna aya nyenginezo zinazoelezea kwamba hakuna kuokoka kwa wale wenye kufanya inadi na adhabu; na ukarimu hautawafikia siku ya Kiyama. "Na rehema yangu inaenea kila kitu, lakini nitawaandikia wale wanaojikinga na yale niliyoyakataza ". (7:156) Lau kungemtosheleza mtu mwenye kuasi kusema "umenihadaa ukarimu wako" basi angeliepuka na adhabu kafiri mwenye kufanya inadi, kama itakavyoondolewa kwa muumini aliyeasi. Wala hapana udhuru baada ya ubainifu.

Aya Ya 7

Ni ubainifu wa ulezi wake wenye kuwa pamoja na ukarimu, kwani ni katika kuangalia kwake vizuri kumuumba mtu kwa mafungu yake yote na kumfanya sawa kwa kuweka kila kiungo mahali pake panaponasibiana nacho; kisha akalinganisha baadhi ya viungo vyake na akavitia nguvu kwa baadhi ya viungo vyengine kwa kufanya wizani na ulinganifu kati yao. Kwa hivyo kiungo hakiwezi kukidhoofisha kuingo chengine; kama vile kula kwa kumega tonge ambako ni kwa ajili ya mdomo na mdomo nao unalikata tonge na kulitafuna, hilo linatimia kwa meno tofauti, halafu inahitajika kulipeleka tonge katika pembe za mdomo na kuligeuza, na kazi hiyo inafanywa na ulimi. Na mdomo katika kula unahitaji kuwekewa chakula, hilo linafanywa na mkono na kazi hiyo inatimizwa na kiganja na kufanya kazi kwake ni kwa vidole vyenye manufaa tofauti. Mkono nao unahitaji kuchukua na kuweka mahali na hilo linafanywa na mguu. Ni kama hivyo kazi za viungo vyengine. Ni maelfu kwa maelfu yasiyohisabika katika mipango yake Mwenyezi Mungu, ambaye anayafanya yote hayo bila ya kutaka kujinufaisha au kumzuia yeye mambo ya mtu ya kusahau shukrani na kuikufuru neema. Yeye Mwenyezi Mungu ni Mola Mkarimu.

Aya Ya 8

Ni ubainifu wa kauli yake "Akakulinganisha sawa" yaani katika Surah yoyote aliyopenda akakufanya - wala hataki ila lile lenye hekima - akakufanya mke na mume, mweupe na mweusi, mrefu na mfupi, mzuri na mbaya na mwenye nguvu na mnyonge na mengineo. Vile vile viungo vyenye kushurikiana kati ya watu kwa namna tofauti mfano mikono miwili , miguu miwili na macho mawili. Pia kichwa na kiwiliwili na kulingana sawa kimo nk. Yote hayo ni katika kulinganisha baadhi ya viungo na vyengine. Mwenyezi Mungu anasema: "Hakika tumemuumba mwanadamu katika hali nzuri mno ." (95:4). Yote hayo yanaishilia kwenye mazingatio mazuri yake Mola hakuna utengenezaji wa mtu katika hilo.

Aya Ya 9

Ni kuzuia kughurika mtu na ukarimu wa Mwenyezi Mungu na kulijaalia hilo ni wasila wa kufuru na uasi, yaani msighurike hakutawafaa kughurika.

Aya Ya 10 - 12: Ni ishara ya kwamba amali za mtu zitahudhurishwa na ni zenye kuhifadhiwa siku ya Kiyama kwa njia nyengine isiyokuwa kukumbuka kwake mtu. Njia ambayo ni kwa kuandika waandishi wa amali katika malaika wenye kuwakilishwa kwa mtu kwa kumchukulia hisabu; kama alivyosema Mwenyezi Mungu: "Na tutamtolea siku ya Kiyama daftari (iliyoandikwa amali yake) atakayoikuta imekunjuliwa (aambiwe) soma daftari yako, nafsi yako leo inakutosha kukuhisabu ". (17:13-14).

Kwa hivyo kusema kwake Mwenyezi Mungu : "Na hakika wenye kuwatunza" Yaani hakika mna wenye kuwatunza kutoka kwetu wanaohifadhi amali kwa kuziandika. Kusema kwake "watukufu wenye kuandika" yaani wenye utukufu na enzi mbele ya Mwenyezi Mungu (s.w.t).

Imekaririka katika Qur'an tukufu kuwasifu Malaika kwa utukufu, na hilo sio mbali kuwa makusudio yake kwa kusaidiwa na mpangilio wa maneno, ni kuwa wao kimaumbile ni wenye kuhifadhiwa na madhambi na maasi.

Hilo linatiliwa nguvu na kauli yake Mwenyezi Mungu: "Bali (hao Malaika) ni waja waliotukuzwa. Hawamtangulii kwa neno, nao wanafanya amri zake ". (21:26-27).

Hilo linafahamisha kuwa wao hawataki isipokuwa analolitaka Mwenyezi Mungu, wala hawafanyi ila waliloamrishwa na Mwenyezi Mungu. Vile vile kauli yake: "Watukufu watenda njema ". (80:16).

Makusudio ya kuandika ni kuandika amali kwa kukutanisha na kauli yake wanajua mnayoyafanya. Kauli yake Mwenyezi Mungu: wanajua mnayoyafanya ni kukanusha makosa yao katika kuihusisha heri na shari kama ilivyotangulia aya ya kuwaepusha na madhambi na maasia, wao ni wenye kuzunguukwa na matendo kama yalivyo na sifa zake, lakini ni wenye kuhifadhiwa nayo. Imekuja katika tafsiri ya aya: "Hakika Qur'an ya Al-Fajiri inashuhudiwa (na Malaika) ". (17:78).

Kwamba waandishi wa amali wa mchana wanapanda nayo, baada ya kutua jua na wanashuka wengine wanaadhika amali ya usiku mpaka Al-Fajiri wanapande na wanashuka Malaika wa mchana na kadhalika.

Aya Ya 13 -14

Ni maelezo yanayobainisha natija ya kuhifadhi amali kwa kuandikwa na waandishi nayo ni kudhihiri siku ya Kiyama. Wema ni wale wenye amali njema na waovu ni wale wenye dhambi.

Aya Ya 15

Dhamiri ni ya moto; yaani waovu watalazimiana nao siku ya malipo.

Aya Ya 16

Inaungana na aya iliyotangulia, inatilia nguvu maana ya kulazimiana nao na moto na kukaa kwao milele. Makusudio ya kutokuwa mbali nao ni kutotoka humo. Aya hii iko katika maana ya aya inayosema: "wala hawatakuwa wenye kutoka motoni ". (2:167).

Aya Ya 17

Ni utisho na kulikuza jambo la siku ya malipo; yaani haiwezi kujulikana nini hakika ya siku ya malipo. Hii ni ibara ya fumbo la kulikuza jambo.

Aya Ya 18

Ni kutilia mkazo ukubwa wake.

Aya Ya 19

Ni ubainifu wa kijumla wa hakika ya siku ya malipo. Hilo ni kwamba athari zote zenye kufungana na sababu za dhahiri ni zenye kukatika, kama kunavyofahamisha kusema kwake Mwenyezi Mungu: "na yatakatika mafungamano yao ". (2:166).

Kuhusu kusema kwake "na amru siku hiyo ni ya Allah" yaani yeye ni mwenye kumiliki amri si mwengine; kama alivyosema: "Leo ufalme ni wa nani" Ni wa Allah mmoja mwenye kushinda " (40:16).

Kusema kuwa neno Amr lina maana ya jambo hakuafikiani. Na mahali hapa.

Utafiti Wa Hadith Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu kusema kwake Mwenyezi Mungu (s.w.t) "Na makaburi yatakapopinduliwa" amesema yatapasuka na watatoka watu. Katika Durril Manthur ametoa Hakim na akaisahihisha kutoka kwa Hudhayfa amesema: "Amesema Mtume(s.a.w.w) : Mwenye kuanzisha heri ikafuatwa atakuwa na malipo mfano wa malipo ya wanaomfuata bila ya wao kupungukiwa. Na mwenye kuanzisha shari ikafuatwa basi atapata dhambi zake na dhambi za mfano wa wanaomfuata bila ya wao kupungukiwa. Akasoma Hudhayfa "Itajua nafsi na ilichokitanguliza na ilichokibakisha nyuma". Katika hiyo hiyo Durril Manthur ametoa Abd bin Hamid kutoka kwa Saleh bin Miswar amesema: "Imenifikilia mimi habari kwamba Mtume(s.a.w.w) amesoma aya hii: "Ewe mwanadamu! Ni nini kinachokughuri kwa Mola wako Mtukufu; kisha akasema ni ujinga wake ".

Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu "Akakufanya kwa sura yoyote aliyopenda" anasema: Lau angetaka angekufanya sura isiyokuwa hii. Katika hiyo hiyo Tafsiri kuhusu "na hakika mna wenye kuwatunza" amesema: "Ni Malaika wawili wawakilishi kwa mtu." Kutoka kwa Saad Assu'ud ni kwamba hao Malaika wawili wanamjia Muumin wakati wa swala ya Al-Fajiri wakishuka wale wengine wa usiku huondoka, linapotua jua hushuka wale wa usiku na kuondoka wa mchana. Hiyo inakuwa ni ada yao mpaka anapofikiwa na mauti yake wakati yakifikia mauti yake husema hao Malaika wawili kumwambia mtu mwema: "Allah akulipe uliyosuhubiana nasi kwa kheri, amali ngapi njema umetuonyesha! Kauli ngapi nzuri umetusikilizisha! Na ni vikao vingapi vya kheri umetupeleka! Basi leo sisi tuko juu ya lile unalolipenda na waombezi kwa Mola wako."

Akiwa ni asi (muovu) humwambia: "Mungu akulipe uliyesuhubiana nasi kwa shari, ulikuwa ukituudhi, ni amali ngapi mbaya ulizotuonyesha! Ni kauli ngapi mbovu ulizotusikilizisha! Na ni vikao vingapi viovu ulivyotupeleka! Basi sisi leo tuko juu ya lile unalolichukia na mashahidi mbele za Mola wako." Katika Majmau kuhusu "Na amri siku hiyo ni ya Mwenyezi Mungu" amepokea Amr bin Shamr kutoka kwa Jabir naye kutoka kwa Abu Jaffar(a.s) amesema: "Amri siku hiyo ni ya Mwenyezi Mungu na siku yote ni ya Mwenyezi Mungu. Ewe Jabir siku ya Kiyama mahakimu wote watakomea, hatabakia hakimu isipokuwa Mwenyezi Mungu."

Makusudio yake Imam ni kwamba, kuwa amri ni ya Mwenyezi Mungu, hakuhusika na siku ya Kiyama tu, bali amri ni ya Mwenyezi Mungu milele, na kuihusisha na siku ya Kiyama, ni kwa kuzingatia kudhihiri hiyo amri na wala sio asili yake yaani kudhihiri kwa kuonekana; siku hiyo hakutakuwa na amri ya mwengine yoyote isipokuwa Yake Yeye Mtukufu.

8

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA MUTAFFIFIN (WAPUNGUZAJI VIPIMO) (NA. 83)

Aya ya 1-21

Kwa jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu

وَيْلٌ لِّلْمُطَفِّفِينَ ﴿١﴾

1. Ole wao wenye kupunguza (vipimo).

الَّذِينَ إِذَا اكْتَالُوا عَلَى النَّاسِ يَسْتَوْفُونَ ﴿٢﴾

2. Ambao wakijipimia kwa watu kwa pishi hujikamilishia.

وَإِذَا كَالُوهُمْ أَو وَّزَنُوهُمْ يُخْسِرُونَ ﴿٣﴾

3. Na wanapowapimia wao kwa pishi au kwa mizani, hupunguza.

أَلَا يَظُنُّ أُولَـٰئِكَ أَنَّهُم مَّبْعُوثُونَ ﴿٤﴾

4. Jee, hawadhani hao kuwa watafufuliwa?

لِيَوْمٍ عَظِيمٍ ﴿٥﴾

5. Katika siku kubwa.

يَوْمَ يَقُومُ النَّاسُ لِرَبِّ الْعَالَمِينَ ﴿٦﴾

6. Siku ambayo watu watasimama mbele ya Mola wa viumbe.

كَلَّا إِنَّ كِتَابَ الْفُجَّارِ لَفِي سِجِّينٍ ﴿٧﴾

7. Si hivyo! Hakika maandishi ya watu waovu yamo katika Sijjin.

وَمَا أَدْرَاكَ مَا سِجِّينٌ ﴿٨﴾

8. Ni lipo la kukujulisha nini hiyo Sijjin.

كِتَابٌ مَّرْقُومٌ ﴿٩﴾

9. Ni daftari iliyoandikwa (amali za watu waovu).

وَيْلٌ يَوْمَئِذٍ لِّلْمُكَذِّبِينَ ﴿١٠﴾

10. Ole wao siku hiyo wenye kukadhibisha.

الَّذِينَ يُكَذِّبُونَ بِيَوْمِ الدِّينِ ﴿١١﴾

11. Ambao hukadhibisha siku ya malipo.

وَمَا يُكَذِّبُ بِهِ إِلَّا كُلُّ مُعْتَدٍ أَثِيمٍ ﴿١٢﴾

12. Wala haikadhibisha ila kila mpetuka mipaka mwingi wa madhambi.

إِذَا تُتْلَىٰ عَلَيْهِ آيَاتُنَا قَالَ أَسَاطِيرُ الْأَوَّلِينَ ﴿١٣﴾

13. Ambaye anaposomewa aya zetu husema: ni ngano za watu wa kale.

كَلَّا بَلْ رَانَ عَلَىٰ قُلُوبِهِم مَّا كَانُوا يَكْسِبُونَ ﴿١٤﴾

14. Si hivyo! Bali yametia kutu juu ya nyoyo zao waliyokuwa wakiyachuma.

كَلَّا إِنَّهُمْ عَن رَّبِّهِمْ يَوْمَئِذٍ لَّمَحْجُوبُونَ ﴿١٥﴾

15. Si hivyo! Hakika wao siku hiyo watazuiliwa kupata rehema ya Mola wao.

ثُمَّ إِنَّهُمْ لَصَالُو الْجَحِيمِ ﴿١٦﴾

16. Kisha wao wataingia motoni.

ثُمَّ يُقَالُ هَـٰذَا الَّذِي كُنتُم بِهِ تُكَذِّبُونَ ﴿١٧﴾

17. Kisha wataambiwa: Hili ndilo ambalo mlikuwa mkilikadhibisha.

كَلَّا إِنَّ كِتَابَ الْأَبْرَارِ لَفِي عِلِّيِّينَ ﴿١٨﴾

18. Si hivyo! Hakika maandishi ya watu wema yamo katika Illiyyin?

وَمَا أَدْرَاكَ مَا عِلِّيُّونَ ﴿١٩﴾

19. Ni lipi la kukujulisha ni nini Illiyyin?

كِتَابٌ مَّرْقُومٌ ﴿٢٠﴾

20. Ni daftari iliyoandikwa (amali za watu wema).

يَشْهَدُهُ الْمُقَرَّبُونَ ﴿٢١﴾

21. Ambayo hushuhudiwa na wenye kukurubishwa.

UBAINIFU

Sura inaanzia kwa kutoa makamio kwa wale wenye kupunguza vipimo katika pishi au mizani na kuwaonya kwamba wao watafufuliwa kwa ajili ya malipo katika siku iliyokuwa kubwa, nayo ni siku ya Kiyama. Kisha inafafanua yale yatakayowapitia siku hiyo waovu na wema. Inavyonasibu zaidi kwa kuangalia mpangilio ni kuwa mwanzo wa Sura unaoelezea makamio kwa wenye kupunguza kipimo, umeshuka Madina. Ama aya zinazofuatia mpaka mwisho wa Sura zinakubali kufungamana na mpangilio wa Makka na Madina.

Aya Ya 1

Ni makamio juu ya wanaopunguza vipimo. Mwenyezi Mungu amelikataza hilo, na ameliita ufisadi katika nchi, kama alivyolielezea katika kauli ya Mtume Shuayb. "Na enyi watu wangu! Timizeni kipimo na mizani kwa uadilifu wala msiwapunguzie watu vitu vyao, wala msieneze uovu katika nchi mkafanya ufisadi ." (11:85).

Aya Ya 2-3

Madhumuni ya aya zote mbili ni shutumu ya aina moja; hayo ni kwamba wao wanachunga haki yao tu! Na wala hawachungi haki ya wengine. Kwa maneno mengine, hawachungi haki za wengine, kama vile wanavyochunga haki zao. Jambo hilo linaleta ufisadi katika jamii ya watu iliyojengwa juu ya uadilifu na haki. Haikutajwa mizani katika aya ya 2 kama ilivyotajwa katika aya ya 3 kwa sababu imesemwa kuwa wapunguzaji vipimo aghlabu walikuwa wakinunua nafaka na mazao, kisha wanachuma, kwa kuyauza kidigo kidogo. Desturi yao ilikuwa zaidi ni kunuliwa kwa pishi, sio kwa mizani ndio ikatajwa pishi peke yake katika aya ya pili. Imesemwa kuwa haikutajwa mizani kwa sababu mizani na pishi ni za kununua na kuuza, ikitajwa moja yao, inatosha kufahamisha juu ya nyengine na yale yaliyotajwa katika pishi yanapita pia katika mizani. Njia hiyo haiwezi kuepuka kuangaliwa vizuri. Imesemwa kuwa aya mbili zinaelezea mazoea waliyokuwa nayo wale ambao Sura imetereshwa kwa sababu yao. Walikuwa wakinunua kwa pishi tu! Na wakiuza kwa mizani na pishi. Njia hii ni madai yasiyokuwa na dalili. Mengi yametajwa kwa njia ya kufupisha juu ya pishi ambayo hayaepukani na udhaifu.

Aya Ya 4-5

Ni swali la kukanusha na kustaajabu. Kuishiria wenye kupunguza vipimo kwa neno "hao" nikuishiria kwa umbali, kwa maana ya kuwa kwao mbali na Rehema ya Mwenyezi Mungu. 'Siku kubwa' ni siku ya Kiyama. Kutosheka kutaja ufufuo kwa kudhani tu, pamoja na kuwa ni wajibu kuitakidi kwa kujua na sio kwa kudhani, ni kwamba, kudhania hatari katika amali yoyote kunawajibisha kuepuka kuifanya amali hiyo hata kama haikujulikana. Kwa hiyo kudhania ufufuo katika siku kubwa ambayo atawaadhibu Mwenyezi Mungu watu kwa yale waliyoyachuma kunakataza kufanya dhambi kubwa ambayo itawajibisha adhabu yenye machungu. Imesemekana kuwa dhana hapa ni kwa maana ya kujua. Aya Ya 6: Makusudio ya kusimama ni fumbo la kuwa kwao hai baada ya kufa, ili waende kwenye hukumu yake Mwenyezi Mungu.

Aya Ya 7 -10

Ni kupinga yale waliyokuwa nayo katika kupunguza vipimo na kughafilika na ufufuo na hisabu. Kuhusu maana ya Sijjin mwenye kuangalia vizuri na kufikiri katika mpangilio wa aya nne, kwa kupima baadhi yake na nyengine na kupima mkusanyiko wake na mkusanyiko wa Illiyyin mpaka kutimia aya nne, ni kwamba makusudio ya Sijjin ni mkabala wa makusudio ya Illiyyin na neon Illiyin linatokana na neno Alaa yaani "juu" kwa hiyo Sijjin ina maana ya chini na kufungika; kama inavyoonyesha kauli yake Mwenyezi Mungu: "Kisha tukamrejeza chini ya waliochini (95:5).

Karibu zaidi ni kuwa maana yake ni jela kwa maana ya kufunga. Makusudio ya maandishi ya watu waovu ni yale aliyowakadiria Mwenyezi Mungu katika malipo na kuyathibitisha kwa hukumu yake. Tunayoyapata katika aya, ni kwamba yule ambayo ameyathibitisha Mwenyezi Mungu katika malipo yao au aliyowaandalia yako katika jela ambayo atafungwa mwenye kuiingia kifungo kirefu au milele.

Maana ya neno Marquum kama alivyosema Raghib ni hati nene. Na imesemwa ni kupanga kitabu. Na neno lake Mwenyezi Mungu ni lenye kuchukua njia zote mbili. Maana ya pili ndiyo yenye kunasibiana zaidi. Kwa hivyo inaishia kwamba maana yake ni kuwa, yale waliyoandikiwa ni yenye kubainishwa; yasiyokuwa na utatanishi wowote. Yaani hukumu ni lazima haibadiliki. Na imefahamika kuwa ni yenye kuhukumiwa wao, yenye kuthibitishwa na yenye kufafanuliwa bila utatanishi wowote. Kauli yake Mwenyezi Mungu: "Ole wao siku hiyo wenye kukadhibisha", ni kuwatakia shari waovu. Yaani na waanagamie waovu,- ambao ni wale wenye kukadhibisha siku hiyo yatahakikika yale aliyowaandikia Mwenyezi Mungu na kuwahukumia malipo. Haya ndiyo yanayofahamika kutokana na kuangalia vizuri (Tadabbur) aya hizi nne, nazo zina mpangilio mmoja wenye kuafikiana.

Watu wana kauli mbalimbali katika tafsiri ya matamko na jumla za aya hizi nne kama vile kuwa maana ya neno kitab ni maandishi ya matendo yao. Na imesemwa ni kuandika na kwamba kuna neno lilioondolewa kukadiria kwake ni: 'hakika kuandika amali ya watu waovu ni katika Sijjin. Imesemwa neno " hakika waovu" ni lenye kuenea zaidi kuliko wenye kukadhibisha kwa sababu linakusanya ukafiri na ufasiki. Na wamesema: " makusudio ya Sijjin ni ardhi ya saba chini, huweka maandishi ya watu waovu." Na imesemwa ni bonde katika Jahannam. Pia imesemwa ni shimo katika Jahannam na imesemwa ni jina la kitabu chao. Imsemwa Sijjin ya kwanza ni mbali ambapo panawekwa kitabu chao na Sijjin ya pili ni jina la kitabu chao. Imesemwa ni kitabu chenye mkusanyiko wa amali mbovu za majini na watu. Imesemwa ni hasara na utwezo. Wamesema kuwa aya ya (9) sio tafsiri ya Sijjin bali ni tafsiri ya kitabu kilichotajwa katika aya ya (7). Lakini ukiangalia vizuri utakuta nyingi za kauli hizi ni kujiamulia tu bila ya dalili yoyote.

Aya Ya 11

Ni tafsiri ya aya iliyotangulia. Kwa dhahiri makusudio ya kukadhibisha ni kukadhibisha kwa kauli iliyowazi, kwa hivyo inahusika na kuwatusi makafiri, wala haiwachanganyi mafasiki katika watu wa imani pia haihusiki na yeyote mwenye kupunguza kipimo bali ni makafiri katika wao. Hayo yanatiliwa nguvu na aya inayofuatia. Lakini kama ikikusudiwa kukabidhisha kimatendo, itakuwa inakusanya waovu katika wenye imani, kama vile ambavyo huenda hayo yanatiliwa nguvu na aya ya (4) "Je, hawadhani hao kuwa watafufuliwa?"

Aya Ya 12

Inajulikana kuwa kizuizi pekee cha maasi si kuamini ufufuo na malipo. Na mwenye kung'ang'ania kwenye matamanio, na kuufungamanisha moyo wake kwa kupetuka mipaka katika dhambi, inakataa nafsi yake kusalimika na kujizuia na yanayokatazwa na kuishia kukadhibisha ufufuo na malipo. Mwenyezi Mungu anasema: "Kisha ulikuwa mwisho wa wale waliofanya ubaya ni kuzikadhibisha aya za Allah na walikuwa wakizicheza shere " (30:10).

Aya Ya 13

Makusudio ya aya za Qur'an, kwa kuunganisha na neno "wakisomewa". Maana yake ni wakisomewa aya za Qur'an ambazo zinawahadharisha na maasi na kuwaonya kwa ufufuo na malipo, husema ni ngano za watu wa kale.

Aya Ya 14

Ni kupinga yale waliyoyasema wenye kukadhibisha kuwa ni ngano za watu wa kale. Anasema Raghib: Rana ni kitu inayokuwa juu ya kitu safi. Mwenyezi Mungu anasema: "Bali yametia kutu juu ya nyoyo zao" yaani hilo limekuwa kama kutu juu ya usafi wa moyo, wakapofuka kujua kheri na shari. Kuwa waliyokuwa wakiyachuma ni kutu juu ya nyoyo zao nikuwa dhambi ni kizuwizi cha kuipata haki kama ilivyo. Katika aya yanadhiri mambo yafuatayo:

Kwanza : Kwamba amali mbaya zina nakshi na picha.

Pili : Kwamba nakshi hizo na picha hizo zinazuiya nafsi kuipata haki kama ilivyo na kuiwekea kizuwizi. Tatu: Kwamba tabia ya mwanzo ya nafsi ni usafi unaotambua haki kama ilivyo na kuipambanua na batili na kupambanua kati ya twaa na maasia Mwenyezi Muungu amesema: "Na (kwa) nafsi na aliyelingamanisha akaifahamisha maasia yake na twaa yake ".(91:7-8).

Aya Ya 15

Ni kukataza kuchuma madhambi yenye kuweka kizuwizi kati ya moyo na kuipata haki. Makusudio ya kuwa wao ni wenye kuzuiliwa na Mola wao siku ya Kiyama, ni kizuiliwa na utukufu wa ukaribu na cheo. Huenda makusudio ni yale aliyoyasema msemaji: "hakika makusudio, ni kuwa wao ni wenye kuzuiliwa na Rehema ya Mola wao". Ama kuondoka kizuizi kwa maana ya kuondoka sababu zenye kuwa kati yake Mwenyezi Mungu na viumbe vyake na maarifa yenye kutimia ya kumjua Mwenyezi Mungu, hilo linapatikana kwa kila mtu. Mwenyezi Mungu amesema: "..na watajua kwamba Allah ni haki iliyodhahiri ."(24:25).

Aya Ya 16

Yaani wataingia na kubaki ndani yake au watafukizwa joto lake kama walivyofasiri wengineo.

Aya Ya 17

Ni kuaibisha. Na mwenye kuyasema hayo ni mtunzaji wa moto au watu wa peponi.

Aya Ya 18-20

Illiyyin ni juu na inafungamana na daraja za juu na vyeo kama vile ambavyo kinyume chake ni Sijjin. Maana ya aya tatu hizi ni mfano wa maana ya aya tatu zilizotangulia ambazo zinakabiliana nazo (aya ya 7, 8 na 9).

Kwa hivyo maana ni kwamba yale ambayo yameandikwa kwa ajili ya watu wema na kuhukumuliwa kuwa ni malipo ya wema wao, yako katika Illiyyin. Ni lipi la kukujulisha nini Illiyyin? Ni jambo lenye kuandikwa na lenye kuandikwa na lenye kupitishwa kwa hukumu ya mkato iliyowazi bila ya uficho. Watu wana kauli nyingi kuhusu aya hizi kama ilivyo katika zile zilizotangulia, isipokuwa miongoni mwa kauli kususu Illiyyin ni kwamba hiyo ni mbingu ya saba chini ya arshi ambako kuna roho za waumini. Na imesemwa ni Sidratul-Muntaha ambako kunaishia amali. Imesemwa ni ubao wa zabarjadi ulioko chini ya arsh, wenye kutungikwa na wenye kuandikwa amali.

Aya Ya 21

Yenye kunasibu zaidi kutokana na maana ya aya zilizotangulia ni kuwa maana ya kushuhudia ni kuona na wenye kukurubishwa ni watu wa peponi, walio na daraja ya juu zaidi kuliko watu wema wote, kama yatakavyokuja maana ya aya ya 28.

Makusudio ya kuona ni kuoneshwa na Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu amesema mfano wa hayo kuhusu moto. "Si hivyo! Lau mngejua ujuzi wa yakini. (Msingejishughulisha na hayo). Hakika mtauona moto ". (102:56). Katika hilo inadhihiri kuwa wenye kukurubishwa ni watu ya yakini. Imesemwa kuwa kushuhudia ni kuhudhuria na wenye kukurubishwa ni Malaika. Makusudio yake ni kuhudhuria Malaika kwenye maandishi ya amali zao wanapoyapeleka kwa Mwenyezi Mungu. Imesemwa wenye kukurubishwa ni watu wema na Malaika wote. Kauli hizo mbili zina muweko wa kuwa makusudio ya kitabu ni maandishi ya amali. Lakini umekwisha elezwa udhaifu wake.

Utafiti Wa Hadith Katika Tafsiri ya Qummi katika Riwaya ya Abul-Jarud kutoka kwa Abu Jaffar(a.s) amesema: Iliteremshwa Sura ya Al-Mutwaffifin kwa Mtume(s.a.w.w) wakati alipofika Madina, wakati huo wakazi wa hapo walikuwa ni waovu zaidi ya watu wote kwa kipimo na wakawa wazuri. Katika Kafi kwa isnadi yake kutoka kwa Abu Hamza Ath-Thimali amesema: "Nimemsikia Abu Jaffar(a.s) , akisema: "Hakika Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametuumba katika watu walio juu zaidi wa Illiyyin. Akaumba nyoyo za wafuasi wetu katika lile tuliloumbiwa sisi isipokuwa viwiliwili vyao. Kwa hivyo nyoyo zao zinapondokea kwetu, kwa sababu zimeumbwa kutokana na lile tuliloumbiwa sisi, kisha akasoma aya hizi (18, 19, 20 na 21). Na ameumba nyoyo za maadui zetu kutoka katika Sijjin na akaziumba nyoyo za wafuasi wao kutokana na lile waliloumbiwa wao isipokuwa viwiliwili vyao, kwa hiyo nyoyo zao zinapondekea kwao kwa sababu zimeumbiwa lile waliloumbiwa wao;" kisha akasoma aya hizi (7, 8, 9, na 10).

Imepokewa hadith mfano wa hiyo katika Kafi kwa njia nyengine kutoka kwa Athimali naye kutoka kwa Abu Jaffar(a.s) .

Na amepokea mfano wake katika Ilalish-Sharaii kutoka kwa Zaid Ash-Shahham kutoka kwa Abu Abdillahi. Na Hadith - kama unavyoona - inatilia nguvu yale tuliyoyatanguliza kuyaeleza katika maana ya aya. Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu kusema kwake Mwenyezi Mungu: "Hakika maandishi ya watu waovu yamo katika Sijjin", anasema : yale aliyowaandikia Mwenyezi Mungu katika adhabu yamo katika Sijjin. Katika hiyohiyo Tafsiri ya Qummi katika riwaya ya Abul-Jarud kutoka kwa Abu Jaffar(a.s) amesema: "Sijjin ni ardhi ya saba na Illiyyin ni mbingu ya saba ".

Lau riwaya hiyo ni sahihi basi itakuwa pepo na moto ziko pande mbili ya juu na ya chini. Kwa hiyo iko haja ya kuangalia vizuri riwaya hiyo; kama vile kuhisabu kaburi kuwa ni bustani ya peponi au ni shimo la Jahannam, na kuhisabu jangwa la Barhut kuwa ni mahali pa Jahannam. Katika Durril Manthur ametoa Ibn Al-Mubarak kutoka kwa Said bin Al-Musayyib amesema: "Salman alikutana na Abdallah bin Salaam, akasema mmoja wao kumwambia mwenzake ukifa kabla yangu njoo uniambie aliyokufanyia Mola wako nami nikifa kabla yako nitakuja kukupa habari. Akasema Abdalla vipi itakuwa? Akasema ndio hakika roho za waumini zinakuwa katika Barzakh katika ardhi zinakwenda popote zinapotaka na za makafiri zitakuwa katika Sijjin, na Mwenyezi Mungu ndiye mjuzi zaidi."

Katika Usulul-Kafi kwa isnadi yake kutoka kwa Zurara naye kutoka kwa Abu Jaffar(a.s) amesema: "Hakuna mja yoyote ila katika moyo wake kuna doa jeupe, akifanya dhambi kutokea doa jeusi, akitubia huondoka huo weusi, akiendelea na dhambi, huzidi weusi mpaka unafunika weupe. Ukifunikwa weupe, mwenye moyo huo hawezi kurudi kwenye heri milele. Na hiyo ndiyo kauli yake Mwenyezi Mungu: "Si hivyo! Bali yametia kutu juu ya nyoyo zao waliyokuwa wakiyachuma".

Imepokewa hadith kwa maana haya katika Durril Manthur kutoka kwa maswahaba kadhaa, kutoka kwa Abu Huraira naye kutoka kwa Mtume(s.a.w.w) . Katika hiyo hiyo Durril Manthur kwa isnadi yake kutoka kwa Abdalla bin Muhammad Al-Hajjal kutoka kwa baadhi ya maswahaba zetu amesema: "Amesema Mtume(s.a.w.w) kumbushaneni, kutaneni na zungumzeni, kwani mazungumzo ni usafi wa moyo. Hakika nyoyo zinashika kutu kama unavyoshika kutu upanga na usafi wake ni mazungumzo.

Kutoka kwa Rawdhatul-Waidhiya amesema: "amesema Al-Baqir(a.s) : "Hakika kitu kinachoharibu moyo kama makosa. Hakika moyo unapofanya makosa basi huendelea kuwa nayo mpaka uyashinde." Amesema Mtume(s.a.w.w) : Hakika muumin akifanya dhambi kunakuwa na doa jeusi katika moyo wake akitubia na kutka msamaha hukwatuka, akizidi na dhambi nalo huzidi. Hiyo ndiyo kutu aliyoitaja Mwenyezi Mungu aliposema: "Si hivyo! Bali yametia kutu juu ya nyoyo zao waliyokuwa wakiyachuma ".

Aya 22-36

إِنَّ الْأَبْرَارَ لَفِي نَعِيمٍ ﴿٢٢﴾

22. Hakika watu wema watakuwa katika neema.

عَلَى الْأَرَائِكِ يَنظُرُونَ ﴿٢٣﴾

23. Wakiwa juu ya malili wanatazama.

تَعْرِفُ فِي وُجُوهِهِمْ نَضْرَةَ النَّعِيمِ ﴿٢٤﴾

24. Utaona katika nyuso zao kunyinyirika kwa neema.

يُسْقَوْنَ مِن رَّحِيقٍ مَّخْتُومٍ ﴿٢٥﴾

25. Watanyweshwa mvinyo wenye kufunikwa.

خِتَامُهُ مِسْكٌ وَفِي ذَٰلِكَ فَلْيَتَنَافَسِ الْمُتَنَافِسُونَ ﴿٢٦﴾

26. Mwisho wake (ni) miski na katika hayo nawashindane wenye kushindana.

وَمِزَاجُهُ مِن تَسْنِيمٍ ﴿٢٧﴾

27. Na cha kuchanganyia ni Tasnim.

عَيْنًا يَشْرَبُ بِهَا الْمُقَرَّبُونَ ﴿٢٨﴾

28. Chemchemi ambayo hunywewa na wenye kukurubishwa.

إِنَّ الَّذِينَ أَجْرَمُوا كَانُوا مِنَ الَّذِينَ آمَنُوا يَضْحَكُونَ ﴿٢٩﴾

29. Hakika wale ambao wamefanya makosa walikuwa wakiwacheka wale walioamini.

وَإِذَا مَرُّوا بِهِمْ يَتَغَامَزُونَ ﴿٣٠﴾

30. Na walipokuwa wakiwapitia wakikonyezana.

وَإِذَا انقَلَبُوا إِلَىٰ أَهْلِهِمُ انقَلَبُوا فَكِهِينَ ﴿٣١﴾

31. Na walipokuwa wakirudi kwa watu wao wakirudi huku wakiona raha.

وَإِذَا رَأَوْهُمْ قَالُوا إِنَّ هَـٰؤُلَاءِ لَضَالُّونَ ﴿٣٢﴾

32. Na walipokuwa wakiwaona wakisema: "Hakika hawa wamepotea!"

وَمَا أُرْسِلُوا عَلَيْهِمْ حَافِظِينَ ﴿٣٣﴾

33. Wala hawakupelekwa wao kuwatunza.

فَالْيَوْمَ الَّذِينَ آمَنُوا مِنَ الْكُفَّارِ يَضْحَكُونَ ﴿٣٤﴾

34. Basi leo wale ambao wameamini wanawacheka makafiri.

عَلَى الْأَرَائِكِ يَنظُرُونَ ﴿٣٥﴾

35. Wakiwa juu ya malili wanatazama.

هَلْ ثُوِّبَ الْكُفَّارُ مَا كَانُوا يَفْعَلُونَ ﴿٣٦﴾

36. Ja, makafiri wamelipwa kwa waliyokuwa wakiyafanya.

UBAINIFU

Ni ubainifu ulio na baadhi ya ufafanuzi wa utukufu wa cheo cha watu wema na ukubwa wa daraja yao mbele ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) na kwamba wao kwa kuwa walikuwa wakidharauliwa na makafiri na kuchekwa na wao watawacheka na kuangalia adhabu wayoipata.

Aya Ya 22

Neno Naim lina maana nyingi. Yaani hakika watu wema watakuwa katika neema nyingi zisizoweza kusifiwa.

Aya Ya 23

Malili ni viti vya enzi vya kifahari vyenye kupambwa. Kutaja kutazama tu; Bila ya kusema ni kutazama kitu gani, kunatilia nguvu kuwa ni kutazama mandari ya pepo yenye kufurahisha na neema zilizomo. Imesemwa kuwa makusudio ya kutazama hapa ni kutazama yale wanayolipwa makafiri.

Aya Ya 24

Hayo anaambiwa Mtume(s.a.w.w) . Na hukumu ni yenye kuenea kwa wote; kwa maana kila mwenye kuangalia kwenye nyuso zao ataona kwenye nyuso zao kupendeza, kwa neema waliyonayo.

Aya Ya 25

Ni mahali pake kusifiwa kwa sifa ya kufungwa kwa vizibo, kwa sababu huzibwa kitu kisafi ili kisalimike na hadaa yoyote na kuchanganyika na kitu kitakachokiharibu.

Aya Ya 26

Imesemwa maana yake ni kufungwa kwake miski badala ya udongo. Na imesemwa maana yake ni kuwa mwisho wa ladha anayoipata mnywaji ni harufu ya miski. Kuhusu kauli yake "nawashindane wenye kushindana" ni kuvutiwa kuyapata yale yaliyosifiwa katika mvinyo wenye kufungwa. Neno "Na katika hayo" ni kusisitiza kuvutia kwa kuihusisha hukumu baada ya kuieneza. Maana yake: Nawashindane wenye kushindana katika neema ya pepo na katika mvinyo wenye kufunikwa ni watu mahsusi ambao watakunywa.

Aya Ya 27

Tasnim kutokana na inavyofasiriwa na aya inayofuatia ni mto katika pepo ambao Mwenyezi Mungu ameuita Tasnim. Temko Tasnim lina maana ya kunyanyua na kujaza.

Aya Ya 28

Aya hii inafahamisha kuwa wenye kukurubishwa watakunywa Tasnim bila ya kuchanganywa. Hayo yanafahamisha haya yafuatayo:

Kwanza : Kwamba Tasnim ni bora kuliko mvinyo wenye kufungwa ambao unazidi tamu kwa kuchanganywa na Tasnim.

Pili : Kwamba wenye kukurubishwa wana daraja ya juu zaidi kuliko wema waliotajwa katika aya (mbali mbali).

Aya Ya 29

Mpangilio unaeleza kuwa makusudio ya wale ambao wameamini ni wale watu wema wenye kusifiwa katika aya, wametajwa wale ambao wameamini kwa sababu imani yao ndiyo sababu ya kuchekwa na kudharauliwa na makafiri na wametajwa makafiri kwa sifa ya wale ambao wamefanya makosa, kwa kuwa huko kuwacheka wale walioamini ni katika makosa.

Aya Ya 30

Yaani wanakonyeza kwa kuonyesha dharau.

Aya Ya 31

Neno Fakihu lina maana ya furaha iliyozidi kiasi yaani baada ya kuwacheka wenye kuamini wanarudi hali ya kuona raha na kufurahi kwa waliyoyafanya. Au linatokana na Fakaha lenye maana ya mazungumzo ya kupumbaza, kwa maana ya kuwa wakirudi kwa jamaa zao wanazungumzia waliyoyafanya hali ya kupumbazika.

Aya Ya 32

Wanawaona wamepotea kwa njia ya kuona au kuwahukumia tu! Kuwa wamepotea.

Aya Ya 33

Yaani hawakupeleka hao makafiri kuwa wawachunge waumini, na kuwahukumia katika haki yao kwa wanavyotaka wao. Aya hii ni kuwaumbua wenye kuwafedhehesha waumini.

Aya Ya 34

Makusudio ya keo, ni siku ya malipo. Na wale ambao wamefanya makosa kuwaita makafiri ni kurudia hakika ya sifa yao.

Aya Ya 35-36

Neno thawabu kwa asili lina maana ya malipo ijapokuwa linatumiwa zaidi katika kheri. Kwa ujumla maana ya aya ni wake ambao wameamini watakuwa katika vyandarua wakiangalia malipo ya makafiri malipo ya matendo yao waliyokuwa wakiwafanyia katika dunia kama kuwacheka kukonyezana wanapowapitia na kurudi kwa jamaa zao hali yakufurahi baada ya kuyafanya hayo na kusema kwao "Hakika hawa ni wenye kupotea".

Utafiti Wa Hadith Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu kusema kwake Mwenyezi Mungu "Na katika hayo na washindane wenye kushindana" amesema: Ni katika tuliyoyataja miongoni mwa thawabu anazozitafuta Muumin. Katika Majmau kuhusu kusema kwake Mwenyezi Mungu (s.w.t) "Na walipokuwa wakiwapitia wakikonyezana." Imesemwa imeshuka kwa Ali bin Abutwalib(a.s) na kundi la waislamu waliokuwa wakielekea kwa Mtume(s.a.w.w) wakadharauliwa na wanafiki, wakawacheka, na wakakonyezana; kisha wakarudi kwa watu wao wakaambia tumemwona kipara tukamcheka; Ndio ikashuka aya hiyo kabla ya kufika Ali(a.s) na wenzake kwa Mtume(s.a.w.w) . Hadithi hiyo imepokewa kutoka kwa Muqatil na Kalbi.

Imepokewa hadithi hiyo katika Kash shaf. Katika hiyo hiyo Kash shaf ametaja Al-Hakim Abul-Qassim Al-Hasakani katika kitabu Shawahidu tanzil kutoka kwa Abu Swaleh naye kutoka kwa Ibn Abbas amesema: "Hakika wale ambao wamefanya makosa ni wanafiki wa Kiquraish na wale 'ambao wameamini' ni Ali bin Abu-Twalib na wenzake."

6

TAFSIRI YA QURANI AL-MIIZAAN

SURA TAKWIR (KUKUNJA) (NA. 81)

INA AYA 29.

Aya 1 - 14

Kwa jina la Allah, Mwingi wa Rehema, Mwenye kurehemu

إِذَا الشَّمْسُ كُوِّرَتْ ﴿١﴾

1. Jua litakapokunjwakunjwa.

وَإِذَا النُّجُومُ انكَدَرَتْ ﴿٢﴾

2. Na nyota zitakapoanguka.

وَإِذَا الْجِبَالُ سُيِّرَتْ ﴿٣﴾

3. Na majabali yatakapoendeshwa.

وَإِذَا الْعِشَارُ عُطِّلَتْ ﴿٤﴾

4. Na ngamia wenye mimba watakapotupiliwa mbali.

وَإِذَا الْوُحُوشُ حُشِرَتْ ﴿٥﴾

5. Na wanyama wa mwitu watakapokusanywa.

وَإِذَا الْبِحَارُ سُجِّرَتْ ﴿٦﴾

6. Na bahari zitapowashwa moto.

وَإِذَا النُّفُوسُ زُوِّجَتْ ﴿٧﴾

7. Na nafsi zitakapokutanishwa.

وَإِذَا الْمَوْءُودَةُ سُئِلَتْ ﴿٨﴾

8. Na kijana mwanamke aliyezikwa angali hai atakapoulizwa.

بِأَيِّ ذَنبٍ قُتِلَتْ ﴿٩﴾

9. Kwa makosa gani aliuawa?

وَإِذَا الصُّحُفُ نُشِرَتْ ﴿١٠﴾

10. Na madaftari yatakapofuniliwa.

وَإِذَا السَّمَاءُ كُشِطَتْ ﴿١١﴾

11. Na mbingu zitakapoondolewa mahali pake.

وَإِذَا الْجَحِيمُ سُعِّرَتْ ﴿١٢﴾

12. Na moto utapokokwa.

وَإِذَا الْجَنَّةُ أُزْلِفَتْ ﴿١٣﴾

13. Na pepo itakaposogezwa.

عَلِمَتْ نَفْسٌ مَّا أَحْضَرَتْ ﴿١٤﴾

14. Itajua nafsi ilichokihudhurisha.

UBAINIFU

Sura inataja siku ya Kiyama, kwa kutaja baadhi alama zake na matukio yake. Inaisifu siku hiyo kwamba yatafunuka ndani ya siku hiyo yale aliyoyafanya mwanadamu. Kisha inaisifu Qur'an kwamba aliyeileta kwa Mtume ni mjumbe wa mbingu ambaye ni Malaika wa wahyi na sio shetani, wala Mtume sio mwenda wazimu aliyepagawa na mashetani. Sura hii inakubaliana kwa mpangilio wake kuwa ni katika Sura za mwanzo. Hili linaungwa mkono na maelezo yaliyomo ndani yake yanayohusu kumtakasa Mtume(s.a.w.w) na visingizio vya kuwa ni mkichaa; ambavyo makafiri walimsingizia mwanzo wa utume wake. Vile vile Sura Al Qalam ambayo ni katika Sura za mwanzo nayo ina maelezo ya kumtakasa Mtume(s.a.w.w) . Sura imeshuka Makka bila ya ubishi.

Aya Ya 1

Maana ya neno Takwir ni kukunja kwa kuzungusha; kama kukunja kilemba juu ya kichwa. Huenda makusudio ya kukunjwa jua ni kuwa giza umbo lake kwa mzunguko.

Aya Ya 2

Neno Inkadarat lina maana ya kuanguka kutoka hewani mpaka kwenye ardhi. Huenda ikawa ni kwa maana ya kugeuka, ikawa makusudio ni kuondoka mwanga wake.

Aya Ya 3

Yaani yataendeshwa kutokana na mtingishiko wa Kiyama yawe kama vumbi lenye kupeperushwa.

Aya Ya 4

Imesemwa kuwa neno Ishar wingi wake ni ushara naye ni ngamia mwenye mimba ya miezi kumi, huitwa hivyo mpaka azae, huenda akaitwa hivyo hata baada ya kuzaa. Na ngamia ndiyo mali yenye thamani zaidi kwa waarabu. Kana kwamba ni ishara ya fumbo kwamba mali yenye thamani ambayo wanaishindania watu itabakia bila ya mtu wa kuimiliki na kuitumia, kwa sababu watu watakuwa wanajishughulisha na kuokoa nafsi zao tu; kama alivyosema Mwenyezi Mungu: "Kila mtu katika wao siku hiyo atakuwa na jambo la kumshughulisha ". (8:37).

Aya Ya 5

Dhahir ya aya kulingana na mpangilio wa aya za kukisifu Kiyama ni kwamba hata wanyama mwitu pia watakusanywa kama watu. Hayo yanatiliwa nguvu na kusema kwake Mwenyezi Mungu: "Na hakuna mnyama katika ardhi wala ndege arukaye kwa mbawa zake mbili ila ni umati kama nyinyi. Hatukupuuza kitabuni (mwetu) kitu chochote kisha watakusanywa kwa Mola wao ". (6:38).

Ama hali yao baada ya kukusanywa haikuelezwa katika maneno yake Mwenyezi Mungu wala yale yanayotegemewa katika hadith. Ndiyo kusema kwake Mwenyezi Mungu katika Sura (6:38). ni umati kama nyinyi na kusema kwake "Hatukupuuza kitabuni kitu chochote" huenda hayo yakafafanua hali yao kwa mwenye huzingatia na kuangalia kwa makini. Pengine husemwa, kukusanywa wanyama ni katika alama za Kiyama na si katika matukio ya Kiyama. Hivyo itakuwa maana ya kukusanywa wanyama; ni kule kutolewa kutoka mwituni na mapangoni mwao.

Aya Ya 6

Imefasiriwa Sujjirat kwa kuwako moto na imefasiriwa kwa kujaa.

Aya Ya 7

Nafsi njema zitakutanishwa na wanawake wa peponi Mwenyezi Mungu anasema: "Humo watakuwa na wake waliotakaswa ". (4:57).

Amesema tena: "Na tutawaoza Mahurilaini " (44:54).

Ama nafsi za waovu zitakutanishwa na mashetani, Mwenyezi Mungu anasema: "Wakusanyeni wale waliodhulumu (nafsi zao) pamoja na wenziwao na wale waliokuwa wakiwaabudu ." (37:22).

Na amesema: "Na mwenye kuyafanyia upofu maneno ya mwingi wa rehema tunamwekea shetani kuwa rafiki yake " (43:36).

Aya Ya 8

Waarabu walikuwa wakiwazika wazima watoto wa kike kwa kuogopa aibu; kama kunavyoonyesha kusema kwake Mwenyezi Mungu: "Anapopewa habari mmoja wao ya (kuzaliwa) mtoto wa kike husawijika uso wake akajaa sikitiko". Anajificha na watu kwa sababu ya habari mbaya ile aliyoambiwa! (Anafanya shauri) Je, akae naye juu ya fedheha hiyo au amfukie udongoni? " (16:58 - 59).

Mwenye kuulizwa kwa hakika ni baba yake aliyemzika nzima ili asiaibishwe, lakini amehisabiwa kuwa mwenye kuulizwa ni kijana mwanamke kwa namna ya kuaibishwa na kufedheheshwa huyo muuaji na kumsahilishia huyo kijana wa kike kumuomba Mwenyezi Mungu amwadhibu muuaji wake. Maneno yako katika mfano wa kusema kwake Mwenyezi Mungu kuhusu Isa(a.s) :

"Na (kumbuka) Allah atakapo sema: "Ewe Isa bin Maryam! Je, wewe uliwaambia watu 'Nifanyeni mimi na mama yangu kuwa waungu badala ya Allah ? " (4:116).

Imesemwa kuwa kutegemeza kuuliza kwa kijana wa kike ni kwa njia ya fumbo. Makusudio yake ni kuuliziwa, mfano wa kauli yake Mwenyezi Mungu: "Kwa hakika ahadi itaulizwa ". (17:34)

Aya Ya 10

Yaani yatafunuliwa kwa ajili ya hisabu. Ama watu wa peponi watakutanishwa na wanawake wema. Ama watu wa motoni kila mtu atakuwa na shetani; yaani nafsi za makafiri na wanafiki zitakutanishwa na mashetani ndio marafiki zao". Katika Durril Manthur ametoa Ibn Abu Maryam, Addiylamiy kutoka kwa Abu Maryam kwamba Mtume(s.a.w.w) amesema kuhusu kauli yake "Jua litakapokunjwa kunjwa ", amesema: "Litakunjwa katika Jahanam ".

Aya Ya 11

Maana ya neno Kushitwat ni kubanduliwa. Kisha Mwenyezi Mungu ataikunja; kama ilivyo katika kauli yake Mwenyezi Mungu: "Na mbingu zitakunjwa kwa uweza wake" (39:67) Na siku itakapopasuka mbingu zilete chungu ya mawingu " (25:25).

Aya Ya 12

Yaani utakokwa mpaka uzidi kuwa mkali.

Aya Ya 13

Makusudio ya kusogezwa ni kwa ajili ya kuingia watu wake.

Aya Ya 14

Makusudio ya nafsi ni jinsi ya nafsi yoyote. Na makusudio ya ilichokihudhirisha ni amali yake iliyoifanya. Aya iko katika maana ya aya inayosema: "Siku ambayo kila nafsi itakuta mema iliyoyafanya yamehudhurishwa na pia ubaya ilioufanya ." (3:30).

Aya Ya 15-29

فَلَا أُقْسِمُ بِالْخُنَّسِ ﴿١٥﴾

15. Naapa kwa nyota zirudizo nyuma.

الْجَوَارِ الْكُنَّسِ ﴿١٦﴾

16. Ziendazo na kujificha.

وَاللَّيْلِ إِذَا عَسْعَسَ ﴿١٧﴾

17. Na kwa usiku unapotoka.

وَالصُّبْحِ إِذَا تَنَفَّسَ ﴿١٨﴾

18. Na asubuhi inapotoa mwanga.

إِنَّهُ لَقَوْلُ رَسُولٍ كَرِيمٍ ﴿١٩﴾

19. Hakika hiyo (Qur'an) ni kauli ya Mjumbe Mtukufu.

ذِي قُوَّةٍ عِندَ ذِي الْعَرْشِ مَكِينٍ ﴿٢٠﴾

20.Mwenye nguvu, Mwenye daraja mbele za Mwenye ufalme.

مُّطَاعٍ ثَمَّ أَمِينٍ ﴿٢١﴾

21 Mwenye kutiiwa huko, Mwaminifu.

وَمَا صَاحِبُكُم بِمَجْنُونٍ ﴿٢٢﴾

22. Wala mwenzenu si mwendawazimu.

وَلَقَدْ رَآهُ بِالْأُفُقِ الْمُبِينِ ﴿٢٣﴾

23. Na hakika alimwona pambizoni mwa mbingu mlimo wazi.

وَمَا هُوَ عَلَى الْغَيْبِ بِضَنِينٍ ﴿٢٤﴾

24. Wala yeye kwa jambo la ghaibu si mwenye kutuhumiwa,

وَمَا هُوَ بِقَوْلِ شَيْطَانٍ رَّجِيمٍ ﴿٢٥﴾

25. Wala (Qur'an) si kauli ya shetani aliyefukuzwa.

فَأَيْنَ تَذْهَبُونَ ﴿٢٦﴾

26. Basi mnakwenda wapi?

إِنْ هُوَ إِلَّا ذِكْرٌ لِّلْعَالَمِينَ ﴿٢٧﴾

27. Hi (Qur'an) siyo ila ni waadhi kwa walimwengu.

لِمَن شَاءَ مِنكُمْ أَن يَسْتَقِيمَ ﴿٢٨﴾

28. Kwa anayetaka kunyooka katika nyingi.

وَمَا تَشَاءُونَ إِلَّا أَن يَشَاءَ اللَّـهُ رَبُّ الْعَالَمِينَ ﴿٢٩﴾

29. Wala hamtataka ila kwa matakwa ya Allah Mola wa viumbe.

UBAINIFU

Niutakaso kwa Mtume(s.a.w.w) kwa wazimu na kwamba Qur'an inayomjia Mtume haina mwingiliano wowote na shetani. Na hiyo Qur'an ni maneno ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) tu anayoletewa Mtume na Malaika wa wahyi ambaye hafanyi hiyana katika ujumbe wake. Na kwamba hiyo Qur'an ni waadhi kwa walimwengu, yenye kuongoza kwa idhini ya Mwenyezi Mungu kwa anayetaka kuongoka katika nyinyi.

Maana yake ninaapa hakika Mtume alimwona Jibril akiwa pambizoni mlimo wazi, ambayo ni sehemu ya juu kabisa kuliko sehemu zote zinazonasibiana na ulimwengu wa Malaika. Imesemwa kuwa maana yake ni hakika Mtume alimwona Jibril na sura yake ya asili wakati wa kuchimbuka jua akiwa yuko sehemu ya juu kabisa upande wa Mashariki. Hakuna dalili inayofahamisha hayo hasa kufungamana kuona kwa sura yake ya asili au kumwona kwa mfano wowote. Ni kama vile zimechukuliwa baadhi ya riwaya kwamba alimuona mwanzo wa Biitha na yeye yuko kati ya mbingu na ardhi amekaa juu ya kiti. Hayo yamechukuliwa kwa kufananisha.

Aya Ya 15 - 16

Aya mbili zinazofuatia hizi zinatilia nguvu kuwa makusudio ya nyota zirudizo nyuma, ziendazo na kujificha, ni nyota zote au baadhi yake. Lakini sifa za baadhi ya nyota zinanasibiana zaidi na sifa zilizoapiwa ambazo ni kurudi nyuma na kwenda kwa kujificha. Nazo ni sayari tano Zohal (Saturn), Mushtara (Jupitar), Mirikh (Mars), Zuhura (Venus) na Zebaki (Mercury). Kwani hizo zina sifa ya kwenda na kurudi na kujificha katika maficho yake kama wanyama wa porini. Imesemwa kuwa makusudio yake ni nyota yoyote. Ama kurudi nyuma ni kule kujificha mchana chini ya mwanga wa jua. Kwenda kwake ni kwenda kunakoonekana usiku na kujificha kwake ni kutua upande wa magharibi yake. Imesemwa kuwa makusudio yake ni Nyati na Paa. Sio mbali kuwa kutaja nyati au paa ni kwa upande wa mithali tu. Na kwamba makusudio ni mnyama wowote wa mwituni. Kwa vyovyote ilivyo, kauli ya kwanza iko karibu zaidi, ya pili iko mbali na ya tatu iko mbali zaidi.

Aya Ya 17

Inaungana na aya mbili zilizotangulia. Neno As'as huja kwa maana ya kuingia usiku na kutoka usiku. Raghib anasema; Ni mwanzo wa usiku na mwisho. Kwa hiyo As'as ni giza jembamba. Yanayosibiana zaidi na jumla na aya inayofuatia ni kuwa makusudio yake ni kutoka kwa usiku. Imesemwa makusudio yake ni kuingia, lalini kauli hii iko mbali.

Aya Ya 18

Inaungana na aya iliyotangulia limetumiwa neno kupumua kwa maana ya kutoa mwanga, kwa sababu asubuhi unakunjuka mwanga wake kwenye anga na giza lililoufunukia linaondoka. Ametaja Zamakhshari njia nyengine katika Kash-Shaf: ukisema nini maana ya kupumua asubuhi? Nitasema: "Ikija asubuhi huja upepo wa asubuhi kwa hiyo umejaaliwa juo upepo ndio pumzi zake". Kauli ya kwanza ndiyo iliyokaribu zaidi.

Aya Ya 19 -21

Ni jawabu la kiapo dhamiri ni ya Qur'an au ni ya yaliyotangulia katika Sura hii kwa maana ya kuwa ni Qur'an. Makusudio ya mjumbe hapa ni Jibril, kama alivyosema Mwenyezi Mungu: "Sema: Anayemfanyia ushinde Jibril hakika yeye ameiteremsha Qur'an moyoni mwako kwa idhini ya Allah (2:97). Kulitegemeza neno kwake kama mjumbe ni dalili kwamba neno ni la Mwenyezi Mungu. Amemsifu Mwenyezi Mungu Jibril kwa sifa sita: Mjumbe: Inafahamisha ujumbe wake na kuleta kwake wahyi wa Qur'an kwa Mtume(s.a.w.w) . Mtukufu: Yaani mwenye utukufu na cheo. Mwenye Nguvu: Yaani mwenye uwezo wa kutekeleza.

Mwenye Daraja mbele ya Mwenyezi Mungu : Yaani mwenye nafasi ya ukaribu mbele za Mwenyezi Mungu. Mwenye kutiiwa huko: Yaani mbele ya

Aya Ya 22

Inaungana na aya ya 19, kupinga kumsingizia kwao wazimu. Kuleta ibara ya "mwenzenu" ni kukadhibisha masingizio yao. Kwa kuonyesha kuwa huyo ni mwenzenu amekaa nanyi akatangamana nanyi kwa muda mrefu, nanyi mnajua zaidi mlivyomkuta na ukamilifu wa akili, rai ya sawa na ukweli wa maneno. Mwenye sifa hizi haambiwi kuwa ni mwenda wazimu. Kumsifu Jibril kwa sifa zilizopita bila ya kumsifu Mtume(s.a.w.w) sio dalili ya ubora wa Jibril kuliko Mtume. Kwa sababu maneno yanakusudia kubainisha kuwa Qur'an ni maneno ya Mwenyezi Mungu yaliyoteremshwa kwa Mtume kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya wahyi sio kwa njia ya fikra za kiwenda wazimu kutoka kwa shetani. Yaani makusudio yake ni kubainisha kusalimika njia ya kushuka na kumtukuza yule anayeiteremsha kwa kutaja sifa zake tukufu na kuzidi kumtakasa na makosa na hiyana. Ama yule mwenye kuteremshiwa hakuna haja ya kutaja sifa nyingi zaidi ya zile wanazomtilia shaka.

Ni miongoni mwa maneno yake Mwenyezi Mungu (s.w.t) kumsifu Mtume(s.a.w.w) hata kwa yale asiyotiliwa shaka katika ubora wake kuliko Malaika wote. Na Mwenyezi Mungu aliwafanya Malaika wote wamsujudie Mtume ambaye ndile Khalifa wake katika ardhi.

Mwenyezi Mungu kuna Malaika anawaamrisha na wanamtii, hapa inaonyesha kuwa ana msaada wa Malaika anaowaamrisha. Muaminifu: Yaani hafanyi hiyana kwa yale anayoamrishwa. Imesemwa Rasul ni kwa maana ya Mtume(s.a.w.w) , lakini kama unavyoona hayo hayaafikiani na aya inayofuatia.

Aya Ya 23

Dhamira ya mwenye kuona inamrudia "mwenzenu" yaani Mtume na mwenye kuonwa ni Jibril. Kwa dhahir pambizoni mlimo wazi ni kama vile ilivyoonyesha aya inayosema: "Na yeye yuko pambizoni juu kabisa " (53:7).

Aya Ya 24

Dhamiri inamrudia Mtume. Jambo la ghaibu ni Wahyi kutofanya ubakhili yaani haufichi huo wahyi wala haubadilishi baadhi yake au wote. Anawafundisha watu kama alivyofundishwa na Mwenyezi Mungu na anawafikishia yale aliyoamrishwa kuyafikisha.

Aya Ya 25

Ni kanusha la kuitegemeza Qur'an na shetani. Shetani ni kwa maana ya yule aliye mwovu aliyefukuzwa, kama vile anavyoitwa na Mwenyezi Mungu Iblis na kizazi chake. Vile vile anaitwa hivyo majini wengine waovu. Mwenyezi Mungu anasema: "Allah akasema: "Basi toka humo kwani umebaidishwa na rehema ." (38:77).

Anasema tena: "Na tumezilinda na kila shetani aliyefukuzwa ." (15:17). Maana yake nikuwa Qur'an siyo ushawishi wa shetani na askari wake wala sio kupagawa na majini waovu kama wanavyopagawa wenda wazimu.

Aya Ya 26

Ameweka wazi Mwenyezi Mungu katika aya ya saba zilizotangulia uhaki wa Qur'an hali ya kuikinga na mashaka wanavyomsingizia aliyekuja nayo kuwa ni mwenda wazimu.

Pili : Kwamba imeteremshwa na malaika wa mbinguni, mwenye cheo kikubwa ambaye ni mwaminifu wa wahyi naye ni Jibril asiyekuwa na kizuwizi chochote kati yake na Mwenyezi Mungu wala kati yake na Mtume.Tatu : kwamba aliyeteremshiwa ni mwenzenu ambaye hali yake haikujificha kwenu, sio mwenda wazimu kama wanavyomzulia. Hakika alimwona malaika mwenye kuchukua huyo wahyi na akauchukua kwake wala si mwenye kuficha aliyopewa wahyi wala kugeuza.

Nne : Kwamba sio ushawishi na kiibilisi na askari zake wala sio kupatwa na shari za majini. Natija ya ubainifu huu ni kwamba Qur'an ni kitabu cha uongofu, anaweza kuongoka nacho mwenye kutaka kwa kuongoka kwenye haki. Ndio kusema kwake Mwenyezi Mungu "Hii (Qur'an) siyo ila waadhi kwa walimwengu." Kusema kwake "Basi mnakwenda wapi?" ni kianzio cha kutaja natija ya ubainifu huo, swali katika aya hii ni la kutahayariza; maana yake ikiwa ni hivi basi mnakwenda wapi, mnaiacha haki yenu nyuma yenu?

Aya Ya 27

Yaani ni waadhi kwa watu, katika wale wanaoweza kuiona haki.

Aya Ya 28

Ni ubainifu kuwa sharti ya kunufaika na waadhi huo ni kutaka kunyooka juu ya haki nako ni kuwa na uthabiti wa utii.

Aya Ya 29

Yameelezwa zaidi maana yake katika aya zilizotangulia zenye kufanana na hii. Aya hii kwa unavyofahamisha mpangilio wa Sura hii ni kuwa iko katika maana ya kukinga uwezekano wa tuhuma kuwa kauli yake Mwenyezi Mungu "kwa anayetaka katika nyingi kunyooka" kwamba wana uhuru wa kutaka kunyooka. Wakitaka watanyooka, wasipotaka hawatanyooka; kwa hiyo Mwenyezi Mungu, kwa kutaka hao wanyooke, ana haja fulani kwao. Ndipo fikira hiyo ikaondolewa na aya hii, kwamba huko kutaka kwao kunyooka hakuwezekani ila tu anapopitisha Mwenyezi Mungu hilo. Hivyo ni kusema vitendo vya mwanadamu vile anavyoitaka, Mwenyezi Mungu pia amevitaka (vitokeo) kupitia kwa matakwa ya binadamu. Yaani ni Mwenyezi Mungu kumtakia mwanadamu afanye kadha wa kadha kwa mapenzi yake (mwanadamu) mwenyewe.

Utafiti Wa Hadith Katika Durril Manthur ametoa Said bin Mansur, Al-Fariyabi, Abdu bin Hamid, Ibn Jariyr, Ibn Hatim na Hakim na amesahihisha kutoka katika njia ya Ali, kuhusu kauli yake "Naapa kwa nyota zirudizo nyuma" amesema ni nyota zinazorudi usiku na kujificha mchana zikiwa hazionekani. Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu aya hiyo hiyo anasema: maana yake ni: Ni naapa kwa Al-Khunnas (jina la nyota) ziendazo kwa kujificha amesema: zinajificha mchana hazibainiki. Katika Majmau kuhusu "zirudizo nyuma"-amesema zinarudi nyuma mchana na zinadhihiri usiku. "Ziendazo" ni sifa yake kwa sababu zinatembea katika Falaki (njia yake). "Ziendazo kwa kujificha" ni katika sifa yake vile vile kwa sababu zinajificha katika ngome zake kama anavyojificha paa kwenye nyumba yake; nazo ni nyota tano Zohal, Mushtara, Mirikh, Zuhura na Zebaki. Hadith hiyo imepokewa kutoka kwa Ali. Kuhusu aya ya 17 inapoingia yaani linapoondoka giza lake. Kutoka kwa Ali.

Katika Tafsiri ya Qummi kuhusu aya ya 17 amesema ni kuingia giza na kuhusu aya ya 18 ni kuondoka giza. Katika Durril Manthur ametoa Ibn Asakir ktuoka kwa Muawiya bin Qurrat amesema: Anasema Mtume(s.a.w.w) kumwambia Jibril ni uzuri ulioje wa alivyokusifu Mola wako. Mwenye nguvu, mwenye daraja, mbele za mwenye ufalme. Mwenye kutiiwa huko, na muaminifu. Ni zipi hizo nguvu zako? Na ni upi huo uaminifu wako? Akasema Jibril: "Ama nguvu zangu ni wakati nilipopelekwa katika miji ya lut nayo ni minne. Katika kila mji kuna wapiganaji laki nne nikawanyanyua kutoka katika ardhi ya chini mpaka wakasikia watu wa mbingu sauti za kuku na kelele za mbwa, kisha nikawaporomosha, wakafa. Ama umanifu wangu sikuamrisha kitu chochote nikakipeleka kwa mwengine.

Riwaya hii haiwezi kupita hivihivi. Ameidhoofisha Ibn Askari. Katika Khiswal kutoka kwa Abu Abdillahi amesema: mwenye kusema katika kila siku ya Shabaan " Astaghfirullaha lladhiy laa ilaha huwa rrahmanurrahim. Al-hayyul qayyuum wa atubu ilayh" mara sabaini huandikwa katika pambizoni mwa mbingu mlimwowazi. Akasema nikauliza nini pambizoni mwa mbingu? Akasema ni sehemu katika Arsh yenye mito yenye kupita. Katika Tafsiri ya Qummi katika hadith aliyoitegemeza kwa Abu Abdillah kuhusu aya ya 25 amesema shetani mwenye kufukuzwa ni makuhani wa Maquraish yananasibishwa maneno yao na maneno ya mashetani.


6

7

8

9

10

11

12

13

14

15

16