MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE 14%

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE Mwandishi:
: SALMANI SHOU
Kundi: Misingi mikuu ya Dini

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE
  • Anza
  • Iliyopita
  • 28 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 30481 / Pakua: 4478
Kiwango Kiwango Kiwango
MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

Mwandishi:
Swahili

1

6

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

SOMO LA SITA

HAJA YA ULIMWENGU KUMHITAJI YULE ASIYEHITAJI CHOCHOTE

Kanuni ya usababisho ni ya kawaida na fani zote na msingi wa juhudi zote za mwanadamu, katika kutafuta elimu na katika shughuli zake za kawaida vilevile. Jitihada za wanazuoni kuvumbua sababu za kila jambo, ama liwe la kimaumbile au la kijamii, hutokana na imani kwamba hakuna kitu kinachojianzisha ndani yake, au chenyewe tu bila sababu na asili kuingilia kati.

Utafiti wa wanafikra duniani pote umewapa wao uwezo wa kufahamu vizuri zaidi mpangilio wenye nguvu sana wa maumbile; jinsi wanavyozidi kusonga mbele kwenye mkondo wa maarifa ndivyo wanavyozidi kujifunga kwenye kanuni ya usababisho. Kiungo baina ya sababu na athari, na kanuni kwamba hakuna kitu kitakachotokea chenyewe kwenye uwanja wa uwepo bila sababu, ni miongoni mwa maamuzi yenye nguvu sana ambayo yamepata kufanywa na mwanadamu na kuthaminiwa kama sharti la kimsingi kwa shughuli za kitaalamu. Yanawakilisha kitu ambacho ni kawaida na cha asili, kinachofyonzwa na akili zetu moja kwa moja bila kukwepa.

Hata mwanadamu aliyeishi kabla ya historia kuanza kuandikwa alielekea kugundua sababu za mambo, na kwa kweli, wanafalsafa waliipata dhana hai ya uhusiaino kati ya sababu na athari kutoka kwenye asili yenyewe na silika ya mwanadamu kabla ya kuiweka katika kalibu (chungu) ya kifalsafa. Kufungiwa kama tulivyo kwenye kuta nne mata, hatukabiliani kamwe na kitu chochote cha kutuka chenyewe kwenye uhai, na kwa kweli, hakuna hata mtu mmoja aliyewahi kamwe kukabiliana, katika historia ya ulimwengu, na kutuka kwa jambo ambalo halitokani na sababu. Kama hali isingekuwa hivyo, tungeweza labda kuwa kisingizio cha kuufikiria ulimwengu kuwa ni kitu cha kutuka chenyewe katika asili yake. Itakuwa ni aina gani ya kutuka kiajali ambako tangu mwanzo wa kuwepo kwa uhai hadi sasa, kumeongoza muingilano huo usiopimika wa vitu vyote, katika mfumo na mtindo wa kushangaza kiasi hicho? Je, inawezekana mpangilio huu tunaoufahamu ukawa ni kuakisi kwa jambo la kutuka na sadifa ya hivi hivi tu?

Kitu chochote kinachoweza kudhaniwa hapa ulimwenguni kilikuwa kimezamishwa kwenye giza la kutokuwepo kabla hakijapata umbile la kiumbe. Hakiwezi kupenya giza la kutokuwepo na kujitokeza kwenye uwanja wa uhai kama kitu kilichopo hadi mkono wa kisababisho wenye uwezo mkubwa uingie kazini.

Uhusianao baina ya chanzo na athari ni uhusiano baina ya vitu viwili vilivyopo, kwa maana kwamba kuwepo kwa kimoja chao kunategemea juu ya kuwepo kwa kile kingine. Kila athari ina uhusiano wa mvuto na uwiano na chanzo chake, kwa kuwa athari hupata kuwepo kwake kutoka kwenye chanzo. Uhusiano huu maalum hauwezi kuharibiwa au kubadilishwa na mwingine.

Wakati wowote unapofikiria asili ya kitu chenye uhusiano wenye kufanana kwa kiumbe hai na kisichokuwa hai, na vyote vikiwa hakuna ambacho ni muhimu kimsingi kwa ajili ya kitu hicho, kitu hicho huitwa 'dharura' kwa maana kwamba hakuna chochote katika asili yake kinachosababisha ama uhai au kutokuwa hai. Kama kitu katika asili yake kinahitaji kutokuwa hai kwake, basi kuwa hai kwake hakuwezekani. Hatimaye, endapo uhai utajitokeza kutoka ndani ya asili ya kitu kwa namna ambayo kwamba akili haiwezi kukiona kwamba ni tegemezi kwa kitu kingine chochote, uhai wa kitu hicho unafanywa kuwa muhimu. Ni kiumbe hai kinachojitegemea, kisichohitaji chochote na kinajikimu kwa njia za asili yake binafsi, kuwepo kwake ndicho chanzo cha viumbe vingine vyote ambapo chenyewe hakitawaliwi na haja au hali yoyote.

Inapaswa kuongezwa hapa kwamba kuwepo kwa maada hakuwezi kupata sifa ya "muhimu" kwa sababu kuwepo kwa kitu chochote cha mchanganyiko wa maada kunategemea kuwepo kwa sehemu zinazokiunda kitu hicho; kinakuwa ni tegemezi juu ya sehemu zake chenyewe kwa ajili ya chanzo na kuendelea kwa uhai wake. Mata ina mielekeo tofauti na ukubwa mbalimbali; yenyewe imetumbukizwa kwenye kiasi na kuongezeka, na inapata ukubwa wake mbali mbali kwa namna ya sifa na tabia. Kiumbe muhimu, kwa kinyume chake, hakihitajii tabia zote hizi.

Vitu vyote ambavyo wakati fulani havikuwepo halafu vikajakuwepo, wakati mmoja vilitawaliwa na dhana ya kufikirika ya uhai na kutokuwa hai. P ale vilipokimbilia kwenye hatua ya uhai, hii ilikuwa ni matokeo ya chanzo ambacho kilivilazimisha mwelekeo huo, kilikuwa ni kichocheo, kipengele cha nje ambacho kilivisukuma vyote kwenye mwelekeo mmoja badala ya ule mwingine. Kwa mneno mengine, kuwepo kwa chanzo ilikuwa ni wakala wa kiumbehai, kama vile kutokuwepo, au kukosekana sababu ni asili ya kutokuwepo kiumbe.

Kwa kawaida, kitu ambacho kinakuja kuwepo kama matokeo ya kuwepo kwa chanzo kamwe hakipotezi asili yake ya kuhitaji, wakati wote kitabia kiumbe chenye kuainishwa na kuhitaji. Kwa sababu hii, haja ya kitu juu ya kuwepo chanzo ni ya kudumu na isiyotanguka, uhusiano wake na chanzo hicho hautakatika japo mara moja. Endapo uhusiano huo ungekatishwa, uhai wa kitu hicho ungesalimu amri mara moja na kutokuwepo, kwa namna ile ile ambayo kwamba, mara jenereta ya umeme inapoacha kufanya kazi, taa zote angavu zilizounganishwa hapo hizimika. Ni kwa sababu hii kwamba chanzo na athari, uhuru kutokana kuhitaji na kutawaliwa na mahitaji ni hali ambazo zinahusiana wakati wote, endapo uhusiano huo ungekatizwa, kusingebakia chochote isipokuwa giza na kutokuwepo uhai.

Hivyo, hakuna jambo linaloweza kuonekana dhahiri hapa duniani mpaka uwezo maalum uwe umewekwa juu yake na kimoja ambacho asili yake iko huru kutokana na kuhitaji na chenyewe ndio chanzo haswa ambacho uhai hububujika kutoka humo. Kama uhai ungekuwa ni sehemu ya asili za vitu, kamwe usingefuata mkondo wa kukoma na kutoweka. Lakini ni ile tabia ya kuhitaji ndio tabia ya msingi kwenye asili zao, ili hata baada ya uhai wao kuanzishwa kwenye mpangilio wa viumbe, sifa yao ya kuhitaji huendelea kuwepo kwa hali yoyote ile. Haviko huru kamwe na kutohitaji chanzo; haiwezekani kwamba athari iweze kupata uhai kwa uhuru kabisa au iendelee kuwepo japo kwa nukta moja bila kutegemea juu ya chanzo. Kwa hiyo inakuwa dhahiri juu yetu kwamba vitu vyote - viumbe hai vyote vinavyoweza kutokea - vinapata wakati wote na kwa kila mara kutoka kwenye asili isiyo na ukomo ambayo ndio hugawa uhai - yaani, ile Nafsi Muhimu, ya Pekee na Muumbaji Muweza - ule uwezo na uhai unaoviruhusu kuwa hai na kubakia kuwepo hai.

Qur'anii Tukufu inasema:

يَا أَيُّهَا النَّاسُ أَنتُمُ الْفُقَرَاءُ إِلَى اللَّـهِ وَاللَّـهُ هُوَ الْغَنِيُّ الْحَمِيدُ ﴿١٥﴾

"Enyi watu! Nyinyi ndio wenye haja kwa Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu ndiye mwenye kujitosha, Msifiwa (Fatir:35:15).

Na tuzingatie pia wito huu wa Qur'ani:

أَمْ خُلِقُوا مِنْ غَيْرِ شَيْءٍ أَمْ هُمُ الْخَالِقُونَ ﴿٣٥﴾

"Au wao wameumbwa pasipo kutokana na kitu chochote, au ni wao ndio waumbaji?" ( Tur: 52:35).

أَمْ خَلَقُوا السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ بَل لَّا يُوقِنُونَ ﴿٣٦﴾

"Au wao wameziumba mbingu na ardhi? Bali hawana na yakini" (Tur: 52:36).

أَمْ لَهُمْ إِلَـٰهٌ غَيْرُ اللَّـهِ سُبْحَانَ اللَّـهِ عَمَّا يُشْرِكُونَ ﴿٤٣﴾

"Au wanae mungu mwingine asiyekuwa Mwenyezi Mungu? Subhanallah! Ametakasika Mwenyezi Mwenyezi Mungu na hao wanao washirikisha naye." (Tur: 52:43).

تَبَارَكَ الَّذِي بِيَدِهِ الْمُلْكُ وَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ ﴿١﴾

"Ametukuka ambaye mkononi mwake umo Ufalme wote; na Yeye ni Mwenye uweza juu ya kila kitu." (Almulku: 67:1).

Chanzo cha viumbe vyote chenyewe hakihitajii kuwa na Asili Wafuasi wa uyakinifu wanatoa uangalifu wa ukosoaji sana kwenye kanuni ya kwamba Mwenyezi Mungu hahitaji kuwa na Asili. Wao wanasema endapo tutadhani Muumbaji ndiye chimbuko la ulimwengu na ndiye anayeweka uhai juu yake, viumbe vyote vikipata vyanzo vyao na uhai wa kuendelea kutoka kwake, ni sababu gani imemuondolea yeye haja ya kuwa na muumbaji, ni kiwakilishi gani kilichosababisha yeye mpaka kuja kuwepo? Katika hotuba iliyotolewa kwenye jumuiya ya 'Londoni Atheist Sosiety,' mwandishi maarufu, Betrand Russell, alisema; "Siku moja, nilipokuwa na umri wa miaka kumi na nane, nilikuwa ninasoma wasifu wa John Stuart Mill. Sentenso moja mahsusi ilinivutia sana: Mill aliandika kwamba siku moja alimuuliza baba yake, ni nani aliyemleta yeye kwenye uhai duniani, na baba yake hakuweza kumjibu." Sababu yake ni kwamba papo hapo aliuliza swali la ni nani aliyesababisha Mwenyezi Mungu kuwepo?

Halafu Russell anaongeza: "Bado ninasadiki kwamba sentenso ile rahisi inadhihirisha ile ghiliba ya chanzo cha msingi. Kwani kama kila kitu lazima kiwe na sababu na chanzo, hali hiyo lazima itumike juu ya kuwepo kwa Mwenyezi Mungu. Kama, kinyume chake, kitu kinaweza kuwepo bila ya sababu au chanzo, kitu hicho inawezekana kiwe ama Mwenyezi Mungu au ulimwengu, na mjadala wote unakuwa hauna maana."[17] Kwa bahati mbaya, wanafalsafa fulani wa nchi za Magharibi ambao wanakubali kuwepo kwa Mwenyezi Mungu wameshindwa kufumbua tatizo hili. Mwana falsafa wa Uingereza Herbet Spencer amesema yafuatayo

kuhusiana na suala hili: Tatizo ni kwamba, kwa upande mmoja, akili ya binadamu hufuata sababu ya kila kitu na, kwa upande mwingine, hukataa fhana zote zisizo na mantiki (kwa vile ukweli wa dhana hizo hauwezi kuthibitishwa bila kurejea kwenye hitimisho). Haitambui wala kuelewa chanzo kisichosababishwa. Mchungaji anapomwambia mtoto kwamba Mwenyezi Mungu ameumba ulimwengu, mtoto huuliza nani aliyemuumba Mwenyezi Mungu?[18] Mahali pengine mwanafalsafa huyu anasema: "Myakinifu hujaribu kujisadikishia mwenyewe kuhusu dunia ambayo ipo na imetokana na yenyewe, milele bila ya kisababisho. Hata hivyo, hatuwezi kukiamini kitu ambacho hakina mwanzo wala asili. Mwanatheolojia huyo anayapeleka mambo haya hatua moja zaidi nyuma kwa kusema kwamba Mwenyezi Mungu aliuumba ulimwengu. Lakini mtoto anamuuliza swali lisilojibika: Nani aliyemuumba Mwenyezi Mungu?[19] .

Tunaweza kuleta hasa upinzani kama huo huo dhidi ya wayakinifu na kuwauliza, endapo tukifuata mlolongo wa usababishaji kinyumenyume, hatimaye tutafika penye chanzo cha msingi. Natuseme kwamba chanzo si Mwenyezi Mungu, bali ni mata. Sasa hebu tuambieni ni nani aliyeiumba mata ya msingi. Ninyi mnaoamini katika kanuni ya usababisho, tujibuni sisi swali hili. Kama mata ndio chanzo halisi cha vitu vyote, ni nini chanzo cha mata? Mnasema kwamba asili ya vitu vyote ni nguvu ya mata, ni nini sababu na asili ya nguvu ya mata? Kwa kuwa mlolongo wa usababisho hauwezi kurudi kwenye kutokuwa na ukomo, jibu pekee wanaloweza kutoa ni kwamba mata ni kitu kisicho na wakati na chenye umilele ambacho hakiwezi kuwekewa mwanzo: mata ni kitu kisichoumbwa, hakina mwanzo wala mwisho, kuwepo kwake hutukia ndani ya asili yake yenyewe.

Hii ina maana kwamba wayakinifu wanakiri kuwepo kwa kanuni ya umilele na kukosa chimbuko; wanaamini kwamba vitu vyote vilitukia kwenye maada ya milele na kwamba uhai unatukia kutoka ndani ya asili yenyewe hasa ya maada, bila ya haja yoyote ya muumbaji. Russell anelezea wazi imani hii kwenye hotuba iliyonukuliwa hapo juu. Yeye anasema; "Hakuna uthibitisho kwamba dunia ilipata kuwa na mwanzo kamwe. Hii fikira ya kwamba vitu lazima wakati fulani vilikuwa vina mwanzo inatokana na ufinyu wa fikra zetu."[20] .

Kwa namna ile ile ambayo Russell anafikiria mata kuwa ni ya milele, wanaomwamini Mwenyezi Mungu wanahusisha sifa ya umilele kwa Mwenyezi Mungu. Imani katika kitu chenye umilele kwa hiyo ni ya shirika, ya kawaida kwa wanafalsafa wa kiyakinifu na kidini. Makundi yote mawili yanaafiki kwamba kuna chanzo cha msingi, lakini wanaomwamini Mwenyezi Mungu wanakiachukulia chanzo cha msingi kama ni chenye hekima, ujuzi wote, na chenye kumiliki uwezo wa kuamua na utashi, ambapo kwa maoni ya wayakinifu, hicho chanzo cha msingi hakina busara wala akili, utambuzi ama uwezo wa maamuzi. Hivyo, kumwondoa Mwenyezi Mungu, kwa hali yoyote ile hakuleti ufumbuzi wa tatizo linaloletwa na suala la kiumbe cha milele.

Zaidi ya hayo, maada ni kituo cha mwendo na mabadiliko, na mwendo wake ni wenye nguvu na imewekwa ndani ya asili yake yenyewe. Sasa, mwendo muhimu hauendani na umilele, na mata na utulivu muhimu ni jinsi mbili ambazo zote ni za kipekee ambazo haziwezi kuunganishwa kwenye kituo kimoja. Chochote kile ambacho kimetulia na hakibadiliki katika asili yake hakiwezi kupokea mwendo na mabadiliko katika asili hiyo.

Ni vipi wenye fikira za ki-Marx, ambao wanaamini kwamba mata inaandamana na tamathali yake yenye dhana ya kutofautiana (tabaini), wanavyoweza kuthibitisha umilele wa maada? Umilele maana yake ni umadhubuti na kutobadilika kwa asili, kutowezekana kwa ukomo, lakini maada katika asili yake ni ufupisho makini wa nguvu na uwezekano; inawiana yenyewe, ikiwa imenasa kabisa katika kuishi na kufariki. Umilele hauendani na mtindo wa uhai uliomo kwenye mata na vipengele na sifa zilizolazimishwa na asili yake. Itikadi ya wale walio na imani juu ya Mwenyezi Mungu kuhusu kanuni isiyobadilika na ya dhahiri inahusika kwa kiumbe ambacho ndani, na, kwa asili yake kinaweza kukubali utulivu na kutobadilika; asili yake hainazo kabisa - na iko mbali nazo - sifa za maada. Asili yenyewe hasa ya maada inakataa kudumu, umilele na uendelevu, kwani kamwe haiwezi kujitenga yenyewe na mwendo, kuwiana na inakataa kuwa chanzo cha msingi au kisichobadilika.

Itakuwa na manufaa hapa kusimulia mazungumzo baina ya Imamu Sadiq(a.s) na mmoja wa wayakinifu wa wakati wake. Myakinifu: "Viumbe viliumbwa kutokana na nini? Imamu: "Havikuumbwa kutokana na kitu chochote (yaani kiasili havikuwa viumbe)." Myakinifu: "Sasa vinakua vipi na kujitokeza kutoka kwenye kutokuwa kiumbe?"

Imamu: "Je, sikusema kwamba vitu vyote duniani havikuumbwa kutokana na chochote? Maana yangu ni hii, kwamba viumbe vyote ki-asili havikuwa viumbe, na halafu vikaja kuwepo. Unataka kusema kwamba dunia ni ya milele, lakini fhana hii si sahihi kwa sababu zifuatazo:

"Kwanza, kama dunia hii ya maada ni ya milele, ina maana kwamba kitu chenye umilele lazima kipatwe na kubadilika na ukomo, jambo ambalo haliwezekani.

"Pili: endapo elementi zinazotengeneza dunia ni vya milele kwa sababu ya asili yao, inawezekanaje basi ziingie kwenye mkumbo wa kifo na kutoweka? Na kama, katika kinyume chake, zinakuwa hazina uhai katika asili zao, ni namna gani uhai unavyoweza kuchomoza kutoka ndani yao? Endapo utasema kwamba viumbe hai hutokana na elementi hai na viumbe visivyo hai hutokana na elementi zisizo hai, tunajibu kwamba asili isiyona uhai ndani mwake na utokanao ndani mwake haiwezi kuwa ya milele na haiwezi kuwa chanzo cha uhai." Myakinifu: "Kama maada iko kama vile usemavyo, kwa nini viumbe vinasemekana kuwa na umilele?" Imamu: "Imani katika umilele wa ulimwengu inashikiliwa na wale wanaokanusha kuwepo kwa mtawala na mpangaji wa maumbile, wanawakataa mitume wa Mwenyezi Mungu, wanafikiria vitabu wanavyokuja navyo wajumbe ni ngano za kale, na kubuni itikadi zinazowaridhisha wao wenyewe."[21] .

Sasa tunasema kwamba, kuwepo kwa kitu hakuwezekani bila ya chanzo cha kitu chenye upungufu, yaani, ambacho majaaliwa yake yamo mikononi mwa chanzo chake na ambacho kudumu kwake kunategemea kuwepo hai kwa chanzo chake. Hali hii haiwezi kutumika kwa kitu ambacho, kinafahamu uhalisi wake na hakioneshi dalili yoyote ya upungufu na ukomo.

Chanzo cha msingi ni chanzo msingi kwa sababu ya kuwa na uhai kamilifu na usiokuwa na kikomo; bila kutawaliwa na asili yoyote, kimeepukana na kuhitaji, mazingira na utegemezi, na hakina dalili ya kugeuka au kubadilika.

Tunapozungumzia kuhusu sababu ya mwanzo na wakati huo huo tunasema kwamba Mwenyezi Mungu ameepukana na haja yote ya kuwa na chanzo, hatuna maana ya kwamba Yeye kwa ujumla anashirikiana na viumbe vilivyoumbwa ile haja ya kuwa na chanzo lakini wakati fulani alikuwa, kama ilivyokuwa, aliondokana na kanuni ya usababisho. Mwenyezi Mungu sio athari kwamba ahitaji chanzo; Yeye si kiumbe kwamba ahitajie muumbaji. Kinyume chake, dalili zote na maajabu ya uhai vinatokana na Yeye, chanzo cha milele cha uhai. Kanuni ya usababisho hutumika kipekee kwenye mazingira ya vile vitu ambavyo kutokuwepo kwao kulitangulia - kabla ya kuwepo kwao.

Vivyo hivyo, maana ya sababu ya mwanzo si kwamba Mwenyezi Mungu alijibuni Mwenyewe, kwamba Yeye alikuwa ndio chanzo chake mwenyewe. Mahitaji ya athari kwa ajili ya chanzo yamo kwenye aina ya uhai ambao kile kilichotangulia kinao; kinakuwepo sio kwa sababu kina uhai kimsingi bali ni kama matokeo ya uhai utokanao na kitu kingine na ulio tegemezi kinaoupata kutoka kwenye chanzo. Lakini kiumbe ambacho asili yake haitawaliwi na hali yoyote na kinaonyesha kutokuwepo kabisa kwa utegemezi na uhusiano umeondolewa kabisa kutoka kwenye mazingira ambamo ile kanuni ya usababisho inafanya kazi.

Endapo kiumbe kwa sababu ya ukamilifu na kutokuhitaji kwa asili yake, kinakuwa hakihitaji chanzo, maana yake ni kwamba hakuna chanzo kilichokiweka katika kiwango maalumu cha uhai na kwamba hakuna sababu inayoweza kuingilia ndani yake. Mlolongo wa kisababisho hauwezi kurefushwa kurudi nyuma bila kikomo, na kukosekana kwa uhusiano ni kwa asili katika dhana yenyewe hasa ya chanzo cha awali. Swali kama: "Hicho chanzo cha awali kilijitokeza lini?" kwa hiyo, huwa halijitokezi; hivyo maswali kama haya hutumika tu juu ya vyanzo vya vitu na tabia zao za kutegemea.

Kuwepo kwa chanzo cha kwanza kunatambulika kwa dhati yake; kuwa kwake chanzo cha kwanza chenyewe, kwa hakika pia kunattmbulikana kwa dhati yake. Tabia zote hizi zinaashiria kujitosheleza, ambapo vitu ambavyo kuwepo kwao kumetokana na vitu vingine huwa vinahitaji chanzo, kwa sababu vinajulikana kwa tabia za kubadilik na kugeuka, kwa kuchipukia kutoka kwenye kutokuwepo na kuingia kwenye kuwepo. Inawezekanaje kudhaniwa kwamba imani katika kuwepo kwa Mwenyezi Mungu ni kukiri kuwepo kwa kuhitilafiana, ambapo imani juu ya asili isiyoanzishwa ya athari kama vile maada iwe haipingani?

Tunaishi kwenye dunia ambayo vitu vyote vimeachwa wazi kwenye kubadilika na kuharibika; ipo dalili ya kutokudumu, kutawaliwa na kufadhiliwa kulikochapwa kwenye kila chembechembe yake. Kuhitaji na kutegemeana kumeota mizizi imara katika uhai wetu na ule wa kila kitu kilichomo duniani na mbinguni. Uhai wetu sio wa kudumu na haukuzuka kutoka ndani ya asili yetu wenyewe; hatukuwa, na halafu tulifunikwa kwenye joho la kuwepo na tukaja kuwa hai. Ili kuweza kuja kwenye uhai, viumbe kama vile sisi lazima tuwe wenye kuomba sana kumfikia mwenye kutoa uhai.

Lakini Yeye Ambaye ni wa milele nawa kudumu, ambaye kuwepo kwake kunatokana ndani ya asili Yake Mwenyewe, na Ambaye kuonekana kwake kuko nje ya wakati, ni wazi kabisas hana haja ya chanzo. Maana ya chanzo katika falsafa ni kile kinacholeta athari kutoka kwenye kutokuwepo kitu hadi kuwepo kwake na kukifunika na vazi la uhai. Uumbaji huu hauwezi kutolewa hoja kwa ajili ya vyanzo vya kimaada, na jukumu moja tu la mata ni kuacha umbile moja ili kuweza kupokea umbo lingine.

Ni kweli kwamba kila kiumbe cha kimaada hupata tabia mpya na iliyo tofauti katika kila nukta kama matokeo ya maendeleo ya ndani kwa ndani. Hata hivyo, usogevu wa kimaumbile wa dunia na mifuatano ya uletaji na uchafuzi inadai mahitaji kudumu ya msaada kwa yule ambaye huumba mwendo, msaada ambao hulea msafara wa haraka wa uhai na kuusukuma kwenda mbele.

7

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

SOMO LA SABA

UKOMO WA NYORORO YA USABABISHO

Wayakinifu wanaweza kung'ang'ania kwa ukaidi kabisa katika kukanusha ukweli na kuleta hoja nyingine yenye kuonekana kama ni nzuri. Wanaweza wakasema, "Hatuikatishi nyororo ya usababisho lakini, kinyume chake tunaiendeleza isiwe na mwisho; tunatetea kanuni ya asili isiyo na ukomo ya kiungo sababishi."

Kama ni hivyo, wanapaswa kujibiwa kama ifuatavyo: Kuchambua dunia ya maumbile kwa namna hii kunasimama kwenye kufikiria juu ya nyororo ya visababisho na athari na mkunjuko wa kudumu wa mfuatano wa vyanzo usio na ukomo. Hata hivyo, kwa vile kila chanzo pia ni athari, kinakosa chenyewe kuwa kwenye asili yake; kinakuwa hakiwezi kuchukua sehemu ya uhai, mbali na chanzo bora zaidi na kilichokitangulia kabla.

Kwa hiyo, ni jinsi gani kila sehemu ya nyororo hiyo, ambayo imetawaliwa na tabia ya kuhitaji kutoka mwisho mmoja hadi mwingine, ilivyoibuka kutoka kwenye hali ya kutokuwa kiumbe? Kuwepo kwa kila sehemu ya nyororo hiyo huonyesha upungufu, kutokuwa na nguvu na chimbuko ndani ya muda uliowekwa, kuwepo kwake kulianza lini? Inawezekanaje vitu vikubwa na vyenye vijisehemu kuibuka kutoka viunganisho vya vitu visivyokuwepo? Je, uhai hububujika kutoka kwenye muungano wa vipengele vingi ambavyo husababisha kifo?

Hata kwa umbali kiasi gani nyororo hii isiyo na ukomo ingerefushwa, bado itakuwa na zile sifa za uhitaji, utegemezi na uibukaji kwa wakati. Nyororo kutoka kwenye ile asili hasa ambayo kwamba kujitawala na uhuru kutokana na kuhitaji hakujitokezi kamwe haiwezi kuchukua sura ya kuwepo hadi itakapoungana na yule ambaye katika asili yake yuko huru kabisa kutokana na kuhitaji - na kiumbe ambaye anazo sifa za utakatifu na ambaye yeye ni kisababisho tu na sio athari. Bila ya kuwepo kwa kitu kama hicho kisichotawaliwa na masharti yoyote, chanzo cha sababu zote na msingi wa uhai wote, mpangilio wa maumbile hauwezi kuelezeka.

Tuseme kwamba kwenye uwanja wa kivita, kikosi cha wapiganaji kinaazimia kumshambulia adui lakini hakuna hata mmoja wao ambaye yupo tayari kuanza vita kwa kurukia katikati ya jeshi la adui. Yeyote anayepewa amri kufanya hivyo jibu lake ni: "Sitashambulia hadi fulani wa fulani aanze kupigana." Kila mpiganaji anajibu hivyo; hapana hata mmoja wao ambaye yupo tayari kushambulia bila kuweka sharti.

Je, katika hali kama hiyo, shambulizi litaweza kutokea kamwe? Kwa vyovyote vile halitatokea, kwa sababu kupigana kwa kila askari ni kwa masharti juu ya kupigana kwa mwenzake. Ni dhahiri kwamba mfululizo wote wa mashambulizi ya masharti hautatokea bila kutimizwa kwa sharti lenyewe, kitu kisichowezekana chini ya mazingira hayo, na matokeo yake, shambulizi halitafanyika.

Kama tukiiendeleza nyororo ya chanzo na athari milele, kuwepo kwa kila kiunganishi kwenye nyororo hiyo kutakuwa kwa sharti la kiunganishi kilichotangulia ambacho nacho baadaye kitakuwa kwa sharti la kuwepo kwa kiunganishi kilichotangulia. Inakuwa kana kwamba kila kiunganishi kwenye nyororo hiyo ya usababishaji kingekuwa kitangaze kwa sauti kubwa kutoka vina vya nafsi zao: "Sitachukua sura ya kuwepo hadi hapo yule mwingine atakapokuwa amekanyaga uwanja wa viumbe." Kila kiunganishi kinategemea juu ya sharti ambalo halijatimizwa, na kila kimojawapo, kwa hiyo, kikiwa kimezuiwa kupata baraka za kuwepo.

Kwa kuwa tunauona ulimwengu wote ukiwa umetapakaa aina tofauti za viumbe, lazima duniani pawepo na chanzo ambacho sio athari, sharti ambalo halitawaliwi na sharti jingine; vinginevyo uso wa dunia usingekuwa umefunikwa hivi na vitu vingi. Chanzo cha msingi ni mmoja, ambaye katika asili yake yu huru na kuhitajia chochote, ambaye anaweza kujiweka mbali na vipengele vyote tofauti vya uhai, na ambaye anaweza kusababisha kutokea mambo ya maajabu kabisa na dalili za asili kabisa. Ni muumbaji ambaye hupanga yote haya na halafu huyaweka kwenye utekelezaji, ambaye huunganisha maumbile yote kwenye utaratibu wa dunia, ambaye wakati wote hutawanyisha uzuri wa uhai juu ya dunia, na ambaye huisukuma mbele ile mandhari kubwa ya maumbile kuelekea kwenye kutimiza lengo la mpangilio wa uhai. Kwa kuifanya dunia si yenye kuumbwa na ya milele, wayakinifu wanajaribu kukanusha haja ya kudumu ya dunia juu ya muumbaji na hapo kuweka uhai wa kujitegemea juu ya dunia. Utaratibu wao, hata hivyo, hauleti matokeo ya kuridhisha.

Wayakinifu wanadhani kwamba dunia inahitaji muumbaji pale wakati wa mwanzo wa uumbaji tu; mara lengo hilo likitimizwa, Mwenyezi Mungu na ulimwengu hawategemeani na hawana kiunganisho baina yao. Kwa matokeo ya itikadi hii, wayakinifu wanaendelea kukanusha hata ule wakati wa mwanzo wa haja, na kwa kukataa wazo la kuwepo mwanzo wa uumbaji, wanadhani wamepata ufumbuzi wa suala la Mwenyezi Mungu na maumbile na wameikomboa dunia kutokana na haja juu ya muumbaji. Hii ni kwa sababu wanadhani kwamba mahitaji juu ya dunia, kuwa ni ya muda na ya mpito tu, ambapo mahitaji hayo ni ya msingi katika asili ya dunia - dunia si chochote bali ni mwendo, muundo wa mwendo wenye ukomo na utegemezi.

Kwa kweli, kila nukta ni mwanzo wa uumbaji; kila muda; kila atomu hapa duniani inajishughulisha na uanzilishi. Ina maana kwamba kitu kizima ambacho hizo atomu ni kama sehemu yake, hivyo hivyo kimeanzika katika muda; hakina asili na nafsi ambayo imejitenga na huru kutokana na ile ya atomu ambazo zinakijenga. Kwa hiyo dunia bado inayo haja ile ile juu ya kuwepo muumbaji ambayo ilikuwa nayo muda uumbaji ulipoanza. Hata kwa kudhaniwa dunia kuwa ya milele, bado isingepata kujitawala kwa uhai. Jibu la wanasayansi juu ya hoja ya Umilele wa dunia.

Kama vile ambavyo binadamu hupoteza uwezo wa kiakili kadiri muda unavyopita hivyo kwamba siku moja taa ya uhai wake inazimika; viivyo hivyo pia ulimwengu nao wakati wote unaelekea kwenye kuporomoka na kukoma. Kwani nishati zilizopo duniani zinaendelea kufifia pole pole; atomu zimegeuka kuwa nishati na nishati hai inazima na kutulia. Mara tu atomu zinapogawanyika kwa ulinganifu na usawa, hakuna kinachobakia isipokuwa ukimya na kutosogea kwa dhahiri. Kwa hiyo, haiwezekani kuichukulia mata kama ni asili ya milele au maudhui ya uhai, na hakuna jinsi nyingine isipokuwa kuiona dunia kama ni kitu kilichoumbwa. Kanuni ya pili ya mwendojoto, kipimo cha ukosekanaji wa nguvu ya joto katika mfumo (entropy) au kupungua kwa nishati ya joto, inatufundisha kwamba ingawaje hatuwezi kuweka tarehe maalum ya kutokeza kwa dunia, kwa hakika dunia ilikuwa na mwanzo. Joto hapa duniani linapungua polepole na kuanguka, kama kipande cha chuma kilichoyeyushwa ambacho hutawanya joto lake hewani hadi mwishowe joto la chuma hicho litakuwa sawa na lile la vitu na hewa inayokizunguka.

Kama ingekuwa hakuna mwanzo au mahali pa kuondokea kwa ajili ya dunia, Atomu zote zilizopo zingemumunyuka na kugeuzwa kuwa nishati kipindi cha miaka isiyokikomo iliyopita nyuma. Katika kipindi cha muda mrefu uliopita joto la dunia lingeweza kufikia kuisha kabisa, kwani kuhusu mata, katika mkondo wa mabadiliko ya mfululizo muendelezo, hatimaye hubadilika kuwa nishati yenye kuharibika. Haiwezekani kwa nishati yote iliyosambaa kugeuka kuwa mata na bonge lenye starehe kwa dunia ya uhai.

Kufuatana na kanuni ambayo imetajwa hapo juu, mara tu nishati itumikayo ikimalizika nguvu yake, utendaji na hisia za kikemikali haziwezi kuendelea kutokea. Lakini kama ilivyo bayana kwamba utendaji na hisia za kemikali vinatokea, kwamba maisha yanawezekana duniani, na kwamba kitu kikubwa sana kama jua hugawanyika kila siku mchana na usiku kwenye tani milioni mia tatu elfu, ni dhahiri kwamba dunia ilianza wakati fulani. Kuangamia kwa sayari na nyota na kutokuweka majua ni uthibitisho wa kifo na mabadiliko katika mpangilio uliopo; vinaonyesha kwamba dunia inaelekea kwenye kutoweka na hatima isiyoepukika.

Halafu tunaona kwamba, sayansi asilia zimeiondoa mata kwenye ngome ya umilele. Sayansi si tu kwamba inathibitisha kuumbwa kwa dunia lakini pia hushuhudia kwamba dunia ilikuja kuwepo katika wakati maalum. Wakati wa kuumbwa kwake, dunia ilijikuta inahitaji nguvu zisizo za kawaida kwani mwanzoni, vitu vyote havikuwa na umbile na havikutofautiana. Ilikuwa muhimu kwa cheche asili ya mwendo na uhai kutua juu ya ulimwengu wa maumbile. Ingewezekanaje mazingira yasiyokuwa na nishati hai, yanayoainishwa na ukimya kabisa na ukosa maumbile, yangekuwa ndio chanzo cha usongevu na uhai?

Umakanika unatuambia kwamba kitu kisichosogezeka wakati wowote kinakuwa kimetulia isipokuwa kinapopatwa na nguvu ya nje yake. Kanuni hii inawakilisha kanuni isiyoweza kukiukwa katika dunia yetu ya maada, na kwa hiyo, hatuwezi kuamini nadharia ya uwezekano au kubahatisha.

Hakuna kitu kisichosogezeka hata kimoja hadi sasa ambacho kimeingia katika mwendo bila ya kusukumwa na nguvu ya nje yake. Hivyo kwa msingi wa kanuni hii ya kimakanika, lazima pawepo na nguvu ambayo ikiwa ni nyingine mbali na dunia hii ya kimaada, inayoumba dunia hiyo na kuipatia nguvu hivyo kwamba inachukua maumbile, inayojitofautisha yenyewe, na inayojipatia sifa mbali mbali. Mwanasayansi mashuhuri Frank Allen, anapendekeza hoja ya kuvutia ifuatayo yenye msimamo wa kukubali kuumbwa kwa dunia na Mwenyezi Mungu: "Watu wengi wamejaribu kuonyesha kwamba dunia hii ya kimaada haihitaji kuwa na muumbaji. Kilicho juu zaidi ya mashaka yote ni kwamba dunia ipo na maelezo ya aina nne yanaweza kupendekezwa kuhusu chanzo chake: "Kwanza, ni kwamba licha ya hayo ambayo tumeyasema hivi punde, tunaiona dunia kama ndoto na madanganyo (kiini-macho) tupu. Ya pili ni kwamba dunia imechomoza kutoka kwenye hali ya utupu kabisa, yenyewe tu hivihivi. Ya tatu ni kwamba dunia haikuwa na mwanzo na kwamba imekuwepo daima. Ya nne ni kwamba dunia imeumbwa.

"Nadharia tete ya kwanza inategemea katika kukubali kwamba hakuna, kiukweli, tatizo linalotakiwa kupatiwa ufumbuzi mbali na tatizo la metafizikia la utambuzi wa mwandamu juu ya nafsi, ambalo pia linaweza kupuuzwa kama ndoto, njozi na kiini macho. Inawezekana kwamba mtu anaweza kusema kwamba treni za kubuniwa, zilizojaa watu wa kubuniwa zinavuka mito hewa ya kubuniwa kupitia kwenye madaraja yasiyo ya kimaada.

"Nadharia tete ya pili, kwamba dunia ya mata na nishati iliyojitokeza na kuwepo yenyewe tu hivihivi, haina maana na ya kipumbavu kama ile ya kwanza, haifai hata kufikiriwa kwa mazungumzo. "Nadharia tete ya tatu, kwamba dunia imekuwepo wakati wote ina ele - menti moja inayofanana na ile dhana ya kuumbwa, kwani ama mata isiyokuwa na uhai, na hiyo nishati vilichanganika nayo au amekuwepo muumbaji wakati wote. Wala uhusishaji wa umilele hauleti tatizo lolote maalum ndani yake yenyewe. Hata hivyo, mwendojoto umethibitisha kwamba dunia inasogea kuelekea kwenye hali ambayo joto la vitu vyote litakuwa kwenye kiwango cha chini kinachofanana na nishati ya kutumika itakuwa haipatikani tena. Kwa hiyo, uhai utakuwa hauwezekani.

"Kama dunia haingekuwa na chimbuko na ilikuwepo tangu milele yote, hali kama ya kifo na kutokuwepo uhai tayari ingekwishatokea. Jua ling'aralo na lenye joto, nyota na dunia iliyojaa uhai vinabeba ushahidi wa kuaminika wa dunia kuanzilika katika wakati; muda maalum katika wakati ulianisha mwanzo wa uumbaji. Hapo basi, dunia haiwezi kuwa vinginevyo mbali na kuwa imeumbwa; lazima ilikuwa kisababisho kikubwa, cha tangu dahari, muumba wa milele, mwenye ujuzi wa kila kitu na kudra, ambaye ndiye aliyeileta dunia kwenye kuwepo."[22]

Kama mwanadamu atafikiria kwa kina japo kidogo na akatafakari kuhusu ukweli kwa mtazamo mpana, ataelewa kwamba akiwa amekabiliwa na maeneo mapana sana ya kijiografia ya maisha na haja ya namna fulani ya kuyatambua, hawezi hata kidogo kuuona uwezo wake binafsi kama wenye kugetosha kwa kazi hiyo. Elimu juu ya mpango wa maumbile iliokusanywa na mwanadamu kupitia juhudi zake zisizochokesha zinakuwa kama ni bure kabisa. Ingawa sayansi imepiga hatua kubwa sana mbele, kuna hitilafu kabisa baina ya wanadamu, ni nini mwanadamu amejifunza, na ni yapi ambayo bado hayajui.

Kwa kiasi ambacho vile vipindi vilivyopita vinahusika ambavyo vimefunikwa na giza nene, kwa jinsi tujuavyo, maelfu au hata mamilioni ya jamii za wanadamu zilizo bora zaidi ya hii iliopo sasa zinaweza kuwa zilikuwepo. Jamii kama hizo bado zinaweza kuja kuwepo tena hapo baadaye. Kile kinachoitwa sayansi na wale wanaoabudu sayansi wa zama hizi za sasa na wao wakaziona kuwa sawa na jumla yote ya ukweli, ni mkusanyiko tu wa sheria zinazotumika kwa upande mmoja tu wa dunia. Matokeo ya bidii zote za binadamu na majaribio ni sehemu ya ujuzi inayohusu nukta moja ndogo ing'arayo - inayoweza kulinganishwa na mwanga hafifu wa mshumaa - uliozungukwa na usiku wa giza uliofunika jangwa pana sana la ukubwa usio na mpaka.

Kama tukirudi nyuma mamilioni ya miaka vumbi la vurugu litafunika njia yetu ikiwa kama moja ya dalili ya nguvu ya udhaifu na ujinga wa mwanadamu anapokabiliwa na utukufu na ukubwa wa maumbile. Inaweza kuwa kwamba kipindi ambamo mwanadamu amekuwepo si chochote zaidi ya muda kidogo tu katika uhai wa dunia; ni hakika kwamba palikuwepo na bahari nyeusi isiyokuwa na uhai ambamo hamkuwepo na dalili ya mwanadamu. Kwa ufupi tunajua kiasi kidogo sana cha mwanzo wa safari yetu na hatujui chochote kuhusu mustakabali wake. Wakati huo huo, ni vigumu kuamini kwamba mazingira muhimu kwa ajili ya uhai yapo kwenye sayari hii ndogo pekee tu. Wanasayansi wengi wa kipindi hiki wanaona eneo la maisha ni kubwa na pana mno; wanawasilisha mamilioni yasiyo na idadi ya sayari kwenye kukodoa macho kwetu na tunazitazama kwa namna mbalimbali. Lakini kile tunachowezeshwa kuona si chochote zaidi ya umbali wa maono ya mdudu mchwa pale inapolinganishwa na ukubwa wa ulimwengu.

Kuelezea safari ya kufikirika tu kwenye dunia isiyo na ukomo, mwanasayansi mashuhuri; Camille Flammarion, anasema yafuatayo katika kitabu chake cha elimu ya nyota: "Tunaendelea kusonga mbele kwa miaka elfu moja, kwa miaka elfu kumi, kwa miaka mia moja elfu, kwa kasi ile ile, bila kutetereka, bila kupunguza kasi ya mwendo wa gari yetu, wakati wote tukienda mbele katika msitari ulionyooka. Tunasonga mbele kwa kasi ya kilomita mia tatu elfu kwa sekunde. Tunadhani kwamba baada ya kusafiri kwa kasi hiyo kwa miaka milioni moja tutakuwa tumefika kwenye mipaka ya ulimwengu huu unaoonekana?

"Hapana, zipo anga kubwa mno za mbali zaidi zenye giza nene ambazo lazima zipitiwe, na huko pia, nyota mpya zinazoonekana katika mipaka ya mbingu. Tunaziendelea hizo, lakini je, tutazifikia kamwe? "Mamilioni zaidi ya miaka, uvumbuzi mpya zaidi, fahari na ukubwa zaidi, ardhi na dunia nyingine zaidi mpya, viumbe vipya vingine zaidi na vitu vya kiroho vinginevyo - je, kavitakwisha kamwe? Upeo haujifungi kamwe; mbingu daima hazizuii njia yetu; anga yenye kuendelea, pengo inayoendelea. Tupo wapi sisi? Ni njia gani ambayo sisi tumepita? Bado tungalipo katikati ya ile nukta - sehemu ya katikati ya duara ipo kila mahali, mzingo wake hauonekani popote.

Hiyo ndio dunia isiyo na mwisho ambayo inaonekana kukaa wazi mbele yetu na ambayo uchunguzi wake ndio kwanza umeanza. Bado hatujaona chochote, na tunageuka nyuma kwa woga, tukianguka kwa kuchoka kutokana na safari hii isiyo na mafanikio. Lakini tutaangukia wapi? Tunaweza kuangukia kwenye umilele kwenye madimbwi yasiyo na kikomo ambamo kina chake hatukifikii kamwe, kama vile ambavyo, hatuwezi kuvifikia vilele vyao. Kaskazini inakuwa kusini; hakuna mashariki wala magharibi, hakuna juu wala chini, hakuna kushoto wala kulia.

Kokote kule tutakapotazama hatuoni mwisho, na ndani ya eneo hili lisilokuwa na mwisho, ulimwengu wetu si chochote zaidi ya kisiwa kidogo kwenye mkusanyiko mkubwa wa visiwa vilivyoenea kwenye bahari isiyo na mwisho. Maisha yote ya mwanadamu, kwa fahari yote ambayo mwanadamu anajigamba nayo katika historia yake kisiasa na kidini, au hata uhai wote wa sayari yetu pamoja na ufahari wake wote, ni sawa na ndoto ya kitambo kinachopita kwa kasi kubwa.

Kama tungependa kuandika tena kazi zote za utafiti ambazo zimeandikwa na mamilioni ya wasomi kwenye mamilioni ya vitabu, wino ambao unahitajika kwa kazi hiyo ni sawa na ujazo ambao hautazidi ujazo wa tenki moja dogo. Lakini kuelezea na kupanga kwa mtindo wa utaratibu, ile miundo ya vitu vyote vilivyopo duniani na mbinguni, katika vipindi visivyoonekana vilivyopita na kwenye mustakabali usiopimika - kuandika, kwa ufupi, miujiza yote ya maumbile - inaweza kuhitaji wino mwingi zaidi kuliko bahari kuwa na maji."[23] .

Kama asemavyo Profesa Ravaillat; "Ili kuwa na utambuzi uliokamilika wa dunia, inatosha kujua kwamba idadi ya kundi la nyota na sayari kwenye anga pana isiyopimika ya ulimwengu ni kuwa zaidi kuliko ile ya chembechembe za mchanga katika pwani zote za dunia hii."[24] Fikra za aina hiyo kuhusu yale tunayoyajua na tusiyoyajua zinatuwezesha kuepuka kifungo katika kifukofuko cha maisha yetu finyu; ili tuweze kutambua kwa unyonge kuhusu tupo wadogo kiasi gani; kwenda zaidi ya haya maisha yetu yenye ukomo, kwa kiwango ambacho tunaweza na kutafakari ukweli kwa uangalifu mkubwa na kwa kuzama zaidi.

4

MWENYEZI MUNGU NA SIFA ZAKE

SOMO LA NNE

KUAMINI UKWELI WA KISICHOONEKANA KUNAHUSISHA MENGI ZAIDI YA MWENYEZI MUNGU

Sifa moja wapo ya Mwenyezi Mungu wa pekee kwa elimu na ibada ya Ambaye Mitume na viongozi wa kidini wanatuitia ni kwamba Yeye hafikiwi kabisa na hisia za utambuzi. Kwa nyongeza, Anazo sifa za kutokuwa na mwanzo au mwisho. Wa kuwepo kila mahali, Ha. Katika dunia yote ya maumbile na uhai wa kihisia ishara Zake zina madhubuni ya kuwepo kwake na matakwa Yake yanaonekana kila mahali katika dunia hii iliyo uhai, mambo yote ya maumbile vikitangaza uwezo wa ile Dhati yenye hekima.

Kwa kweli, dhati kama hiyo ambayo binadamu hawezi kuitambua kwa milango yake ya fahamu, ambayo kwa vyovyote vile haikupambwa kwa rangi za kimaada, na ambayo hailingani na uzoefu na mawazo yetu ya kawaida, ni vigumu sana sisi kuidhania. Pindi inapokuwa vigumu kudhania kuwepo kwa kitu, inakuwa rahisi kukataa (kuwepo kwake). Watu wanaotaka kutatua suala la kuwepo kwa Mwenyezi Mungu kwa kutumia muundo wa mipaka yao wenyewe ya ki-akili na ufinyu wa mawazo huwa wanahoji inawezekana vipi kuamini kitu kisichoonekana.

Wanashindwa kuzingatia ukweli kwamba utambuzi wa fahamu, ambayo imewekewa mipaka, inaweza kumsaidia mwanadamu kujua na kutambua muundo mmoja tu wa asili; haiwezi kugundua miundo mingine ya asili na kupenya ukubwa wote wa maumbile. Viungo vya fahamu havituruhusu kuendelea hatua moja mbele kuvuka ng'ambo ya vipengele vya nje ya tukio, kwa namna ile ile tu ambayo sayansi za majaribio haziwezi kubeba fikra ya mwanadamu kuvuka mipaka ya hisia za kiwango cha juu zaidi.

Endapo mwanadamu, kwa kupitia nyenzo na vigezo vya kisayansi, hawezi kutambua kuwepo kwa kitu, hawezi kukanusha kuwepo kwa kitu hicho kwa sababu tu hakiendani na vigezo vya kilimwengu, isipokuwa labda atupe baadhi ya ushahidi kwamba hicho kitu husika hakiwezekani. Tunagundua kuwepo kwa kanuni ya busara kutoka ndani ya utimilifu wa tukio kwamba ina uwezo wa kutafsiri. Endapo, basi, kusimama kwa hoja ya ukweli wa kisayansi kunawezekana tu kwa njia ya hisia za moja kwa moja, itakuwa hapana budi kuacha ukweli mwingi wa kisayansi, kwani mambo mengi ya kisayansi hayawezi kutambulika kwa njia ya uzoefu wa kihisia au kufanya vipimo.

Kwa kadiri ambavyo uhakika wa dunia ya kimaada uhusikanavyo, hakuna mtu mwenye busara ambaye atachukulia kikawaida kutokukiona au kutokigusa kwake kitu maalum katika maisha yake ya kila siku kuwa sababu ya kutosha kukikataa. Hataweza kuhukumu kwamba hakipo, kitu chochote kinachoshindwa kuingia kwenye upeo wa utambuzi wake wa hisia. Vivyo hivyo hili litasisitiza ukweli wenye nguvu zaidi wa vitu visivyo vya ki-maada.

Tunapokuwa kuhakikisha sababu ya jambo katika majaribio ya kisayansi, hali hii haituelekezi kukanusha kanuni ya usababishaji. Sisi tutasema tu kwamba sababu hatuijui kwa sababu kanuni hiyo inajitegemea juu ya jaribio maalum tu; hakuna jaribio linaloweza kukanusha kuwepo kwa asili. Je, sio kweli kwamba vitu vyote tunavyokubali na kuamini kwamba vipo, vina uwepo wake wenye uhusiano wa jinsi ile ile kama ya kwetu au kama ya vitu vile tunavyoviona kwa macho? Je, tunaweza kuona au kuhisi kila kitu katika dunia hii maumbile? Hivi ni Mwenyezi Mungu tu ndiye ambaye hatuwezi kumwona kwa fahamu zetu? Wayakinifu (wa ki-maada) wote wanatambua kwamba vitu vingi tunavyovijua vinakuwa na maada na uhalisia ambao hatuwezi kuhisi na kidesturi hatuvijui. Vipo viumbe visivyoonekana vingi tu hapa ulimwenguni.

Maendeleo ya sayansi na ujuzi katika zama hizi vimegundua ukweli mwingi sana wa aina hii, na mojawapo ya milango yenye mafanikio sana katika utafiti wa kisayansi ni ubadilishaji vitu vya kimaada kuwa nguvu ya nishati. Wakati viumbe na maumbile yayoonekana katika ulimwengu huu vinapotaka kuzalisha nishati, hulazimika kubadili sura zao za asili na kugeuka kuwa nishati. Sasa, je, nishati hii - mhimili ambamo huzunguka misogeo mingi na mabadiliko ya ulimwengu - inaonekana na kugusika? Tunajua kwamba nishati ni chanzo cha nguvu lakini asili ya nishati bado inabakia ni kitendawili.

Tuchukue umeme ambamo nyingi ya sayansi yetu, ustaarabu wetu na maisha vimetegemea. Hakuna mtaalamu wa fizikia kwenye maabara yake - au mtu awaye yeyote, juu ya jambo hilo, ambaye anashughulika na vifaa na zana za umeme - anayeweza kuuona umeme wenyewe au kuhisi na kugusa uzito au ulaini wake. Hakuna mtu anayeweza kutambua moja kwa moja njia ya umeme kwenye waya; anaweza tu kutambua kuwepo kwa mkondo wa umeme kwa kutumia vifaa muhimu.

Fizikia ya kisasa inatuambia kwamba vitu ambavyo tuna hisia ya utambuzi ni thabiti, vigumu na imara, na hakuna nguvu inayoonekana kwa macho katika kusogea kwao. Lakini licha ya muonekano na wa nje, kwa kweli kile tunachokiona na kutambua ni mlundikano wa chembe ndogo ndogo (atomu) ambazo wala sio thabiti, ngumu, wala imara; vyote hivi si chochote isipokuwa migeuko, mabadiliko na misogeo. Kile ambacho viungo vyetu vya hisia vinadhania kuwa ni imara na hakisogei kinakosa uimara na utendaji na kutosogea; kinavikusanya vyote; misogeo, mabadiliko na maendeleo kwa pamoja, bila ya hili kutambulika kwetu sisi kwa njia ya uchunguzi wa hisia wa moja kwa moja.

Hewa inayotuzunguka ina uzito mkubwa na hutoa shinikizo wakati wote kwenye mwili, kila mtu hubeba shinikizo la kilo 16,000 la hewa. Lakini hatuhisi usumbufu kwa sababu shinikizo la hewa limewekwa sawa na shinikizo la ndani ya mwili lenyewe. Ukweli huu wa kisayansi uliothibitishwa ulikuwa haujulikani hadi wakati wa Galileo na Pascal, na hata sasa hivvi hisia zetu haziwezi kutambua[11] . Sifa zilizotolewa kwenye vipengele vya kimaumbile na wanasayansi katika misingi ya majaribio ya hisia na maamuzi ya kimantiki haziwezi kutambuliwa moja kwa moja. Mathalani mawimbi ya radio yapo kila mahali na bado hayaonekani popote. Hakuna mahali maalum ambapo hakuna nguvu ya mvutano ya kitu fulani chenye umbo, lakini kwa hali yoyote hii haikiondoi kwenye kuwepo kwake au kupunguza umbo lake.

Fikra kama vile uadilifu, uzuri, mapenzi, chuki, uadui, hekima ambazo hutengeneza ulimwengu wetu wa kiakili, hazina uwepo unaoonekana na wa wazi kabisa au mwelekeo mdogo kabisa wa kimwili; hata hivyo, tunazifikiria kuwa ni ukweli. Mwanadamu hajui kiini cha umeme, mawimbi ya radio au nishati, ya elektroni na nutroni, hutambua kuwepo kwao kwa njia ya matokeo na athari zao tu.

Uhai ni dhahiri kwamba upo; hatuwezi kukanusha kwa vyovyote. Lakini tutaweza kuupima vipi na kwa kutumia njia gani tunaweza kupima kasi ya fikra na dhana? Kutokana na yote haya ni wazi kabisa kwamba kukanusha chochote kilichopo nje ya upeo wa uoni wetu wa kiakili na kusikia ni kinyume na mantiki na kanuni za kawaida za akili. Kwa nini wakana Mwenyezi Mungu wanashindwa kutumia kanuni za kawaida za sayansi kuhusu suala mahsusi la kuwepo kwa uwezo unaotawala maumbile yote? Myakinifu fulani wa Misri alikwenda Makka ili aanzishe mjadala na huko 8

alikutana na Imamu Sadiq(a.s) . Imamu akamwambia, "Anza kuuliza maswali yako." Myakinifu kutoka Misri hakusema kitu. Imamu: "Unakubali kwamba dunia ina juu na chini?" Mmisri: "Ndio." Imamu: "Kwa hiyo unajuaje kile kilichomo chini ya ardhi?" Mmisri: "Sijui, lakini nadhani hakuna chochote chini ya ardhi." Imamu: "Kudhania ni dalili ya kutokuwa na uwezo unapokabiliwa na jambo ambalo huna uhakika nalo. Sasa niambie, umewahi kamwe kwenda juu angani?" Mmisri: "Hapana."

Imamu: "Hii ni ajabu ya kiasi gani kwamba hujawahi kwenda Magharibi au Mashariki, kwamba hujateremka chini ya ardhi au kuruka juu angani hadi mbinguni, au kupita juu yake ili ujue yaliyoko huko, lakini hata hivyo unavikanusha vile vilivyopo huko. Mtu yeyote mwenye busara angeweza kukataa ukweli wa kile asichokijua? Na unakanusha kuwepo kwa Muumba kwa sababu huwezi kumwona kwa macho yako!" Mmisri: "Hakuna mtu aliyewahi kuzungumza nami kwa namna hii kabla yako." Imamu: "Kwa hiyo, kwa kweli unayo mashaka kuhusu kuwepo kwa Mwenyezi Mungu; unadhani Anaweza kuwepo na Anaweza asiwepo?"

Mmisri:"Labda ndivyo" Imamu: "Ewe mtu, mikono ya mtu asiyejua haina uthibitisho wowote; asiyejua kamwe hawezi kuwa na ushahidi wa aina yoyote. Ufahamu vema kwamba kamwe hatuna wasi wasi wa aina yoytote au kusitasita kuhusu kuwepo kwa Mwenyezi Mungu. Je, hulioni jua na mwezi, mchana na usiku, vinapishana wakati wote na vikifuata njia maalum iliyowekwa? Kama vina uwezo wao vyenyewe, hebu viondoke kwenye njia zao na visirudi tena. Kwa nini wakati wote vinarudi? Endapo viko huru katika kubadilishana na kubiringika kwao, kwa nini usiku haugeuki kuwa mchana na mchana kuwa usiku? Ninaapa kwa Jina la Allah kwamba vitu hivi havinav uhuru wa kuchagua katika misogeo yao; ni Yeye Ndiye husababisha vitu hivi kufuata njia iliyowekwa; ni Yeye Ndiye anayeviamuru vitu hivi: na ukuu na ufahari ni vya kwake pekee." Mmisri: "Unasema kweli!"

Imamu: "Kama unadhani kwamba maumbile na muda vinawapeleka watu kimbele mbele, sasa kwa nini wao haviwarudishi kinyume nyume? Na kama vinaweza kuwarudisha nyuma, kwa nini haviwapeleki kimbele mbele? Tambua kwamba mbingu na ardhi vinatii matakwa Yake. Kwa nini mbingu haziporomoki na kuanguka ardhini? Kwa nini matabaka ya ardhi hayapinduki chini juu na kwa nini hayapandi na kufika juu mbinguni? Kwa nini hao waishio juu ya ardhi hawagandamani?" Mmisri: "Mwenyezi Mungu Ambaye ni Mola na Mlezi wa mbingu na ardhi ndiye anayevilinda vitu hivi visiporomoke na kuangamia." Yale maneno ya Imamu sasa yalianzisha mwanga wa imani kuangaza kwenye moyo wa Mmisri; aliukubali ukweli na akaingia kwenye Uislamu[12] .

Tusije tukasahau kwamba sisi tumefungwa ndani ya mfumo wa maada na mapana yake; hatuwezi kubunia kitu kisichokuwa na mipaka kwa kutumia tabia zetu za kawaida za kifikra. Endapo tutamuambia mwanakijiji kwamba kuna jiji kubwa na lenye watu wengi liitwalo London, akilini mwake atafikiria juu ya kijiji kikubwa, labda mara kumi zaidi ya ukubwa wa kijiji chake, na itakuwa hivyo hivyo kuhusu majengo yake, jinsi watu wanavyovaa, namna wanavyo endesha maisha yao na wanavyoingiliana katika shughuli zao. ataona kwamba tabia za watu kila mahali ni hizo hizo kama zilivyo kijijini kwake.

Jambo pekee tunaloweza tu kumwambia ili kusahihisha namna yake isiyo sahihi ya kufikiria ni kwamba London kwa kweli ni sehemu ya makazi ya watu, lakini sio ya namna unayodhania wewe, na hali zake sio za namna moja na zile unazoona pale kijijini kwako mwenyewe. Tunachoweza kusema kuhusiana na Mwenyezi Mungu ni kwamba Mwenyezi Mungu yupo, na kwamba Yu ana uhai, uwezo na ujuzi, lakini kuwepo Kwake na ujuzi na uwezo wake sio vya namna ile tuliyo na mazoea nayo. Kwa njia hii tunaweza, kwa kiwango fulani, kuepuka mipaka iliyowekwa katika uelewa wetu. Kwa myakinifu vile vile, ni vigumu yeye kutambua kiini cha msingi wa vitu asili (maada).

Ingawa inaonyesha kuwa vitu vyenye kuhisia ni vitu tunavyojua kwa uwazi na ufasaha zaidi, hatuwezi kutegemea moja kwa moja juu ya vitu hivyo pekee katika mambo ya kisayansi na kifalsafa. Tukiweka pembeni misimamo yote yenye shabiki, lazima tutathmini asili halisi ya vitu vya hisia na kiwango ambacho vinaweza kumsaidia mwanadamu katika kugundua ukweli. Vinginevyo, vitatupotosha, kwa sababu utambuzi wa hisia unahusiana tu na sifa fulani za mielekeo ya nje ya vitu vyenye kuhisia. Hauwezi kutambua ukamilifu wa sifa hizo au asili na kiini tu cha vitu vyenye kuhisi, tukiviacha vitu visivyokuwa na hisia.

Jicho ambalo ndio njia ya uhakika zaidi ya utambuzi wa ukweli, mara nyingi, hushindwa kutuonyesha sisi ukweli. Jicho linaweza kutazama mwanga pale tu ambapo urefu wa mawimbi yake haupungui 4% ya mikroni (kipimo cha urefu wa mamilioni ya mita) na sio zaidi ya 8% ya microni na, kwa hiyo, haliwezi kuona mwanga wa juu zaidi ya rangi ya urujuani au chini zaidi ya rangi nyekundu. Zaidi ya hayo, makosa yanayofanywa na utambuzi wa hisia hutengeneza sehemu muhimu kwenye vitabu vya saikolijia: jicho linajulikana kwa kufanya makosa mengi sana.

Rangi tunazozitambua katika ulimwengu wa nje, kwa kweli, si rangi. Hiyo ni mitetemo iliyoko kwenye marefu tofauti ya mawimbi. Uzoefu wa hisia zetu za macho, una marefu mbalimbali ya mawimbi ya mwanga, kwa mujibu wa utaratibu wake mahsusi kama rangi. Kwa maneno mengine, kile tunachokitambua kwa njia ya hisia zetu kimewekewa mipaka na muundo na uwezo wa hisia hizo. Mathalan, muundo wa hisia za macho katika wanyama fulani kama vile ng'ombe na paka husababisha waone uhalisi wa nje wa kitu usiobadilika, kama kimepakwa rangi. Kutokana na maoni ya uchunguzi wa kisayansi, utaratibu ndani ya hisia za macho ya mwanadamu ambao humruhusu kuona rangi haupo wazi kabisa na nadharia ambazo zimetangulizwa hadi sasa zote ni za kubuni. Suala la uwezo wa mtu kuona rangi halieleweki vizuri na lenye utata.

Ili kuweza kuona jinsi hisia ya mguso inavyoweza kudanganywa, unaweza kujaza maji kwenye mabakuli matatu: la kwanza yajazwe maji ya moto sana, la pili maji ya baridi sana, na la tatu maji ya vuguvugu. Halafu weka mkono mmoja kwenye maji ya moto na mwingine kwenye maji ya baridi, na uiache humo kwa muda kiasi. Kisha iweke mikono yote kwenye maji ya vuguvugu, na utaona kwa mshangao wako mkubwa kwamba utapata hisia zinazohitilafiana. Mkono moja utakuambia kwamba yale maji ya vuguvugu ni ya baridi sana, na mwingine utadai kwamba ni ya moto sana. Kwa kweli, maji ni yale yale, na joto lake linafahamika.

Sasa, akili na mantiki zinasema kwamba haiwezekani maji kuwa moto na baridi kwa wakati mmoja, kuwa na sifa mbili zinazo tofautiana. Ni hisia ya mguso ndio yenye dosari, baada ya kupoteza hali yake ya kujidhibiti kama matokeo ya yale mabakuli mawili ya maji ambamo mikono ilitumbukizwa. Inachokihisi kinatofautiana na ukweli, na mantiki na akili hulionesha kosa hilo. Ikiwa hali ni hii, tutawezaje kutegemea utambuzi wa hisia bila ya mwongozo wa kigezo cha akili na fikira? Je, kuna njia yoyote ya kujilinda dhidi ya dosari za utambuzi wa hisia zaidi ya uamuzi wa busara? Wakati fulani mtu alimuuliza Amirul-Mu'minin(a.s) , "Je, umewahi kumuona Mola Wako?"

Yeye akajibu:"Sitamwabudu kamwe Mola ambaye siwezi kumwona!" Huyo mtu halafu akauliza: "Wewe ulimwona vipi? Hebu tuelezee." Yeye(a.s.) akajibu:"Ole wako wewe! Hakuna mtu ambaye amewahi kumuona Yeye kwa jicho halisi, lakini nyoyo zilizojaa ukweli wa imani zimemzingatia Yeye." [13] Kwa hiyo ni uamuzi wa akili ndio unaopewa dhamana ya kusahihisha makosa ya utambuzi wa hisia, na chanzo cha uamuzi huo kiko nje ya upeo wa himaya ya hisia. Kwa hiyo, utambuzi wa hisia hauwezi kuzalisha uoni wa kiakili wenye uhalisi, manufaa yake ni ya mazoezi ya vitendo tu. Wale wanaotegemea utambuzi wa hisia pekee katika uchunguzi wao hawataweza kuyatatua kamwe matatizo ya uhai na kitendawili cha maumbile.

Kutokana na tathmini ya ufanisi wa utambuzi wa hisia, tunafikia hitimisho kwamba hata kwenye nyanja ya hisia za kimajaribio, yenyewe peke yake haiwezi kutoa ujuzi wa uhakika kwa mtu na kumwongoza kwenye ukweli. Kwa ukweli wenye nguvu zaidi, hali itakuwa ni vivyo hivyo katika mambo ambayo yapo nje ya upeo wa utambuzi wa hisia. Wafuasi wa metafizikia (falsafa ya uchunguzi wa chanzo cha uhai na maarifa) wanasadiki kwamba kama ilivyo katika njia ile ile ambamo majaribio na upimaji ndio mbinu za uchunguzi na utambuzi zinatakiwa kufuatwa kwenye sayansi ya hisia, ni uwezo wa kufikiria ndio njia ya kugundua ukweli kwenye mambo yahusuyo falsafa ya kuchunguza chanzo cha uhai na maarifa - metafizikia.

UMUHIMU WA KANUNI ZA UHAI

Sayansi inasema kwamba ni uhai ndio unaoumba uhai. Maisha ya viumbe hai yanawezekana tu kwa njia ya kizazi, kuzaana na kutengenezeka upya kwa aina husika. Hakuna chembe ya uhai hata moja ambayo imegundulika kuzaliwa na kiini asili kisicho na uhai. Hata aina ndogo za viumbe vyenye uhai, kama vile kuvu na vimelea, haviwezi kuwepo na kukua isipokuwa pawepo na kisababisho ambacho chenyewe ni kishiriki katika uhai kiwe ni chenye kuonekana kwenye mazingira yake.

Kwa mujibu wa ushahidi wa sayansi, dunia ilipita kwenye vipindi virefu ambapo hapakuwepo na uwezekano wa uhai kwa sababu ya joto kali sana lililokuwepo. Hapakuwa na uoto wowote ulioweza kuonekana kwenye uso wa sayari hii na hapakuwepo na mito au chemchem. Angahewa ilijaa metali zilizoyeyuka na milipuko ya volkano. Baadaye, wakati ambapo gamba la dunia lilipoanza kupoa, ni vitu visivyo na uhai tu ndivyo vilivyoweza kuonekana kwa mamilioni ya miaka. Kwa ufupi wakati wote wa kukurukakara zote za mabadiliko zilizofanyika kwenye uso wa ardhi, hapakuwepo na dalili za uhai juu yake. Ni vipi basi uhai ulivyojitokeza ghafla?

Hapana shaka uhai ulitokeza muda fulani baada ya kutokeza kwa ardhi; ni kwa muda mrefu kiasi gani utengenezaji huo ulifanyika na jinsi ulivyotokea, hilo halijukani. Kwa karne nyingi watafiti wamekuwa wakijitahidi kwenye maabara zao kugundua muujiza wa uhai, hili jambo la ajabu kwelikweli, lakini hadi sasa hawajakaribia hata kidogo kukifumbua kitendawili hiki. Mtafiti mmoja ameandika kwenye kitabu kiitwacho 'Distant World' "ni neno kichawi lililoje hili, la uhai! Je, hivi kuishi kulikuja kuwepo kutokana na kutokuwepo kitu chochote? Hivi dutu ya viumbehai inaweza kutokana na dutu viumbe visivyo hai? Au upo mkono fulani wenye uwezo na ubunifu unaofanya kazi hii? Wakati mwingine inapendekezwa kwamba inawezekana uhai umekuja kwenye sayari yetu kutoka kwenye maumbile mengine ya kimbingu, kwa sababu wakati ambapo aina ya chini sana ya uhai - viini vya mbegu za mboga - vinavyoogelea kwenye angahewa ya umbile la kimbinguni hupanda kufikia kilele cha juu sana, miale ya jua inaweza kuvibeba kwa njia ya shinikizo hadi kwenye anga, hivyo kwamba hatimaye vinafika kwenye uso wa umbile jingine la kimbinguni ambamo hustawi na kujiendeleza.

"Nadharia tete hii haiashirii maendeleo japo kidogo tu katika kupata ufumbuzi wa kitendawili hiki kikubwa, kwa sababu endapo nadharia hii ingekuwa ya kweli, bado hatujajua ni jinsi gani uhai ulivyojitokeza, ama ulitoka kwenye mojawapo ya sayari zilizopo kwenye mfumo wa jua na sayari zake au mojawapo ya 'Nyota ya Shiraa.' Kama vile ambavyo saa haikutengenezwa kwa kulundika pamoja springi, vikorokoro, bolti na nyenzo, vivyo hivyo, pia uumbaji wa uhai hauwezekani bila kuwepo moyo - yaani kile kinachouweka uhai kwenye msongo - na wito ambao hutamka 'kuwa hai!'" Tunatambua kwamba maada ndani mwake na yenyewe inakosa uhai na kwamba hakuna elementi ya kimaada yenye kumiliki uhai bila ya kusaidi wa.

Hivyo basi, uhai hauwezi kufikiriwa kutokea kutokana na uchanganyaji wenye mpangilio mzuri wa chembehai zinazounda kitu. Swali linajitokeza kwamba kwa nini kitu chenye uhai hakiwezi kujinakili kama kilivyo isipokuwa kwa kuzaliana na kuota upya kwa spishi husika. Utendaji wa kikemikali na athari zake wakati wote zinaendelea katika viumbe visivyo na uhai bila ya dalili yoyote ya uhai kuonekana ndani yao. Kusema kwamba kitu cha kimaada kina mwelekeo wa mkusanyiko na kwamba uhai ghafla hujitokeza wakati wa maendeleo na mabadiliko yake ni kufafanua jambo la uhai na lenye umuhimu ambalo tunalitambua kihisia; sio kuelezea chimbuko la uhai na sababu yake.

Zaidi ya hayo, chembechembe za maada kiasili hazikuwa hazikuwa zenye kutofautiana zenyewe kwa zenyewe; kwa hiyo ni lazima kuna sababu iliyofanya kazi kuleta mkusanyiko wa baadhi yao na kuzuia mkusanyiko wa zingine. Na ni sababu gani ya baadhi ya chembe chembe kupewa uhai na zingine kunyimwa uhai? Jambo pekee la kutokea kutokana na mchanganyiko wa elementi mbili au zaidi ni kwamba kila elementi inaipatia elementi nyingine baadhi ya sifa ilizokuwa nazo; inawezekanaje itoe zawadi ya kitu ambacho hainacho? Elementi zinapata sifa ya pamoja kama matokeo ya kuchanganyika, sifa ambayo haiwezi kutoka nje ya sifa ambazo kila elementi inazo, lakini uhai pamoja na tabia yake ya kipekee haina kufanana kokote na sifa za maada.

Uhai unajionyesha wenyewe katika njia ambazo kwamba maada haiziwezi, na katika namna nyingi, kwa kweli, uhai hutawala maada. Ingawaje uhai huonekana kutegemea maada, yenyewe maada ikiwa ndio umbile linaloupokea uhai, msogeo, dhamira na hatimaye utambuzi na ujuzi huonekana kwenye maada pale tu uhai unapotupa miale yake juu yake. Kwa hiyo, sio haki kujaribu kutafsiri uhai kilingana na athari za kikemikali.

Ni kipengele kipi kinachotengeneza chembechembe kwa aina nyingi tofauti na kwa mipango tofauti na halafu kikaziweka kwenye muundo uliofikiriMwenyezi wa? Kinachotayarisha chembechembe zinazozaliana ambazo huhamisha tabia na upekee wa akina baba kwa watoto wao, bila ya kosa hata kidogo kutokea katika utekelezaji wa shughuli hiyo. Tunaona kwamba chembehai zinazo tabia fulani mahsusi katika sehemu zao mbalimbali, miongoni mwao ikiwa ni ukarabati, ujenzi upya, uhifadhi wa spishi, na uwezo wa mabadiliko.

Kila chembehai ndani ya mwanadamu hufanya kazi katika wakati unaotakiwa na kwa namna inayotakiwa. Mgawanyo wa kazi na utendaji wake miongoni mwa chembehai ni wa kipekee. Zimegawanywa katika idadi inayihitajika kuhakikisha ukuaji wa mwili, na kila chembehai huenda pale mahali ilipopangiwa kwenye ubongo, mapafu, ini, moyo na figo. Mara chembehai zinapokuwa zimechukua nafasi zao zilizopangiwa, hazishindwi hata kwa nukta moja katika kutekeleza kazi zao muhimu; zinatawanya na kuondoa vitu visivyohitajika na visivyo na maana na kutunza hasa tu ule ujazo wao unaolingana.

Kuhusisha upambanuzi huu wa kipekee ambao unalengo la kuunda, kwa uwiano unaostahili, viungo na sehemu, vinavyohitajiwa na viumbe hai, kwenye mambo yatendayo bila kufikiri na yasiyo na fahamu ni tafsiri isiyotosheleza kabisa. Ni mtu gani mwenye mawazo huru ambaye angekubali ukosefu wa mantiki kama huu? Uhai, kwa hiyo, ni nuru inayoangaza kutoka kwenye upeo wa juu sana juu ya vitu vya kimaada ambavyo vina uwezo wa kuipokea; inaviweka vitu hivyo kwenye msogeo na kuweka kila kimoja kitaalamu kabisa mahali pake maalumu.

Ni utashi wenye mwongozo wa Muumba, uwezo Wake wa kuamua kwa njia ambayo inahakikisha mwendo na ukuaji kuelekea kwenye ukamilifu, na hekima Yake yenye maarifa mengi na yenye athari nyingi, ambayo ndio inayouweka muujiza mkuu wa uhai, na sifa zake zote, kwenye vitu visivyo na uhai.

Mtu ambaye anautambu a ukweli huona uelekeo wa kudumu wa uhai ukipita kwenye kiini cha kitu kinachobadilika na kutembea. Humtafakari Mwenyezi Mungu katika hali Yake ya kuendelea uumbaji na uanzilishaji, msukumo Wake usio na kikomo wa vitu vyote kuelekea kwenye ukamilifu.


4

5

6

7

8

9

10

11

12

13

14