MUANDAMO WA MWEZI

MUANDAMO WA MWEZI 12%

MUANDAMO WA MWEZI Mwandishi:
Kundi: Midahalo na majadiliano kielimu

MUANDAMO WA MWEZI
  • Anza
  • Iliyopita
  • 23 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 63003 / Pakua: 7159
Kiwango Kiwango Kiwango
MUANDAMO WA MWEZI

MUANDAMO WA MWEZI

Mwandishi:
Swahili

1

2

3

4

5

6

7

16

MUANDAMO WA MWEZI

SEHEMU YA KUMI NA TANO

FUNGA YA 'ARAFAH

Katika sehemu hii, ni vyema kwanza nikanukuu yote nilioyasema kuhusu maudhui hii, kisha ndio nikanukuu jawabu niliojibiwa na kuijadili. Kuhusu suala hili nilisema: Anasema Sheikh Nassor Bachoo: "Jambo la kusikitisha ni kwamba ikiwa Waislamu watakubali kuwepo tafauti ya siku na tarehe baina yao, hapana shaka watakuwa wanafunga saumu ya Arafa siku tafauti na inavyotakiwa.

Kwa hivyo lengo na faida ya funga yenyewe litakuwa halikupatikana. Mbali na kukosekana huko Makka jambo baya zaidi ni kwamba watakuwa wanafunga siku ya pili yake ambapo watakuwa wanafunga siku ya 'Idul-Adh-ha'; siku ambayo ni Haramu kufunga.

Ni vyema tuzingatie kwamba funga hii ya Arafa pamoja na Iddi yake ni vitu ambavyo havina mahusiano na kuandama mwezi kutokana na kila nchi inavyoona mwezi wake. Bali chanzo cha funga ya Arafa ni uhusiano wa ile siku ambayo mahujaji wanaposimama katika uwanja wa Arafa. Na jambo la kusimama Arafa linapatikana sehemu moja tu ulimwenguni ambayo ni siku inayosadifu tarehe 9 Dhul-Hijjah huko mji wa Makka; sio tarehe tisa ya nchi nyengine yoyote ile. Kwa uthibitisho zaidi wa funga ya siku ya Arafa tunajifunza kuwa Mtume (s.a.w.) alipotueleza umuhimu wa siku hii, na kila alipotaja siku hii ya Arafa alitumia neno 'siku' wala hakutumia neno 'tarehe'.

Funga ya 'siku' ya Arafa." Mwisho wa kunukuu. Sasa tatizo moja linalowatatiza watu kuhusu suala zima la kuwa na miandamo tafauti ni tatizo hili la funga ya Arafa. Kwa kweli hili si tatizo lakini tatizo tunalo sisi wenyewe katika udha ifu wetu wa kukiweka kila kitu mahala pake na kutoa hukumu kwa mujibu wa misingi inavyotuelekeza. Siisahau kauli ya Dr. Al-zuhailiy yenye maana kwamba makosa mengi ya kifiq-hi yanatokana na kuwacha misingi yake ya kiusuli, na kwamba lau watu walikuwa wanaifata misingi hio, basi makosa yasingelitokea au ingelikuwa nadra sana kutokea.

Sasa suala tunaloulizwa ni kuwa kama muandamo kila watu wawe na wao, itakuwaje ikitokea siku ya Arafa kuwa kwetu ni mwezi nane, ilhali Arafa inakuwa mwezi tisa? Tukifunga tutakuwa tumefunga mwezi nane; tukifunga siku ya pili itakuwa Arafa imeshakwisha?

Jawabu ya suala hili: ni kuwa kwanza inatakiwa tujue kwanini tunafunga siku hio: nini sababu: je sababu ni Arafa au sababu ni mwezi muandamo? Tumeeleza huko nyuma nini illa ambayo, kwa Kiswahili, huwa tunaifasiri kuwa ni Sababu. Tukasema kwamba wengine wanatafautisha baina ya sababu na illa. Sababu - kwao - ni kitu kisicho na uhusiano na kitu chenye kupewa hukumu. Tukatoa mfano wa kutenguka kwa jua kuwa ni sababu ya kuwajibikiwa na Sala. Na illa ni kitu chenye uhusiano na kitu chenye kupewa hukumu, kama kuumwa ndio illa ya kuruhusika kula mchana wa mwezi wa Ramadhani.

Kwa maana hii, utakuwa umefahamu kwamba sababu ya:

1) Kutuwajibikia Sala ya Adhuri na Laasiri - kwa mfano - ni kutenguka jua. Ushahidi wake ni Aya inayosema: (Simamisha sala kwa kutenguka jua).

2) Sababu ya kufunga au kuwajibikiwa na funga ni kuuona mwezi. Kama ilivyo Hadithi inayosema:(Fungeni kwa kuuona) . Sasa hapa tuna mambo mawili: Moja: ni munasaba wa kufunga siku hio ya Arafa. Pili: ni sababu ya kufunga siku hio ya Arafa. Kisimamo cha Arafa ni Munasaba: wa kufunga siku hio: si sababu: Sababu: ya kufunga siku hio, ni muandamo wa mwezi wa mfunguo tatu. Wala usidhani kwamba tarehe tisa ya mwezi huo ndio sababu: "laa" (sio hivyo), bali tarehe tisa ni wakati wa kufunga: si sababu ya kufunga. Na hili linabainishwa zaidi na riwaya tuliotangulia kuinukuu huko nyuma, nayo ni riwaya ya Amiri wa Makka, yenye kusema: "Alituusia Mjumbe wa Allah - rehema na amani ziwe juu yake - tuabudu kwa kuuona, kama h atukuuona na wakashuhudia mashahidi wawili waadilifu, tuabudu kwa (kufata) ushahidi wao." Tumesema huko nyuma kwamba neno Nansuk (tuabudu) wengine wameifasiri ibada hii kuwa ni ibada ya hija nayo ndio tafsiri yenye muelekeo madhubuti zaidi, kwani neno hili hutumika sana kwa maana ya ibada ya hija, kama Allah (S.W.) anavyosema kuhusu ibada ya hija: Mukimaliza Nusuki (ibada) zenu (za hija). Na kwa hivyo imekuja katika "A'WNU AL-MA'ABUDI: SHARHU SUNANI ABI DAUD" kuhusu maana ya Hadithi hio tulioinukuu hapo juu kuwa maana yake inahusiana na ibada za hija. Anasema mwenye kusherehesha: "Na maana yake ni: 'Tuhiji kwa kuuona (mwezi), yaani mwezi muandamo wa mfunguo tatu." Ni wazi kwa maelezo haya au kwa mujibu wa Hadithi hii kwamba sababu ya ibada za hija - ikiwemo funga ya Arafa - ni kuandama kwa mwezi wa mfunguo tatu.

Sasa - tukirudi katika munasaba - ni kuwa munasaba si lazima kuwa mtu ausherehekee siku ile ile ya munnasaba huo. Kwa mfano, tunaposherehekea tokeo fulani lililotokea tarehe fulani katika historia, si lazima kuwa tuifanye sherehe yetu siku na tarehe ile ile: "Laa" tunaweza kuweka sherehe yetu siku nyengine. Sikusudii kufananisha sherehe yetu na mas-ala haya, ninachokusudia ni kukupa mfano utaoweza kufahamu kwawo tafauti baina ya Munasaba na Sababu.

Kwa hivyo, funga imeambatanishwa na muandamo wa mwezi, kama vile sala ilivyoambatanishwa na mtenguko wa jua. Utapolifahamu hili, utakuwa umefahamu kwamba, siku ya kufunga ni tarehe tisa mfunguo tatu, sawa siku hio imeafikiana na Arafa au imetafautiana, kwani sababu tayari imepatikana, na kilichotafauti ni kuafikana wakati wa tarehe ya baadhi ya sehemu na kuafikiana wakati mmoja wa Munasaba. Na Munasaba haufanywi kuw a ni illa wala haufanywi kuwa ni sababu ya hukumu. Hilo ni mosi.

Pili : ni kuwa: hata ikiwa kweli kilicho sahihi ni kwamba watu wakisimama Arafa na sisi tufunge hata ikiwa tarehe nane kwetu kwa mujibu wa muandamo wetu - tumeona kwamba kielimu hili ni kosa lakini tujaalie ni hivyo - basi elewa kwamba hili halijahalalisha kwamba na muandamo wa Ramadhani uwe mmoja. Ukitafakari kidogo hapa, utaona kwamba dai hili ni kujenga hoja juu ya Qiyas baina ya mambo mawili yaliotafauti. Arafa ni tokeo ambalo linatokea Makka tu, wakati Ramadhani ni tokeo la dunia nzima. Kwa hivyo, hata tukisema kwamba kilicho sahihi ni kufunga kwa ajili ya tokeo hilo au munasaba huo wa Arafa, basi itakuwa ni kwa sababu munasaba huo unatokea sehemu moja tu: kwetu hautokei. Kwa lugha nyengine, lau na sisi tulioko nje ya Makka ingelikuwa tunatakiwa tusimame Arafa yetu huko tuliko siku ya tarehe tisa, basi tungefanya hivyo kwa mujibu wa muandamo wetu, kama vile tunavyofunga kwa kufata muandamo wetu, na kusali kwa sababu ya mtenguko wetu wa jua. Wakati Ramadhani ni tokeo la dunia: watu wa Makka wanafunga na sisi tunafunga. Kwa hivyo, haya ni matokeo mawili tafauti huwezi kuyafanyia Qiyas kwani miongoni mwa masharti ya lazima ya Qiyas ni "Kupatikana usawa baina ya Shina na Tawi" na usawa hapa haupo. Kilicho sahihi, ni kufanya Qiyas cha Sala na funga. Kwani:

1) Wajibu wa Sala umefungamanishwa na kutenguka na kuzama kwa jua - kitu cha kimaumbile (Natural phenomenon). Kwa hivyo mtenguko wa jua ni sababu: si munasaba.

2) Wajibu wa funga umefungamanishwa na muandamo wa mwezi - kitu cha kimaumbile (Natural phenomenon). Kwa hivyo kuandama kwa mwezi ni sababu: si munasaba.

3) Jua - ambalo kutenguka kwake ndio sababu ya kuwajibikiwa na sala - likitenguka katika nchi moja, watu wa nchi nyengine hawawajibikiwi na sala. Kwa hivyo, Qiyas sahihi ni kuwa kuonekana kwa mwezi - ambayo ni sababu ya kuwajibika funga - katika nchi moja isiwe sababu ya kufunga kwa watu wa nchi nyengine. Hiki ni Qiyas sahihi. Ama kisimamo cha Arafa si Qiyas sahihi, kwani kisimamo cha Arafa ni Munasaba si Sababu wakati muandamo wa mwezi na kutenguka jua ndio Sababu. Au ukipenda kufanya Qiyas chengine sahihi, basi ni kile tulichotangulia kukinukuu kutoka kwa Sheikh Al-uthaimin, aliposema: "Na wakati wa mwezi ni kama wakati wa siku. Kama vile ambavyo miji inatafautiana katika kuanza kujizuia (na kula n a kunywa na jimai: yaani kuanza kufunga) na (inavyotafautiana katika) kufuturu kwa siku (daily au, basi vivyo hivyo inawapasa watafautiane katika kujizuia na kufuturu kwa mwezi (monthly au). Na (kama) inavyojulikana kwamba tafauti za kisiku zina athari zake kwa makubaliano ya Waislamu. (Watu) waliyo upande wa mashariki, hakika wao wanaanza kufunga kabla ya waliyo upande wa magharibi na wanafuturu kabla yao.

Wala haiwezekani mtu akasema kwamba kauli yake Allah (S.W. inayosema):"Sasa waingiliyeni (wake zenu) na tafuteni kile Allah alichokuandikiyeni, na kuleni na kunyweni mpaka ukubainikieni uzi mweupe kutokana na uzi mweusi wa alfajiri, kisha timizeni saumu hadi usiku." Na kauli yake (Mtume) s.a.w.:"Usiku ukitokeza kutoka hapa na mchana ukaondoka kutokea hapa na jua likatua, basi aliyefunga ameshafungua (au na-afungue)." (Haiwezekani mtu akasema kwamba Aya hio na Hadithi hii) kwamba ni za ujumla wa Wa islamu wote katika miji yote. Basi vivyo hivyo tunasema kuhusu ujumla wa kauli yake Allah (S.W.):﴿ فَمَن شَهِدَ مِنكُمُ الشَّهْرَ فَلْيَصُمْهُ (Atayeushuhudia mwezi miongoni mwenu na-aufunge).

Na kauli hii - kama unavyoona - ina nguvu yake kwa mujibu wa lafdhi (yake) na mtazamo sahihi na Qiyas sahihi vile vile: Qiyas cha wakati wa siku kwa (kuulinganisha) na wakati wa mwezi (month). Mwisho wa kunukuu.

Tatu : ni kuwa: kutokukiwahi kisimamo cha Arafa kwa baadhi ya Waislamu wa sehemu nyengine za dunia ni kitu cha lazima. Chukulia - kwa mfano - kuna nchi ambazo siku hio ya mwezi tisa, jua linatua Saudia kwao bado ni usiku au alfajiri ya siku hio hio. Ikiwa watafunga kwa munasaba wa Arafa, inakuwa Arafa haipo tena, labda wawe ni wenye kufata kauli ya wenye kujuzisha kusimama Arafa usiku ndio watakuwa nao wamefunga siku ya Arafa, lakini tatizo bado litabakia katika siku ya Idi.

Siku ya pili - tujaalie ni J/tatu - asubuhi watu wa miji ya Saudia wanasali Idi - wao kwao ni magharibi ya J/pili, na Idi haisaliwi magharibi. Hata wakifika asubuhi - J/tatu kwao - Makka tayari jua limetua, na kwa hivyo ni J/nne. Utaona kwamba mitazamo ya kiakili na hoja za kimaandiko zilizojengeka katika misingi imara ya kifani, inaonesha kwamba kufunga na kufungua - sawa ikiwa Ramadhani au Mwezi tisa mfunguo tatu - basi ni jambo linalofatana na miandamo ya mwezi. Na kilicho sahihi - kama tulivyobainisha - ni kuwa muandamo wa mbali usitendewe kazi mbali. Kwa hivyo, kufunga ni tarehe tisa, sawa imeafikiana na munasaba wa Arafa au haikuafikiana, na kwa kufata tarehe tisa watu wote wa dunia itawezekana kufunga na itawezekana kula Siku Kuu tarehe kumi. Ama tukifata munasaba wa kusimama Arafa, watu wa nchi nyengine hawatoweza kufunga kwani hakuna maafikiano ya wakati wa kufunga baina ya Makka na nchi zao, labda kwa wale wenye kufata kauli ya wenye kujuzisha kusimama Arafa usiku, lakini hata hivyo Idi wataikosa.

Ama tukirudi katika nadharia ya Sheikh Bachoo aliposema: " Ni vyema tuzingatie kwamba funga hii ya Arafa pamoja na Iddi yake ni vitu ambavyo havina mahusiano na kuandama mwezi kutokana na kila nchi inavyoona mwezi wake. Bali chanzo cha funga ya Arafa ni uhusiano wa ile siku ambayo mahujaji wanaposimama katika uwanja wa Arafa." Mwisho wa kunukuu. Tukirudi katika maelezo hayo tunakuta kuwa maelezo hayo yanaifanya ibada ya saumu ianzwe kabla ya kufika sababu yake, kwani Arafa inaanza tarehe tisa baada ya kutenguka jua Adhuhuri, wakati wafungaji huwa tayari wameshafunga tangu kabla ya Alfajiri. Jambo hili la kutangulia "Kilichosababishwa kabla ya kilichosababisha" halipo kamwe katika soko la elimu! Ilivyo ni kutangulia "Kilichosababisha kabla ya kilichosababishwa," kama unavyotangulia mtenguko wa jua au kuzama k wake (ambao ni sababu) halafu ndio ikafatia sala (ambacho ndicho kilichosababishwa).

Ama maneno ya Sheikh Nassor Bachoo aliposema: "Kwa uthibitisho zaidi wa funga ya siku ya Arafa tunajifunza kuwa Mtume (s.a.w.) alipotueleza umuhimu wa siku hii, na kila alipotaja siku hii ya Arafa alitumia neno 'siku' wala hakutumia neno 'tarehe'. Funga ya 'siku' ya Arafa." Mwisho wa kunukuu.

Tunasema kwamba: kuitwa siku hio kuwa ni siku ya Arafa na isiitwe siku ya mwezi tisa si hoja ya kuwa lazima tufunge sawa na Saudia, kwani mtegemezo huu ni kulitegemeza (neno hilo Arafa) kwa ajili ya kuitukuza ile ibada inayofanyika katika eneo hilo." Na hii ni kawaida ya Warabu kuyanasibisha majina ya siku kwa kuyapa majina ya sehemu ambazo kuna matokeo fulani adhimu yaliyotokea au yanatokea katika sehemu hizo. Siku ya vita vya Uhudi - kwa mfano - huiita Yawmu Uhud (Siku ya Uhudi), na Uhudi ni jina la sehemu. Halkadhalika vita vya Hunain: vinaitwa Yawmu H unain (Siku ya Hunain). Anasema Allah kuhusu vita hivyo: "Na siku ya Hunain wingi wenu ulipokupendezesheni." Na Hunain ni jina la mji. Halkadhalika vita vya Badr; Badr ni sehemu. Lakini tunaviita vita hiv yo "Yawmu Badri (Siku ya Badr). Anasema Sahaba Hassan bin Thabit, Mshairi wa Mtume(s.a.w.w):

Nyuso siku ya Badri zilimngojea Mwingi wa rehema alete ushindi. Tazama Sahaba Hassan: ameinasibisha siku hio kwa kuipa jina la sehemu ya Badr, kwa ajili ya utukufu wa yale yaliofanyika hapo. Kwa hivyo kunasibishwa siku ya Arafa na sehemu hio ya Arafa, si kwa sababu tufunge sawa sawa, bali ni kwa utukufu wa yale yanayotendeka. Na yanayotendeka hapo ni Munasaba wa kufunga si Sababu ya kufunga kama tulivyotangulia kubainisha. Na inampasa msomi - mwanachuoni na Talibu Al-ilm (mwanafunzi) - kutafautisha baina ya vitu viwili hivyo. Mwisho wa kunukuu nilioyasema katika kitabu.

JAWABU NILIOJIBIWA NI KAMA IFATAVYO

Baada ya kuyaeleza hayo nilioyaeleza, ndugu zangu walinijibu juu ya maudhui hio kama ifatavyo:

Funga Ya 'Arafah Neno 'Arafah au 'Arafah ni jina linalotokana na uwanja au viwanja maalum vilioko nje kidogo ya Mji Mtukufu wa Makkah. Mahujaji wote ambao wamehirimia kutekeleza Ibada ya Hijja hukusanyika katika viwanja hivyo. Jambo hilo la kwenda kusimama kwenye viwanja hivyo kwa kuomba dua na kumtaja Allaah ni katika nguzo kubwa ya ibada hiyo ya Hijja. Inampasa kila Hajji kusimama au kushiriki hata kwa muda mdogo katika mchana huo. Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amebainisha hayo kwa kusema:

(Hijja ni 'Arafah) Jambo hilo linathibitisha kwamba mtu yeyote asiyetekeleza ibada ya kusimama 'Arafah anapokuwa Makkah, atakuwa hakuipata ibada hiyo ya Hijja. Watu humiminika na kusimama kwenye uwanja wa 'Arafah siku ya tarehe 9 - Dhul-Hijjah ya kila mwaka. Ikumbukwe kwamba tarehe 9 hiyo ni ya huko Makkah pahala ambapo inafanyika ibada ya Hijja wala siyo ya pahala pengine popote duniani. Ni vyema kuzingatia kwamba funga hii ya 'Arafah pamoja na 'Iyd yake ni vitu ambavyo havina mahusiano na kuandama kwa mwezi kutokana na kila nchi inavyoona mwezi wake. Chanzo cha funga hii ya 'Arafah ni ule uhusiano wa ile siku ambayo Mahujjaji wanaposimama katika uwanja wa 'Arafah. Ambapo jambo la kusimama 'Arafah linapatikana sehemu moja tu ulimwenguni ambayo ni siku inayosadifu tarehe 9 - Dhul-Hijjah huko mji wa Makkah, sio tarehe 9 ya nchi nyengine yoyote ile.

Kwa maneno mengine ni kuwa tutakapotofautiana katika kufunga Siku ya 'Arafah na 'Iydul-Hajj itakuwa kama kwamba kila nchi ina uwanja wake wa 'Arafah na Makkah yake. Kwa uthibitisho zaidi wa funga ya siku ya 'Arafah tunajifunza kuwa Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kila alipokuwa akieleza umuhimu wa siku hii alitumia neno "siku" wala hakutamka neno "tarehe." Ama kwa mujibu wa maelezo ya ndugu yetu Juma, kama kawaida yake yeye anaona kuitwa "Siku ya 'Arafah" haina maana kuwa lazima tufunge sawa na Saudia, bali anaona kuwa hiyo ni "Idhaafatu-Tashriif" (yaani kuitengeneza siku hiyo kwa ajili ya utukufu wa pahala hapo au kwa ajili ya utukufu wa tokeo lenyewe). Sisi kwa upande wetu tunamuuliza ndugu Juma, Je yapo maandiko yoyote ya kilugha au ya kisheria yanayotufunza kuwa pahala pakitumika "Idhaafatu-Tashriif" huwa haparuhusiki tena kutoa mafunzo mengine yaliyomo ndani ya "idhaafa" hiyo? Tujuavyo sisi zipo Aya nyingi za Qur-aan ambazo zimetumika ndani yake hiyo "Idhaafatu-Tashriif" lakini utakuta wanavyuoni wa tafsiri wametoa mafunzo mengine yapatikanayo katika "idhaafa" hizo.

Akaendelea ndugu Juma kutoa kikwazo ambacho anaona kuwa haiwezekani kufunga siku ya 'Arafah sawa na tokeo lenyewe huko Makkah kwa kisingizio cha kuwa kuna nchi zinazotofautiana kwa masaa mengi. Kisha akasema: (Na (kama) inavyojulikana kwamba tafauti za kisiku zina athari zake kwa makubaliano ya Waislamu. Waliyo upande wa mashariki, hakika wao wanaanza kufunga kabla ya waliyo upande wa magharibi na wanafuturu kabla yao). Kama ni hivyo tofauti ni nchi zilizo Magharibi kwa nchi zilizo za Mashariki zinatofautiana, sisi tunamuuliza ndugu Juma vipi tena kwa nchi zilizo jirani kama vile Omani na Dubai , au Omani ya Yemeni, Je! Kuna suala la Mashariki na Magharibi hapa? Au kama ni hivyo basi mbona Juma hakubali uwezekano wa kufunga pamoja nchi zote za Mashariki kwa wakati mmoja na zote za Magharibi kwa wakati mwengine?

JAWABU

Kwanza Kimsingi ni kuwa hamukujibu hoja zangu moja moja kama nilivyoeleza mimi. Mukhtasari wa nilioyaeleza ni kuwa:

a) Ibada za Hija zina Sababu yake.

b) Hadithi imeonesha kuwa sababu ya ibada hizo ni muandamo wa mwezi wa mfunguo tatu. Hadithi imesema: "Alituusia Mjumbe wa Allah - rehema na amani ziwe juu yake - tuabudu kwa kuuona, kama hatukuuona na wakashuhudia mashahidi wawili waadilifu, tuabudu kwa (kufata) ushahidi wao."

Tumesema katika kitabu kwamba neno Nansuk (tuabudu) wengine wameifasiri ibada hii kuwa ni ibada ya hija nayo ndio tafsiri yenye muelekeo madhubuti zaidi, kwani neno hili hutumika sana kwa maana ya ibada ya hija, kama Allah (S.W.) anavyosema kuhusu ibada ya hij a: Mukimaliza Nusuki (ibada) zenu (za hija). Na kwa hivyo imekuja katika "Awnu Al-Ma'abudi: Sharhu Sunani Abi Daud kuhusu maana ya Hadithi hio tulioinukuu hapo juu kuwa maana yake inahusiana na ibada za hija. Anasema mwenye kusherehesha: "Na maana yake ni: 'Tuhiji kwa kuuona (mwezi), yaani mwezi muandamo wa mfunguo tatu." Ni wazi kwa maelezo haya au kwa mujibu wa Hadithi hii kwamba sababu ya ibada za hija - ikiwemo funga ya Arafa - ni kuandama kwa mwezi wa mfunguo tatu.

c) Kwa hivyo, kwa mujibu wa Hadithi hii, sababu ya kuingia ibada ya hijja -funga yake ya mwezi 9 na idi yake mwezi 10, ni muandamo wa mwezi wa mfunguo tatu. Ama kisimamo cha Arafa nimejibu kwamba haiwezekani kuwa ndio sababu ya kufunga kwani, kisimamo kinakuwa baada ya kutenguka jua adhuhuri, wakati wafungaji wameshafunga tangu alfajiri, na sababu hutangulia kwanza kisha ndio kikaja kilichosababishwa; yaani kwa lugha nyengine sababu ya ibada huwa haitanguliwi na ibada yenyewe; bali kwanza hutangulia sababu kisha ndio ikaja ibada ambayo ndio iliosababishwa.

Kwa hivyo, ikiwa sababu ya ibada za hija kikiwemo kisimamo cha Arafa na funga yake ni muandamo wa mfunguo tatu, basi sisi tupo pale pale kwamba Hadithi sahihi ya Ibn Abbaas na Kuraib imethibisha kwamba muandamo wa mbali hautendewi kazi mbali. Kwa hali hii, sisi Afrika Mashariki, na kwangine, hatuwezi kufunga kwa kufata mwezi tisa wa Saudia, kwani muandamo kila mtu ana wake; wala hatuwezi kufanya hivyo kwa kufata kisimamo cha Arafa kwani kisimamo cha Arafa sio sababu ya ibada za Hijja kikiwemo kifungo hicho; bali muandamo wa mwezi ndio sababu kama Hadithi ilivyosema.

MNASEMA

Ndugu Juma ni vyema aelewe kwamba upo uwezekano wa kufunga 'Arafah siku moja dunia nzima kama tulivyoelezea katika kurasa za nyuma za kitabu hichi kwamba dunia nzima inashirikiana katika mchana mmoja na inashirikiana katika usiku mmoja ingawaje kuna nchi zinazotanguliza na nyengine zinazofuatia. Mfano nchi zote za Afrika zinaweza kushirikiana kufunga siku moja kwani baadhi ya nchi za Afrika zinatofuatiana kwa masaa machache tu sio usiku mzima wala mchana mzima. Katika kitabu cha Shaykh Naaswir Bachuu imeandikwa kwamba tofauti iliyopo kwa nchi za Kiislamu zilizo Mashariki ya mbali kama Phillipines na Indonesia na zile zilizo Magharibi ya mbali kama Al-Maghrib yaani Morocco ni tofauti ya masaa 9 tu. Kwa hivyo upo uwezekano wa kitaalamu (Kijiografia) wa kuweza kufunga kwa pamoja katika siku hiyo hiyo moja. Tofauti iliyopo ni ya masaa tu. Tunafunga siku moja sio wakati mmoja wala sio dakika moja. Msisitizo upo katika kufunga siku moja sio kuanza wakati mmoja.

JAWABU

Ama kudai kwamba uko uwezekano wa kufunga Arafa duniani kote siku moja, hilo si da sahihi. Nimekupeni mfano wa mimi mwenye mwezi wa 5 na wa 6 2009 nilikuwa Hong Kong, nikampigia simu ndugu yangu aliye Marekani nikamuuliza ni saa ngapi huko kwenu akanijibu ni saa kumi jioni; wakati huo Hong Kong tumeshali Alfajiri tushatoka Msikiti baina ya saa 11 na nusu mpaka 12 au 12 kasoro kidogo. Tazama tafauti iliokuwepo hapo. Hii ina maana jua likitua U.S.A jioni baada ya masaa mawili, labda na nusu, Hong Kong watu wanaingia makazini asubuhi kweupe na jua liko juu. Utaona kwamba, Kiislamu, ikiingia Ijumaa Hong Kong, Marekani bado ni Alkhamisi. Waislamu walioko Hong Kong wakifunga Arafa mchana wa tarehe 9, Marekani bado ni usiku hawawezi kufunga; Waislamu wa Hong Kong wakifuturu jioni, Marekani ni wakati wa mwisho mwisho wa alfajiri au ni asubuhi. Kwa ufupi ni kuwa baadhi ya States za Amerika na Hong Kong, tafauti haipungui masaa kumi na mbili.

Kwa hivyo, dai hilo si sahihi. Na hapa inabainika kwamba kauli sahihi ni ya kufata tarehe 9 mfunguo tatu kwa mujibu wa muandamo wan chi zetu, kwani tukifanya hivyo Waislamu wote duniani wataweza kufunga tarehe 9 na kula siku kuu tarehe 10. Ama tukifata muandamo mmoja hilo halitowezekana kwani mchana wa mwezi 10 wa nchi moja, tuseme hio Hong Kong, ni usiku katika nchi nyengine tuseme hio Marekani; jua likitua Hong Kong itakuwa tayari Kisharia ni mwezi 11, wakati Marekani ndio kwanza wajitayarisha kwenda kusali idi bado kwao ni mwezi 10. Utaona Al-Nadhar, Athar na migawanyiko ya kijografia, yanatoa jawabu sawa kwamba kilicho sahihi ni kila watu kufata muandamo wao.

Ama baadhi ya nchi kama mulivyosema - Za Africa kwa mfano - sipingi kwamba kuna uwezekano, ninachopinga ni kuwa dalili ni tafauti na kitendo hicho. Kama Ibn Abbas kakataa kuchukua muandamo wa Sham wala tafauti baina yake na Madina haifiki masaa hayo ya masaa 9 na akatoa hoja kwamba "Hivi ndivyo alivyotufunza Mtume s.a.w.", basi vipi itawezekana Kisharia kwamba watu wa Africa nzima wafunge sawa sawa.

MNASEMA

Ndugu Juma anasema: (Utapolifahamu hili, utakuwa umefahamu kwamba, siku ya kufunga ni tarehe tisa mfunguo tatu, sawa siku hio imeafikiana na Arafa au imetafautiana,....) [uk. 141]

JAWABU

Nyinyi ndugu zangu munanukuu maneno "Utapolifahamu hili..?" Bila ya ku nukuu maelezo yenyewe yalionipelekea kusema "Utapolifahamu hili". Sasa msomaji atafahamu nini? Huu sio mjadala wa kielimu wenye lengo la kutafuta natija sahihi. Ilikuwa munukuu jawhari ya maneno yangu kasha ndio muyajibu.

MNASEM

a) Sisi tunamjibu kwamba: Sasa kama anaruhusu kutafautiana, tena kwanini imeitwa (Funga ya 'Arafah) isiitwe "Funga ya tarehe 9"? Kisha ndugu Juma anaamini kwamba: (Arafa ni tokeo ambalo linatokea Makka tu, wakati Ramadhani ni tokeo la dunia nzima.) Kama kawaida yake ndugu Juma anajikanganya kila mara, kama kweli anaamini kila nchi ifunge kwa muandamo wake na 'Arafah, kila nchi ifunge kivyake, inakuaje tena Ramadhaan iwe ni ya dunia nzima, 'Arafah iwe kila mtu na yake?

JAWABU

Ama kwanini imeitwa (Funga ya 'Arafah) isiitwe "Funga ya tarehe 9", nimeshakuelezeeni kwa urefu katika Kitabu. Nimesema: Tunasema kwamba: kuitwa siku hio kuwa ni siku ya Arafa na isiitwe siku ya mwezi tisa si hoja ya kuwa lazima tufunge sawa na Saudia, kwani mtegemezo huu ni kuli tegemeza (neno hilo Arafa) kwa ajili ya kuitukuza ile ibada inayofanyika katika eneo hilo." Na hii ni kawaida ya Warabu kuyanasibisha majina ya siku kwa kuyapa majina ya sehemu ambazo kuna matokeo fulani adhimu yaliyotokea au yanatokea katika sehemu hizo. Siku ya vita vya Uhudi - kwa mfano - huiita Yawmu Uhud (Siku ya Uhudi), na Uhudi ni jina la sehemu. Halkadhalika vita vya Hunain: vinaitwa Yawmu Hunain (Siku ya Hunain). Anasema Allah kuhusu vita hivyo: Na siku ya Hunain wingi wenu ulipokupendezesheni." Na Hunain ni jina la mji. Halkadhalika vita vya Badr; Badr ni sehemu. Lakini tunaviita vita hivyo "Yawmu Badri (Siku ya Badr). Anasema Sahaba Hassan bin Thabit, Mshairi wa Mtume(s.a.w.w) :

Nyuso siku ya Badri zilimngojea Mwingi wa rehema alete ushindi. Tazama Sahaba Hassan: ameinasibisha siku hio kwa kuipa jina la sehemu ya Badr, kwa ajil i ya utukufu wa yale yaliofanyika hapo. Kwa hivyo kunasibishwa siku ya Arafa na sehemu hio ya Arafa, si kwa sababu tufunge sawa sawa, bali ni kwa utukufu wa yale yanayotendeka. Na yanayotendeka hapo ni Munasaba wa kufunga si Sababu ya kufunga kama tulivyotangulia kubainisha. Na inampasa msomi - mwanachuoni na Talibu Al-ilm (mwanafunzi) - kutafautisha baina ya vitu viwili hivyo.

Ama kauli yenu: "Kama kawaida yake ndugu Juma anajikanganya kila mara, kama kweli anaamini kila nchi ifunge kwa muandamo wake na 'Arafah, kila nchi ifunge kivyake, inakuaje tena Ramadhaan iwe ni ya dunia nzima, 'Arafah iwe kila mtu na yake?" Mwisho wa kunukuu. Ninasema: hata hili pia nalo munalifanya kuwa ni hoja ya kielimu!!! Zote mbili - Ramadhani na Arafa - ni za dunia nzima, tafauti ni katika kuingia nyakati zake. Ramadhani ni refu Waislamu ni lazima watakutana kwani hakuna tafauti ya muandamo wa mwezi mzima; kuna tafauti ya siku moja mbili, Arafa ni tokeo la siku moja, inapotafautiana miandamo hupelekea kutafautiana kwa tarehe za kufunga na kula siku kuu.

MNASEMA

Hebu tuangalie hoja nyengine ya ndugu Juma katika uk 142 wa kitabu chake anapodai kunukuu maneno ya Shaykh Al-'Uthayminiy, anaposema: ("Na wakati wa mwezi ni kama wakati wa siku Kama vile ambavyo miji inatafautiana katika kuanza kujizuia (na kula na kunywa na jimai: yaani kuanza kufunga) na (inavyotafautiana katika) kufuturu kwa siku (daily) basi vivyo hivyo inawapasa watafautiane katika kujiz uia na kufuturu kwa mwezi (monthly)

a) Suala linakuja: Je! Kama anavyosema miji inatafautiana kufuturu kwa mwezi kama inavyotafautiana kwa siku. Sasa vipi katika nchi moja iliyo kubwa kama Tanzania ambayo ina mikoa inayotafautiana kuanza k ula na kunywa kama Dar es Salaam na Kigoma? Je! Mbona haitafautiani kwa mwezi? Inafunga kwa muandamo mmoja lakini Dar es Salaam na Kigoma zinatafautiana katika kuanza kula na kunywa (kufuturu) kwa zaidi ya dakika 45?

JAWABU

Hatuzungumzii watu wanatenda nini; tunazungumzia nini kinatakiwa Kisharia kitendwe. Watu wa Kigoma ikiwa muandamo kwao ni tafauti na Dar-es-Salam, basi ilivyo ni kuwa wafunge kwa mujibu wa Muandamo wao kama wanavyosali kwa mujibu wa mtenguko wao na kufuturu kwa mujibu wa kuzama jua kwao. Kinachotazamwa si tangazo au amri ya serikali, bali ni muandamo wa mwezi. Na hili - kama munavyojua - ni jambo ambalo wanavyuoni wamelizungumzia na wako walioeleza kama hivyo. Nchi kama Urusi, hasa kabla ya kugawanyika, vipi utamwambia mtu wa State moja ya mbali na iliotafauti kabisa na State nyengine kwamba wafunge sawa. Kinachozinagatiwa si suala la nchi moja bali ni umbali na tafati za matalai.

Pamoja na hayo, kama nilivyokuelezeni mara nyingi kwamba, suala la umbali gani watu wafunge sawa, linabakia kuwa ni uwanja wa ijtihad kwa kutokuwepo andiko lenye kuonesha umbali gani; ingawa andiko limeonesha kwamba muandamo wa mbali si hoja kwa walio mbali, kilichojificha ni umbali gani. Kwa hivyo, ukweli kwamba muandamo wa mbali si hoja kwa waliombali hili ni andiko ambalo lazima tusallim amri mbele yake; na je umabali huo uwe kiasi gani; hapa wenye elimu wana uwanja mpana wa kujitahidi na kutoa fat-wa na sisi tutatazama ilio na nguvu. Kwa hivyo, ikiwa watu wa Kigoma wamechukua ijtihad ya wanavyuoni wetu wakubwa waliotangulia wa Africa Mashariki, hilo linatoa nafasi kwani hapa uwanja wa ijtihad upo. Ama kutwambia kuwa dunia nzima tuwe na muandamo mmoja: hili ni kinyume na andiko na ni kinyume na maumbile yenyewe ya dunia.

MNASEMA

b) Kwa nini basi nchi kama Omani na Dubai zinatafautishwa katika kuangalia mwezi wakati ambapo nchi hizo hazina tofauti kubwa katika kuanza kula na kunywa? Wala hazina tofauti ya matlai wala masaa ya kuanza na kuingia kwa siku?

JAWABU

Imarati ni maamuzi ya serekali zao kufata Saudia; nalo ni kosa kwani wao na Oman ndio walio karibu zaidi na wana matalai sawa. Na nimekwambieni kuwa mjadala wetu si watu wanafanya nini: bali nini kinatakiwa kitedwe Kisharia. Vyenginevyo na mwengine anaweza kukuulizeni mbona Suudia wanafata muandamo wao; mbona Misr wanafata muandamo wao, n.k. Kwa hivyo, tuko pale pale kwamba hatuzungumzii nini watu wanafanya; bali tunazungumzia nini kinatakiwa kifanywe Kisharia.

MNASEMA

c) Tujuavyo sisi nchi zote za Uarabuni zinapata usiku wao mmoja na mchana wao mmoja, kwa hivyo hakuna shida yoyote katika kufunga 'Arafah siku moja kwa wote.

JAWABU

Sijakwambieni kuwa haiwezekani; nimesema kwamba ushihidi tulio nao ni kuwa:

1) Ibada za Hijja ikiwemo funga hio ya Arafa inategemea muandamo wa mwezi: si kisimamo cha Arafa. Kisimamo cha Arafa ni munasaba na muandamo wa mwezi ndio sababu ya ibada hizo.

2) Muandamo wa mbali si hoja kwa walio mbali.

MNASEMA

Shaykh Naaswir Khamiis 'Abdur-Rahmaan wa Mombasa Kenya ameandika kitabu chake "Mwezi Ko-Ongo" na amethibitisha tofauti ya masaa baina ya nchi mbali mbali mfano: "tofauti ya mji wa Mombasa na nchi ya magharibi ya mbali mwa Afrika kama Algeria ni masaa mawili na dakika ishirini na nane (2:28)" - uk 22. Katika jambo la kuonesha ufinyu aliokuwanao ndugu yetu Juma, ule wa kutokufanya uchunguzi wa kina katika mas-ala haya, yeye anaamini kwamba jambo hili limeanzishwa na Shaykh Naaswir Bachuu na wala halikuwepo ulimwenguni kama anavyodai mwenyewe kwa kauli yake ifuatayo: (Ninasema: Enyi walimwengu wenzangu tazameni hoja za kielimu hizo!!!!!!! Kwani nyinyi Wazanzibari kabla ya kuja fikra hio ya Sheikh Nassor Bachoo ya kufunga kwa muandamo mmoja)

JAWABU

Jambo gani hilo ambalo nimedai kuzushwa na Sheikh Nassor Bachoo? Hebu ninukulieni hilo jambo. Fikra ninayosema kuwa kaja nayo Sheikh Nassor Bachoo Zanzibar ni fikra ya kututaka tufunge kwa muandamo mmoja. Kwa Zanzibar yeye ndiye aliyeitangaza, kuilingania na kuitungia kitabu. Wala sikusema kuwa katika dunia yeye ndiye muasisi wa fikra hio. Ama yale mulioyanukuu kutoka kwa Sheikh Nassor Khamis, sio yalionifanya mimi nikapigwa na mshangao huo: ((Ninasema: Enyi walimwengu wenzangu tazameni hoja za kielimu hizo!!!!!!! Kwani nyinyi Wazanzibari kabla ya kuja fikra hio ya Sheikh Nassor Bachoo ya kufunga kwa muandamo mmoja). Kwa hivyo, musichanganye mambo. Mimi nilishagaa hivyo kwa sababu ya maneno haya ya Sheikh Nassor. Alisema Sheikh Nassor: "Pili kama ingalikuwa hakuna dhana ya kuwa mwezi ukionekana popote watu wafunge, Ibnu Abbas (r.a.) asingekuwa na haja ya kumuuuliza Kurayb juu ya habari za mwezi wa Sham kwa kusema:

"Kis ha (Ibn Abbas) akataja (habari) ya mwezi na akasema: "Ni lini mliuona mwezi?...akasema: "Wewe umeuona?" Hapo ndio nikashanga na nikasema: Hio ndio hoja nyengine ya Sheikh Bachoo, kwamba lau hakuna dhana ya kuwa mwezi ukionekana popote watu wafunge, basi Ibn Abbas asingekuwa na haja ya kumuuliza Kuraib "Lini mumeuona mwezi!!!" Ninasema: Enyi walimwengu wenzangu tazameni hoja za kielimu hizo!!!!!!! Kwani nyinyi Wazanzibari kabla ya kuja fikra hio ya Sheikh Nassor Bachoo ya kufunga kwa muandamo mmoja, mulikuwa hamuwaulizi watu wanaotoka nchi nyengine masuala kama hayo wanapokuja kwenu na nyinyi muko kati kati ya mwezi pamoja na kwamba nyote zamani mukifata muandamo wenu? Sasa kama nyinyi mulikuwa mukiuliza suala hilo hilo kwanini Ibn Abbas na yeye asiulize hata kama dhana hio haipo? Mimi binafsi nina kawaida ya kuwauliza wageni walioko nchi hii ninayoishi suala hilo, na natarajia kwamba pia nimewasikia watu wengi wenye kuwauliza wageni suala hilo. Kwa hakika shubuhati kama hizi hazifai katika kujadili mambo ya kielimu. Kwa ufupi ni kuwa hata kama dhana hio ilikuwepo, dhana hio inabomolewa na kukataa kwake - Ibn Abbas - kuukubali mwezi wa Sham, na kujenga hoja kwa Hadith marfu'u kwamba hayo ndio mafunzo ya Mtume(s.a.w.w) kwao. Sasa uko wapi uhusiano wa maneno yangu na nakala ya Sheikh Nassor Khamis?

MNASEMA

Sasa sisi tunataka kumtihibitishia ndugu Juma kuwa wapo watu wengi ambao pengine hawakuwafikiana na Shaykh Naaswir Bachuu katika baadhi ya mambo au misimamo lakini kwa bakhti nzuri katika hili suala la kufunga 'Arafah na kusali siku ya 'Iydul-Adh-ha wanafuata Makkah na wanaungana na ulimwengu mzima. Mfano mzuri kabisa ni ndugu zetu wa Tarika ya Kadiria, takriban wote wanafunga 'Arafah kwa kufuata tarehe 9 - Dhul-hijjah ya Saudia (Makkah). Hayo yanathibitishwa na aliyekuwa kiongozi wao Mkuu wa Tarika hiyo mwanachuoni maarufu Al-Marhuum Shaykh Muhammad Naaswir Abdulla Al-Qaadiry ambaye aliandika kitabu alichokiita: "Kitabu 'Arafah" na kuandika kwenye gamba la kitabu hicho kwamba: "Nguzo Kubwa Ya Hijjah Ni 'Arafah Tarehe Tisa Mfunguo Tatu Na Kuswali 'Iydul-Hajj Sawa Na Makkah." Katika uk 22 wa kitabu chake hicho pia ameandika kama ifuatavyo: "Waislamu wote ulimwenguni wafunge Sunnah ya 'Arafah sawa na 'Arafah ya Makkah."

Kisha katika uk 74 ameandika Fatwa zifuatazo: "'Arafah ya Makkah tarehe 9 mwezi wa Mfunguo Tatu (Dhul-Hajj) ndiyo 'Arafah ya Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Ta'ala) na ndiyo 'Arafah ya Waislamu wote popote walipo ulimwenguni." "Wananaokwenda Hijja, kwao ni haramu kufunga siku hiyo ya 'Arafah huko 'Arafaati (Makkah) na waliobaki majumbani, kwao ni Sunnah kubwa kufunga siku hiyo hiyo ya 'Arafah ya Makkah kokote waliko ulimwenguni." "Tarehe 10 Mfunguo Tatu (Dhul-Hajj) ndiyo siku ya 'Iyd ya Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Ta'ala) na 'Iyd ya dunia nzima kwa Waislamu wote. Kufunga siku hiyo yote kamili ni haramu. Anayeswali 'Iyd tarehe 10 ya Makkah amefanikiwa na ole wake yule anayeswali 'Iyd siku atakayo mwenyewe. Kwa ujumla kufunga tarehe 9 Mfunguo Tatu kwa Mahujaji 'Arafah ni Haramu. Na kufunga kwa Waislamu wote ulimwenguni tarehe 10, 11, 12 na 13 Mfunguo Tatu ni Haramu."

"Hivyo ni jambo baya kabisa na lenye kutia huzuni sana kuwaona baadhi ya ndugu zetu Waislamu wanaacha kufunga siku ya 'Arafah Aliyoiteua Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Ta'ala) na badala yake wanafunga siku ya kuchinja tarehe 10 (ya Makkah) wakisingizia kuwa ndiyo siku yao ya 'Arafah waitakayo wao waliyoichagua wao wenyewe ambayo kufunga siku hiyo ni haramu."

JAWABU

Haya! Hoja iko wapi humu! Je hii ni hoja kwamba alivyosema Sheikh Muhammad Nassor ni sahihi au ni hoja kwamba kuna watu wanaafikiana na nyinyi katika hilo? Ikiwa ndio munatoa hoja kwamba alivyosema Sheikh Muhammad Nassor ni sahihi; nitakutakeni dalili ya usahihi huo; ikiwa munatoa hoja kwamba kuna watu wanaafikiana na nyinyi katika hilo; hapo sikupingini. Lakini suala letu bado lipo: 1) Nini sababu ya kufunga Arafa.

2) Je sababu ni kisimamo cha Arafa.

3) Je ni muandamo wa mwezi wa mfunguo tatu.

4) Je tufate muandamo mmoja au kila mtu wake.

Mimi ushahidi nilio nao ni kuwa:

1) Sababu ya kufunga Arafa ni muandamo wa mfunguo tatu, kama ilivyonena Hadithi ya Amir wa Makka.

2) Kisimamo cha Arafa si sababu kwani sababu hutangulia kisha ndio kikija kilichosababishwa. Kama linavyotenguka jua ndio ukaingia wajibu wa kusali; au unavyoingia mwezi wa Ramadhani ndio ukaja wajibu wa Ramadhani. Ama kisimamo cha Arafa kinaanza baada ya kutenguka jua wakati wenye kufunga wanaanza kufunga tangu Alfajiri. Kwa hivyo, kisimamo cha Arafa ni munasaba ni sababu.

3) Kila watu wafate muandamo wao kwa mujibu wa Hadithi ya Ibn Abbas na Kuraib.

12

MUANDAMO WA MWEZI

SEHEMU YA KUMI NA MBILI

KUANDAMA KWA MWEZI KATIKA SEHEMU MOJA KUNATOSHELEZA KUANDAMA KWAKE DUNIA NZIMA

MNASEMA

12. Kuandama Kwa Mwezi Katika Sehemu Moja Kunatosheleza Kuandama Kwake Dunia Nzima Katika maelezo yaliyopita tumeeleza kwamba Hadiyth zote za Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) zilizotaja amri hii ya kufunga na kufungua ni Sahihi na ni zenye kukubalika mbele ya Wanavyuoni wala hazina khitilafu yoyote juu ya usahihi wake. Hadiyth zote hizo zimetaja amri hii ya hukumu ya kufunga na kufungua kwa ujumla - yaani ni jambo linalotekelezeka kwa watu wote katika siku moja. Wala agizo hilo halihusishi nchi fulani pasi na nchi nyengine. Ni agizo la ujumla 'aam.

Pia ni wazi kwamba agizo hilo la Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) halikutaja suala la kuwepo kwa matlai wala masafa gani, wala chengine chochote. Wala hakuna katika maelezo sahihi ya Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ambayo yanakubalika na Wanavyuoni yaliyotaja kwamba 'kila nchi ifunge na ifungue kwa miandamo yao!' Kama ilivyoelezwa kwamba hoja inayotegemewa na baadhi ya Wanavyuoni wachache juu ya mas-ala haya ni kisa cha masimulizi ya Kuraib, masimulizi ambayo hayana ufafanuzi wa kina kama walivyoeleza hayo baadhi ya Wanavyuoni wengine na kuonyesha kuwa yana utatanishi (ihtimaalati). Jambo ambalo linaifanya hoja yake kuwa dhaifu. Kama yalivyoelezwa hayo na Wanazuoni wa fani ya "Usulul-Fiqhi."

JAWABU

Inaonesha tunaendelea kukariri yayo kwa yayo katika kila sura. Kudai kwamba Hadithi zote ni agizo la ujumla 'aam, ni kweli hilo ni agizo la ujumla lakini je ujumla huo uko mahala gani katika Hadithi hizo. Ujumla upo katika wenye kuamrishwa kwamba "Fngeni kwa kuuona". Kwa hivyo, ujumla unaopatikana ni kuwa watu wote wafunge kwa kuuona. Tumesema kwamba Lamu iliomo katika neno (Liru-uyatihi) inaitwa Harfu Jarri li-tta'alil. Yaani ni harufu yenye kulitia neno kasra na kuonesha sababu ya maneno yaliotangulia au sababu ya hukumu iliotajwa. Kwa hivyo, maana ya haya ni kuwa kuuona mwezi iwe ndio sababu ya kufunga au kwa lugha nyengine sababu ya kufunga iwe ni kuuona mwezi. Hii ndio maana ya maneno:"Fungeni kwa kuuona:" hakuna hapa kinachoonesha mas-ala ya kufunga kwa muandamo mmoja wala zaid i ya mmoja. Yaani ujumla hauambatani na sehemu bali unaambatana na walioamrishwa kwamba watu wote wafunge kwa kuuona: sio watu wote wafunge sawa. Ujumla huo ni sawa na ujumla uliomo katika Aya:"Simamisha sala kwa kutenguka jua" , na ujumla uliomo katika Hadithi isemayo:Usiku ukitokeza kutoka hapa na mchana ukaondoka kutokea hapa na jua likatua, basi aliyefunga ameshafungua (au na-afungue). Wala haina maana kuwa watu wa nchi moja wasali kwa kutenguka jua nchi nyengine, na wala haina maana kwamba usiku wa nchi moja ukiingia watu wa nchi nyengi wafuturu. Bali ujumla uliomo katika Aya ni kuwa watu wote wasali kwa kutenguka jua; na ujmla ulio katika Hadithi ni kuwa watu wote wafuturu kwa kuingia usiku: hakuna ndani ya maandiko haya mas-ala ya ujmla wa sehemu: ni ujumla wa wanaomrishwa.

Ama kauli yenu: "Pia ni wazi kwamba agizo hilo la Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) halikutaja suala la kuwepo kwa matlai wala masafa gani, wala chengine chochote" pia haikujengeka katika misingi ya kielimu. Wanavyuoni inapotajwa hukumu huwa wanaitafuta illa (sababu) ya hukumu hio. Ikiwa sababu imetajwa kwa uwazi, basi ni hivyo: hio ndio maslak njia yake; ikiwa haikutajwa basi huwa wanaitafuta kwa njia tafauti Masalik 'illa njia za kutafuta sababu. Kisha wakiipata ndio huifanyia Qiasi baina yake na baina ya kitu ambacho hukumu yake ha ikutajwa. Kwa hivyo, baada ya kuzikusanya sifa zote zenye kufaa kuwa sababu ya kwanini Mtume(s.a.w.w) akaamuru hivyo, tunapata sababu mbili kama nilivyoeleza katika kitabu, kwamba:

Moja ni kuwa: iwe hivyo ndivyo walivyoamrishwa na Mtume(s.a.w.w) kutokuuchukua mwezi wa Sham, kwa sababu huko ni Sham. Kwa hivyo, Sham iwe ndio illa (sababu) ya kutokuuzingatia muandamo. Hii inamaanisha kwamba lau Kuraib alikuwa anatoka Misri au Pemba wangeukubali muandamo huo. Illa (sababu) hii ni dhaifu, haifai kuifanya kuwa ndio illa (sababu) ya hukumu hio ya Mtume(s.a.w.w) iliomo katika Hadithi ya Kuraib na Ibn Abbas. Kwani:

a) Ni (It is an intrasitive cause as opposed to a transitive one). Yaani ni sababu ambayo hai vuuki mahala pake, nayo inapingwa na sababu nyengine yenye kuvuuka mahala pake.

b) Ni "Kulifanya jina kuwa ndio sababu." Na inavyotakiwa sifa iwe ndio sababu: sio jina. Naam! Jina linaweza wakati mwengine kufanywa illa (sababu) ikiwa lina maana ya sifa. Katika jina "Sham" maana hii haipo. Pili ni kuwa: iwe Mtume(s.a.w.w) kawaamrisha hivyo kwa sababu Sham ni mbali. Illa (sababu) hii, ni sahihi na imekamilisha masharti ya utoaji wa illa (sababu).

Kwa hivyo, natija ni kuwa Mtume(s.a.w.w) kawaamrisha hivyo kwa sababu Sham ni mbali, sio kwa Sababu kule ni Sham. Tafauti za matlai, kwa sababu ya umbali au kwa sababu za kijografia, ni katika mambo yanayothibiti kwa njia ya Qias. Na Qias, nijuavyo, kwa Sunni, Ibadhi na Jumhur kwa ujumla ni dalili katika dalili za Kisharia. Kwa hivyo, kusema: "Pia ni wazi kwamba agizo hilo la Mtume(Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) halikutaja suala la kuwepo kwa matlai wala masafa gani, wala chengine chochote" hakukujengeka katika misingi ya elimu, kwani elimu haiangalii nassun (andiko) tu; bali inaangalia andiko na Qias pia. Ama kauli yenu: "Wala hakuna katika maelezo sahihi ya Mtume(Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ambayo yanakubalika na Wanavyuoni yaliyotaja kwamba 'kila nchi ifunge na ifungue kwa miandamo yao" si kauli sahihi. Kwani ikiwa munataka Hadithi iseme "Jamani kila nchi na muandamo wao" basi riwaya yenye lafdhi hii haipo. Ama riwaya yenye maana hii ipo nayo ni riwaya ya Kuraib na Ibn Abbaas, nayo ni Hadithun Marf'u'u kwa mujibu wa lafdhi yake.

Pili ni kuwa kama vile ambavyo hakuna Hadithi ambayo lafdhi yake inasema: "Jamani kila nchi na muandamo wao" pia hakuna Hadithi yenye kusema "Jamani fungeni kwa muandamo mmoja". Kwa hivyo, suala hili linarejeshwa katika dalili zake nyengine kwa mujibu wa fani zinavyoeleza. Na tumeona kwamba Ibn Abbaas kaukataa muandamo wa Sham na akasema "Hivi ndivyo alivyotufunza Mtume(s.a.w.w) ". Kwa hivyo, mafunzo ya Mtume(s.a.w.w) , ni kutokuuzingatia mwezi wa mbali.

Ama kauli yenu: "Kama ilivyoelezwa kwamba hoja inayotegemewa na baadhi ya Wanavyuoni wachache juu ya mas-ala haya ni kisa cha masimulizi ya Kuraib, masimulizi ambayo hayana ufafanuzi wa kina kama walivyoeleza hayo baadhi ya Wanavyuoni wengine na kuonyesha kuwa yana utatanishi (ihtimaalati)" pia si kauli sahihi. Kwanza walioizingatia Hadithi ya Kuraib ndio Jumhur kama tunavyoshuhudia leo practically (kimatendo) kwamba asilimia kubwa ya Waislamu wa madhehebu mbali mbali duniani wanafata msimamo huu. Pili ni kuwa usahihi na udhaifu haupimwi kwa wingi na uchache hata kama ilikuwa munavyodai nyinyi ndio kweli kauli ya Jumhur; bali kipimo ni dalili za Kisharia. Ama kudai kuwa masimulizi ya Kuraib hayana ufafanuzi, sijui munataka ufafanuzi gani. Riwaya imeshaeleza kwa uwazi kwamba Ibn Abbaas kaukataa muandamo wa Sham na akasema kuwa hivyo ndivyo Mtume(s.a.w.w) alivyowaamuru, bado munasema kuwa haina ufafanuzi?! Ni wazi kwamba hamutaki wala sidhanii kuwa mumekuwa musiofahamu kiasi hicho hata ikawa hamuifahamu Hadithi hii.

Ama dai kwamba masimulizi hayo yana utatanishi (ihtimaalati), tumeshayajibu sana na sijui ni utatanishi (ihtimaalati) gani munaoukusudia. Ibn Al-Qayyim katika nakala mulizomnukuu kwa kughushi na Al-Suyuti katika nakala mulioibutua kipande wamesema: Kauli yake (Ibn Abbaas aliposema): 'Hivi ndivyo alivyotuamuru Mtume(s.a.w.w) ,' ina uwezekano kwamba makusudio kwayo ni kuwa yeye Mtume(s.a.w.w) katuamuru tusiikubali shahada ya mtu mmoja katika kufuturu, au katuamuru kwamba tutegemee uoni wa mji wetu: wala tusitegemee uoni wa wengine. Na hii maana ya pili ndipo inapomili tarjama (yaani heading) ya mtunzi (wa kitabu hiki), lakini maana ya mwanzo ina uwezekano (huu na ule) basi ushahidi wake hauendi sawa kwani uwezekano wa namna tafauti unaifisidi dalili, kana kwamba wameona kwamba chenye kufahamika akilini ni maana ya pili wakajenga dalili juu yake. Kwa hivyo, ihtimal wanayoikusudia wao ni kuwa inawezekana kuwa maana iliokusudiwa ni kutokuchukua ushahidi wa mtu mmoja katika kufuturu; na inawezekana ikawa maana iliokusudiwa ni kwamba tutegemee uoni wa mji wetu: wala tusitegemee uoni wa wengine. Kisha wakabainisha kwamba maana ya pili ndio sahihi na kwamba maana ya mwanzo ndio yenye ihtimal (utata kama munavyoita), kwa hivyo maana ya mwazo si sahihi.

Lakini tunasema kwamba bila shaka dai hilo kwamba riwaya hio ina uwezekano kwamba makusudio yake ni kuwa Mtume(s.a.w.w) katuamuru tusiikubali shahada ya mtu mmoja katika kufuturu, ndio maana ya maneno "Hivi ndivyo alivyotuamuru Mtume s.a.w." ni dai dhaifu kwani:

1) Ibn Abbaas aliukataa muandamo wa Ramadhani huko Sham; si muandamo wa mfunguo mosi. Kama riwaya yenyewe inavyosema: "Ukaniandamia mwezi wa Sham nami niko Sham", na muandamo wa Ramadhani hauhitaji mashahidi wawili, bali shahidi mmoja anatosha.

2) Pili katika riwaya mulioitolea hoja - nayo ni riwaya dhaifu: riwaya ya bedui - tunapata kwamba Mtume (s.a.w.) mwenyewe kauchukua muandamo wa mtu mmoja (bedui) katika mwezi wa mfungo.

MNASEMA

Kwa hivyo agizo hilo la kufunga na kufungua kwa pamoja litaendelea kuwa hivyo kwani hakuna riwaya sahihi isiyo na utata yenye kuvua ujumla huu. Tamko hili ni: "Tamko lisilo na mipaka maalum."

JAWABU

Riwaya sahihi isio na utata yenye kuuvua ujumla huo iko: ni riwaya ya Kuraib na Ibn Abbas. Na wala hakuna utata wowote ndani yake; utata munao nyinyi wenyewe.

MNASEMA

Ama jambo la kusema kila watu na mtenguko wao wa jua kwa hivyo wana wakati wao wa kuswali na kufunga (Swaum) ndio hivyo hivyo; ni vyema ieleweke hivyo ni vitu viwili tofauti. Swala imeambatana na mitenguko ya jua na Swaum imeambatana na kuandama kwa mwezi. Mas-ala ya nyakati za Swala yameshaelezwa na kufafanuliwa na Mwenyewe Mwenyezi Mungu katika Qur-aan na pia Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amelibainisha kwa uwazi kabisa katika Hadiyth. Wala hakuna ikhtilafu yoyote mbele ya Wanazuoni juu ya jambo hilo. Ijmai ya Wanazuoni wamekubaliana kuwa kila sehemu, wala si kila nchi nzima inaweza kusali kwa wakati mmoja. Kwani mtenguko wa jua unaweza kutofautiana hata katika nchi moja. Angalia Dar es Salaam na Kigoma wanaswali na kufuturu tofauti, lakini wanafunga kwa mwandamo mmoja. Kila sehemu itaswali kwa wakati wake kwa kutegemea mtenguko wake wa jua. Mwenyezi Mungu Amebainisha hayo katika Surat Bani Israil (17: 78) kama ifuatavyo:"Simamisha Swala jua linapopinduka (likaenda magharibi) mpaka giza la usiku". Kwa upande wa Swaum hapakupatikana ufafanuzi wa kina ambao unakubali ka mbele ya "Jamhur" ya Wanazuoni. Hakuna hoja isiyokuwa na utata katika jambo la kuanza kufunga na kufungua kwa kutegemea kila nchi au kila eneo moja peke yake. Kwa mantiki hiyo ndio maana "Jamhur" ya Wanavyuoni wetu wakaonelea ni bora kutegemea Sunnah, yaani Hadiyth za Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) zilizo wazi ambazo zinaashiria umoja katika kufunga kwa pamoja. Kukamata andiko sahihi ni bora kuliko kung'ang'ania jambo lisilofahamika ambalo lina utatanishi.

"Kutumia madondoo kama Qur-aan au Sunnah ni bora zaidi kuliko kuiwacha (au kuipuuza na kuzingatia dalili zenye utata)".

JAWABU

Kuwepo kwa andiko na ijmaa ya nyakati tafauti za Sala na kutokuwepo kwa andiko la wazi juu ya wapi hadi wapi tufunge, ndiko kuliko juzisha kufanya Qias hicho cha sala na funga. Qias sharti yake ni kuwepo kwa msingi nacho ni kitu ambaho hukumu yake imetajwa; tawi nacho ni kitu ambacho hukumu yake haikutajwa; hukumu nayo ni moja katika hukumu tano za kifiq-hi; na illa jami'a (sababu yenye kuvijumuisha) vitu viwili hivyo na - kwa hapa - ni ukweli kwamba:

1) Jua ni kipimo cha wakati.

2) Jua ni sababu ya kuwajibikiwa na ibada.

3) Mwezi ni kipimo cha nyakati.

4) Mwezi ni sababu ya kuwajibikiwa na ibada.

5) Jua likitenguka sehemu moja: haiwi sababu ya watu wa sehemu nyengine yenye matalai tafauti kuwajibikiwa na sala.

6) Kwa hivyo, na kuonekana kwa mwezi katika sehemu ya mbali kusiwe ni sababu ya watu wan chi ya mbali kuwajibikiwa na ibada ya funga.

Ama kauli yenu: "Kwani mtenguko wa jua unaweza kutofautiana hata katika nchi moja. Angalia Dar es Salaam na Kigoma wanaswali na kufuturu tofauti, lakini wanafunga kwa mwandamo mmoja". Haya ndio niliokwambieni kuwa ni mas-ala ya ijtihad, au yanayojuzu kufanyiwa ijtihad. Yaani wapi hadi wapi tufunge sawa, hilo halikubainishwa na riwaya yoyote; lakini ukweli kwamba muandamo wa mbali usiwe hoja kwa walio mbali; hili limebainishwa na riwaya ya Ibn Abbaas na Kuraib. Kwa hivyo, ikiwa watu wa Kigoma wamefata ijtihad fulani ya wanavyuoni juu ya mas-ala ya masafa gani, hili kwa ujumla linakubalika. Lisilokubalika ni kufunga dunia nzima kwa muandamo mmoja. Na hili ndilo ninalotafautiana na nyinyi. Ama ukweli kuwa mbona basi tunafuturi tafauti na watu wa Kigoma; hili halijuzu ijtihadi kwa sababu ya kuwepo andiko la wazi kwamba wasifuturu hadi jua lituwe. Kwa ufupi ni kuwa, masafa gani tufunge sawa; hapa ijtihad inajuzu kwa sababu ya kukosekana andiko lenye kuhadidi masafa; masafa gani tufuturu sawa, hili halijuzu ijtihad kwa sababu ya kuwepo andiko lenye kubainisha suala hili.

Ama kusema kwenu: "Kwa upande wa Swaum hapakupatikana ufafanuzi wa kina ambao unakubalika mbele ya "Jamhur" ya Wanazuoni. Hakuna hoja isiyokuwa na utata katika jambo la kuanza kufunga na kufungua kwa kutegemea kila nchi au kila eneo moja peke yake. Kwa mantiki hiyo ndio maana "Jamhur" ya Wanavyuoni wetu wakaonelea ni bora kutegemea Sunnah, yaani Hadiyth za Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) zilizo wazi ambazo zinaashiria umoja katika kufunga kwa pamoja". Ninasema: kutopatikana ufafanuzi wa kina ndiko kunakohalalisha kufanya Qias, kwani lau palikuwa na andiko, basi Qias kisingelijuzu kama walivyosema: kwenye andiko hakuna Qias. Lakini sijakufahamuni muliposema : Kwa manti ki hiyo ndio maana "Jamhur" ya Wanavyuoni wetu wakaonelea ni bora kutegemea Sunnah, yaani Hadiyth za Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) zilizo wazi ambazo zinaashiria umoja katika kufunga kwa pamoja". Ni Jumhur ya wanavyuoni wenu gani?

Pili : ni kuwa na Hadithi ya Kuraib pia ni sunna ya Mtume(s.a.w.w) iliowazi.

Tatu : ni kuwa na Hadithi mulioitegemea nyinyi pia haiko wazi kwani inasema"Fungeni kwa kuuona" . Kweli Hadithi hii ko wazi katika kubainisha kwamba kufunga hakutakiwi ila baada ya kuuona mwezi; lakini haiko wazi katika kubainisha je tufunge kwa muandamo mmoja au kila watu wawe na muandamo wao. Ufafanuzi huu, unapatikana katika Hadithi ya Kuraib ambayo hamuitaki: munaipiga chenga!!!

Ama kauli yenu: "Kukamata andiko sahihi ni b ora kuliko kung'ang'ania jambo lisilofahamika ambalo lina utatanishi". Nimeshakufahamisheni kwamba Hadithi ya Kuraib pia infahamika na haina utatanishi, na kwamba Hadithi: "Fungeni kwa kuuona" ndio ambayo inafaa au inaelekea kuambiwa kuwa ina utata, kwani haikufafanua je tufunge kwa muandamo mmoja au miandamo tafauti.

Ama kanuni isemayo: "Kutumia madondoo kama Qur-aan au Sunnah ni bora zaidi kuliko kuiwacha (au kuipuuza na kuzingatia dalili zenye utata)". Kanu ni hii ni ushahidi wetu dhidi yenu, lakini kama munavyojionea wenyewe nyinyi hizi fani hamuzijui: munasukuma tu. Maana ya kanuni hii ni kuwa ikiwa neno - kwa mfano - halifasiriki katika uhakika wake, basi hupewa hukumu ya majazi: lakini sio kuwa liachwe. Na kwa ufupi ni kuwa andiko lolote likiwa linaweza kutendewa kazi basi haliwachwi: huwa linatendewa kazi. Na kwa maana hii, yanaingia maandiko mawili ambayo dhahir yake ni kuwa yana mgongano. Maandiko hayo huwa hayawachwi yote wala haliachwi moja madamu yanaweza kutendewa kati yote, bali kila moja hupewa maana linoyostahiki. Kwa hivyo, sisi ndio tulioitumia kanuni hii: sio nyinyi, kwani sisi tumezitendea kazi Hadithi zote mbili: Hadithi "Fungeni kwa kuuona", na Hadithi "Hivi ndivyo alivyotuamuru Mtume(s.a.w.w) " katika masimulizi ya Kuraib. Kusu Hadithi "Fungeni kwa kuuona", tumesema kwamba maana ni kuwa watu wote ni lazima wafunge kwa kuuona mwezi, yaani kuonekana kwa mwezi ndio kuwe sababu ya mfungo; na Hadithi ya Kuraib na Ibn Abbaas tumesema inatoa ubainifu wa kwamba muandamo wa mwezi wa mbali si hoja kwa waliombali. Kwa hivyo, kanuni hio hamukuielewa na mungeielewa musingelipata tabu katika kuzifasiri Hadithi mbili hizo.

MNASEMA

Ama suala la kuingia alfajiri na kujizuilia kula na kunywa katika hukmu ya kuanza kufunga au kuanza kufuturu wakati wa kuzama kwa jua, mambo hayo hayana mjadala au khitilafu kama hizo kwani Mwenyewe Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Ameshayafafanua katika Qur-an Tukufu kama ifuatavyo:"Na kuleni na kunyweni mpaka ubainike kwenu weupe wa Alfajiri katika weusi wa usiku. Kisha timizeni Swaum mpaka usiku" . (2: 187) Jambo hilo la k utokuwepo khitilafu yoyote katika mas-ala haya, inamaanisha kwamba kila sehemu itajizuilia kula na kunywa kutokana na kuingia alfajiri yake na kila sehemu itafuturu baada ya kuzama jua kwa upande wake.

JAWABU

Haya! Iko wapi hio hoja katika Aya hii?!"Na kuleni na kunyweni mpaka ubainike kwenu weupe wa Alfajiri katika weusi wa usiku. Kisha timizeni Swaum mpaka usiku" . Je hapa wanaombiwa ni watu wan chi moja au wan chi zote? Nadhani jawabu iko wazi kwamba ni watu wan chi zote. Sasa je usiku ukiingia nchi moja na watu wan chi nyengie nao wafuturu? Kama si hivyo, basi vipi Hadithi "Fungeni kwa kuuona" iwe ni dalili ya kufunga sawa duniani kote; lakini Aya"Na kuleni na kunyweni mpaka ubainike kwenu weupe wa Alfajiri katika weusi wa usiku. Kisha timizeni Swaum mpaka usiku". isiwe hoja kwamba tufuturu sawa ilhali ujumla ulioko huku ndio ulioko kule? Kwa kweli, ndugu zetu humujui mukisemacho, na Aya hii ni hoja dhidi yene: si hoja yenu.

Ama kauli yenu kwamba: "Suala la kuingia alfajiri na kujizuilia kula na kunywa katika hukmu ya kuanza kufunga au kuanza kufuturu wakati wa ku zama kwa jua, mambo hayo hayana mjadala au khitilafu". Mwiso wa kunukuu. Nami nasema: Eleweni kwamba kwa kutokuwepo khilafu hizo, ndio imewezekana kufanya Qias sahihi kisichopingika kwa wenye kujua taratibu za Qias, kwani ikiwa Aya inasema:"Na kuleni na kunyweni" na hii ni amri ya ujumla kwa watu wote, na pamoja na hayo wanaokula si wote bali ni baadhi tu ambao usiku umeingia kwao; basi na Hadithi "Fungeni kwa kuuona" haijawa dalili ya kuwa watu wote wafate muandamo mmoja. Ukiniambia "Kule kuna dalili kwamba waliokusudiwa ni wale ambao usiku umeigia kwao". Nitakujibu kwamba na huku kuna dalili kwamba wanaomrishwa katika Hadithi"Fungeni kwa kuuona" ni wale ambao mwezi kwao umeandama. Kule dalili ni ijma'a; huku dalili ni Hadithi ya Ibn Abbaas ya kuukataa muandamo wa mbali na kusema: "Hivi ndivyo alivyotuamuru Mtume(s.a.w.w) ".

MNASEMA

Ama ile hoja inayotolewa na baadhi ya ndugu zetu kama Juma isemayo: "Mbona watu wa nchi fulani wakifuturu nyinyi hamfuturu nao?" Au "Wakifuturu watu wa Saudia na nyinyi mufuturu basi." Bahati nzuri kwa upande wetu tumeshajibu mara nyingi katika makala haya kwamba jambo hili haliingizwi katika mjadala kama huu kwani jambo hilo halizungumzwi hata katika nchi moja yenye kufuata muandamano mmoja. Tumetoa maelezo kwamba katika Tanzania, Mji wa Dar-es-salaam hauwezi kufuturu sawa na mji wa Kigoma kwani kuna tofauti ya zaidi ya dakika 40. Jua linazama au kuchomoza dakika 40 kabla ya Kigoma. Kwa hivyo, Dar es Salaam wanaanza kufuturu mwanzo wakati bado jua halijatua Kigoma. Al-Marhuum Shaykh Abdulla Al-Farsy alipokua akiifasiri Aya ya Quran isemayo:"Kisha timizeni Swaum mpaka usiku" . Aliitolea maelezo yafuatayo: "Na ilipoambiwa:"Fungeni Swaum mpaka usiku" . Muradi ni magharibi - jua likishakuc hwa tu, ndio usiku wenyewe uliokusudiwa, kama alivyobainisha hivi Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam), na akahimiza watu wafungue jua tu likishakuchwa, na wakawie kula daku"

JAWABU

Kwanza ni lazima tufahamiane ni kwa sababu gani pakatolewa hoja hio. Hoja hio imetolewa kujibu dai kwamba Hadithi "Fungeni kwa kuuona" ni Aam (ya ujumla). Na kwa hivyo, inawahusu Waislamu wote wan chi zote. Hapo ndio na sisi tukajibu kwamba na Aya isemayo: (Simamisha sala kwa kutenguka jua), pia ni ya jumla: haiwahusu watu wa nchi fulani pasi na nyengine. Na Hadithi"Usiku ukitokeza kutoka hapa na mchana ukaondoka kutokea hapa na jua likatua, basi aliyefunga ameshafungua (au na-afungue)" pia ni ya jumla. Sasa je ujumla huu unamaanisha kuwa watu wa Maka au nchi nyengine wakifuturu, watu wote wafuturu pamoja nao? Sisi hapa tunajibu hoja ya kuwepo kwa ujmla katika maandiko haya, kwamba ujumla tu haojatoa jawabu madamu kuna maandiko mengine ambayo nayo ni lazima yazingatiwe ili tuwe tumeyatendea kazi maandiko yote na kufikia maana sahihi.

Sasa ukweli kwamba "Jua linazama au kuchomoza dakika 40 kabla ya Kigoma. Kwa hivyo, Dar es Salaam wanaanza kufuturu mwanzo wakati bado jua halijatua Kigoma" hakujahalalisha kufunga kwa muandamo mmoja duniani madamu kuna andiko sahihi la Hadithi lililoonesha hivyo. Bali hali kama hizi zitabaki kama ni uwanja wa i jtihadi. Ama pale kwenye andiko, ni lazima andiko litendewe kazi.

13

MUANDAMO WA MWEZI

SEHEMU YA KUMI NA TATU

MAANA YA JAMHURI KATIKA MATUMIZI YA KISHARI'AH

MNASEMA

13. Maana Ya Jamhuri Katika Matumizi Ya Kishari'ahKwanza : ni vyema kuelewa kwamba mjadala huu wa mwezi katika hukumu ya kufunga na kufungua ni mkongwe wala haukuanza leo. Wala hii si fikra aliyoianzisha Shaykh Naaswir Bachuu kama walivyofahamu hayo baadhi ya watu kama akina ndugu Juma. Ukweli ni kuwa Shaykh Naaswir ni miongoni mwa Mashaykh wanaoendeleza harakati hizi za kufuata muandamo mmoja. Mtazamo huu wa kufunga kwa pamoja uliokuwepo tokea karne nyingi zilizopita umeshaelezwa katika kitabu cha "Kuandama kwa Mwezi" cha Shaykh Naaswir Bachuu uk 129 - 133. Wanavyuoni wakubwa kama Dr. Wahbah Zuhailiy, Shaykh 'Abdur-Rahmaan Al-Juzairy, Alqanuji, Sayyid Saabiq, Ibnu Taymiyah, Ibnu Quddama Almaqdisiy, Shaykh Muhammad 'Aliy Assaabuniy na wengine wengi ni miongoni mwa waliosema kuwa msimamo wa kufunga kwa muandamo mmoja ndio "Rai ya Jamhur."

JAWABU

Hakuna katika kitabu changu sehemu niliodai kuwa Sheikh Nassor Bachoo ndiye aliyeanzisha mjadala huu. Nilichokisema ni hiki: Kwa kwetu - Afrika Mashariki - kusema kwamba mwezi muandamo wa nchi moja ni muandamo kwa nchi nyengine zote za dunia ni kitu kipya. Mutakumbuka kwamba na jambo hili pia kalizungumzia Sheikh Nassor katika kitabu chake aliposema: Pamoja na kuwa mgogoro wa kuandama kwa mwezi umeanza kuonekana hadharani katika jamii za Waislam wa hapa Afrika ya Mashariki katika miaka ya hivi karibuni.

Ama dai kwamba msimamo wa kufunga kwa muandamo mmoja ni rai ya jumhuri, hatuwezi kukubaliana kwani ukweli unaonekana tafauti na hivyo. Kwa ufupi mimi nimelijibu suala hilo hivi: Wengi katika wale wenye msimamo wa kufunga kwa muandamo mmoja huwa wanapenda kudai kwamba rai yao hio ni rai ya Jumhuri (majority) ya Umma, nalo ni kosa kwani ikiwa wanakusudia Jumhuri ni idadi ya wanavyuoni wengi, basi rai ya kwamba kila watu na muandamo wao bila shaka itakuwa ndio yenye kufatwa na wanavyuoni wengi kwani ni rai ya Mashafi nao ndio walio wengi duniani katika madhehebu za Kisuni. Pia rai hii ni rai ya Mashia Imamiyya nao ni wa pili au wa tatu kwa wingi katika madhehebu za Kiislamu.

Ikiwa tunakusudia Jumhuri kwa idadi ya madhehebu, basi - katika madhehebu zilizoko leo duniani - rai ya kuwa kila watu wana muandamo wao ni rai ya Mashafi, Maibadhi, Mashia Imamiyya, pia - kutokana na aliyoyanukuu Al-shaukaniy kutoka kwa Al-imamu Yahya na Al-hadawiyya miongoni mwa Zaidiyya, inaonesha kwamba hii ndio kauli ya madhehebu hio ya Shia-Zaidiyya. Na ndio msimamo wa sasa wa Madhehebu ya Kiwahabi huko Saudia, na ndio kauli sahihi kwa Mahanafi kwa mujibu wa alivyosema Al-sayyid Saabiq kama tutavyonukuu baadae Inshaa Allah..

Pili : ni kuwa kauli ya kufunga kwa muandamo mmoja imenasibishwa kwa Al-imamu Malik. Lakini riwaya hio ya Al-imamu Malik imesimuliwa na watu wa Iraq, ama kule Madina alipokuwepo mwenyewe Al-imamu Malik, watu wa Madina wamesimulia kutoka kwake akisema: "Funga haiwalazimu kwa habari isipokuwa watu wa mji (ule ule) ambao (mwezi) umeonekana."

Tatu : ni kuwa: madhehebu zote ambazo zinajulikana kuwa ndizo zenye msimamo wa kufunga kwa muandamo mmoja zina wanavyuoni si kidogo ambao hawakuiafiki rai hii. Kama Al-kaasaniy, naye ni Hanafi. Na akawanukuu Abu Muslim wanachuoni wengine wa Kihanafi wenye kauli hii. Anasema: "Na alichokichaguwa mwenye kitabu cha "AL-TTAJRID" na wengineo katika Mashekhe wa Mahanafi, ni kuzingatia tafauti za Matalai. Amesema Al-zayla'i naye ni miongoni mwao (Mahanafi): 'Nayo (kauli hio) ndio yenye kuelekea zaidi.' Na amesema Ibn Al-hammam miongoni mwao (Mahanafi) na kushikana na dhahiri ya masimulizi (ya Hadithi ya Kuraib) ni (jambo) lenye hadhari zaidi..na hakuna shaka kwamba hii ni bora kwani ni nassu (andiko la wazi) na ile (Hadithi inayosema: 'Fungeni kwa kuuona') ina uwezekano wa kuwa makusudio ni kuwaamuru watu wa kila matalai kuwa na uoni wao wa mwezi muandamo." Mwisho wa nakala kutoka katika kitabu cha Al-imamu Abu Muslim.

Anasema Al-sayyid Saabiq: "Na akasema Ikrima na Salim na Is-haq na ndio (kauli) sahihi kwa Mahanafi..kwamba watu wa kila mji wanazingatia muandamo wao wala hauwalazimu muandamo wa wenzao." Mwisho wa kunukuu. Ninasema: bila shaka watakuepo wengine wengi ambao vitabu v yao hatujavisoma au hatujaviona kamwe.

Pia ukitazama maneno ya Ibn Rushd Al-qurtubiy - naye ni mwanachuoni wa Kimaliki - utaona hakutoa msimamo wake kwa uwazi, lakini maneno yake yanaonesha kwamba anaelemea katika kauli kwamba kila watu wana muandamo wao. Anasema - baada ya kuinukuu Hadithi ya Kuraib na kutoa maelezo -: "Dhahiri ya Riwaya hii inamaanisha kwamba kila mji una uoni wao (wa mwezi muandamo) ukiwa mbali au karibu. Na Qiyas kinatoa tafauti baina ya miji ya mbali na miji ya karibu."

Mwisho wa kunukuu.

Na Ibn Al-arabiy - naye ni miongoni mwa wanavyuoni wakubwa wa Kimaliki - anasema: "Na wakatafautiana katika kuifasiri kauli hii ya Ibn Abbas (yaani Hadithi ya Kuraib). Ikasemwa: '(Ibn Abbas) Kaikataa (habari hio aliopewa na Kuraib) kwa kuwa ni ya mtu mmoja. Na ikasemwa kwa kuwa miji (miwili hio ya Madina na Sham) matalai yake yametafautiana, nayo ndio (kauli) sahihi..na mfano wake ni lau uliandama usiku wa Ijumaa huko Aghmat (Morocco) na ukaandama huko Ishbiliyya (Mji wa Spain) usiku wa J/mosi, ba si inakuwa kila mji una muandamo wake."

Na mfano wa kauli hii ya kuzingatia tafauti za miandamo kwa kutafautika miji kwa umbali au kwa kutafautika matalai, ndio kauli ya Ibn Majishun na Al-mughira miongoni mwa wanavyuoni wa Kimalik. Anasaema Ibn Rushd Al-qurtubiy: "Na wakakubaliana kwamba hilo halizingatiwi katika miji ilio mbali mbali kama Al-andalus (Spain) na Hijaz (Saudia)." Na kauli hii kaisema pia Ibn Abdil-Barri katika wanavyuoni wa Kimalik. Changanya na ukweli kwamba Al-imamu Malik mwenyewe kuna riwaya mbili juu ya kauli gani aliitegemea, na riwaya ya kwamba kila watu na muandamo wao ndiyo yenye kuelekea zaidi kutoka kwake kwani ndio riwaya iliosimuliwa na watu wa Madina ambako Al-imamu Malik mwenyewe alikuwa akiishi.

Nne ni kuwa: kama tulivyotangulia kusema kwamba mas-ala ya kufunga kwa muandamo mmoja yamo katika vitabu tu: si katika matendo: kimatendo ni Waislamu wachache sana duniani wanaofata rai hio. Kwa mfano nchi za India na Pakistan na Bangladesh - ambazo zina Mahanafi wengi - ukiwauliza wakazi wa nchi hizo wenye kuishi Ghuba: "Kwenu mwezi umeandama lini?" Watakwambia siku tafauti na muandamo wa nchi nyengine ambazo labda zimetangulia. Na nchi hizo zote zina Maulamaa.

Tano : ni kuwa: kauli ya kuwa kila mji na muandamo wake imesimuliwa kutoka kwa Maimamu wengine wakubwa - ukitoa Maimamu wanne - kama Ikrima miongoni mwa Wafuasi wa Masahaba, na Moh'd bin Al-qasim na Salim na Is-haq bin Rahawaih na Al-tirmidhiy akainasibisha na watu wa elimu (Maulamaa). Kwa hivyo, tunasema kwamba kusema kwamba kauli ya muandamo mmoja ni kauli ya Jumhuri ya Umma, ni jambo la kufikiriwa. Kwa hali yoyote ile, mimi sisemi kwamba kilichosawa ni kinachosemwa na Jumhuri,( laa): sisemi hivyo, bali ninachosema ni kuwa kilicho sahihi ni chenye ushahidi madhubuti uliojengeka juu ya misingi ya kielimu, lakini naona watu hapa wamekuwa wakipiga kampeni kwa kutumia jina Jumhuri nayo si sahihi. Na mas-ala kama haya yako mengi: utasikia hii ndio kauli ya Jumhuri, mara ukisoma kitabu chengine utakuta kauli kinyume na hio kwamba ndio kauli ya Jumhuri!!! Cha kustaajabisha zaidi ni kuwa wakati mwengine utakuta kitu chenye tafauti mashuhuri, basi atatokea mtu anayetaka kuipamba rai yake, anasema: "Umma umekubaliana juu ya jambo hili!" Mwisho wa kunukuu nilioyasema kitabuni.

Bila kusahau kwamba hata leo hii, Jumhur ya Waislamu duniani hawafati miandamo ya nchi nyengine. Kwa hivyo, hiki ni kitu tunakishuhudia hatuhitaji andiko. Lakini - kama nilivyosema - ikiwa Jumhur inasema tufunge kwa muandamo mmoja au inasema kama tunavyosema sisi, yote mawili si hoja katika uwaja wa Sharia, bali hoja ni je wana dalili gani, na wapinzani wao wana dalili gani. Chukua - kwa mfano - walio wengi katika Sunni, wanasema tufunge mikono chini ya kitovu, tukichukulia kwamba Sunni wengi ni Hanafi. Au wanasema tufunge juu ya kitovu, tukichukulia kwamba Sunni wengi ni Shafi. Wakati Salafia wana hoja ambazo ndio sahihi kwao kwamba mikoni inafungwa juu ya kifua. Sitaki kusema kipi ni sahihi, nataka kusema kwamba wingi si hoja ya Kisharia. Bali leo, ukitazama katika madhehebu za Sunni utakuta kwamba Salafiyya ndio wachache. Sasa tuseme ndio dalili zao zitakuwa hazifai? Bila shaka kitachotazamwa ni dalili: si wingi na uchache.

MNASEMA

Msimamo huu kwa kweli umejengeka katika misingi imara uliopokewa moja kwa moja kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) pale aliposema: (Fungeni kwa kuona mwezi - muandamo..)

JAWABU

Tumeshabainisha sana kwamba (Fungeni kwa kuona mwezi - muandamo..) ni Hadithi na "Hivi ndivyo alivyotuamuru Mtume(s.a.w.w) " pia ni Hadithi. Na huwezi kuyakataa mafunzo ya Mtume(s.a.w.w) , bali unaweza kuyatafutia maana sahihi

MNASEMA

Wanavyuoni wa Shari'ah wameieleza "Jamhur" kwa maana ya kukubaliana jambo "Maimamu wanne wa Kisunni" na hata kama ikitokea kujitoa Imamu mmoja katika hao wanne kwenye jambo fulani bado jambo hilo litachukuliwa ni la msimamo wa "Jamhur" midam watatu kati yao wana msimamo mmoja.

Ama tukichunguza katika kitabu cha ndugu Juma tunakuta ameeleza maana ya Jamhur kinyume na hivyo. Ameieleza "Jamhur" katika mtindo usioelezwa katika vitabu vya Shari'ah. Miongoni mwa udhaifu alioutaja ndugu Juma katika kueleza maana ya "Jamhur" ni vile alivyoeleza kuwa (tunasema kwamba kusema kwamba kauli ya muandamo mmoja ni kauli ya Jumhuri ya Umma, ni jambo la kufikiriwa.). Sisi tunasema kwamba kitu cha kwanza cha kufikiriwa ni hii tafsiri ya ndugu Juma katika maana ya neno "Jamhur." Tunamuomba nd ugu Juma asijifanye kama yule kipofu aliyeingia kwenye nyumba ya mtu na kujigonga kwa vitu vilivyokuwemo ndani, kisha akawalaumu sana wenye nyumba. Sasa inafaa kujiuliza ni nani wa kulaumiwa baina ya kipofu na mwenye nyumba? Bila shaka wa kulaumiwa ni yule bwana kipofu kwani vitu vilikwishapangwa akamtupia lawama mwenye nyumba. Kwa hivyo nasi tunamtanabahisha vizuri na mwenye nyumba lakini kwa sababu ya kutokuona kwake ndio ndugu Juma kuwa Wanavyuoni wenye kuaminika wamekwishakuieleza maana halisi ya "Jamhur" katika matumizi ya Shari'ah ingawa yeye kwa makusudi akajitia upofu na kuanza kusema: (naona watu hapa wamekuwa wakipiga kampeni kwa kutumia jina Jumhuri nayo si sahihi.) Kisha akaendelea kusema: (basi atatokea mtu anayetaka kuipamba rai yake, anase ma: "Umma umekubaliana juu ya jambo hili!")[5]

Kama kweli ndugu Juma ni msomi ingekuwa jambo la busara atoe majina ya vitabu vya Wanavyuoni wenye kukubalika waliosema kuwa rai ya kufuata muandamo mmoja sio rai ya Jamhur. Pili tunamuuliza ndugu Juma ni rai ipi aliyoikuta yeye ambayo imetajwa kuwa ni rai ya Jamhur kisha isiwe ni rai ya Jamhur? Ilikuwa ni wajibu wake kama anataka kuikosoa atoe ushahidi wa maandiko na madondoo ili uwe ushahidi. Kwani tunavyojua sisi ni kuwa kila rai iliyotajwa kuwa ni ya Jamhur panakuwa na maandiko yenye kukubalisha jambo hilo , hata kama ipo khitilafu ya baadhi ya Wanazuoni.

Tunamnasihi ndugu yetu Juma kuwa anapojaribu kuelezea mas-ala yoyote ya kielimu, basi ni vyema apite katika njia zake zenye kukubalika kitaalamu wala asidhani kuwa anaweza kufaulu bila ya kupita katika njia hizo. Ni vyema aelewe kwamba asipopita katika njia hizo atapotea. Mshairi mmoja wa kiarabu anasema hivi: "Unatarajia kuokoka (kufaulu) bil a ya kupita katika njia zake (Elewa kwamba) jahazi haiwezi kwenda kwenye nchi kavu." Mshairi mwengine anasema: "Ukiliendea jambo (ukitaka kulifanya jambo) bila ya kupita katika njia zake utapotea (na kuwapoteza wenzako). Na ukiliingia jambo katika njia zake utaongoka (na utaongoza wenzako)."

JAWABU

Ni wanavyuoni wa Sharia gani hio waliosema kuwa Jumhur ni kukubaliana jambo kwa "Maimamu wanne wa Kisunni"?! Yaani mulivyowafahamu nyinyi hao wanavyuoni ni kuwa hawa Waislamu wote tokea Masahaba kauli zao ni mataka tu: Maimamu wane ndio wanye haki ya kuzungumzia dini?!!!

Jumhur linatumika kwa maana tafauti. Inatumika Jumhur ya Umma, na hii ndio Jumhur yenye nguvu. Yaani kitu kilichokubaliwa na waliowengi katika Umma, kuanzia Masahaba hadi Maimamu wa madhehebu zote na hadi leo. Pia linatumika kumaanisha Jumhur ya Kisunni, hii ndio hio mulioitaja nyinyi. Na kuna jumhur ya Mashafi, ya Kiibadhi, ya Kishia n.k, yaani walio wengi katika wanavyuoni wa madhehebu hizo. Kwa hivyo, Jumhur halitumiki kwa maana moja. Ndio maana ukisoma vitabu tafauti vya kifi-qhi utaona ibara kama "Jumhuru ya wanachuoni wa madhehebu fulani au wa fani fulani". Na utakuta Jumhur ya Ummah. Na unaweza kukuta kwamba hii ni kauli ya Jumhur; hapa itabidi umfahamu muandishi je anakusudia Jumhur gani.

Anasema Dr. Al-Zuhaili: "Wamekubaliana Jumhur ya watu wa adab (literature)." Na anasema: "Na wakapinga Jumhur ya Mashafi na Mahanafi". Na akasema: "Wakasema Jumhur ya watu wa Usuli". Anasema Al-Imamu Al-Jitali: "Na hio ni kwa sababu kwa (mtazamo wa) Jumhuri ya watu wa elimu". Na anasema: "..Kwa Mashekhe wetu na Jumhur ya Ummah". Anasema Bakli 'Abdil-Rahman: "Na wakasema jumhur ya Maulamaa wetu (wa Kiibadhi)". Anasema Sheikh Al-Khalili: "Na Jumhur ya Umma wakatoa ushahidii". Haya yako katika kila kitabu unachokisoma taqriban utayakuta, wala mtu mwenye elimu yake hayaulizi.

Ama kama Jumhur ni makubaliano ya Maimamu wane wa Kisuni, basi jumhur haitokuwa hoja kamwe, kwani Maimamu wane wametanguliwa na vigogo wengi katika Masahaba na wafuasi wao na Maimamu wakubwa waliokuwa mabingwa sana. Na wote hawa walikuwa na fikra tafauti na za Maimamu wane: yaani mwengine hukubaliana na mwengine hutafautiana. Wametangulia kabla yao akina Jabir bin Zaid na wanafunzi wake; Al-Hasan Al-Basari na wanafunzi wake; Al-Awzai na madhebu yake; Mafaqihi wa Madina; wa Iraq; wa Sham kwa maelfu. Kwa hivyo, kama jumhur:

1) Ni kauli ya Maimamu wane wa Kisuni, itakuwa haina nguvu kwani Umma uliowatangulia ni mkubwa na ulikuwa na vigogo ambao walisifika kushinda wote waliokuja baada yao.

2) Kama ni idadi ya madhehebu, basi madhehebu zenye kufunga kwa miandamo yao leo na zamani ni watu wa madhehebu zote taqriban. Miji ya Pakistan, Bagladesh na India yenye Mahanafi wengi wanafata miandamo yao. Misri ambako Mashafi - nadhani - ndio wengi wanafata muandamo wao. Nchi za Afrika Magharibi zenye Malik wengi pamoja na nchi za Afrika Kaskazini za Kiarabu zenye Malik wengi, zinafata miandamo yao. Nchi za Ghuba, Iraki, Sham na Al-Yaman, Mashariki ya mbali wote hawa wanafata miandamo yao, na waliowengi katika nchi hizo ni Masunni wa madhehebu nne. Kwa hivyo, bado naendelea kusema kwamba kudai kuwa kauli ya muandamo mmoja ni kauli ya Jumhuri ya Umma, ni jambo la kufikiriwa.

MNAEMA

Tukiendelea kumfahamisha ndugu Juma juu ya kauli zake alizoziandika kwenye kitabu chake ambazo sio za kielimu ni kule kusema kwake kwamba: (kama tulivyotangulia kusema kwamba mas-ala ya kufunga kwa muandamo mmoja yamo katika vitabu tu: si katika matendo: kimatendo ni Waislamu wachache sana duniani wanaofata rai hio.) Tunamfahamisha ndugu Juma kwamba kitu cha msingi kinachofaa kuzingatia katika mas-ala yoyote yale ya Dini ni ule usahihi wake, sio kuangalia wingi au uchache wa wafuasi. Mfano mzuri ni haya madhehebu ya Ibadhi yenye wafuasi wachache mno duniani ukilinganisha na madhehebu mengine kama Hanafi na mengineyo. Je kwa sababu ya uchache wao ndio unataka kusema Ibadhi hawako katika haki?

Kwa hiyo uchache wa wafuasi sio kipimo cha haki au batil. Ni vyema ndugu Juma awe makini katika uandishi hususan katika jambo la kujenga hoja, asikubali kutawaliwa na taasub za aina hizo.

JAWABU

Hapa nakubaliana na nyinyi 100%. Na hilo nilikwisha kulisema katika kitabu na humu kabla yakufika hapa pia nimelisema. Kitabuni nilisema: Kwa hali yoyote ile, mimi sisemi kwamba kilichosawa ni kinachosemwa na Jumhuri,( laa): sisemi hivyo, bali ninachosema ni kuwa kilicho sahihi ni chenye ushahidi madhubuti uliojengeka juu ya misingi ya kielimu. Na humu katika jawabu hii, nimekwambieni hivyo kwamba je uchache wa Salafia unawafanya kuwa hawako sahihi?! Na nyinyi mukaniambia je uchache wa Maibadhi unawafanya kuwa hawako sahihi. Kwa hivyo, nukta hii tumekubaliana. Lakini tumetafautiana katika tafsiri ya neno Jumhur.

Ama kauli yenu: "Pili tunamuuliza ndugu Juma ni rai ipi aliyoikuta yeye ambayo imetajwa kuwa ni rai ya Jamhur kisha isiwe ni rai ya Jamhur?" inaonesha hamutaki kusoma: munataka kukosoa tu. Mara ngapi utakuta vitabuni kuwa hii ndio rai ya Jumhur kisha ukisoma kitabu cha pili utakuta rai kinyume kwamba ndio rai ya Jumhur. Kwa mfano, mas-ala ya kuziletea ta-awil Aya za Sifat. Al-Asha'ira wanadai kuwa huo ndio mwenendo wa Al-Salaf (Masahaba, wafuasi wao na Maimamu wakubwa wakiwemo wane); wakati Salafiyya wanadai kutokuziletea ta-awil Aya hizo ndio mwenendo wa Al-Salaf na Maimamu. Na wote wana ushahidi wao wakimaandiko. Bali utakuta kwamba Umma umekubaliana juu ya hili wakati ni kitu chenye khilafu. Kwa mfano, utakuta mara nyingi kwamba "Umma umekubaliana kuwa Hadithi za Al-Bukhari na Muslim zote ni sahihi". Halafu tunakuta Maulamaa wengi, kama Ibn Taymiyya, Ibn Al-Qayyim, Al-Albanni, Al-Qannubi, Ibn Al-Jawzi na mamia ya Maimamu wa Kisuni, wanazidhoofisha baadhi ya Hadithi hizo. Sasa hayo makubaliano ya Umma yako wapi? Kwa hivyo, ndugu zanguni, kwa ujumla vitabu vya binaadamu vyote vina makosa. Haitoshi mtu kutoa hoja kuwa kuwa fulani kasema; ni lazima utafute ukweli wenyewe ukoje.

MNASEMA

Mukhtasari Wa Nukta Muhimu (1) Msimamo wa kufunga na kufungua kwa muandamo mmoja duniani ndio rai ya Jamhur. Wala si rai itokayo kwa Shaykh Naaswir Bachuu. Ndugu Juma hakuwa makini katika kukisoma kitabu alichokiandika Shaykh Naaswir Bachuu: "Kuandama Kwa Mwezi" uk 162 - 163. Wafuatao ni baadhi ya Mashaykh wa Afrika Mashariki waliowahi kubainisha jambo hilo :-

JAWABU

Si kweli huu si msimamo wa Jumhur ya wanavyuoni wa Umma, bali hata ya wanavyuoni wa Kisunni bali hata ya Maimamu wane wa Kisuni. Ama wanavyuoni wa Umma, leo Umma una madhehebu nane kuu: nne za Kisuni, Salafiyya, Ibadhi, Shia Imamiyya Ithnashariyya na Zaidiyya. Wenye msimamo huu kimatendo ni baadhi ya Salafiyya walio nje ya Saudia. Ama wale wa Saudia walikuwa na msimamo huo na baada ya kuuchunguza kupitia kwa wanavyuoni wao wakuu kama Sheikh Bin Baz na Ibn 'Uthaimin na Bodi ya wanavyuoni wakuu, wameweza kugundua kuwa msimamo huo ni makosa na kwahivyo wamebadilisha msimamo huo na sasa wanafunga kwa mujibu wa muandamo wao. Ama nchi zenye Madhehebu za Hanafi na Malik, Maulamaa wao pia wanafata miandamo ya nchi zao. Bali Al-Imamu Malik mwenyewe kuna riwaya mbili juu ya Msimamo gani alifata na riwaya kwamba kila mtu na muandamo wake ndio riwaya iliopokewa huko Madina ambako yeye mwenyewe Al-Imamu Malik alikuwa akiishi. Kwa hivyo, narejea tena kwamba dai kwamba msimamo wenu ni msimamo wa Jumhur - hata kama yuko aliyeandika hivyo - basi ni dai la makosa na vitabu vimejaa makosa tele, kitu muhimu ni tahqiq: sio kuchukua tu fulani kasema.

Ama kudai kwenu: "Ndugu Juma hakuwa makini katika kukisoma kitabu alichokiandika Shaykh Naaswir Bachuu" kunaonesha kuwa nyinyi hamukuwa makini katika kukisoma kitabu changu wala cha Sheikh Nassor, kwani nilichokisema mimi ni kuwa huu ni msimamo mpya kwa kwetu Afrika ya Mashariki, na hivi ndivyo alivyosema Sheikh wetu Nassor Bachoo pia. Nimekupeni marejeo katika sehemu mbili redieni mutazame. Kwa hivyo, nyinyi munanibandika kitu ambacho sikukisema.

MNASEMA

i) Al-Marhuum Shaykh Juma 'Abdul-Waduud wa Zanzibar katika kuelezea msimamo wa kufunga pamoja alisema ifuatavyo: "Hii ni rai nayo na wengi wamesema (hivyo) kama Imamu Malik, Ahmad na kundi kubwa la Hanafi."[7]

ii) Shaykh Abdillahi Naaswir wa Kenya ameeleza yafuatayo: "Wako wanaosema kwamba mwezi ukionekana mji mmoja, basi Waislamu wengine popote walipo wafunge. Hayo ni maoni ya Hanbali, Maliki na Hanafi" (Imenukuliwa kutoka kitabu chake Swaum--Nguzo Ya Nne uk. 22 - 23 chapa ya 1985.).

JAWABU

Kuhusu Al-Imamu Malik, nimeshakujibuni kwamba hakuna uthibitisho kwani riwaya kutoka kwake zinagongana. Na wanavyuoni wa madhehebu yake wametafautiana, lakini pia kusema kwamba walio wengi ni wenye kusema kuwa tufate muandamo mmoja ni kitu cha kufikiriwa kwani Ibn Rushd Al-Qurtubi - naye ni katika vigogo wa Kimalik - anasema: "Na wakakubaliana kwamba hilo halizingatiwi katika miji ilio mbali mbali kama Al-andalus (Spain) na Hijaz (Saudia)." Na haya pia yamenenwa na Ibn Abdil-Barri - naye ni katika Malik pia. Na wanavyuoni wa Kihanafi wametafautiana - kama tulivyoeleza katika kitabu - lakini hadi leo hii wanachokitendea kazi Mahanafi na Malik ni kufata miandamo yao kama tunavyoshuhudia katika nchi zao.

MNASEMA

iii) Al-Marhuum Shaykh Hemed bin Juma bin Hemed -aliyekuwa Mufti Mkuu Wa Tanzania Katika hotuba yake iliyonukuliwa neno kwa neno na gazeti la Al-Jihaad toleo No: 4 la tarehe 18/03/1994 sawa na 6/Shawaal/1416 lililotolewa na MSAUD. Katika maelezo mengi aliyoyatoa Shaykh Mkuu huyo kwenye kadhia iliyosababisha kuandama mwezi siku iliyo ikiaminika kuwa ni mwezi (tarehe) 28 ya Ramadhaan alikuwa na haya ya kusema:

"Nyinyi Waislamu wezangu, mwaniambia mimi, kwa ile tukio lenyewe lote, kadhia nilivyoeleza, mwaweza nambia nimewafungisha siku ishirini na nane? Basi tumefungua, Alhamdulillah rabbil aalamin. Linalofuata, mimi nitoe shukrani kubwa kwa watukufu, kutusaidia namna hiyo, na kuondosha tatizo hilo Pia nashukuru sana, kwa bahati kubwa tuliyoipata mwaka huu, ya kihistoria, kufungua siku moja, sisi na wa Saudia, Cairo na Muscat Oman na wapi, kufungua siku moja, nadhani kihistoria, mimi mpaka leo, nina miaka, huu wa sitini na sita, lakini sikumbuki kupata bahati hii. Sikumbuki kupata bakhti hii. Nimemuuliza mzee wangu, Mzee Gumsani, una miaka mingapi, ananiambia themanini na nne, sijui themanini na ngapi! Je iko siku umebahatika hivyo, asema bado sijapata. Je, bahati iliyoje hii? Hadhi kubwa tuliyoipata ya kufungua siku moja, wa Saudia, Cairo, Maskati Oman na miji kadha kadhaa ya Kiarabu.

Tunamuomba Mwenyezi Mungu Aiendeleze bahati hii, ili kuimarisha umoja huu. Mungu ajaalie 'Arafah pia iwe moja. Ndio zina matatizo, na 'Iyd ya mfunguo mosi iwe moja. Matatizo haya yaondoke InshaAllaah!" Mwisho wa kunukuu.

JAWABU

Haya! Hoja yenu iko wapi hapa?! Anachokizungumzia Sheikh Hemed ni kuwa watu mara hio waliuona mwezi muandamo sawa; wakafunga sawa: si kwamba mwezi ulionekana sehemu moja watu wa miji yote wakafunga.

MNASEMA

(2) Imeshawahi kutokezea mara nyingi dunia nzima (au sehemu kubwa ya dunia) kufunga na kufungua kwa pamoja, yaani katika siku moja. Mfano mzuri uliowahi kutokea ni huo hapo juu alioueleza Mufti Mkuu Shaykh Hemed bin Juma katika tokeo la mwaka 1994. Pia katika mwaka wa 2007 takriban dunia nzima ilifunga siku moja ya tarehe 13/09/2007.

JAWABU

Haijapata kutokea dunia nzima kufunga siku moja, wala hata sehemu kubwa zaidi ya dunia; na hilo haliwezekani kifaki wala kijografia. Lakini inawezekana nchi nyingi zikafunga pamoja. Na huu sio mjadala wetu: mjadala wetu ni je walifunga kwa kufata muandamo wan chi moja au walifunga kwa miandamo yao.


10

11

12

13

14

15

16