HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU15%

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU Mwandishi:
: AZIZI NJOZI
Kundi: Wanawake

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU
  • Anza
  • Iliyopita
  • 33 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 48296 / Pakua: 5931
Kiwango Kiwango Kiwango
HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU

Mwandishi:
Swahili

1

12

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU

MIRATHI

Zama za kale mwanamke alikuwa harithi kitu na, hata aliporithi, alitendewa kama mtoto. Alikuwa hana haiba ya kisheria inayojitegemea. Kwa mujibu wa baadhi ya mifumo ya kisheria ya kale, mtoto wa kike alipata urithi lakini watoto wake hawakupata. Kwa upande mwingine, mtoto wa kiume sio tu anapata urithi yeye mwenyewe, bali pia watoto wake walirithi mali iliyoachwa na mababu zao. Baadhi ya mifumo mingine ya sheria ilimruhusu mwanamke kurithi lakini si kwa kupata asilimia maalum au kwa lugha ya Qur'ani 'gawio lililopangwa.' Walichokifanya ilikuwa ni kumruhusu mzazi kuusia kuwa apewe, kama muusiaji anataka.

Wanahistoria na wachunguzi wameeleza kwa kina aina mbali mbali za sheria zilizokuwepo kale, lakini kwa sasa hatutaki kwenda kwa undani zaidi. Kwa sasa ufupisho tulioueleza hapo juu unatosha. Kwa nini mwanamke alinyimwa urithi? Sababu kuu ya kumnyima mwanamke urithi ilikuwa ni kuzuia kuhama kwa mali kutoka familia moja kwenda nyingine. Kwa mujibu ya imani za kale, mchango wa mwanamke katika uzazi haukuwa wa thamani sana. Akina mama walitumika kama mifuko tu ambamo mbegu ya baba ilikua na kuwa mtoto.

Kwa sababu hii waliamini kuwa watoto wa mtoto wa kiume walikuwa sehemu ya familia lakini watoto wa mtoto wa kike hawakuwa sehemu ya familia yake, kwa vile walikuwa sehemu ya familia ya babu yao mzaa baba. Hivyo kama binti angepata urithi, hiyo ingemaanisha kuhamisha mali kwenda kwa watoto wake (binti), watoto ambao hawahusiani na familia ya marehemu.

Marehemu Dr. Musa Ameed anasema kuwa katika siku za kale dini na sio mahusiano mengine yoyote ya asili, ndio ilikuwa msingi wa uundwaji wa familia. Babu, mbali na kuwa mkuu wa kijamii wa watoto na wajukuu wake, pia alikuwa mkuu wao wa kidini. Utekelezaji wa sherehe za kidini na matendo ya ibada yalikabidhiwa kwa kizazi kinachofuatia kupitia kwa watoto wa kiume tu. Wahenga waliwaona wanaume peke yao kuwa ndiyo njia ya kuhifadhi na kuendeleza kizazi.

Baba wa familia mbali na kumpa maisha mwanaye wa kiume, pia alimkabidhi imani na matendo ya kidini. Kwa mujibu wa Maveda wa Kihindi na Wagiriki na sheria za kirumi, nguvu ya kizazi ilikuwa kwa wanaume tu, na hivyo dini za familia zilikuwa ni miliki ya wanaume pekee, na wanawake hawakuwa na usemi wowote isipokuwa kupitia kwa baba zao au waume zao. Kwa vile hawakuweza kushiriki katika utekelezaji wa sherehe na shughuli za kidini, basi walikosa faida na manufaa yote ya kifamilia. Hivyo mfumo wa urithi ulipokuja wanawake walitengwa.

Kutengwa kwa wanawake katika urithi kulikuwa na sababu nyingine pia, mojawapo ikiwa ni kuwa hawakuwa wakakamavu vya kutosha kuwa askari. Katika jamii ambazo ziliweka umuhimu mkubwa katika matendo ya kishujaa na nguvu ya kupigana, na mpiganaji alionekana kuwa bora kuliko watu laki moja wasio wapiganaji, mwanamke alinyimwa urithi kwa vile hakuwa na uwezo wa kupigana. Kwa sababu hii, Waarabu wa zama za kabla ya Uislamu, walikuwa hawakubali suala la mwanamke kurithi mali, maadamu kulikuwepo wanafamilia wa kiume hata kama kiukoo walikuwa ni ndugu wa mbali.

Hii ndio sababu walishangazwa sana Qur'ani iliposema wazi wazi kuwa;"Wanaume wana sehemu katika kile kinachoachwa na wazazi na ndugu wa karibu, kiwe kikubwa au kidogo - gawio lililopangwa." (Suratul Nisa, 4:32). Ilipata kutokea wakati fulani ndugu yake na Hasan bin Thabit, mshairi maarufu, alifariki katika siku hizo, huku akiacha mke na binti zake wengi. Binamu zao wa mfumo dume waligawiana mali zote na hawakuwapa chochote mjane na binti zake. Mjane alilalamika kwa Mtume ambaye aliwaita ndugu wa mume. Walisema kuwa mwanamke hakuwa na uwezo wa kubeba silaha na kupigana na adui. Ni wanaume waliojilinda wao na wanawake. Hivyo ni wao tu waliokuwa na haki ya kurithi mali.

Walipofikia hapo Mtume akawasomea amri ya Allah, kama ilivyo katika Aya hiyo hapo juu. Urithi wa mtoto wa kiume wa kupanga. Waarabu wa kipindi cha kabla ya Uislamu wakati fulani walimfanya mtu fulani kuwa mtoto wao wa kiume wa kupanga. Mtoto huyu wa kupanga kama mtoto halisi, alichukuliwa kuwa mrithi. Mila ya kujipatia watoto wa kupanga ilikuwepo katika mataifa mengine pia kama vile Urumi na Iran.

Mtoto wa kiume wa kupanga, kama ilivyo kwa mtoto halisi alikuwa na haki zote ambazo mabinti halisi wa kuzaliwa hawakuwa nazo. Haki hizi zilikuwa ni pamoja na haki ya kurithi. Halikadhalika kumuoa mke wa mtoto wa kupanga hakukuwa kunaruhusiwa. Qur'ani Tukufu ilipiga marufuku mila hizi. Urithi wa mshirika Mila nyingine, iliyokuwa ya kawaida miongoni mwa Waarabu wa kabla ya Uislamu ilikuwa ni ile ya ushirika (alliance). Watu ambao hawakuwa na uhusiano wa damu walikula yamini ya undugu kuwa; "Damu yako ni damu yangu, uchokozi wowote dhidi yako utakuwa ni uchokozi dhidi yangu; utarithi mali yangu na mimi nitarithi mali yako."

Kwa mujibu wa ushirika huu, makundi yote yalikuwa yakiwajibika kumlinda mshirika wake katika kipindi chote cha uhai wao, na mmoja wao alipokufa, mshirika aliyebaki alichukua mali za marehemu. Mke kama sehemu ya mirathi. Wakati fulani zama za kabala ya Uislamu, Waarabu walikuwa wakimhesabu mjane kuwa sehemu ya mali ya mume aliyefariki na hivyo, yeye pia alirithiwa.

Ikiwa marehemu alikuwa na mtoto wa kiume kutoka kwa mke mwingine, huyo alikuwa na uwezo wa kumrushia mjane kipande cha nguo kama ishara ya kumrithi. Baada ya hapo alikuwa na uhuru wa kumwamulia atakavyo au kumfanya vyovyote apendavyo kwa raha zake. Alikuwa na hiari ya ama kumuoa yeye mwenyewe au kumuozesha kwa mtu mwingine na yeye kuchukua mahari. Mila hii ambayo haikuwepo miongoni mwa Waarabu peke yao ilipigwa marufuku na Qur'ani.

Kuhusiana na suala hili la mirathi katika madaraja mbali mbali, sheria za jamii za kale za Wahindi, Wajapan, Warumi, Wagiriki (wayunani) na Wairani zilikuwa ama haziruhusu wanawake kurithi au zilikuwa zinawabagua (yaani walikuwa wanapewa kidogo sana). Kutokana na uchache wa nafasi hatuwezi kuyaandika hapa yote yaliyoandikwa na wataalamu wa fani hii. Mila ya kuwarithi wanawake katika kipindi cha Sasania. Hayati Saeed Nafisi katika kitabu chake, 'Social History of Iran from the Sasanian times to the end of the Ummayad period' ameandika kuwa; "Tabia nyingine ya kuvutia au kushangaza ya utamaduni wa Wasasania ilikuwa ya kwamba mvulana alipobaleghe, baba yake alimuozesha mwanae huyo mmoja wa wake zake wengi (wa baba huyo).

Katika zama hizo mwanamke hakuwa na haki yoyote ya kisheria. Baba na mume walikuwa na madaraka makubwa sana juu ya mali ya mwanamke. Lilikuwa ni jukumu la baba au mkuu wa familia kumuoza binti yake alipofikia umri wa miaka 15. Lakini umri wa kuoa kwa wavulana ulikuwa miaka 20. Baada ya kuolewa binti huyo hakuwa na haki ya kurithi mali ya baba yake au mlezi wake.

Hakuwa na haki ya kuchagua mume, lakini alikuwa na hiari ya kufanya ndoa ya haramu ikiwa baba yake alishindwa kumuoza baada ya kuwa amevunja ungo. Katika hali hiyo, pia hakuruhusiwa kurithi chochote kutoka kwa baba yake. Hapakuwa na kikomo cha idadi ya wanawake ambao mwanaume angeweza kuoa. Kumbukumbu za Wagiriki zinaonyesha kuwa mume alikuwa akimiliki mamia ya wanawake katika nyumba yake.

Vitabu vya kidini vya Wazoroastria vinaonyesha kuwa kanuni za ndoa katika zama za Sasania zilikuwa tata na zilizokorogeka. Urithi wa mwanamke katika Uislamu. Sheria ya mirathi ya Kiislamu imeepukana na mapungufu yote ya huko nyuma. Kitu kinachopingwa na wale wanaodai kutetea usawa kati ya mwanaume na mwanamke, ni kwamba gawio la mwanamke ni nusu ya gawio la mwanaume.

Kwa mujibu wa sheria ya Kiislamu mtoto wa kiume hupata mara mbili ya mtoto wa kike, kaka hupata mara mbili ya dada yake na mume hupata mara mbili ya kile anachopata mke wake. Gawio la baba na mama ndio halifuati utaratibu huu. Ikiwa marehemu ana watoto, na wazazi (wa huyo marehemu) wako hai, kila mmoja wa wazazi wawili atapata moja ya sita ya mali iliyoachwa na marehemu. Ni kutokana na nafasi maalum ya mwanamke katika mahari, matunzo, huduma za kijeshi na baadhi ya sheria za jinai ndio maana gawio lake limefanywa kuwa nusu ya lile la mwanaume.

Kwa sababu zilizotajwa hapo awali, Uislamu unachukulia matunzo na mahari kuwa ni mambo muhimu na ya lazima katika kuiimarisha ndoa. Yanatoa hakikisho la maelewano na masikilizano. Kuyaondoa ni kulitikisa jengo zima la familia na kumsukumia mwanamke katika umalaya. Kwa vile mahari na matunzo ni wajibu wa lazima wa mume, basi ni wazi kuwa majukumu ya kifedha ya mwanamke yamepunguzwa sana na mzigo wa mwanaume umeongezwa. Ili kufidia jukumu zito alilonalo mwanaume, gawio lake la urithi limepangwa kuwa mara mbili ya lile la manamke.

Ni mahari na matunzo yaliyopunguza gawio la mwanamke. Pingamizi la wa-Magharibi. Baadhi ya watu wa Magharibi wanapokosoa udogo wa gawio la mwanamke la urithi na wanapolitumia hili kama silaha ya propaganda dhidi ya Uislamu, wanadai kuwa hakuna ulazima wowote wa kupunguza gawio la mwanamke ili kuja kulifidia kwa mahari na matunzo. Je, kuna haja yoyote ya kupita vichochoroni na kuzunguka vichaka? Kwanini gawio la mirathi la mwanamke lisilingane na gawio la mwanaume ili tusilazimike kulifidia kwa mahari na matunzo?

Hawa mabwana ambao wanaonekana kumpenda mfalme kuliko mfalme mwenywe anavyojipenda wamechanganya habari. Sababisho wamelipeka kwenye matokeo na matokeo wameyapeleka kwenye sababisho. Wanafikiri kuwa mahari na matunzo ni matokeo ya nafasi ya pekee kuhusiani na urithi, wakati ambapo ukweli ni kinyume chake. Aidha, wanaelekea kuwa na mawazo kuwa kipengele cha fedha ndio kitu pekee kinachozingatiwa, kama hiki kingekuwa ndio kigezo pekee basi kusingekuwa na haja ya mfumo wa mahari na matunzo wala mfumo unaotoa tofauti ya gawio kati ya mwanaume na mwanamke.

Kama tulivyoeleza mwanzo, Uislamu umezingatia vipengele vingi, vingine ni vya asili na vingine ni vya kisaikolojia. Umezingatia mahitaji maalumu ya mwanamke, yanayotokana na jukumu lake la uzazi. Kimsingi mwanaume hana mahitaji hayo. Mbali na hayo, kwa upande mwingine, uwezo wa mwanamke wa kuzalisha ni mdogo kuliko wa mwanaume na kwa upande mwingine matumizi yake ni makubwa kuliko ya mwanaume.

Kwa nyongeza, kuna vipengele vingine mbali mbali vya kujirembesha kuhusiana na mfumo wa akili zao. Kwa mfano mwanaume mara zote hupenda kutumia fedha zake kwa ajili ya mwanamke anayempenda. Vipengele vingine vya kisaikolojia na kijamii, vinavyosaidia kuimarisha mahusiano ya kifamilia pia vimezingatiwa. Kwa kuzingatia nukta zote hizi, Uislamu umefanya mahari na matunzo kuwa ni wajibu wa lazima. Hivyo sio suala la pesa, ambalo inaweza kusemwa kwamba kuna haja ya kupunguzwa mgao wa mwanamke sehemu moja na kumfidia sehemu nyingine. Pingamizi la waasi wa kipindi cha awali cha Uislamu. Tumesema kuwa mahari na matunzo ni sababisho na nafasi ya pekee ya mwanamke na tofauti zilizopo katika mirathi ni matokea yake. Nukta hii haijaanzishwa leo. Ilikuwepo hata katika siku za awali za Uislamu.

Katika karne ya pili Hijria alikuwepo mtu mmoja aliyeitwa Ibn Abi alAwja, ambaye hakuwa akiamini juu ya dini. Kwa kutumia fursa ya uhuru wa kidini (imani) ya wakati ule alikuwa akielezea waziwazi mawazo yake ya kikafiri. Wakati fulani alikuwa akija katika Masjid al-Haram (Makka) au Masjid Nabawi (Madina) na alikuwa akijibizana na wanavyuoni wa wakati ule juu ya kanuni za Uislamu.

Moja ya pingamizi lake dhidi ya Uislamu lilihusu mirathi. Alikuwa akisema; "Ana kosa gani huyu mwanamke maskini anayepata sehemu moja wakati mwanaume anapata sehemu mbili." Kwa mujibu wake yeye hii ilikuwa ni dhulma kwa mwanamke. Imam Jafar as-Sadiq(as) katika kumjibu alisema kuwa:hali iko hivyo kwa sababu mwanamke amesamehewa kazi za jeshi. Na zaidi ya hilo Uislamu umemuamrisha mwanaume kulipa mahari na kumtunza mkewe na katika baadhi ya kesi za jinai ambapo ndugu wa mhalifu walipaswa kulipa fedha za damu (kufidia mtu aliyeuliwa) mwanamke aliondolewa (alisamehewa) katika malipo hayo. Hizi ndio sababu zilizofanya gawio lake lipunguzwe. Hivyo Imam Jafar Sadiq(as) alieleza wazi wazi nafasi ya pekee ya mwanamke juu ya mirathi, sheria ya mirathi na matunzo, kusamehewa kwake kutoa huduma ya jeshi na malipo ya fedha za damu. Maimamu wengine pia walijibu hivyo hivyo walipoulizwa swali hilo.

13

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU

I- TALAKA

Hakuna zama kama hizi za kwetu ambapo uzingativu umefanywa sana kwenye hatari ya kusambaratika kwa familia na madhara yake. Na tena, hakuna zama kama hizi za kwetu ambapo mtu amekabiliana na hatari halisi ya kusambaratika huko. Kuongezeka kwa Talaka katika maisha ya kisasa. Huko nyuma uzingativu sana haukuwekwa katika tatizo la talaka, sababu zake na madhara yake pamoja na mbinu za kulizuia vilikuwa havijadiliwi sana na bado idadi ya talaka ilikuwa ndogo sana. Hakuna shaka kuwa ongezeko la talaka hivi sasa ikilinganishwa na zamani linatokana na kuongezeka kwa sababu za talaka.

Maisha ya kijamii yamebadilika mno kiasi cha kuwa sasa kuna uwezekano mkubwa zaidi wa kuvurugika kwa familia, na hii ndio sababu jitihada za wasomi na watu wanaoshughulikia masuala ya kijamii zimeshindwa kuzaa matunda. Inasikitisha kuwa kizazi kijacho kinakubaliwa na hatari zaidi. Gazeti la Kimarekani, 'Newsweek' katika makala inayovutia yenye kichwa cha habari 'Divorce in America' (Talaka katika Marekani) linaandika kuwa ukiwa Marekani ni rahisi zaidi kupata talaka kuliko kupata taksii.

'Newsweek' linaandika zaidi kuwa methali mbili kuhusu talaka zinajulikana zaidi miongoni mwa Wamarekani kuliko methali nyingine zozote zile. Mojawapo ni kuwa 'Usuluhishi mgumu kabisa kati ya mume na mke ni bora kuliko talaka.' Methali hii ina umri wa miaka 400 na zaidi. Ya pili ambayo imebeba ujumbe ulio kinyume na hii methali ya kwanza imepata umaarufu katika nusu ya pili ya karne ya 20. Inasema kuwa 'penzi la pili ni tamu zaidi kuliko la kwanza." Makala inaonyesha kuwa methali ya pili ndiyo inayofanya kazi zaidi nchini Marekani. Jinamizi la talaka linajivutia kwake, sio kwa ndoa mpya tu, bali hata za mama zao na za wanandoa waliooana zamani huko.

Tangu wakati wa Vita vya pili vya Dunia na kuendelea, kwa wastani idadi ya talaka kwa mwaka si chini ya laki nne (400,000). Katika hizo ndoa zilizovunjika, 40% zilikuwa zimeweza kudumu kwa miaka kumi na zaidi na 13% ndizo zilikuwa zimeweza kudumu kwa zaidi ya miaka 20. Wastani wa umri wa talaka (umri wa wanawake wanaotalikiwa) wa wanawake milioni mbili ilikuwa ni miaka 45, 62% ya hao walikuwa na watoto wenye umri wa chini ya miaka 18 wakati ndoa ilipokuwa inavunjika. Wanawake hawa, kwa kusema kweli, wanaunda kizazi maalum.

Ingawa mwanamke wa Kimarekani hujisikia huru kabisa baada ya talaka, lakini bado hao waliotalikiwa, wawe vijana au wa umri wa kati, huwa hawana furaha. Kutokuwa kwao na furaha kunaweza kupimwa kutokana na ongezeko la idadi ya wanawake wanaowaita madaktari wa akili au ambao ni walevi wa kupindukia. Katika kila wanawake wanne, mmoja ni mlevi.

Idadi ya wanawake waliotalikiwa wanaojinyonga ni kubwa mara tatu kuliko ya wale wenye waume. Kwa kifupi ni kuwa mara tu mwanamke anapoibuka mshindi katika mahakama ya talaka hugundua kuwa maisha baada ya talaka sio kitanda cha maua ya waridi. Ni vigumu ulimwengu kuwa na maoni mazuri juu ya mwanamke anayeivunja ndoa yake, nyumba thabiti kabisa ya mahusiano ya mwanadamu. Jamii inaweza kumheshimu mwanamke huyo na pengine kumuonea wivu, lakini haiwezi kumuona kuwa ni mtu aliyeingia katika maisha ya mtu na kumletea furaha (mumewe).

Katika makala hii ya gazeti la Newsweek suali limeibuka kuwa ongezeko hili la talaka linalozidi kukua linatokana na mwenendo usio kubaliana kati ya mume na mke, au sababu nyingine. Mwandishi wa makala hii amesema kuwa hata kama tofauti za tabia na kutopatana zitakubaliwa kuwa sababu ya kutengana kwa wanandoa waliooana hivi punde, nini tunaweza kusema juu ya talaka za wanandoa walioishi ndani ya ndoa kwa muda mrefu?

Tukizingatia msaada wa kisheria unaotolewa na sheria ya Marekani kuhusiana na talaka, tunaweza kusema kuwa kutofautiana kwa mihemko na tabia sio sababu ya kutengana kwa wanandoa walioishi kwa miaka kumi au zaidi. Katika zama za vidonge vya kuzuia mimba, mapinduzi ya ngono (ufuska) na kuboreka kwa hadhi yao ya kisheria, wanawake wengi wametokea kuamini kuwa furaha na raha ni bora kuliko uimara wa maisha ya ndoa.

Mara nyingi unaweza kuona kuwa mume na mke wanaishi pamoja kwa miaka, wana watoto, kila mmoja anashiriki furaha na huzuni ya mwenzake lakini ghafla mke anaomba talaka bila ya kuwepo mabadiliko yoyote ya ki-mali au hadhi na makubaliano ya mume. Sababu ni kuwa, mpaka jana, mwanamke alikuwa tayari kuvumilia uchoshi wa maisha, lakini hayuko tayari kufanya hivyo leo.

Ongezeko la kesi za talaka haliko Marekani peke yake. Sehemu yoyote ambayo utamaduni wa Kimagharibi umejipenyeza kwa kiasi fulani, kiwango cha talaka kiko juu. Hata katika nchi za Mashariki, talaka imekuwa ni jambo la kawaida zaidi katika miji mikubwa ya kisasa kuliko katika miji midogo na vijiji. Mazingira yanayochangia talaka nchini Marekani. Tayari tumeshalinukuu gazeti la Newsweek likisema kuwa mwanamke wa kimarekani hujali zaidi starehe na burudani kuliko uthabiti na uimara wa maisha ya familia.

Sasa hebu tupige hatua moja mbele ili tuone kwanini amechukua mwelekeo huo. Hapana shaka kwamba tabia hii sio ya asili wala ya kuzaliwa nayo. Imetokana na sababu fulani za kijamii. Ni mazingira ya Marekani yaliyosababisha akili hii ya mwanamke wa Kimarekani. Baadhi ya watu wa Magharibi wanafanya jitihada kubwa kumsukumia mwanamke wa Mashariki katika mwenendo wanaoufuata wanawake wa Kimarekani.

Kama wakifanikiwa majaaliwa ya mwanamke wa Mashariki na familia ya Mashariki hayatakuwa na tofauti na yale ya mwanamke wa kimarekani na familia ya Kimarekani. Gazeti maarufu la Ufaranza litolewalo kila siku linaandika kuwa katika migahawa zaidi ya 200 na nyumba za kulala wageni katika jimbo la Califonia, wafanyakazi (wahudumu) wa kike wanavaa nguo za nusu uchi. Nguo hizo ambazo ni za kuogelea zinatambuliwa kuwa ndio sare za kazini katika miji ya San-Fransisco na Los Angeles.

Katika jiji la New York kuna kumbi nyingi za sinema zinazoonyesha filamu za ngono tu, na picha za uchi za wanawake zinaweza kuonekana zikionyeshwa mbele ya milango ya kuingilia kumbini. Majina ya filamu za ngono ni ya aina hii; "Wanaume wanaobadilishana wake zao', 'Wasichana wasio na maadili,' 'Magauni ambayo hayafichi chochote.' Maktaba kuna vitabu vichache sana vya hadithi za kubuni (fiction books) ambavyo katika majalada yake hakuna picha za wanawake walio uchi.

Majina ya vitabu kama vile 'Tabia ya ngono ya wanaume wa kimarekani,' 'Tabia ya ngono ya wanaume wa Kimagharibi,' Tabia ya ngono ya vijana walio chini ya miaka 20,' 'Mbinu mpya za ngono zilizotokana na habari mpya kabisa," vimekuwa maarufu na vingi mno. Mwandishi wa makala katika gazeti hili la Kifaransa anauliza kwa mshangao na wasiwasi; "Marekani unakwenda wapi?' Katika mazingira kama haya ikiwa mwanamke wa Kimarekani amepoteza mizania yake na anajali burudani na raha zaidi kuliko uaminifu kwa mume wake na familia, hawezi kulaumiwa. Ni mazingira ya kijamii ambayo yameharibu kila mzizi wa mfumo wa utakatifu wa familia.

Inashangaza kuwa viongozi wa zama zetu wanazipa nguvu na msukumo zaidi sababu zinazosababisha talaka na kusambaratika kwa maisha ya familia na kwa upande mwingine wanapiga mayowe na kelele kuwa kiwango cha talaka kimekuwa kikubwa mno. Hii ni sawa na kumwambia mtu afagie bohari na kuomba asichafue nguo zake. Nadharia tano. Hebu tuangalie, iwapo kimsingi talaka ni nzuri au mbaya. Swali ni je ni jambo zuri kuuacha wazi mlango wa talaka, hata katika hatari ya kusambaratika kwa maisha ya familia? Ikiwa ni jambo zuri basi hakuna tatizo hata kama kiwango cha talaka kitakuwa kikubwa.

Na ikiwa sio jambo zuri, je talaka ipigwe marufuku kabisa na ndoa ifanywe kuwa ya milele? Wazo la tatu ni kuwa talaka isipigwe marufuku kisheria, kwani katika baadhi ya hali haiepukiki, lakini wakati huo huo jamii ichukue kila hatua inayowezekana kuondosha sababu za mikwaruzano na kutengana kwa mume na mke na hivyo kuwanusuru watoto kukosa familia.

Ni dhahiri kuwa sheria peke yake haiwezi kufanya chochote ikiwa jamii yenyewe inazipalilia sababu zinazosababisha talaka. Ikiwa talaka haifai kupigwa marufuku kabisa, je iruhusiwe katika muundo gani? Je ni nani awe na mamlaka ya kutoa talaka? Mwanaume peke yake, mwanamke peke yake au wote? Na wazo la mwisho ni kuwa je mwanaume na mwanamke wote wafuate taratibu zinazofanana katiksa kutoa au kuomba talaka au kila jinsia iwe na utaratibu wake?

Yote kwa yote, hizi ni nadharia tano zinazohusiana na Talaka: Talaka inayotolewa bila kikwazo chochote cha kisheria au kimaadili. Hawa ni wale wanaoitazama ndoa kwa mtazamo wa kupata raha tu, ambao hawaipi utakatifu wowote, na ambao hawajali thamani ya kijamii ya familia. Wanafikiri kuwa mara tu baada ya ndoa kuvunjika na ndoa mpya kuchukua nafasi ya ndoa ya zamani (iliyovunjilka) wanaume na wanawake walioachana hupata furaha zaidi.

Yule anayesema kuwa penzi la pili ni tamu kuliko penzi la kwanza ndiye huiunga mkono nadharia hii. Katika nadharia hii, sio tu kwamba thamani ya kijamii ya kifamilia imesahauliwa lakini pia furaha na kuridhishana kunakosababishwa na ndoa kumepuuzwa pia. Hivyo nadharia hii ni ya kipuuzi na ya kitoto kabisa. Ndoa ni taasisi takatifu. Ni muungano wa mioyo na roho, taasisi ambayo lazima itunzwe kwa usalama na isiharibiwe.

Neno talaka linapaswa kuondolewa kutoka katika kamusi ya jamii ya wanaadamu. Mwanaume na mwanamke wanaooana lazima wajue kuwa hakuna kitakachowatenganisha zaidi ya kifo. Hii ndio nadharia ambayo imekuwa ikitetewa na Kanisa Katoliki kwa karne nyingi na bado inatetewa. Wanaoiunga mkono nadharia hii wanazidi kupungua dunaini.

Hivi sasa ni Italia na Hispania tu wanoifuata. Ni mara nyingi tu tunasikia kwamba, hata Italia, wanaume na wanawake wanaipinga sheria hii na jitihada zinafanyika ili sheria ya talaka itambuliwe rasmi. Watu wengi hawako tayari kuendelea kutaabika na michosho ya ndoa zao zisizo na mafanikio. Miaka kadhaa huko nyuma, gazeti la 'The Daily Express' lilichapisha makala yenye kichwa cha habari, 'Ndoa Italia ina maana kifungo kwa mwanamke.' Makala hii ilisema kuwa, hivi sasa kutokana na kutokuwepo kwa talaka, watu wa Italia wanajiingiza katika mahusiano ya haramu (zinaa). Zaidi ya Waitalia milioni tano walikuwa wakiamini kuwa maisha yao yamejaa madhambi. Gazeti la Italia litolewalo kila siku liliandika kuwa kuzuia talaka kumesababisha tatizo kubwa sana kwa Waitalia. Wengi wao walilazimika kuukana uraia wa Italia kwa sababu hiyo.

Taasisi fulani ya Italia ilipoitisha kura ya maoni, 97% ya wanawake wa Italia walijibu 'hapana' kwa swali lililoulizwa kuwa iwapo talaka ilikuwa ni jambo linalochukiza katika kanuni za dini. Bado kanisa linashikilia msimamo wake na kuendelea kutoa hoja kuutetea (msimamo huo). Hapana shaka yeyote kuwa ndoa ni taasisi takatifu na inatakiwa idumu. Lakini inaweza tu kudumu iwapo wanandoa wote wawili wanashirikiana. Kuna hali ambapo maelewano kati ya mke na mume huwa hayawezekani.

Katika hali kama hizi nguvu za sheria haziwezi kuwapatanisha na kuwaunganisha kwa jina la muungano wa ndoa. Nadharia ya kanisa imeshindwa kabisa kufanya kazi. Sio ajabu muda si mrefu kanisa lenyewe likabadilisha msimamo wake. Hivyo hatuhitaji kuijadili nadharia hii zaidi. Ndoa inaweza kuvunjwa na mwanaume sio mwanamke.

Katika ulimwengu wa zamani watu wengi walikuwa na mtazamo huu, lakini sasa hatudhani kuwa una wafuasi. Hivyo hatuhitaji kuijadili pia. Ndoa ni taasisi takatifu na mfumo wa kifamilia unaheshimika, lakini mlango wa kutoa talaka kwa masharti fulani, uwe wazi kwa wanandoa wote na taratibu za kuvunja ndoa zinapaswa zifanane kwa jinsia zote mbili.

Watetezi wa kufanana kwa haki za familia ambao kwa makosa walikuita usawa wa haki kati ya mwanaume na mwanamke, wanaiunga mkono nadharia hii. Kwa mujibu wa watu hawa, masharti yanayofanana, mipaka inayofanana na vikwazo vinavyofanana vinapaswa vitumike kwa wote wawili, mwanamke na mwanaume wakati wa kuvunja ndoa. Wanapinga suluhishi jingine ambalo ni la kidhalimu na linalobagua.

Hapana shaka ndoa ni taasisi takatifu, mfumo wa familia unaheshimika, talaka ni jambo linalochukuza na ni jukumu la jamii kuondoa visababisho vyote vya talaka, lakini bado talaka haiwezi kuzuiwa moja kwa moja na kwamba mamlaka ya kutoa au kuomba talaka yapo kwa wote wawili, mwanamke na mwanaume. Hata hivyo utaratibu wa kufuatwa katika uvunjaji wa ndoa uwe tofauti kati ya jinsia hizi mbili. Talaka ni moja ya haki zisizofanana (lakini zinazolingana) kati ya mwanaume na mwanamke. Hii ndio nadharia inayowakilisha maoni ya Uislamu na nchi za Waislamu zinaifuata.

14

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU

II- TALAKA KATIKA ZAMA ZETU

Talaka imekuwa tatizo la dunia kwani wote wanalinung'unikia na kulilalamikia. Wale ambao sheria zao zinazuia talaka kabisa wanalalamikia kutokuwepo kwa njia ya kuepuka ndoa zisizo na mafanikio. Halikadhalika wale walioruhusu talaka, wanaume na wanawake, wanalalamikia ongezeko la talaka na kuyumba kwa maisha ya familia na madhara yake. Wale waliotoa haki ya kutoa talaka kwa wanaume peke yao, wanaeleza kutoridhishwa kwao na mambo mawili.

Kwanza: baadhi ya watu wa ovyo, baada ya miaka ya maisha ya ndoa, ghafla huwataliki wake zao wa zamani ambao wameishi nao katika kipindi bora kabisa cha ujana wao (hao wanawake) kwa sababu tu sasa wanatamani kuwa na mke mpya.

Pili: baadhi ya watu wakorofi wanakataa kuwataliki wake zao, na ilhali hakuna uwezekano wowote wa kufikia maelewano na kuendelea na maisha ya ndoa pamoja.

Mara nyingi hutokea kuwa, kwa sababu mbali mbali tofauti kati ya mume na mke hufikia hatua ambayo hakuna uwezekano wowote wa usuluhishi, na kiuhalisia wanatengana. Katika hali hiyo, njia pekee ya maana ni kuvunja uhusiano wao kisheria, uhusiano ambao kiuhalisia tayari umeshavunjika na kumruhusu kila mmoja wao kutafuta mwenzi mpya maishani. Lakini baadhi ya wanaume ili kuwatesa wake zao na kuwanyima haki ya kufurahia unyumba, hukataa kuwataliki wake zao.

Wanamuacha mwanamke, kwa mujibu wa Qur'ani, katika hali ya kuning'inia (talaka ya kuangika). Watu hawa wako mbali kabisa na mafundisho ya Uislamu, ingawa wanatumia mamlaka ya sheria ya Kiislamu kwa tabia yao isiyofaa. Mwenendo wao huwapa maoni wale wasiojua Uislamu vyema kuwa hivi ndivyo Uislamu unavyotaka talaka iwe.

Wakosoaji wanauliza kwa kejeli kuwa iwapo ni kweli kwamba Uislamu umeruhusu wanaume kuwatesa wake zao kadri wapendavyo wakati fulani wanawapa talaka na wakati fulani wanaibatilisha na bado wakati huo huo wanajiridhisha mioyoni mwao kuwa wametumia haki yao halali na ya kisheria.

Wakosoaji wanasema kuwa kitendo hiki ni mfano mzuri wa dhuluma na ukatili. Wanauliza: "Kama ni kweli, kama Waislamu wanavyodai kuwa sheria za Kiislamu zimeundwa kwa kuzingatia msingi wa haki na uongofu, je ni hatua gani ambazo Uislamu umechukua kuzuia aina hii ya dhulma?" Juu ya ukatili na dhulma ya matendo hayo, hakuna shaka yeyote kuwa ni matendo yasiyofaa.

Uislamu, kama tutakavyoonyesha hapa, umezingatia hali hii na una njia za kukabiliana na tatizo hili. Swali muhimu ni: ipi njia bora ya kuzuia dhulma na ukatili huu? Je vitendo vya dhulma vinatokana na ubovu wa sheria ya talaka? Au sababu zake zitafutwe sehemu nyingine? Je matendo haya yanaweza kukomeshwa kwa kurekebisha sheria au hatua nyinginezo zinapaswa kuchukuliwa? Uislamu una njia zake za kutatua matatizo ya kijamii. Baadhi wanafikiri kuwa yanaweza kutatuliwa kwa imma kuunda sheria mpya au kurekebisha zilizopo. Lakini Uislamu unaelewa kuwa sheria ina mipaka yake. Inaweza kufaa tu katika mahusiano makavu ya kimikataba. Lakini katika mahusiano ya hisia za moyo (kama mapenzi), sheria peke yake haiwezi kufanya mambo mengi, na lazima tuangalie hatua nyingine pia. Kama tutakavyoonyesha baadaye Uislamu unaitumia vyema nguvu ya sheria pale tu ambapo kweli sheria inaweza kufanya kazi. Haujashindwa katika hili.

TALAKA ZA AIBU/ ZA KUUMBUA

Kwanza tuliangalie tatizo la talaka za kuumbua na kuaibisha katika zama hizi. Kimsingi, Uislamu unapinga kabisa talaka. Unataka talaka isiwepo. Umeiruhusu talaka kama njia ya mwisho ambapo kutengana hakuepukiki. Wale wanaoowa wake wapya kila mara na kuwaacha wa zamani, Uislamu unawakana na umewaita kuwa ni maadui wa Mwenyezi Mungu. Kitabu maarufu cha hadithi, al-Kafi, kinasimulia kisa kifuatacho; Mtukufu Mtume alimuuliza mtu mmoja; "Umemfanya nini mke wako?" Akasema "Nimemtaliki,' Mtume akamuuliza; "Je ulimuona anafanya jambo lolote baya?" "hapana sikuona." Mwanaume yule alioa tena. Mtume akamuliza, 'Je umeoa mke mwingine?" "Ndio" Baada ya muda fulani Mtume akamuuliza tena, "Umemfanya nini mke wako?" Nimemtaliki" Je amefanya kosa lolote?" "Hapana" Mtu yule alioa mara ya tatu. Mtume akamuliza tena kama alikuwa ameoa mke mpya. Akajibu ndio, Baada ya muda fulani Mtume akamuuliza tena, "Umemfanya nini mke wako?" "Nimemtaliki" "Je amefanya kosa lolote?" "Hapana". Mtume akasema kuwa Mwenyezi Mungu hampendi na anamchukia mtu ambaye hubadilisha wake kila mara, na wanawake wanaobadilisha waume kila mara. Watu hao ni maadui wa Mwenyezi Mungu. Iliripotiwa kwa Mtume kuwa Abu Ayub Ansari alikuwa ameamua kumtaliki mke wake. Mtume alikuwa akimjua mwanamke huyo vizuri.

Alijua pia kuwa uamuzi wa Abu Ayub haukuwa na sababu za maana. Mtume akasema, "Kumtaliki Umme Ayub (mke wa Abu Ayub) ni dhambi kubwa." Mtume alisema kuwa Jibril alimuusia mno juu ya kuwatendea wema wanawake mpaka akahisi kuwa hairuhusiwi kumtaliki mwanamke isipokuwa kama amezini. Imam Ja'far Sadiq(a.s) amesema kuwa: Mtukufu Mtume(s.a.w.w) amesema;"Hakuna kitu kinachopendeza kwa Mwenyezi Mungu kama nyumba ambayo ndani yake ndoa inafungwa na hakuna jambo linalochukiza mbele ya Allah kama nyumba ambayo ndani yake talaka inatolewa."

Imam Ja'afar Sadiq(a.s) pia amesema kuwa: neno'Talaka' limetajwa tena na tena katika Qur'ani na maelezo yake ya kina yametolewa kwa sababu Allah anachukia kutengana kwa wanandoa. Al-Tabarisi katika kitabu chake "Makarim al- Akhlaq" amemnukuu Mtume akisema:"Oeni lakini msitoe talaka kwani talaka huitikisa Arshi ya Mwenyezi Mungu".

Hadithi kama hizi pia zimo katika vitabu vya Kisunni. Abu Daud katika kitabu chake, Sunan amesimulia kwamba Mtume amesema:"Mwenyezi Mungu hajaruhusu jambo lolote lenye kuchukiza kama talaka." Kwa maneno mengine, ingawa Allah ameruhusu talaka, bado talaka ndilo jambo analolichukia mno. Viongozi wakubwa wa kidini (Maimamu) walikuwa wakijiepusha mno kutoa talaka kwa kadri inavyowezekana. Katika maisha yao matukio ya talaka yalikuwa na sababu za msingi sana. Kwa mfano, Imam Baqir(a.s) alimuona mwanamke.

Alikuwa akimpenda sana mke huyo, lakini wakati fulani aligundua kuwa mwanamke huyu alikuwa na chuki na uadui mkubwa dhidi ya Imam Ali ibn Abi Talib. Ilimbidi amtaliki. Alipoulizwa kwa nini alimtaliki na ilhali alikuwa akimpenda sana, Imam alisema kuwa hakutaka kuishi na kaa la moto wa Jahanamu pembeni yake. Uvumi usio na msingi. Inafaa kuelezea hapa uvumi usio na msingi uliotungwa na makhalifa wa ukoo wa Abbas. Uvumi huu ulienea mno kiasi cha kuweza kurekodiwa na waandishi mashuhuri katika vitabu vyao. Kwa mujibu wa uvumi huo, Imam Hassan Mujtaba(a.s) , mtoto wa Imam Ali ibn Abi Talib(a.s) ni mmoja wa wale waliooa wake wengi na kuwataliki.

Uvumi huo ulienezwa karne moja baada ya kufariki kwa Imam. Uvumi huu ulienezwa mno kiasi cha kuwa hata wafuasi wake waliuamini bila kuzingatia ukweli kuwa kitendo hicho cha kuchukiza sio stahili ya Imam Mtukufu na kisingetarajiwa kwake, mtu aliyekuwa akienda Hija kwa miguu, na aligawa nusu ya mali yake kwa maskini zaidi ya mara ishirini.

Kama tunavyojua, tofauti na watoto wa kizazi cha Imam Husayn(a.s) ambao waliongozwa wakati ule na Imam Sadiq(a.s.) watoto wa kizazi cha Imam Hassan(a.s) walishirikiana na Bani Abbas wakati wa kuuangusha utawala wa kiukoo wa Bani Umayya. Awali Bani Abbas walielezea imani na utii wao kwa watoto wa kizazi cha Imam Hassan(a.s) , lakini walipofanikiwa kupata madaraka waliwasaliti na wengi wao waliwatenga, ama kwa kuwaua au kwa kuwafunga gerezani. Katika kuendeleza sera yao hii, Bani Abbas walianzisha kampeni za propaganda dhidi ya kizazi cha Imam Hassan(a.s) .

Moja ya hila walizozifanya ilikuwa ni kumshutumu babu yake na Imam Hassan ambaye pia ni ami yake na Mtukufu Mtume, Abu Talib(a.s) , kuwa hakupata kusilimu na alikufa kafiri. Walitaka kujenga hoja kuwa wao kwa vile ni kizazi cha ami mwingine wa Mtume, aliyekuwa amesilimu, wanastahili zaidi kuwa makhalifa. Ili kufikia lengo lao walitumia fedha nyingi sana na walibuni visa vingi vya uongo. Idadi kubwa ya Masunni ambao walishawishika na propaganda hizi, bado wanaamini kuwa Abu Talib alikuwa kafiri.

Ingawa utafiti wa hivi karibuni kabisa uliofanywa na wanazuoni wa Kissuni umebainisha ukweli wa jambo hili kwa kiasi kikubwa, lakini hata hivyo bado baadhi yao wanatia shaka. Uzushi mwingine uliozushwa na Bani Abbas, ulikuwa kwamba Imam Hassan(a.s) alirithi ukhalifa baada ya baba yake, lakini kwa vile alikuwa mtu muasherati, hakuweza kutawala vizuri na akalazimika kuusalimisha ukhalifa kwa adui yake makini, Muawiya ambaye alimpatia fedha na kwa kutumia fedha hizo Imam Hassan alijishughulisha na kuoa na kutoa talaka.

Kwa bahati nzuri, utafiti wa wanazuoni wa zama zetu umekiweka wazi chanzo cha uzushi huu. Mtu wa kwanza kutamka uzushi huu alikuwa ni Kadhi (Qazi) aliyeteuliwa na khalifa Mansur aliyemwelekeza kubuni na kusambaza uzushi dhidi ya Imam. Mwanahistoria mmoja, alipokuwa akitoa maoni yake dhidi ya uongo huu, anahoji kuwa ikiwa Imam Hassan(a.s) alioa wanawake wengi kiasi hicho mbona watoto wake hatuwaoni? Kwa nini idadi ya watoto wake ni ndogo? na ilhali tunajua kuwa Imam hakuwa tasa na njia za kuzuia mimba au kutoa mimba hazikuwa mila ya zama hizo?

Tunashangaa wepesi wa kuamini wa baadhi ya wakusanyaji wa hadithi za Kishia. Wanaweza vipi kuandika kuwa Imam Hassan(a.s) alikuwa na tabia ya kutaliki wanawake, wakati wao wenyewe wanaripoti kuwa Mtukufu Mtume na Maimamu wamesema kuwa Allah anaichukua talaka na anamkana mwanaume ambaye ana tabia ya kuwataliki wake zake.

Kamwe haikutokea kwa mabwana hawa kuchagua moja katika haya mambo matatu; (i) Talaka si kitu kibaya, (ii) Imam Hassan(a.s) hakuwa na ada ya kuwataliki wakeze au (iii) Imam Hassan(a.s) hakuambatana na mafundisho ya Uislamu. Lakini cha ajabu ni kuwa si tu wanaamini juu ya usahihi wa hadithi inayosema talaka inachukiza mbele ya Allah, lakini pia wakati huo huo, licha ya kuwa wafuasi waaminifu kwa Imam, wananukuu ripoti kuwa, Imam alikuwa na tabia ya kuwataliki wanawake mara kwa mara. Wanaziruka ripoti hizi bila kuzitolea maelezo.

Baadhi ya wanahadith (Muhadithina) wamekwenda mbali zaidi kiasi cha kusimulia kwamba Imam Ali(a.s) hakuwa akifurahia tabia ya mtoto wake. Katika hotuba yake ya hadhara aliwaomba watu wasimuozeshe binti zao kwa vile alikuwa na tabia ya kuwataliki. Lakini inasemekana kuwa watu walijibu kuwa lilikuwa ni jambo la fahari kwao kwamba binti zao walipata kuwa wake za mtoto (mjukuu) wa Mtume hata kwa muda mfupi.

Inaelekea kuwa baadhi ya watu walikuwa na fikra kuwa talaka si jambo baya ikiwa mwanamke mwenyewe na familia yake walikuwa radhi. Wanafikiri kuwa talaka inachukiza tu iwapo upande wa pili haikuridhia, lakini hakuna tatizo kabisa kama mwanamke ameridhia kuishi na mwanaume anayejifaharisha naye kwa siku chache. Hata hivyo huu sio uhalisia. Ridhaa ya mwanamke au wazazi wake haibatilishi ubaya wa talaka.

Talaka inachukiza kwa vile Uislamu unataka ndoa idumu na familia iwe imara. Ridhaa ya wanandoa pia haibadilishi ubaya wa talaka. Uislamu hauioni talaka kuwa inachukiza kwa baadhi tu ya tabaka la wanawake. Ni suala la kanuni.

Tumelijadili suala hili la Imam Hassan(a.s) si tu kwa nia ya kuurudia uongo wa kihistoria dhidi ya mtu mwenye umuhimu wa kihistoria, lakini pia kuwaonya wale watu waovu ambao wanaweza kujiingiza kwenye vitendo vya namna hii na kuhalalisha tabia yao hii kwa kutumia mfano wa Imam Hassan(a.s) kama kiigizo chao.

Hapana shaka yoyote kuwa talaka ni jambo lenye kuchukiza sana katika Uislamu. Kwa nini Uislamu haukuharamisha talaka? Hapa maswali kadhaa yanaibuka. Kama talaka haipendezi na inachukiwa kiasai hicho na Allah, kwa nini haikuharamishwa moja kwa moja na Uislamu? Uislamu ungekuwa angalau umeweka masharti ya kuthibitisha usahihi wa talaka (yaani yawepo mambo ambayo hayo yakifanywa yatachukuliwa kuwa ni sababu tosha ya kutoa talaka).

Katika hali hiyo mtu yeyote ambaye angetaka kumtaliki mke wake angelazimika kisheria kueleza sababu zake za msingi mbele ya mahakama ya sheria za kutaka kutoa talaka. Swali la pili ni kuwa; "Sentensi hii ina maana gani?: Katika vitu vyote vilivyoruhusiwa, talaka ndio kitu kinachochukiwa zaidi kwa Mwenyezi Mungu." Kama inaruhusiwa haiwezi kuchukiza na kama inachukiza haiwezi kuruhusiwa. Kuruhusiwa na kuchukiza ni maneno mawili yanayokinzana. Mwisho, je idara ya mahakama inayoiwakilisha jamii, ina haki ya kuingilia suala la talaka kiasi cha kuweza kuibatilisha? Au kuweza kusikiliza mashauri mpaka idhihirike kuwa usuluhishi hauwezekani na hivyo hakuna namna isipokuwa kuvunja ndoa?

5

HAKI ZA WANAWAKE KATIKA UISLAMU

MWANAMKE KATIKA QUR'ANI

Sasa tunataka kujibu swali iwapo Uislamu unamtazama mwanamke kuwa ni sawa na mwanaume kama binadamu au unamuona ni wa hadhi ya chini kuliko mwanaume. Falsafa maalum ya Uislamu juu ya haki za kifamilia. Kuhusiana na haki za mwanaume na mwanamke, Uislamu, una falsafa yake maalum ambayo ni tofauti, yale yaliyotokea miaka 1400 iliyopita na yanayotokea hivi sasa. Uislamu hauamini kuwa katika mambo yote mwanaume na mwanamke wana haki na majukumu yanayofanana.

Katika mambo fulani haki na majukumu yao ni tofauti na matokeo yake ni kuwa katika baadhi ya mambo nafasi yao inafanana na ya wanaume na katika baadhi ya mambo haifanani na ya wanaume. Hii sio kwa sababu Uislamu, kama falsafa nyingine, unamtazama mwanamke kwa dharau au jinsia yake sio bora kama ya mwanaume.

Uislamu unazitofautisha jinsia hizi mbili kwa sababu nyinginezo za msingi. Unaweza kuwasikia wafuasi wa mifumo ya Kimagharibi wakitaja kanuni za Kiislamu kama vile mahari, matunzo, talaka, ndoa za mitala na mengineyo, kuwa haya yote ni kama matusi kwa mwanamke na yanashusha hadhi yake. Wanawapotosha watu kuwa sheria na kanuni hizi hazina maana na ulazima na zinamfanya mwanaume aonekane ni bwana mkubwa. Wanasema kwamba katika kipindi chote cha historia, kabla ya karne ya 20, sheria na kanuni zote duniani ziliwekwa kwa kuzingatia kuwa mwanaume ni mwenye jinsia bora zaidi na kwamba mwanamke aliumbwa kwa maslahi na starehe ya mwanaume. Sheria zilizopitishwa na Uislamu pia ziko hivyo hivyo, zinampendelea mwanaume.

Wanadai kuwa Uislamu ni dini ya jinsia ya kiume. Hawamtambui mwanamke kuwa ni binadamu kamili. Hii ndio sababu haujampa haki sawa na mwanaume. Ungekuwa unamtambua kuwa ni binadamu kamili usingeruhusu ndoa za mitala (mke zaidi ya mmoja), usingehesabu ushahidi wa wanawake wawili kuwa ni sawa na wa mwanaume mmoja, usingeamuru gawio la mwanamke liwe nusu ya gawio la mwanaume, usingeamrisha papangwe bei ya mwanamke chini ya kivuli cha mahari na usingemfanya mwanamke awe tegemezi kwa mwanaume kwa upande wa matunzo, badala ya kufanya ajitegemee kiuchumi na kijamii.

Kwa kuzingatia yote haya ni dhahiri kuwa mafundisho ya Uislamu yanamtazama mwanamke kwa jicho la dharau. Uislamu unadai kuwa dini ya usawa lakini, katika mahusiano ya kifamilia hakuna usawa wowote uliozingatiwa. Wanashikilia kuwa katika suala la haki, Uislamu wazi wazi unampendelea mwanaume na ndio maana umempa miliki zote hizi. Tukipenda tunaweza kuweka hoja yao katika muundo wa kimantiki kuwa: Kama Uislamu unamhesabu mwanamke kuwa ni binadamu kamili ungekuwa umempa haki sawa na zinazofanana na zile za mwanaume, maadamu haujafanya hivyo basi haumhesabu kuwa ni binadamu kamili.

Usawa au kufanana? Hoja hii imejengwa juu ya msingi kwamba kwa vile heshima ya binaadamu ni sawa kwa mwanaume na mwanamke, hivyo lazima wote wapate haki zinazofanana bila kujali majukumu yao katika maisha. Hapana shaka, utu na heshima yao ni sawa kwao wao wote; wote wanapaswa kuwa na haki sawa. Lakini vipi kuhusu kufanana kwa haki zao?

Ikiwa badala ya kufuata kibubusa mawazo ya Kimagharibi tutaamua kufikiri sisi wenyewe, swali la kwanza linalokuja akilini ni iwapo kweli haki sawa zinamaanisha haki zinazofanana. Kwa kweli hayo ni mambo mawili tofauti. Usawa ni haki ya kuwa na daraja sawa kithamani na hadhi ambapo kufanana maana yake ni kulandana. Inawezekana baba akagawa mali zake kwa watoto wake watatu kwa usawa lakini sio kwa kulingana. Jaalia mali yake inajumuisha vitu mbali mbali kama vile maduka, mashamba na badhi ya mali zilizokodishwa. Baba kwa kuzingatia vipaji vyao na mambo ambayo kila mmoja anapenda, anaamua kumpa mmoja duka, mwingine shamba na wa tatu mali zilizokodishwa.

Anazingatia kuwa thamani ya mali aliyopewa kila mmoja wao ni sawa na wengine na kila mmoja amepewa kutokana na kipaji chake. Hivyo aligawa mali yake kwa usawa lakini sio kwa kulingana. Uwingi ni tofauti na ubora, na usawa ni tofauti na kufanana. Uislamu hauamini juu ya kulingana (uniformity) kwa mwanaume na mwanamke. Lakini wakati huo huo hauwapendelei wanaume katika maswala ya haki. Umezingatia kanuni ya usawa kati ya mwanamke na mwanaume lakini haukubaliani na kufanana kwa haki zao. Usawa ni neno linalifurahisha, kwa sababu linaashiria hali ya kutobagua. Lina utukufu maalum. Linaamsha na kuleta heshima, hasa linapohusiana na haki. Ni neno zuri lilioje 'Usawa na Haki.' Mtu yeyote mwema atafurahishwa na uzuri wake. Lakini hatuwezi tukaelewa ni kwa jinsi gani mambo yalifika hatua hii kiasi cha kuwa wengine ambao walikuwa vinara wa sayansi na falsafa nao wanataka kuingiza mawazo yao juu ya kufanana kwa haki kati ya wanawake na wanaume huku kwetu.

Hii ni sawa na mtu kuuza viazi vitamu kwa jina la mapeasi. Hapana shaka kuwa Uislamu haujatoa haki zinazofanana kati ya mwanaume na mwanamke katika mambo yote. Lakini pia haujaamuru majukumu na adhabu zinazofanana kwa jinsia hizi mbili. Yote kwa yote ni kuwa thamani ya jumla ya haki za mwanamke sio ndogo kuliko ile ya mwanaume. Tunataka kuthibitisha nukta hii. Hapa linazuka swali, kwa nini haki za mwanaume na mwanamke hazijafanana katika mambo yote. Je isingekuwa vizuri zaidi kama haki zao zingekuwa zinafanana katika mambo yote? Ili kulijadili hili swali kikamilifu, tutajadili chini ya vichwa vya habari vitatu. Mtazamo wa Uislamu juu ya nafasi ya mwanamke kutokana na maumbile yake. Athari za tofauti za kimwili kati ya mwanaume na mwanamke. Je, hili linasababisha tofauti ya haki zao pia? Ni nini falsafa ya sheria za Kiislamu, ambazo wakati fulani zinatofautisha kati ya mwanaume na mwanamke? Je falsafa hii bado ni thabiti?

Nafasi ya mwanamke katika utaratibu wa Kiislamu.

Qur'ani sio mkusanyiko tu wa sheria. Sio chombo cha sheria na kanuni kavu bila maelezo ya madhumuni yake. Ina sheria na pia ina historia, mawaidha ya kidini, maelezo ya malengo ya maisha, na maelfu ya mambo mengine katika sehemu mbalimbali, Qur'ani huelezea mambo yenye sura ya kisheria na katika sehemu nyingine hueleza lengo la maisha. Hufunua siri za dunia, mbingu, mimea, wanyama na wanaadamu. Huelezea siri za maisha na kifo, heshima na aibu, kupanda na kushuka, mali na umaskini.

Qur'ani sio kitabu cha falsafa, lakini kimeelezea kwa ufasaha sana maoni yake (Qur'ani) juu ya falsafa ya masomo matatu ya msingi; Ulimwengu, mwanadamu na jamii. Haiwafundishi wafuasi wake sheria peke yake, na haijishughulishi na mawaidha na nasaha (maonyo) peke yake, bali kwa kupitia tafsiri yake ya maisha (maumbile), huwapa wafuasi wake mtazamo maalum na namna pekee ya kufikiri. Msingi wa kanuni za Kiislamu juu ya masuala ya kijamii kama vile umiliki, serikali, haki za kifamilia n.k ni tafsiri ya maisha na mambo mengine tofauti tofauti.

Moja ya mambo yaliyoelezwa katika Qur'ani ni kuumbwa kwa mwanaume na mwanamke. Qur'ani haijakaa kimya juu ya jambo hili. Haijaacha mwanya kwa wadukuzi wa kifalsafa kuibua falsafa yao juu ya kanuni za mwanaume na mwanamke. Uislamu umetoa maoni yake juu ya mwanamke. Ili kujua maoni ya Uislamu juu ya mwanamke, tutazame Qur'ani inachosema juu ya tabia yake ya ndani. Dini nyingine pia zimelizungumzia suala hili, lakini ni Qur'ani peke yake ambayo katika Aya kadhaa inaelezea wazi wazi kuwa mwanamke ameumbwa kutokana na spishi za mwanaume, na wote mwanamke na mwanaume wana tabia za ndani zinazofanana.

Akimzungumzia Adam, Mwenyezi Mungu anasema;"Yeye (Allah) aliwaumba nyinyi wote kutokana na nafsi moja, na kutokana nayo (hiyo nafsi moja) akamuumbia mwenza wake (Suratun-Nisaa 4:1). Na juu ya mwanadamu kwa ujumla, Qur'ani inasema; "Amewaumbieni wake zenu kutokana na nyinyi. ' (Suratul Nisaa, Suratul Aali Imran na Suratul Ruum). Tofauti na vitabu vingine vya kidini hakuna sehemu yoyote katika Qur'ani ambapo imetajwa kuwa mwanamke ameumbwa kwa kutumia vitu duni au kuwa ana asili ya ukupe au ni wa asili ya upande wa kushoto. Uislamu hauungi mkono dhana ya kibiblia kuwa mwanamke ameumbwa kutokana na ubavu wa kushoto wa Adam. Uislamu hauna mtazamo wa dharau juu ya asili ya mwanamke na tabia zake za ndani.

Kuna nadharia nyingine ya dharau kwa wanawake iliyokuwa imeenea sana siku za nyuma, na imeacha alama mbaya katika siku za nyuma, na imeacha alama mbaya katika fasihi ya dunia. Kwa mujibu wa nadharia hiyo mwanamke ndio chanzo cha madhambi yote. Kuwepo kwake tu kunahamasisha uovu. Mwanamke ni shetani mdogo. Inasemekana kuwa katika kila dhambi na uhalifu uliotendwa na mwanaume kuna mkono wa mwanamke. Wanaume wenyewe hawatendi madhambi, ni wanawake wanaowasukumia kwenye madhambi. Pia inasemekana kuwa shetani hawezi kumwendea mwanaume moja kwa moja. Ni kupitia mwanamke ndio huwapotosha wanaume.

Shetani humchochea mwanamke na mwanamke humchochea mwanaume. Adam aliondolewa peponi kwa sababu ya mwanamke. Shetani alimshawishi Hawa, na ni Hawa aliyemshawishi Adam. Qur'ani imesimulia kisa hiki cha peponi lakini hakuna iliposema kuwa shetani au nyoka alipompotosha Hawa na Hawa akampotosha Adam. Haimlaumu Hawa wala haimuondoi katika hatia. Qur'ani inasema;"Tulimwambia Adam, 'Kaa Peponi; wewe na mke wako, na kuleni humo matunda popote mpendapo lakini msiusogelee mti ule msije kuwa miongoni mwa madhalimu ." (Suratul Baqara, 2:35). Inaweka kiwakilishi cha watu wawili. Pia Qur'ani inasema; "Kisha Shetani aliwatia wasiwasi." "Naye akawaapia (kuwaambia) kwa hakika mimi ni mmoja wa watoao shauri njema kwenu . (Suratul Aaraf 7:20-21).

Hivyo Qur'ani inapinga vikali dhana ya uongo iliyokuwa imeenea sana wakati wa kuteremshwa Qur'ani na miwangwi ambayo bado inasikika katika sehemu mbali mbali za dunia hii leo. Ilimuondoa mwanamke katika mashitaka kwamba yeye ni mchochezi wa dhambi na kwamba yeye ni shetani mdogo. Nadharia nyingine ya dharau kwa mwanamke ambayo imekuwepo ni juu ya nafasi ya kiroho ya mwanamke.

Ilidaiwa kuwa mwanamke hawezi kuingia peponi. Hana uwezo wa kiroho na msaada wa Mungu kumuwezesha kufanya hivyo. Hana uwezo wa kufikia ukaribu wa Mwenyezi Mungu kama mwanaume anavyoweza kufanya. Lakini Qur'ani katika Aya mbali mbali imesema wazi wazi kuwa malipo ya pepo na ukaribu na Mwenyezi Mungu havitegemei jinsia ya mtu.

Inategemea na imani na amali (vitendo), na hakuna tofauti kati ya mwanamke na mwanaume juu ya hili katika Qur'ani, wametajwa watakatifu wa kiume na watakatifu wa kike. Qur'ani imewatukuza wake wa Adam na Ibrahim na mama yake Nabii Isa na Musa. Imewataja wake wa Nuhu na Lut kuwa hawakuwa stahili ya waume zao na haijamshahau mke wa Firauni ambaye ametajwa kuwa ni mwanamke mtukufu aliyekuwa mikononi mwa mwanaume muovu. Katika visa vyake Qur'ani imeweka mizania. Mashujaa wake ni wa kiume na wa kike. Wakati, ikimzungumzia mama yake Nabii Musa, Qur'ani inasema, "Tulimjulisha mama yake Musa kwa kumwambia;'Muweke katika sanduku na mtupe katika mto. Mawimbi yatamfikisha ufukweni . (Suratul Taha; 20:39). Juu ya mama yake Issa, Qur'ani inasema kuwa alifikia daraja tukufu ya kiroho kiasi kwamba malaika walikuwa wakiongea naye wakati anasali. Alikuwa akipokea chakula kutoka peponoi. Daraja la kiroho lilimshangaza hata Zakaria, Mtume wa wakati huo.

Kumekuwa na mifano mingi ya wanawake mashuhuri na watakatifu katika historia ya Uislamu. Ni wanaume wachache tu wanaweza kufikia daraja la Khadija, mke kipenzi wa Mtume(s.a.w.w) na hakuna mwanaume anayefikia daraja la bibi Fatima Zahra, binti kipenzi wa Mtume isipokuwa Mtume mwenyewe na Imam Ali(a.s) . Ana daraja kubwa kuliko hata la watoto wake ambao ni Maimamu, na hata la Mitume wote isipokuwa Mtume wa mwisho.

Uislamu hauwabagui wanawake dhidi ya wanaume katika 'safari ya kumuendea Allah' isipokuwa humuona mwanaume kuwa mwenye kufaa zaidi kuchukua jukumu la utume, ambalo yaweza kuelezewa kama safari ya kurudi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwenda kwa watu. Nadharia nyingine ya dharau kwa wanawake inahusiana na kujihini na kutooa/kutoolewa. Baadhi ya dini zinaona kuwa tendo la ndoa ni kitu kichafu, kwa mujibu wa imani ya wafuasi wake, wanaoweza kufikia kilele cha juu cha daraja la kiroho ni wale tu ambao watamaliza maisha yao yote bila kuoa/kuolewa. Kiongozi mmoja wa dunia wa kidini anasema, "Kateni mti wa ndoa kwa shoka ya ubikira.' Viongozi hawa wa kidini wanavumilia ndoa tu kama uovu wenye nafuu.

Kwa maneno mengine wanashikilia kuwa kwa kuwa watu wengi hawawezi maisha ya bila kuoa/kuolewa na inaeleweka kwamba hawataweza kujidhibiti na hivyo kujiingiza katika zinaa za wanawake/wanaume wengi, basi ni bora waoe ili wasije kukutana na mwanamke zaidi ya mmoja. Watu hawa wanatetea kukaa bila kuoa au kuolewa na kujihini kwa sababu wanaona tendo la ndoa si kitu kizuri. Wanaona upendo kwa mwanamke kuwa ni uovu mkubwa wa kimaadili.

Uislamu unapinga vikali upuuzi huu. Unaiona ndoa kuwa ni taasisi tukufu na kukaa bila kuoa/kuolewa kuwa ni uchafu. Kumpenda mwanamke ni sehemu ya tabia ya Mtume. Mtukutu Mtume amesema; "Napenda vitu vitatu, manukato, mwanamke na swala." Bertrand Russel anasema, "Dini zote, isipokuwa Uislamu, zinalitazama tendo la ndoa kwa jicho baya. Uislamu unalitazama kwa maslahi ya kijamii, umeliwekea utaratibu maalum na kulidhibiti, lakini haulitazami kama uchafu." Nadharia nyingine ya dharau kwa mwanamke ni kuwa mwanamke ameumbwa kwa maslahi ya mwanaume. Uislamu hausemi hivyo. Umeeleza malengo ya maisha kwa uwazi kabisa. Imeeleza kuwa dunia, mbingu, hewa, mawingu, mimea na wanyama vyote vimeumbwa kwa ajili ya mwanadamu. Haijasema mwanamke ameumbwa kwa ajili ya mwanaume. Kwa mujibu wa Qur'ani mwanaume ameumbwa kwa ajili ya mwanamke na mwanamke ameumbwa kwa ajili ya mwanaume.

'Wao (wanawake) ni nguo zenu na nyinyi (wanaume) ni nguo zao (2:187). Ingekuwa Qur'ani imeeleza kuwa mwanamke ni nyongeza (kiambatanisho) ya mwanaume na aliumbwa kwa ajili ya starehe yake (mwanaume) mtazamo huu ungekuwa umetazamwa katika sheria za Kiislamu, lakini Qur'ani haijasema hivyo. Hauyaelezei malengo ya maisha hivi. Haumuoni mwanamke kuwa ni kiambatanisho tu cha mwanaume. Ndio maana mtazamo huu haujazingatiwa katika sheria za Kiislamu. Nadharia nyingine ya dharau kwa mwanamke ni kuwa mwanamke ni uovu usioepukika. Katika siku za nyuma, watu walimtazama mwanamke kwa dharau sana na walimuona kuwa ni chanzo cha mikosi na aina zote za matatizo.

Kinyume chake Qur'ani imesisitiza kuwa mwanamke ni baraka kwa mwanaume na ni chanzo cha raha na faraja kwake. Kwa mujibu wa nadharia nyingine ya dharau kwa mwanamke ni kuwa hawakuthamini mchango wa mwanamke katika uzazi. Waarabu wa kabla ya Uislamu na baadhi ya jamii nyingine waliomuona mwanamke kama mfuko tu wa kukuzia mbegu ya mwanaume.

Sehemu mbali mbali ya Qur'ani imesema:'Tumewaumba kutokanana na mwanaume na mwanamke. ' Wazo hili limeelezwa katika Aya nyingine za Qur'ani. Hivyo Uislamu ulikomesha fikra hiyo kuwa mwanamke ni mfuko tu wa kukuzia mbegu ya mwanaume. Ni dhahiri sasa kuwa Uislamu hauna kabisa mitazamo yoyote ya kumdharau mwanamke. Sasa muda umefika wa kueleza kwa nini haki za mwanaume na mwanamke hazifanani. Ni kufanana, hapana, Ni kulingana, sawa.

Tayari tumeshasema kuwa katika suala la mahusiano ya kifamilia na haki za mwanamke na mwanaume, Uislamu una falsafa yake ambayo ni tofauti kabisa na ile iliyokuwa ada (kawaida), miaka 1400 iliyopita na ilivyo sasa. Pia tumesema kuwa hakuna ubishi wowote kuwa mwanaume na mwanamke ni sawa kama binadamu na haki zao za kifamilia zinapaswa kuwa sawa kithamani. Kwa mtazamo wa Uislamu wao wote ni binadamu na hivyo wana haki sawa. Nukta inayopaswa kuangaliwa hapa ni kuwa mwanaume na mwanamke, kwa sababu ya tofauti zao za kijinsia, wanatofautiana katika mambo mengi. Asili yao haitaki wafanane.

Nafasi hii inataka wasifanane katika haki nyingi, majukumu, wajibu na adhabu. Katika nchi za Magharibi jitihada inafanyika sasa kuzifanya haki na majukumu yao kufanana, na kupuuza tofauti zao za asili na za ndani. Hapa ndio kuna tofauti kati ya mtazamo wa Kiislamu na mfumo wa Kimagharibi katika nchi yetu, nukta inayobishaniwa ni suala la kufanana kwa haki sio usawa wa haki kati ya mwanamke na mwanaume. Usawa wa haki ni nembo tu ambayo imewekwa kwa makosa katika zawadi hii ya Kimagharibi.

Mwandishi wa kitabu hiki katika vitabu na hotuba zake mara zote amejiepusha kutumia nembo hii ya uongo na kamwe hajakubali kulipa jina la usawa jambo ambalo kiuhalisia ni kufanana kwa haki. Ulaya ya kabla ya karne ya 20 ni mfano dhahiri wa dhulma kwa mwanamke. Mpaka mwanzoni mwa karne ya 20 mwanamke wa Ulaya alinyimwa haki za kibinadamu katika maisha ya kila siku na kisheria. Hakuwa na haki sawa wala zinazofanana na mwanaume.

Ni katika muongo uliopita ambapo kutokana na harakati za pupa, wameanza kumpa haki zake za msingi, lakini bado hajaweza kupata haki zinazochukuana na maumbile yake na mahitaji yake kimwili na kiroho. Kama mwanamke anataka haki na usawa na furaha katika familia lazima alitupilie mbali wazo la kufanana kwa haki. Hiyo ndio njia pekee ya kuimarisha uchangamfu kati ya mwanaume na mwanamke.

Katika hali hiyo, sio tu kwamba mwanaume atazikubali haki za mwanamke, lakini pia atakuwa tayari kumpatia, na katika baadhi ya mambo atatoa haki nyingi zaidi tena bila kumdanganya. Halikadhalika hatudai kuwa katika jamii ya Kiislamu mwanamke anapata haki sawa na mwanaume. Mara nyingi tumesema kuwa ni muhimu kwamba nafasi ya mwanamke iangaliwe upya na apewe haki lukuki ambazo Uislamu umempatia, na ambazo amekuwa akinyimwa katika kipindi chote cha historia. Hata hivyo, haifai kuiga staili na mifumo ya Kimagharibi kibubusa, mifumo ambayo imesababisha madhara makubwa huko Magharibi kwenyewe.

Tunachodai ni kuwa kutofanana kwa haki kati ya mwanaume na mwanamke, kwa mujibu wa mipaka ya maumbile na tofauti zao ndio kutenda haki zaidi. Hukidhi mahitaji ya haki za asili vizuri zaidi, hutoa hakikisho kwa furaha ya familia na huisukuma jamii mbele katika njia ya maendeleo bora zaidi. Inaweza kukumbukwa kuwa tunadai kuwa haki ya asili inataka kwamba, katika baadhi ya mambo, kuwe na kutokufanana kwa haki ya mwanaume na mwanamke.

Kwa vile linahusiana na falfsafa ya haki, suala hili lina sura ya kifalsafa asilimia mia moja. Linahusiana pia na kanuni ya haki na usawa, kanuni kuu za sheria ya Kiislamu na falsafa ya uanazuoni wa Kiislamu. Ni kanuni ya usawa iliyoleta mafundisho ya kukubaliana kati ya akili na sheria ya Mwenyezi Mungu. Kwa mujibu wa elimu ya sheria ya Kiislamu au tuseme ya Kishia, kama ikithibitika kuwa usawa unataka kuwa katika hali fulani, basi sura hiyo ndiyo itachukua sura ya kisheria bila kujali hoja zozote nyingine dhidi yake, kwani kwa mujibu wa mafundisho ya msingi ya Uislamu, sheria lazima katika hali yoyote isivunje au kuhalifu uadilifu wa asili na haki na za msingi.

Wanazuoni wa Kiislamu kwa kufafanua kanuni za usawa waliweka msingi wa falsafa ya haki, ingawa kufuatia matukio fulani ya kihistoria yasiyofurahisha, hawakuweza kuiendeleza kazi nzuri waliyoianza. Walikuwa ni Waislamu ambao, kwa mara ya kwanza walilitupia macho suala la haki za kibinadamu na kanuni za usawa, na walizitoa katika haki yake ya asili na kama kanuni zinazojitegemea bila kuathiriwa na sheria za kimikataba. Waislamu walikuwa vinara katika fani ya haki za asili za binadamu. Lakini hawakujaaliwa kuiendeleza kazi yao na hatimaye, baada ya karne nane, iliendelezwa na wasomi na wanafalsafa wa kizungu na wakajichukulia sifa hiyo.

Wazungu walileta falsafa za kijamii, kisiasa na kiuchumi na walijulisha watu, jamii na mataifa juu ya thamani ya maisha na haki za binadamu. Kwa maoni yetu mbali na sababu za kihistoria kulikuwa na sababu za kisaikolojia na kimkoa pia, ambazo ziliwazuia Waislamu wa Mashariki (Asia) kuendeleza suala la haki za msingi za binadamu.

Ni moja ya tofauti kati ya hulka ya nchi za Mashariki (Asia) na zile za Magharibi. Nchi za Mashariki zinazingatia maadili na za Magharibi zinazingatia haki. Mtu wa Mashariki ana upendo zaidi na anaamini kuwa lazima asamehe awe na moyo wa ubinadamu. Lakini mtu wa Magharibi anaamini kuwa kama binadamu lazima azijue na kuzilinda haki zake na lazima asiruhusu wengine wazipore. Utu unahitaji maadili na haki pia. Utu unahusiana na haki na maadili. Moja tu katika hizi haitoshi kuwa kigezo cha sifa bora za binadamu. Uislamu ulikuwa na hadi sasa unazingatia yote mawili haki na maadili.

Katika Uislamu, dhati, kusamehe, na matendo mema ni sifa takatifu na za kibinadamu. Lakini wakati huo huo mtu kujua haki zake na kuwa tayari kuzitetea, ni jambo takatifu na la kibinadamu. Hata hivyo, nchi za Mashariki kwa kiasi kikubwa zimekaliwa na Waislamu, na kwa hiyo, japokuwa awali yote yalikuwa yakizingatiwa maadili na haki lakini pole pole walijikuta wanabaki kushikilia maadili peke yake. Hivi sasa tunashughulikia suala la haki ambalo pia linaweza kuwa suala la kifalsafa na linafaa kujadiliwa kwa kirefu.

Inahusiana sana na maana halisi ya haki na ukweli halisi wa haki uadilifu na sheria uliokuwepo hata kabla ya kuwepo kwa sheria duniani, na ambao maana zake haziwezi kubadilishwa na sheria yoyote.

Montesquieu anasema, "Kabla ya sheria kutungwa na watu, kulikuwepo mahusiano yenye uadilifu baina ya watu kwa msingi wa sheria ambazo zilitawala mahusiano baina ya vitu vyote vilivyokuwepo. Ni kuwepo kwa mahusiano haya kulikosababisha kuundwa kwa sheria hizi. Kusema kwamba kabla ya watu kutunga sheria hapakuwa na uadilifu au dhuluma katika kuyaongoza na kuyadhibiti mahusiano ya watu ni sawa na kusema kuwa kabla ya mduara kuchorwa, nusu vipenyo vyake havilingani." Herbert Spencer anasema; "uadilifu unachaganganyika na kitu fulani mbali na hisia; yaani haki za msingi za binadamu. Lazima tuheshimu haki za binadamu ili uadilifu uwepo kiuhalisia." Wengi wa wasomi wa Ulaya wana mtazamo kuwa maazimio yote ya haki za binadamu yamechukuliwa kutoka katika haki za msingi za binadamu. Kwa maneno mengine, haki za msingi za binadamu zimechukuwa sura ya maazimio ya haki.

Kama tunavyojua, Montesquieu, Spencer n.k. wamesema kitu kimoja, juu ya uadilifu kama walichosema wanafalsafa wasomi wa Kiislamu juu ya msingi wa razini wa wema na uovu na kanuni ya usawa. Miongoni mwa Waislamu wamekuwepo wasomi ambao wamekana kuwepo kwa haki za asili na wanashikilia kuwa uadilifu ni jambo la kimkataba.

Halikadhalika, imani hii imekuwepo miongoni mwa wazungu. Mwanafalsafa wa Kiingereza, Thomas Hobbes alikana kabisa na akadai kuwa uadilifu sio kitu halisi. Azimio la haki za binadamu ni falsafa sio sheria. Ni kejeli kusema kuwa Azimio la Dunia la haki za binadamu ambalo linatoa hakikisho la usawa wa haki kati ya mwanaume na mwanamke, imeidhinishwa na Bunge la nchi fulani, wanaume na wanawake wa nchi hiyo wanapaswa kuwa na haki sawa.

Hata hivyo, si jambo lililo katika mamlaka ya kisheria kwa Bunge la nchi yoyote kuidhinisha au kukataa Azimio kwa vile yaliyomo humo kwenye Azimio, hayana sura ya kimkataba, hivyo hayaangukii kwenye mamlaka yake ya kisheria. Azimio la Dunia hushughulikia haki za asili, zisizoondosheka na zisizobatilishika za binadamu na kama inavyodaiwa na Azimio lenyewe, haki hizi ni sehemu muhimu na ya lazima ya heshima ya mwanadamu na zimebuniwa na mamlaka yenye nguvu ya maumbile yenyewe.

Kwa maneno mengine, haki hizi zimetolewa na kupewa wanaadamu na chanzo kile kile kilichowapa akili, utashi na heshima. Kama ni hivyo, hali ya mambo yaliyomo katika Azimio hili inalazimisha kuwa hakuna mamlaka yoyote ya binadamu inayoweza kuyabuni au kuyafuta. Sasa hapa linakujaje suala la kuidhinisha Azimio hilo katika chombo cha kutunga sheria? Kwa kusema kweli, Azimio la Haki za Binadamu ni falsafa sio sheria. Na kama ni hivyo inafaa kuidhinishwa na wanafalsafa na sio na watunga sheria (wabunge).

Hakuna Bunge ambalo linaweza kutunga falsafa kwa kulumbana na kupiga kura. Vinginevyo kwa nini, muswada unaoelezea nadharia ya Einstein juu ya 'relativity' (kwamba vipimo vya mwendo nafasi na wakati vinawiana) au nadharia nyingine inayosema kuwa kuna maisha katika karne nyingine haijapelekwa Bungeni ili ikaidhinishwe na chombo kitukufu? Kiuhalisia, sheria ya asili haiwezi kupitishwa au kukataliwa kama sheria ya kimkataba.

Kupitisha sheria ya asili (maumbile) ni sawa na kupitisha sheria kuwa kupandikiza chipukizi la mpeasi kwenye muepo (tufaa) kutafanikiwa lakini kupandikiza mpeasi kwenye mforosadi (mulberry) hakutafanikiwa. Kila azimio lolote linapotolewa na kikundi cha wanafalsafa, kila taifa hupeleka kwa wanafalsafa wake, na kama watalipitisha basi ndio wananchi wote wa nchi hiyo wanapaswa kuzingatia maelekezo yake kama ukweli wa ziada wa kisheria. Mamlaka ya kisheria itapaswa kutopitisha sheria inayopingana na maelekezo hayo.

Lakini mataifa mengine hayatalazimika kuyazingatia maazimio haya maadamu hayajathibitishwa, kwa mujibu wa maoni yao, kuwa haki hizo zipo duniani. Na zaidi ya haya, kwa vile suala hili haliwezi kupimwa au kujaribiwa, halihitaji vifaa au maabara n.k Ni suala la kifalsafa ambalo vifaa vyake ni ubongo, akili na nguvu ya hoja. Hata kama mataifa mengine yatalazimika kuwafuata walio wengi katika suala la mantiki na falsafa na wanahisi kuwa hawana uwezo wa kutosha wa kufikiri kifalsafa wao wenyewe, sisi Waislamu hatuwezi kufuata mfano wao.

Tumeonyesha huko nyuma kuwa tuna uwezo mkubwa wa kushughulikia masuala ya mantiki na kifalsafa. Kwanini tuwafuate wengine leo? Inashangaza kwamba wakati wasomi wa Kiislamu walitilia uzito sana kanuni ya uadilifu na haki za msingi za binadamu na wanazikubali kama sheria ya dini, bila kusita wala ubishi wowote, yote haya yakakubaliwa na akili (kuwa ni haki), leo mambo yameharibika kiasi cha kuwa tunataka wabunge waidhinishe kutambuliwa kwa haki za binadamu. Falsafa haiwezi kuthibitishwa kwa kujaza kuponi.

Ni kejeli na dhihaka kubwa kuliko hata hiyo iliyotangulia, kujaribu kuamua suala la haki za binadamu kwa kuandaa kura za maoni kwa wavulana wadogo na wasichana wadogo. Je ni akili kweli kuchapisha kuponi na kuwaambia wavulana na wasichana wadogo waijaze ili kujua asili ya haki za binadamu na kama ni za aina moja au mbili. Hata hivyo, hapa tunataka kulijadili suala la haki za mwanamke kwa utaratibu mzuri na kifalsafa, na kwa kuzingatia haki za msingi za binadamu.

Tungependa kujua kama kanuni zinazotaka wanadamu wote wapate na kufaidi haki zao za msingi walizopewa na Mwenyezi Mungu, zinalazimisha au hazilazimishi kuwa mwanaume na mwanamke wawe na nafasi moja sawa katika haki zao. Tunawaomba wasomi, wanafalsafa na wanasheria wa nchi yetu, ambao wanaweza kuwa ni watu pekee wenye mamlaka ya kutoa maoni juu ya suala hilo na kuziangalia hoja zetu kwa jicho la umakinifu.

Tutawashukuru sana kama watatoa maoni yao ya kimamlaka kukubaliana na hoja zetu au kuzipinga. Katika kulijadili suala hili, ni muhimu kwanza kujadili msingi wa haki za binadamu. Haki za mwanaume na mwanamke zitajadiliwa baadaye. Katika muktadha huu, haitakuwa makosa kuzungumzia kidogo harakati za kutaka mabadiliko katika karne chache zilizopita, ambazo zimeleta wazo la usawa wa haki kati ya mwanaume na mwanamke.

Tazamo fupi la historia ya haki za wanawake Ulaya. Mazungumzo ya haki za binadamu yalianza karne ya 17. Waandishi na wanafalsafa wa karne ya 17 na 18, kwa uvumilivu mkubwa, waliyatangaza na kuyaeneza mawazo yao juu ya suala la haki za msingi na zisizobatilishika za binadamu. Jeans-Jacques Rouseau,Voltaire na Montesquieu ni miongoni mwa waandishi na wanafalsafa hawa. Matokeo ya kwanza ya kivitendo ya kuenea kwa mawazo yao yalikuwa ni mapambano ya muda mrefu kati ya watawala na raia wa Uingereza. Mwaka 1688 Waingereza walifanikiwa kumshawishi mfalme akubali kuwapa baadhi ya haki za kisiasa na jamii walizokuwa wameziandika katika hati iliyojulikana kama 'The Bill of Rights.' Matokeo mengine muhimu ya kuenea kwa mawazo haya yalikuwa ni Vita vya Uhuru vya Wamarekani dhidi ya Uingereza.

Makoloni kumi na tatu ya Uingereza huko Amerika ya kaskazini yaliasi, kufuatia kuwekewa kodi kubwa sana, na hatimaye walipata uhuru wao. Mwaka 1776 mkutano ulifanyika Philadelphia, mkutano ambao ulitoa Azimio la Uhuru. Dibaji yake inasema; "Tunauchukulia ukweli huu kuwa dhahiri kwamba watu wote wameumbwa wakiwa sawa na kwamba wamepewa na muumba wao haki fulani zisizoondosheka, na kwamba miongoni mwa hizo ni haki ya kuishi, uhuru na kupata furaha au kufurahia.

Ili kuhakikisha kupatikana kwa haki hizi, serikali zinawekwa na watu, zinapata madaraka yao kutokana na idhini ya watawaliwa; na kwamba wakati wowote serikali ya muundo wowote inapokiuka malengo haya, ni haki ya watu kuibadilisha au kuiondoa, na kuweka serikali mpya, ikijengwa chini ya msingi wa kanuni hizi na kupata madaraka yake kwa utaratibu huu, itawahakikishia wananchi usalama na furaha yao.

Na lile linaloitwa Azimio la Haki za Binadamu lilitolewa baada ya Mapinduzi ya Ufaransa, lina kanuni fulani za jumla zinazoonekana kuwa sehemu muhimu na ya lazima ya katiba ya Ufaransa. Azimio lina dibaji na ibara 17. Ibara ya kwanza inasema kuwa watu wote huzaliwa wakiwa huru na hubaki huru katika maisha yao yote. Haki zao zinafanana. Katika karne ya 19 mawazo mapya yalitokeza katika uwanja wa haki za binadamu kiuchumi, kijamii na kisiasa. Haya yalisababisha kuibuka kwa ujamaa, ushiriki wa wafanyakazi katika faida na kuiondoa serikali kutoka mikononi mwa mabepari kwenda mikoni mwa wavuja jasho (wafanyakazi).

Hadi mwanzoni mwa karne ya 20, majadiliano yote yalikuwa yamejikita juu ya haki ya watu dhidi ya serikali au haki za tabaka la wavuja jasho dhidi ya waajiri na makabaila. Katika karne ya 20, suala la haki za mwanamke dhidi ya haki za manaume liliibuka. Ni juzi tu katika karne ya 20 ambapo Uingereza iliyokuwa ikijulikana kama demokrasia kongwe, ilipotambua usawa wa haki kati ya mwanaume na mwanamke. Ingawa Marekani kiujumla ilikuwa imezitambua haki za binadamu katika karne ya 18 katika Hati ya Azimio la uhuru, lakini bado haki ya kupiga kura kwa wote ilitolewa mwaka 1920.

Ufaransa pia ilitoa haki ya wanawake kupiga kura katika karne ya 20. Kwa kiasi fulani, katika karne ya 20 sehemu kubwa ya watu duniani walijitokeza kuunga mkono mabadiliko makubwa katika mahusiano kati ya mwanaume na mwanamke, katika nyanja za haki na majukumu. Kwa mujibu wao lengo la uadilifu wa kijamii halingeweza kufikiwa kwa kufanya mabadiliko baina ya mataifa na kati ya wafanyakazi na waajiri na mabepari bila pia kuleta mabadiliko katika mahusiano kati ya mwanaume na mwanamke.

Hii ndio maana dibaji ya Azimio la Haki za Binadamu kwa wote, lililotolewa mwaka 1948 linasema kwamba "Ambapo heshima ya utu wa mtu mmoja mmoja na usawa wa haki kati ya mwanaume na mwanamke" Machafuko yaliyosababishwa na maendeleo ya kuboreka kwa mashine (mitambo) katika karne ya 19 na 20, na hali mbaya ya wafanyakazi iliyofuatia, hasa kwa wafanyakazi wa kike, yalisababisha macho yaelekezwe kwenye masaibu ya mwanamke na ndio maana suala la haki zao lilizingatiwa sana.

Mwanahistoria anasema, "Kwa vile serikali ilikuwa haijali, masaibu ya wafanyakazi na tabia ya waajiri wao, mabepari walifanya walivyopenda". Wamiliki wa viwanda walikuwa wakiwaajiri wanawake na watoto kwa ujira mdogo sana, na kwa vile masaa ya kufanya kazi yalikuwa mengi mno, wengi wao waliugua magonjwa mbali mbali na wengine walikufa katika umri mdogo." Hii ilikuwa ni historia fupi ya harakati za Haki za Binadamu Ulaya.

Kama tunavyojua, ibara zote za Azimio la Haki za Binadamu ambazo ni mpya kwa wazungu, zilishawekwa na Uislamu katika karne 14 zilizopita, na baadhi ya wasomi wa Kiarabu na Kiirani katika vitabu vyao wamefanya ulinganisho kati ya mafundisho ya Uislamu na maelekezo (masharti) ya ibara hizi. Bado kuna tofauti katika baadhi ya vipengele vya maazimio haya na mafundisho ya Uislamu. Hili ni somo la kuvutia. Kwa mfano Uislamu unakubali usawa kati ya haki ya mwanaume na mwanamke, lakini haukiubali kufanana kwa haki hizi. Heshima ya mwanadamu na haki za binadamu. Ambapo kuitambua heshima na utu wa mwanadamu na haki zisizoondosheka za wanaadamu wote ni msingi wa uhuru, haki na amani duniani."

"Ambapo kutozingatia na kudharau haki za kibinadamu kumesababisha vitendo vya kishenzi na kuikasirisha dhamira njema ya mwanadamu na kuja kwa ulimwengu ambao ndani yake watu watafurahia uhuru wa kujieleza na imani, na uhuru wa kuondokana na hofu na shida imetamkwa kuwa ni hamu kubwa ya watu wa kawaida." "Ambapo italazimu, ikiwa mwanadamu hana kimbilio, kama njia ya mwisho, ana haki ya kuasi utawala wa kidhalimu, na kwamba haki za binadamu zitapaswa kulindwa na utawala wa kisheria." "Itakapobidi, kukuza maendeleo ya uhusiano wa kirafiki kati ya mataifa." "Ambapo watu wa Umoja wa Mataifa, katika heshima ya utu wa mwanadamu na katika usawa wa haki za mwanaume na wanawake, na wamedhamiria kukuza maendeleo ya kijamii na kiwango cha ubora wa maisha, katika hali ya uhuru zaidi." "Ambapo Baraza kuu la umoja wa Mataifa linatamka Azimio hili la Haki za Binadamu kwa wote kama kigezo cha wote cha kupimia mafanikio ya watu wote na mataifa yote ili hadi kufika mwisho kila mtu na chombo cha jamii, kwa kulizingatia Azimio akilini mwao walijitahidi kwa kufundisha na kutoa elimu, kukuza tabia ya kuheshimu haki hizi na uhuru na kwa hatua za kimaendeleo za kitaifa na kimataifa, ili kulinda utambulisho na zingatio miongoni mwa nchi wanachama wenyewe na miongoni mwa watu wa nchi zilizo chini ya mamlaka yao ya kisheria" Kama tulivyoona mwanzo, kila neno na kila sentensi katika azimio hili limepigiwa hesabu kali, limechukuliwa kwa uangalifu mkubwa. Hili ni dhihirisho la maw azo ya wanafalsafa na wanasheria wataka mabadiliko wa karne nyingi. Nukta muhimu za dibaji ya Azimio la haki za binadamu.

Azimio hili lina ibara 30, japo baadhi ya ibara zimezidi kiasi na baadhi ya nukta zimerudiwa katika ibara nyingi. Nuktra muhimu za ibara ni kama ifuatavyo: Binadamu wote wana haki za msingi zisizobatilishika na haki ya kutambuliwa utu wao. Utu wa binadamu na haki za binadmau ni kwa ajili ya wote na hivi havigawiki. Vinawahusu watu wote bila kujali rangi, utaifa au jinsia. Binadamu wote ni wanafamilia, hivyo hakuna aliyebora kuliko mwingine. Kuzitambua kikamilifu haki za binadamu na utu wa binadamu ni msingi wa uhuru, haki na amani. Yaliyomo katika Azimio yanaashiria kuwa chanzo cha matatizo yote, vita, vitendo vya kishenzi vinavyofanywa na mtu mmoja mmoja na watu dhidi ya wengine ni kutozitambua haki za binadamu na utu wa binadamu.

Kutozitambua huku huwalazimisha baadhi kuasi dhidi ya wengine na hivyo kuhatarisha amani na usalama. Hitajio na kinachotamaniwa kikubwa zaidi katika kufanikisha azma hii ni kuzaliwa kwa dunia ambayo ndani yake kutakuwa hakikisho la uhuru wa imani, usalama na hali nzuri kimaisha pamoja na hakikisho la kuondokana na ukandamizaji, hofu na umasikini. Azimio lenye ibara 30 limeundwa ili kufikia lengo hili. Imani juu ya heshima kwa utu wa mwanadamu na haki za msingi za kibinadamu lazima ikaziwe na kuingizwa pole pole akilini mwa watu wote, kupitia ufundishaji na elimu.

Heshima kwa utu wa mwanadamu. Kwa vile Azimio la Haki za Binadamu limeundwa kwa msingi wa heshima kwa utu, uhuru na usawa kwa nia ya kufufua haki za binadamu, lazima liheshimiwe na kila mtu makini. Sisi watu wa Mashariki (Asia) tumekuwa tukiamini juu ya kuuheshimu utu wa binadamu kwa muda mrefu. Uislamu umetilia sana mkazo katika kuuheshimu utu pamoja na haki za binadamu, uhuru na usawa. Hao waliyoyahamasisha haya, wanastahiki shukrani zetu.

Hata hivyo, haya ni maandishi ya kifalsafa yaliyoandikwa na mikono ya kibinadamu, sio malaika. Hivyo kila mwanafalsafa anayo haki ya kuyachambua na kuonyesha nukta zake dhaifu. Hapana shaka kwamba Azimio la haki za Binadamu lina udhaifu wake, lakini hivi sasa hatuna nia ya kuonyesha udhaifu huo. Badala yake; tunaonyesha nukta zake nzuri.

Msingi wa Azimio hili ni heshima ya utu wa mwanadamu kwa sababu, kwa kuwa nazo hizo, mwanadamu anapata haki fulani ambazo viumbe wengine hawapati, kwa vile hawana utu huo. Hii ndio nukta nzuri ya Azimio hili. Falsafa ya Kimagharibi inamshusha hadhi mwanadamu. Hapa tena tulikutana na swali kongwe la kifalsafa; Ni nini asili ya utu wa mwanadamu ambao humtofautisha yeye na farasi, ng'ombe na njiwa? Hapa ndipo inapodhirika migongano kati ya msingi wa Azimio la Haki za Binadamu na tathhmini ya Kimagharibi juu ya mwanadamu. Falsafa ya Kimagharibi toka zamani imekuwa ikimshushia hadhi mwanadamu.

Chanzo cha yote ambayo yalikuwa yakisemwa zamani kuhusu mwanadamu na cheo chake kitukufu ilikuwa ni katika Mashariki (Asia). Sasa mifumo mingi ya falsafa ya Ulaya inayakejeli yote hayo. Mwanadamu kwa mtazamo wa Kimagharibi, amekuja (duniani) akiwa na cheo cha mashine. Kuwepo kwa roho na asili ya ukarimu kumekataliwa.

Wazo kwamba ulimwengu una lengo la msingi linaonekana kuwa ni wazo la kupinga maendeleo. Sasa hakuna mtu katika nchi za Magharibi anayeweza kusema kuwa mwanadamu ni mfalme wa viumbe. Kwa mujibu wa nadharia ya sasa ya kizungu, imani hiyo ilikuwa ni chipukizi (tawi) la unajimu wa Ptolem, ambayo ilikuwa inaaminika kuwa dunia ndio kitovu cha ulimwengu na nyota ziliaminika kuwa zinaizunguka dunia. Sasa kwa kuwa nadharia hii imeshakufa na kwa kutoweka kwake, hakuna nafasi tena ya mwanadamu kudai kuwa ni mfalme wa ulimwengu.

Kwa mujibu wa Wazungu, hata zamani ilikuwa ni kwa sababu ya ubinafsi wake ndio maana akajifanya kuwa bora kuliko viumbe wengine. Maisha yake ni ya kiumbo tu. Mtu akishakufa, mwili wake huoza na hapo ndio mwisho wa habari! Mzungu haamini kuwa roho inaweza kuishi peke yake. Kwa mtazamo huu, hajioni kuwa na tofauti yoyote kati yake na mimea na wanyama. Kwa hiyo anaona kuwa hakuna tofauti yoyote ile ya msingi kati ya asili ya vipawa vya kiakili na kiroho vya mwanadamu na sifa nyingine za maada kama vile joto, linalotoka kwenye makaa ya mawe.

Maisha kwa viumbe vyote, ikiwa ni pamoja na mwanadamu, yanamaanisha mapambano yasiyokwisha ya kuweza kuishi. Hii ndio kanuni ya msingi ya maisha. Mwanadamu mara zote amekuwa akipambana ili awe mshindi katika mapambano haya, na ili kuilinda nafasi (hadhi) yake amebuni kanuni za kimaadili kama vile uadilifu, wema, ushirikiano, uaminifu n.k. Kwa mujibu wa baadhi ya matapo yenye nguvu ya kifalsafa ya Kimagharibi mwanadamu ni mashine tu inayosukumwa na maslahi ya kiuchumi. Dini, maadili, falsafa, sayansi, fasihi na sanaa nyingine, vyote ni vikorombwezo tu. Miundo mbinu yake ni mfumo wa uzalishaji mali na ugawaji wa mali, na mambo haya ndiyo yanayotawala nyanja zote za maisha ya mwanadamu.

Sio hivyo tu, baadhi ya wanafalsafa wa Kimagharibi wana mtazamo kwamba vipengele vya kijinsia ndivyo vyenye ushawashi halisi wenye nguvu katika shughuli zote za mwanadamu. Maadili, falsafa, sayansi, dini na sanaa vyote hivyo ni miundo ilyobadilishwa na kurekebishwa ya jinsia. Hatuelewi ni jinsi gani tunaweza kuzungumzia utu wa mwanadamu na haki za msingi na ni jinsi gani tunaweza kuzifanya kuwa msingi wa matendo yetu yote, ikiwa tunakana kwamba maisha hayana lengo lolote la msingi, ikiwa tunafikiri kuwa mapambano ya kuweza kuishi na mapambano yatakayombakisha mwenye nguvu zaidi ndio sheria pekee zinazotawala maisha, ikiwa tunaamini kuwa mwanadamu ni mashine tu kama mashine nyingine (lakini) iliyopewa mikono ya binadamu, ikiwa tunashikilia kuwa hakuna roho na kwamba yote yanayozungumzwa juu ya roho ni kuzidisha chumvi kwa kiroho, ikiwa tunashikilia kuwa maslahi ya kiuchumi na ngono ndiyo yanayosukuma shughuli zote za mwanadamu, ikiwa tunajali kuwa wema na uovu ni dhana linganifu tu, ikiwa tuna maoni kuwa muongozo wa kimungu wa asili na wa kimaono ni upuuzi na ikiwa tutasema kuwa mwanadamu ni mtumwa wa matamanio yake na anaweza kunyenyekea kwa nguvu tu.

Maoni ya Kimagharibi juu ya mwanadamu yanapingana na utu wake na yameiporomosha hadhi yake katika kila pembe katika pembe ya sababu ya kuumbwa kwake, umbile lake, nia yake na dhamira yake. Baada ya kufanya yote haya, nchi za Magharibi zimetangaza Azimio la hali ya juu lenye busara kuhusu utu wa mwanadamu na cheo na haki za msingi zisizoondosheka na takatifu, na wametoa wito kwa kila mtu kulitekeleza hilo. Kabla ya kutoa Azimio hili la hali ya juu zuri na lenye busara, nchi za Magharibi kuhusu utakatifu na haki za asili za mwanadamu, wangeipitia upya tafsiri yao juu ya mwanadamu.

Tunakiri kuwa sio wanafalsafa wote wa Kimagharibi wana mtazamo huu. Wengi wao wanamtazama mwanadamu kama tunavyofanya sisi watu wa Mashariki (Asia). Tuna mtazamo ambao watu wengi wa Magharibi wanaung'ang'ania na ambao unawashawishi watu duniani kote. Azimio la Haki za Binadamu lilipaswa litolewe na wale ambao wanamuona mwanadamu kuwa ni zaidi ya roboti ambao wanafikiri kuwa malengo yake hayaishii kwenye silika za kibinadamu na kinyama na ambao wanaamini juu ya dhamira ya kibinadamu. Azimio la Haki za Binadamu lilipaswa litolewe na watu wa Mashariki ambao wanaamini kuwa mwanadamu ni khalifa wa Mwenyezi Mungu katika dunia. Qur'ani Tukufu inasema:

"Kwa hakika nitamuweka khalifa katika ardhi." (2:30) Ni wale tu wanaoamini kuwa mwanadamu ana lengo na makusudio ndio wanaoweza kuzungumzia juu ya haki za binadamu.

"Enyi watu, bila shaka lazima mjitahidi sana kwa ajili ya Mola wenu, kujitahidi kukubwa kabisa hadi mtakapokutana Naye." (84:6). Azimio la haki za binadamu linaifaa mifumo ile ambayo inaamini kuwa mwanadamu ana muelekeo wa asili wa kutenda mema;"Naapa kwa roho na kwa yule aliyeifanya kuwa timilifu na aliyeipa ujuzi (elimu) juu ya uovu na uchamungu." (91:7-8). Azimio la haki za Binadamu haliafikiani na njia za fikra za Kimagharibi.

Kufikiri kwao kunazifaa tu tabia za watu wa kimagharibi ambao huua hisia za kibinadamu, hucheza na tabia za wanaadamu, hujali fedha zaidi kuliko mtu, huabudu mashine (mitambo), huona mali kama Mungu na huwanyonya wanaadamu wengine. Ubepari umepata nguvu na mamlaka yasiyo na kikomo kiasi cha kuwa ikitokea kuwa milionea mmoja atamrithisha mbwa wake kipenzi mali zake, mbwa huyo ataheshimika kuliko watu, watu wengi tu watamtumikia mbwa huyo kama makatibu muhtasi na makarani na wataonyesha heshima ya hali ya juu kwa mbwa huyo.

Leo hii swali kubwa la kijamii kwa mujibu wa Qur'ani, ni je, mwanadamu amejisahau mwenyewe? Sio tu kwamba amejisahau yeye tu bali amemsahau hata Mungu wake pia. Akili zake zote amezielekeza kwenye maisha ya kidunia na mali na amepuuza kabisa kujifikiria na kujipima. Anafikiri kuwa amepoteza roho yake. Mawazo kama haya ni ya hatari sana na yanaweza kuondoa kabisa thamani ya utu na ubinadamu.

Ustaarabu wa sasa unaweza kuzalisha kila kitu chenye ubora wa juu kabisa, lakini hauwezi kumtengeneza mtu halisi. Gandhi anasema kuwa mzungu anastahili kuitwa bwana wa dunia. Anamiliki raslimali zote za kidunia na anafanya vitu ambavyo mataifa mengine wanaamini kuwa ni Mungu tu anayeweza kuyafanya.

Lakini ni kitu kimoja tu ambacho mzungu hawezi kukifanya nacho ni kujifikiria na kujipima. Hilo peke yake linatosha kuthibitisha kutokuwa na maana kwa kumeremeta kwa ustaarabu wa kisasa. Kama ustaarabu wa Kimagharibi umemtaabisha mzungu kwa ulevi na ngono basi ni kwa sababu ya kujisahau na kujipoteza badala ya kujitafuta. Uwezo wake wa kivitendo wa kuvumbua, kugundua na kuzalisha zana za kivita unatokana na kujikwepa nafsi yake na sio kwa sababu ya uwezo wake wa kipekee wa kujidhibiti. Kuogopa kwake upweke, ukimya wake na tamaa yake ya fedha kumemfanya asiweze kusikia sauti yake ya ndani.

Kushindwa kwake kujitawala ndio kichocheo chake cha kuuteka ulimwengu. Hii ndio sababu kila anakokwenda mzungu hueneza mitafaruku na ghasia. Kama mtu akipoteza nafsi yake mwenyewe, hakuna faida yoyote kuushinda ulimwengu. Wale ambao wamefundishwa na Injili kuwa wamisionari wa ukweli, upendo na amani, wanazunguka kutafuta dhahabu na watumwa. Badala ya kutafuta msamaha wa Mwenyezi Mungu na uadilifu katika ufalme wa Mungu, kama Injili inavyofundisha wanatumia dini yao kama kifutio cha madhambi zao (kwa kumfanya Yesu, Mtume mtukufu wa Mungu kuwa kafara ya dhambi kwa kila amuaminiye). Badala ya kufundisha na kuhubiri ujumbe wa Mungu, wanawadondoshea mabomu watu wasio na hatia. Hii ndio sababu, Azimio la Haki za Binadamu linakiukwa na nchi za Magharibi. Falsafa inayofuatwa na watu wa Magharibi katika maisha yao kivitendo inafanya kushindwa kwa Azimio hili kusiepukike.


4

5

6

7

8

9

10

11

12

13