• Anza
  • Iliyopita
  • 13 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 6870 / Pakua: 3804
Kiwango Kiwango Kiwango
JAWABU KWA WAPINGA MAULIDI

JAWABU KWA WAPINGA MAULIDI

Mwandishi:
Swahili

JAWABU KWA WAPINGA MAULIDI

MWANZO WA KITABU

MUANDISHI NI: SEHIKH ABILLAHI NAASIR

MAULIDI NI MOJA KATI YA SHEREHE ZA KITAMADUNI ZA KIISLAMU. SHEREHE ZA MAULIDI NI ZENYE KUPEWA KIPAU MBELE SANA NA WATU WA MUAMBAO WA AFRIKA YA MASHARIKI, SABABU KUU ILIYO WAFANYA WAO KUWA NA SHAUKU YA MAULIDI KILA IFIKAPO MFUNGUO SITA, NI KULE KUWA WAO, NI WAISLAMU WENYE MAPENZI NA MTUME WAO.

KATIKA ZAMA ZA MIAKA KAMA ISHIRINI AU KUMI NA TANO ILIYOPITA, KULIANZA KUINGIA VURUGU LA BAADHI YA WAISLAMU WENYE SIASA KALI, LILILOWATANGAZIA WENGINE UHARAMU WA MAULIDI, HAIDHURU KATIKA USEMI WAO HUO, HUWA WANATOA DALILI MBALI MBALI, LAKINI WAKATI MWENGINE DALILI ZAO HUWA HAZIKUBALIKI KIMANTIKI.

KITABU HIKI KILICHOKO MIKONONI MWENU NI KITABU KILICHO KUSANYA JUMLA YA MAKALA MABALI MBALI ZILIZITAYARISHWA NA SHEIKH ABDILLAHI NAASIR, KWA AJILI YA KUJIBU HOJA MBALI MBALI ZA WAPINGAJI WA MAULIDI. NA MIMI KWA UPANDE WANGU NIMEAMUA KUUWEKA UTANGULIZI HUU, ILI TU NIWEZE KUTOA MTAZAMO WA SUALA HILI LILIVYO INGAWAJE NI KWA UFUPI KABISA. NINATARAJI WAISLAMU WENZETU WATAFAIDIKA NA MAELEZO HAYA, NA WATALITUMIA JICHO LA KUTAFAKARI KATIKA KUYAANGAZA YALIOMO NDANI YA MAKALA HIZI. NINAMUOMBA MOLA MTUKUFU ATUNUSURU NA SHARI ZA UJINGA WETU, NA ATUPE UFUNUO WA ELIMU ITOKAYO MBINGUNI. KWANI YEYE TU NDIYE MJUZI NA KIONGOZI WA WACHA MUNGU.

AAMIN YAA RABBAL AALAMIIN.

MKUSANYAJI WA MAKALA:

SALIM SAID AL-RAJIHIY

SHEREHE ZA MAULIDI:

Maulidi ni Kiswahili cha neno la Kiarabu, mawlid. Neno hili lina maana ya "mazazi" au "kuzaliwa kwa" (birthday). Kwa kawaida, linapotumiwa na Waislamu, huwa na maana ya siku aliyozaliwa Mtume Muhammad (s.a.w.w.), au hafla ya kuisherehekea siku hiyo.

Waislamu wa ulimwengu mzima, ifikapo tarehe 12 ya Mfungo Sita (Rabiul Awwal), husoma maulidi na kuisherehekea siku hiyo kwa furaha kubwa. Sherehe hizo, kwa dasturi, haziishii tarehe hiyo tu, bali huendelea hata kwa miezi miwili mitatu baada ya hapo. Hili huwa ni kwa sababu ya Waislamu wa kila nyumba, kila mtaa, kila mji na kila nchi kutaka kushiriki katika sherehe hizo na kupata baraka zake. Vile vile huwapa Waislamu nafasi ya kutembeleana na kushirikiana katika sherehe hizo - jambo ambalo lisingewezekana lau watu wote wangeliamua kuzifanya sherehe hizo siku hiyo hiyo moja tu.

Kwa nini kusoma maulidi?

Waislamu husoma maulidi kwa sababu mbalimbali. Kati ya hizo ni: (i) kuikumbuka na kuitukuza siku aliyozaliwa mbora wa viumbe vyote, aliyetutoa vizani na kututia kwenye nuru;

(ii) ni njia moja ya kutoa shukrani zetu kwa neema hiyo;

(iii) katika sherehe hizo, hupatikana fursa ya kukumbushana maisha ya bwana mkubwa huyo na mafunzo yake;

(iv) hupatikana fursa ya Waislamu wa madhihabi na mataifa mbalimbali kushirikiana na kuziweka kando hitilafu zao; na

(v) mikusanyiko hiyo huleta athari kwa wasio Waislamu ya kuupenda Uislamu, na hata kusilimu.

Wanaopinga na sababu zao

Lakini, hata hivyo, kuna baadhi ya Waislamu -- japokuwa wao si wengi kama wanaoyasoma -- ambao hupinga kusomwa maulidi; na hutoa sababu zao. Kati ya sababu hizo ni:

(i) maulidi hayakuwako zama za Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Basi kwa nini yazuliwe sasa?

(ii) hayakusomwa na maswahaba wala waandamizi wao. Kama kweli yangelikuwa ni sawa kuyasoma, bila shaka mabwana wakubwa hao wangelikuwa ni wa mbele kufanya hivyo;

(iii) kuweka ada ya kusoma maulidi ni kuigiza Wakristo walioweka siku ya Krismasi; na Mwislamu haruhusiwi kufanya hivyo;

(iv) kwenye sherehe za maulidi hufanywa baadhi ya mambo ambayo ni ya munkar (yanayochukiza, bali ni haramu kamwe, katika sharia ya Kiislamu);

(v) hakuna ushahidi wowote, wa Qur'ani wala Hadithi za Mtume Muhammad (s.a.w.w.), unaothubutisha usawa wa kuyasoma maulidi, sikwambii kuyatilia nguvu.

Kwa nguvu ya hujja hizo, mara nyingi viongozi wa wanaopinga maulidi huwaonyesha wafuasi wao kuwa wale wanaosoma maulidi ni watu waliopotea kwa "kuzua" mambo yasiyo na msingi katika dini yetu hii. Jambo hili limeleta mchafuko -- unaofufuka aghalabu kila ifikiapo miezi ya kusoma maulidi -- ambao unahatarisha umoja na masikizano, sio baina ya Waislamu wa madhihabi mbalimbali peke yao, bali hata wale wa madhihabi mamoja!

Mchafuko huu huzidi kukua kwa sababu ya lugha kali inayotumiwa na pande zote mbili -- za wanaounga na wanaopinga maulidi -- katika kutetea misimamo yao; na hilo haliwezi kusaidia katika kutatua usawa uko wapi. Liwezalo kutatua hitilafu hii ni kuijadili ki-ilimu na kwa lugha nzuri ya kuhishimiana. Na hilo ndilo nililokusudia kulifanya, kuanzia makala yanayofuatia haya, Inshallah.

ABDILAHI NASSIR

P.O. BOX 84603

MOMBASA

4 Rabiul Awwal, 1423

17 Mei, 2002

1

JAWABU KWA WAPINGA MAULIDI

MAKALA NO: 1

MUANDISHI NI: SEHIKH ABILLAHI NAASIR

WANAVYOSEMA WAPINGA MAULIDI NA MAJIBU YETU

Katika makala yetu ya kwanza tuliahidi kuzijadili ki-ilimu, moja baada ya moja, hujja zinazotolewa na wanaopinga maulidi. Kwa hivyo leo tunaanza:

Hujja yao ya kwanza ni kwamba: maulidi hayakuwako zama za Mtume Muhammad (s.a.w.w.) Kwa hivyo, kuyaleta baada ya yeye kufariki dunia, ni bid'a (uzushi). Na kila bid'a, kwa maneno yake mwenyewe Bwana Mtume (s.a.w.w.), ni upotevu. Kwa hivyo, kila anayesoma maulidi amepotea!

MAJIBU YETU:

Ni kweli kwamba maulidi, hivi tunavyoyasoma, hayakuwako zama za Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Lakini si kweli kwamba, kulifanya kila ambalo halikuwako zama hizo, ni upotevu. Kama ni hivyo, basi bila shaka Waislamu wote leo -- wakiwamo wanaopinga maulidi -- wangelikuwa wamepotea kwa kuwa (katika zama zao mbalimbali) wamefanya, na wanaendelea kufanya, mambo ambayo hayakuwako zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.)!

Kwa mfano, katika zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.), misikiti haikuwa ikitandikwa chochote (watu wakisujudu juu ya mchanga); lakini leo inatandikwa majamvi, busati na mazulia! Kiwanja kitakatifu cha Al-Kaaba kilikuwa ni mchanga mtupu na mawe; lakini leo kimetandikwa marumaru! Watu walikuwa wakenda kuhiji kwa kupanda ngamia au majahazi; lakini leo wanakwenda kwa ndege, meli za kisasa na mabasi ya anasa (luxury)! Watu, walipokuwa wengi msikitini, walikikhutubu kwa kupaza sauti zao; lakini leo wanatumia vipaza sauti (loud speakers)! Misahafu ilikiandikwa kwa mkono, juu ya ngozi na mifupa, na kutolewa nakala chache; lakini leo inachapwa kwa mashini, juu ya karatasi za fakhari, na kutolewa nakala mamilioni kwa mamilioni!

Lakini hakuna anayesema -- hata hao wanaopinga maulidi hawasemi -- kwamba Waislamu waliobuni mambo hayo wametuletea bid'a au wamepotea. Kwa nini? Kwa sababu kwao wao, na kwa wanaosoma maulidi, uzushi wa aina hiyo si bid'a; sio alioukusudia Bwana Mtume (s.a.w.w.). Alioukusudia yeye ni ule wa kuzua jambo katika dini hii ambalo halitokani nayo (maa laysa minhu). Hilo ndilo lililo wazi kutokana na Hadithi mashuhuri ya Bwana Mtume (s.a.w.w.) inayosema: "Yoyote atakayezua, katika dini yetu hii, jambo ambalo halitokani nayo, litarudishwa (litakataliwa)."

Ukiitaamali vizuri Hadithi hiyo, itakudhihirikia kwamba Bwana Mtume (s.a.w.w.) hakutuzuia kuzua (kubuni), katika dini hii, kila ambalo halikuwako zama zake. Kama angelitaka kutuzuia hivyo, Hadithi hiyo isingelisema hivyo, bali ingelisema hivi: "Yoyoye atakayezua jambo katika dini yetu hii, litakataliwa." Na lau ingelisema hivyo, basi yote yale tuliyoyataja hapo juu yasingeliruhusiwa; yangelikuwa bid'a.

Lakini Hadithi haikusema hivyo. Ilivyosema ni: " Yoyote atakayezua ambalo halitokani nayo, litakataliwa." Kwa kuongeza kifungu cha maneno tulichokichapa kwa italiki (yaani "ambalo halitokani nayo"), ni wazi kwamba Mtume Muhammad (s.a.w.w.) hakukusudia kuwazuia Waislamu kufanya kila ambalo halikuwako zama zake. Alilolikusudia ni kutuachia wazi mlango wa kubuni mambo katika dini hii bora tu yawe yanatokana nayo.

Sasa suali hapa ni: jee, maulidi si katika mambo yanayotokana na "dini hii", hata kama hayakuwako zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.)?

Majibu yetu ni: Maulidi, na yaliyomo maulidini, si mageni na "dini hii", bali yanatokana nayo, kama tutakavyobainisha kwa urefu zaidi katika majibu yetu ya hujja Na. (v) ya wapinzani wake inshallah.

Kwa hivyo, kuwa tu jambo halikuwako zama za Mtume Muhammad (s.a.w.w.) si hujja ya kuwazuia Waislamu kulifanya. Wanalozuiliwa Waislamu kulifanya ni kuzua jambo na kulifanya ni dini hali ya kuwa halina asili na dini. Na maulidi si hivyo!

Inshallah, katika makala yanayofuatia, tutaijadili hujja yao ya pili.

ABDILAHI NASSIR

P.O. BOX 84603

MOMBASA

13 Rabiul Awwal, 1423

26 Mei, 2002

2

JAWABU KWA WAPINGA MAULIDI

MAKALA NO: (2)

MUANDISHI NI: SEHIKH ABILLAHI NAASIR

WANAVYOSEMA WAPINGA MAULIDI NA MAJIBU YETU

Katika makala yetu kabla ya haya, tulijibu hujja ya kwanza ya wanaopinga maulidi. Leo tunaendelea na hujja yao ya pili. Katika hujja yao ya pili wanasema: Maulidi hayakusomwa na maswahaba wala waandamizi wao (taabi'in). kama kweli yangelikuwa ni sawa kuyasoma, bila shaka mabwana wakubwa hao wangelikuwa ni wa mbele kufanya hivyo.

MAJIBU YETU:

Hakuna Mwislamu yoyote anayekataa kuwa maswahaba ni watu watukufu. Wala hakuna anayekataa kuwa wao ndio kiungo chetu sisi na Bwana Mtume (s.a.w.w.). Lakini, pamoja na utukufu wote huo, wao walikuwa ni binadamu; hawakuwa ni ma'asumin. Walikiweza kufanya jambo, wakaswibu (wakapata); kama ambavyo walikiweza kufanya jambo, wakakosea. Na mifano ya yote mawili hayo ni mingi katika historia yao.

Kwa hivyo, kuwa tu jambo fulani halikufanywa na maswahaba, haliwi ni hujja sahihi ya kuwazuilia Waislamu kulifanya jambo hilo. Hujja ya pekee iliyo sahihi ni iwapo lile ambalo hawakulifanya wao, waliacha kulifanya kwa sababu ndivyo alivyoamrisha Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.), au waliacha kulifanya kwa sababu linapingana na maamrisho ya Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.). Ikiwa walifanya hivyo ndipo jambo hilo litakapokuwa ni hujja; lakini si kwa sababu ya kuwa halikufanywa na maswahaba, bali ni kwa sababu tu ya kuwa ndivyo alivyoamrisha Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.), au ni kwa sababu tu ya kuwa linapingana na mafunzo ya Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.) -- na hivyo ndivyo Kiislamu.

Kwa hivyo si sawa kuyapinga maulidi kwa sababu tu hayakusomwa na maswahaba na waandamizi wao. La sawa ni kuyapinga kwa sababu tu yamekatazwa na Mwenyezi Mungu au Mtume Wake (s.a.w.w.), au yanapingana na maamrisho yao. Na hilo, mpaka hivi sasa, wapinzani wa maulidi hawajaweza kulithubutisha.

Tunasema hivyo kwa sababu, mmoja kati ya misingi muhimu ya sharia ya Kiislamu, inyaokubaliwa na wanazuoni wa wanaosoma maulidi na wale wa wanaopinga maulidi, ni kwamba -- tunapokuja kwenye mambo kama ya maulidi, ujenzi wa msikiti, mavazi, na kadhaalika -- kila kitu ni halali mpaka kithubutishwe kuwa ni haramu. Kwa hivyo, kwa msingi huu, uharamu wa maulidi haitaki uthubutishwe na wanaoyasoma, bali inataka uthubutishwe na wanaoyapinga. Wala wasilithubutishe hilo kwa vichwa vyao (Sura 16:116), bali kwa kutoa ushahidi wa maneno ya Mwenyezi Mungu au Mtume Wake s.a.w.w. (Sura 4:59). Na hilo pia, mpaka dakika hii, wapinzani wa maulidi hawajaweza kulifanya.

Mwanzo mwanzo wa kuzuka madhihabi haya ya kupinga maulidi, wafuasi wake waliyapinga mambo mengi yaliyozuka katika zama zao. Kati ya mambo hayo ni kuvuta sigara, kupiga simu ya mdomo (telephone), kujiwekea kashida mbele ya mtu anaposwali, kumwamkia mtu kwa: "Umeamkaje?", kupana mikono baada ya swala, kutandika busati misikitini, na hata kuvaa nguo yenye thamani inayozidi dirhamu 100 (mia)!

Yote hayo waliyapinga kwa hujja ya kuwa hayakuwako zama za Mtume (s.a.w.w.), na kwamba hayakufanywa na maswahaba na waandamizi wao! Lakini, baada ya kutambua walikosea wapi, walirudi nyuma, wakayakubali yote hayo. Kwa maneno mengine, yakawa sio bid'a tena!

Leo, kwa hujja hizo hizo, waandamizi wao wameanza kusema vibula vivunjwe! Kesho watasema na minara nayo ivunjwe! Kesho kutwa watasema mimbari za mbao au za mawe, nazo pia ziondolewe, zirudishwe zile za vigogo vya mtende; hata vya mnazi havitafaa! Baada ya hapo ni nini kitakachowazuia wasitwambie tuondoe banka (panka) misikitini, turudi kujipepea kwa nguo zetu kama ilivyokuwa zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.)? Au twende hijja kwa ngamia au farasi badali ya ndege? Au ni lipi litakalowazuia kutuamrisha kuisoma Qur'ani katika ngozi na mbao, kama ilivyokuwa zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.) na maswahaba, badali ya hii miswahafu mizuri mizuri tuliyonayo?

Ni matumaini yetu kwamba, kama ambavyo watangulizi wao walirudi nyuma na kuyakubali yale waliyoyafanya ni bid'a mwanzo, wao nao watafuata nyayo zao, wayaone maulidi, na mengine kama maulidi, kuwa sio bid'a iliyokatazwa na Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Alhamdulillaah, baadhi yao wameanza kuona hivyo na kufanya sherehe za mazazi ya Bwana Mtume (s.a.w.w.). Lakini badali ya kuyaita maulidi, huyaita seera!

Inshallah, katika makala yanayofuatia, tutazijadili hujja zao nyengine.

ABDILAHI NASSIR

P.O. BOX 84603

MOMBASA

25 Rabiul Awwal, 1423

7 Juni, 2002

13 Rabiul Awwal, 1423

26 Mei, 2002

3

JAWABU KWA WAPINGA MAULIDI

MAKALA NO: (3)

MUANDISHI NI: SEHIKH ABILLAHI NAASIR

WANAVYOSEMA WAPINGA MAULIDI NA MAJIBU YETU

Bado tunaendelea na hujja za wanaopinga maulidi.

Hujja yao ya tatu ni kuwa: kuweka ada ya kusoma maulidi ni kuigiza Wakristo walioweka siku ya Krismasi; na Mwislamu haruhusiwi kufanya hivyo.

MAJIBU YETU:

Mwislamu hazuiliwi kufanya jambo kwa sababu tu linafanywa na Mkristo au kafiri yoyote mwengine. Analozuiwa ni kufanya jambo kama linalofanywa na Mkristo, au kafiri yoyote mwengine, linapokuwa linakwenda kinyume na mafunzo ya Kiislamu; na hilo sio linapofanywa na Mkristo au kafiri yoyote tu, bali hata linapofanywa na Mwislamu mwenziwe; haruhusiwi kulifanya.

Tunaposoma historia, kwa mfano, tunaona jinsi Bwana Mtume (s.a.w.w.) -- katika Vita vya Handaki -- alivyokubali shauri la Salman Farisi la kuchimba handaki kama walivyokifanya Wafursi kwao. Na Wafursi, wakati huo, hawakuwa ni Waislamu, bali walikuwa ni makafiri waliokiabudu moto! Jee, kwa kuwaigiza makafiri hao katika uchimbaji wa handaki, Bwana Mtume (s.a.w.w.) alikosea?

Hali kadhaalika, tukija kwenye hijja mathalan, tunaona jinsi mahujaji wanavyokwenda baina ya Swafaa na Marwa, na jinsi wanavyochinja wanyama mwisho wa hijja yao. Lakini vitendo kama hivyo, kabla ya Uislamu, vilikuwa vikifanywa na makafiri! Basi kama kuigiza Wakristo hakuruhusiwi, kwa nini Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.) wakatuamrisha kufanya mambo ambayo dhahiri yake ni sawa na kuwaigiza makafiri?

Ukivizingatia vizuri vitendo hivyo utaona kwamba, japokuwa kwa dhahiri vinafanana na vile vya makafiri, kwa kweli huwezi kusema kuwa ni sawa na kuwaigiza makafiri. Kwa nini? Kwa sababu waliyokuwa wakiyafanya makafiri mwahali humo, walikuwa wakiyafanyia masanamu yao, waliyoyaweka humo. Kwa hivyo yao ilikuwa ni shirk (ushirikina). Lakini tunayoyafanya sisi Waislamu, baada ya kuondolewa mbali masanamu hayo, huwa tunamfanyia Mwenyezi Mungu Mmoja tu, asiye na mwenziwe (mshirika). Kwa hivyo yetu ni tawhid (kumpwekesha Mwenyezi Mungu).

Hali kadhaalika tunapokuja kwenye Krismasi. Japokuwa Krismasi, kama maulidi, hufanywa kwa kusherehekea mazazi ya Mitume ya Mwenyezi Mungu (Nabii Muhammad s.a.w.w. na Nabii Isa a.s.), lakini sherehe mbili hizo -- kama ambavyo kila mtu anajua -- si sawa. Sherehe zinazofanywa Krismasi ni tafauti kabisa na zinazofanywa maulidini, kama ambavyo Wakristo wanavyomchukulia Nabii Isa a.s. (Yesu Kristo) ni tafauti kabisa na vile Waislamu wanavyomchukulia Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Kwa mfano, Waislamu hawamchukulii Mtume Muhammad (s.a.w.w.) kuwa ni Mungu, wala ni Mtoto wa Mungu, wala ni Roho Mtakatifu.

Kwa hivyo kuwa tu jambo fulani lilitangulia kufanywa na makafiri -- wawe ni Wakristo ama ni wengineo -- haiwi ni hujja ya kuwazuilia Waislamu kulifanya jambo hilo maadamu watayatoa yote ya ukafiri yaliyokuwamo humo. Na hivyo ndivyo maulidi yalivyo. Zaidi ya kuwa zote mbili -- Krismasi na maulidi -- ni sherehe za mazazi ya Mitume ya Mwenyezi Mungu, hakuna jengine linalofanana katika sherehe hizo.

Kama tutashikilia kuwa ni haramu Waislamu kuwaigiza Wakristo, au makafiri wowote kwa jumla, katika jambo lolote -- hata kama halipingani na dini yetu -- basi sio wanaosoma maulidi tu, bali hata wanaoyapinga pia watakuwa makosani. Kwani ni nani kati yao aliyeacha gari au ndege, akaendelea kupanda punda, farasi au ngamia? Ni nani, anayejimudu, aliyeacha kutumia umeme (spaki), akaendelea na kuni au mafuta ya taa? Ni nani anayeradhiwa kujipepea kwa kipepeo au nguo yake, akaacha -- ikiwa anayo nafasi -- kutumia banka au AC (Air Conditioner)? Ni nani anayepanda kwa miguu mpaka ghorofa ya 15, au ya 10, akaacha lifti? Kwa nini hawayaachi yote hayo ili wasiwe wanawaigiza Wakristo au makafiri wengine, maana yote hayo yameanzishwa na wao.

Kwa hivyo si sawa kuwazuilia Waislamu kusoma maulidi kwa sababu tu ya kuwa, kufanya hivyo, ni kuwaigiza Wakristo katika sherehe zao za Krismasi.

Inshallah, katika makala yanayokuja, tutaijadili hujja yao ya nne.

ABDILAHI NASSIR

P.O. BOX 84603

MOMBASA

2 Rabiuth Thani, 1423

14 Juni, 2002

4

JAWABU KWA WAPINGA MAULIDI

MAKALA NO: (4)

MUANDISHI NI: SEHIKH ABILLAHI NAASIR

WANAVYOSEMA WAPINGA MAULIDI NA MAJIBU YETU

Tunaendelea na hujja za wanaopinga maulidi na majibu yetu.

Katika hujja yao ya nne wanasema: Kwenye sherehe za maulidi hufanywa baadhi ya mambo ambayo ni ya munkar (yanayochukiza, bali ni haramu kamwe, katika sharia ya Kiislamu).

MAJIBU YETU:

Hiyo si hujja madhubuti. Kwa nini maulidi yote yatupwe kwa sababu tu ya kufanywa baadhi ya mambo ambayo ni ya munkar katika sherehe zake? Kwa nini hayaondolewi hayo ya munkar, kama yako, yakabakishwa yasiyo ya munkar? Kwani tunda likiwa limeoza kidogo hutupwa lote, au hukatwa pale palipooza likaliwa pale pazuri palipobaki?

Katika hili tuna funzo zuri kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Yeye aliondoa tawafu ya Al-Kaaba, na Swafaa na Marwa, kwa sababu mwahali humo mulikuwa na munkar (masanamu) au aliamrisha yaondolewe hayo masanamu na watu waendelee kutufu? Tutaona kuwa Mwenyezi Mungu hakutuzuia kufanya jambo zuri lililokuwako (kutufu na kusa'yi) kwa sababu tu katika ibada hizo palikuwa na munkar (masanamu). Alilolifanya ni kuondoa munkar uliokuwako, akatuacha tuendelee na mazuri yaliyobaki (tawafu).

Kwa hivyo, kama katika maulidi kuna munkar wowote, la sawa ni uondolewe munkar huo, na maulidi yaachwe yaendelee. Si kumtupa jongoo na ung'ongo (ujiti) wake.

Kidokezo

Baada ya kutoa makaratasi yetu kwa wiki tatu, makundi mawili ya wanaopinga maulidi yamejitokeza. La kwanza limejita "Ahlu-Tawheed"; na la pili linajita "Wakereketwa wa Sunna Malindi". Na yote mawili hayakutoa anwani zao!

Ahlu-Tawheed wametoa makaratasi yenye jina la "Uzushi na Shirk Ndani ya Barzanji na Vitabu Vyengine vya Maulid". Katika makaratasi hayo, wamenukuu baadhi ya madondoo ambayo -- kwa maoni yao -- ni shirki. Lakini hawakutueleza vipi kuwako madondoo hayo katika vitabu hivyo, hata kama yatakuwa ni shirki kweli, yanafanya maulidi yoyote mengine (yasiyo na hayo wanayoyaona wao kuwa ni shirki) hayafai kusomwa.

Wakereketwa wa Sunna Malindi, kwa upande wao, wametoa makaratasi yenye jina la "Chapa ya Kwanza (1): Majibu ya Abdillah Nassir". Katika makaratasi hayo, ambayo wameahidi kuendelea nayo, hawajazungumzia maulidi. Walilolifanya ni kunizungumza mimi binafsi -- kwa ya kweli na ya uwongo! Lakini na wao pia, kama wenzi wao, hawajatueleza vipi vyovyote vile vitakavyokuwa mimi binafsi -- iwe ni kwa wema ama kwa uovu -- ni hujja tosha ya kuyafanya maulidi yawe hayafai kusomwa! Pengine watalieleza hilo katika makala yao yatakayofuatia.

Hata hivyo si nia yangu, kwa sasa, kuyajibu makaratasi hayo kwa sababu kutatutoa nje ya mfululizo wetu huu. Nia yangu inshallah ni kuendelea kuzijibu hujja zao zote nilizozidondoa katika makaratasi yetu ya kwanza ya tarehe 4 Rabiul Awwal, 1423 / 17 Mei, 2002. Baada ya hapo ndipo nitakapojibu hayo yaliyomo katika makaratasi yao hayo.

Kwa hivi sasa, napenda kuwahakikishia wanaosoma maulidi kwamba yote waliyoyataja katika makaratasi yao mawili hayo tutayajibu kiilimu na kistaarabu, kama ilivyo dasturi yetu, na kama tulivyofanya mpaka sasa, pamoja na kuonyesha kwamba hayana mashiko.

Kwa hivyo, tunawaomba wale walionayo makaratasi hayo wayaweke, wangojee majibu yetu inshallah.

ABDILAHI NASSIR

P.O. BOX 84603

MOMBASA

9 Rabiuth Thani, 1423

21 Juni, 2002

5

JAWABU KWA WAPINGA MAULIDI

MAKALA NO: (5)

MUANDISHI NI: SEHIKH ABILLAHI NAASIR

WANAVYOSEMA WAPINGA MAULIDI NA MAJIBU YETU

Tunaendelea na hujja za wanaopinga maulidi na majibu yetu.

Katika hujja yao ya tano wanasema: Hakuna ushahidi wowote, wa Qur'ani wala Hadithi za Mtume Muhammad (s.a.w.w.), unaothubutisha usawa wa kuyasoma maulidi, sikwambii kuyatilia nguvu.

MAJIBU YETU:

Katika majibu yetu ya hujja yao ya pili, tulieleza kwamba -- kwa mujibu wa msingi mmoja kati ya misingi muhimu ya sharia ya Kiislamu -- anayetakikana kuthubutisha kuwa maulidi hayafai kusomwa si anayesema yasomwe; ni anayesema yasisomwe. Kwa hivyo ushahidi wa Qur'ani na Hadithi unaotakikana si wa kutolewa na sisi tunaosema ni sawa kusoma maulidi, bali ni wa kutolewa na wao wanaoyakataza. Jee, wanao ushahidi huo? Kama wanao, twaukaribisha.

Hata hivyo, kama ushahidi wanaoutaka wapinga maulidi, wa Qur'ani na Hadithi, ni unaosema kwa kutasua (nassun qat'iyy / categorically), "Enyi mlioamini! Someni maulidi"; basi ushahidi huo hakuna. Lakini tunauliza, kwa sharia ya Kiislamu, ni lazima jambo litasuliwe katika Qur'ani au Hadithi ya Bwana Mtume (s.a.w.w.) ndipo liruhusiwe kufanywa? Jee, hakuna mambo ambayo Waislamu -- wakiwamo wanaopinga maulidi -- huyafanya pamoja na kuwa hawana ushahidi wa Qur'ani wala Hadithi zilizoyataja mambo hayo?

Kwa mfano, ni nani kati ya wanaopinga maulidi anayeweza kututolea ushahidi wa kutasua -- wa Qur'ani au Hadithi ya Mtume Muhammad (s.a.w.w.) -- wa Waislamu kuruhusiwa kujenga vyuo (colleges) na vyuo vikuu? Au kutoa digrii? Au kujenga hospitali na zahanati? Au kujenga nyumba za mayatima (orphanages)? Au kuunda vyama vya ushirika? Au kuweka mashindano ya kusoma Qur'ani na kuyatolea zawadi, na mengine mengi kama hayo? Jibu ni: hakuna! Kama uko, tunaomba tutolewe. Jee, kwa kuwa hauko, ndio watakuwa Waislamu wote -- wakiwamo wanaosoma maulidi -- wanakosea kwa kuyafanya mambo hayo kwa sababu tu hakuna aya au Hadithi inayoyataja? Kama ni hivyo, basi kwa nini wao wanayafanya? Kama sio hivyo, basi kwa nini wanatukataza kuyasoma maulidi kwa sababu hiyo hiyo?

Katika Qur'ani na Hadithi kuna mambo ambayo uhalali wake umetasuliwa (specified). Mfano wa hayo ni kumpwekesha Mwenyezi Mungu, kuswali, kufunga (saumu), kutoa zaka, kuhiji, kuowa, kufanya biashara, kufanya uadilifu, na kadhaalika. Kuna na ambayo uharamu wake pia umetasuliwa; kama kumshirikisha Mwenyezi Mungu, kuzini, kula riba, kuiba, kudhulumu, kusema uwongo, kusengenya, na kadhaalika. Yote hayo ni mambo ambayo ushahidi wake -- wa kuyatasua khaswa -- unaweza kutolewa katika Qur'ani na / au Hadithi za Bwana Mtume (s.a.w.w.).

Kuna na ambayo hayakutasuliwa isipokuwa yametajwa kwa jumla (generally) tu. Hayo, kinyume na yale yaliyotasuliwa tuliyoyataja hapo juu, yana uwanja mkubwa wa jinsi ya kuyatekeleza maadamu hayatachanganywa na ya haramu. Hebu tuangalie mifano miwili mitatu:

1. Mayatima: Tunaposoma Qur'ani na / au Hadithi, tunaona kwamba tunahimizwa kwa jumla tuwatizame, tusiwatupe; tuwahurumie, tusiwatese. Vipi? Hilo hatukutajiwa tafsili zake isipokuwa tumeachiwa sisi, bora tu tusitie la haramu. Kwa sababu hii ndio ukaona hakuna aliyezuia kujengwa nyumba za mayatima (orphanages) japokuwa hazikutajwa kwa jina katika Qur'ani wala Hadithi za Mtume Muhammad (s.a.w.w.)!

2. Ilimu: Tunaposoma Qur'ani na / au Hadithi, tunaona jinsi tunavyohimizwa, bali kufaradhiwa, kusoma na kuitafuta ilimu popote ilipo. Hatukupawa tafsili ya namna ya kulitekeleza hilo. Kwa hivyo, maadamu hatulitii la haramu, tuko huru kusoma kwa ubao, kitabu, tepu, video, redio, runinga, mtandao, na kadhaalika; kama ambavyo tuko huru kusoma madrasa, nyumbani, msikitini, chuoni (college) au kwenye vyuo vikuu; na kama ambavyo tuko huru kukaa majamvini, vitini au madeskini. Hakuna hata mmoja wa mashekhe wa wanaopinga maulidi anayewazuia watu kuyafanya hayo, na tuliyoyataja hapo juu yanayohusu mayatima, kwa sababu tu hayakutajwa kwa jina katika Qur'ani wala Hadithi za Mtume Muhammad (s.a.w.w.)!

Basi kwa nini kuyapinga maulidi?

Inshallah, katika makala yanayofuatia haya, tutazidondoa aya za Qur'ani na Hadithi za Bwana Mtume (s.a.w.w.) ambazo, japokuwa hazikutaja maulidi kwa jina, zinaunga kwa jumla yale yanayofanywa na yanayofanyika maulidini.

ABDILAHI NASSIR

P.O. BOX 84603

MOMBASA

16 Rabiuth Thani, 1423

28 Juni, 2002

6

JAWABU KWA WAPINGA MAULIDI

MAKALA NO: (6)

MUANDISHI NI: SEHIKH ABILLAHI NAASIR

WANAVYOSEMA WAPINGA MAULIDI NA MAJIBU YETU

Kama tulivyoeleza katika makala yetu ya wiki iliyopita, sio kila kitu kimetajwa kinaga ubaga katika Qur'ani na / au Hadithi. Kuna yaliyotajwa hivyo; kuna na yaliyotajwa kwa jumla, kama maulidi. Lau Waislamu (wanazuoni wao) wangekataa kila jambo ambalo halikutajwa kwa jina katika Qur'ani na / au Hadithi, wangelibaki nyuma kwa karne 14, na wasingekuwa na maendeleo yoyote.

Sasa tuje kwenye maulidi.

Japokuwa -- kama tulivyoeleza katika makala yetu ya wiki iliyopita -- maulidi hayakutajwa kwa jina katika Qur'ani wala Hadithi, lakini yamekusanya mengi yaliyoamrishwa au yaliyopendekezwa na Qur'ani na / au Hadithi. Hapa chini tutayataja baadhi yake tu:

1. Kusoma na kusikiliza Qur'ani: Tunaposoma Qur'ani (k.m. Sura 73:4 na 20), tunaona jinsi Mwenyezi Mungu anavyotuamrisha tuisome. Na tunapokuja kwenye Hadithi zake, tunaelezwa kwamba Bwana Mtume (s.a.w.w.) alikuwa akipenda sana mtu amsomee yeye Qur'ani, na yeye akisikiliza.

Jee, pale tunapoyafungua maulidi yetu kwa mmoja wetu kuisoma Qur'ani, na wengine tukawa tunamsikiliza, huwa -- kama hatukufanya la sunna -- tumefanya lipi la bid'a?

2. Kumswalia Mtume (s.a.w.w.): Katika Qur'ani Tukufu (Sura 33:56), Mwenyezi Mungu anatuamrisha tumswalie Mtume Wake (s.a.w.w.) baada ya kutwambia kuwa Yeye na Malaika Wake hufanya hivyo pia. Isitoshe! Na kila Ijumaa, khatibu hutukumbusha juu ya mimbari, kwa kututajia Hadithi ya Mtume (s.a.w.w.), kuwa yoyote atakayemswalia yeye mara moja, Mwenyezi Mungu atamswalia (atamrehemu) mtu huyo mara kumi!

Jee, katika kikao kimoja tu cha maulidi, waliohudhuria humswalia Mtume (s.a.w.w.) mara ngapi? Zidisha mara hizo kwa kumi ujue Mwenyezi Mungu hukurehemu wewe mara ngapi katika kikao hicho. Jee, ni lipi hapo -- kama halitakuwa sunna -- lililo bid'a?

3. Kumhishimu na kumtukuza Bwana Mtume (s.a.w.w.): Katika Qur'ani Tukufu (Sura 7:157), Mwenyezi Mungu anawasifu, na kuweta "wenye kufaulu", wale ambao humtukuza na kumhishimu Mtume Wake (s.a.w.w.), wakamsaidia na kuyafuata yale aliyoyaleta. Lakini tutawezaje kuyafanya hayo kama mtu mwenyewe hatumjui vilivyo?

Waswahili husema: "Jambo usilolijua ni usiku wa kiza"; na "asiyekujua hakuthamini". Kwa hivyo, bila ya kumjua Mtume (s.a.w.w.) vilivyo -- historia yake, sifa zake, cheo chake, utukufu wake, na kadhaalika -- vipi tutaweza kumthamini na kumtukuza? Ndipo wanazuoni, kwa kuwa si kila mtu aweza kusoma vitabu, wakabuni maulidi ili yawe ni chombo cha kumjulisha Bwana Mtume (s.a.w.w.) apate kuhishimiwa na kutukuzwa. Hivyo katika maulidi, watu hupata fursa ya kuelezwa yote ya Mtume (s.a.w.w.). Na kwa kuyajua hayo, watu humpenda; na kama ilivyo dasturi ya kila apendaye kumfuata yule anayempenda, watu humfuata.

Jee, kama maulidi yanasaidia watu kumjua Mtume (s.a.w.w.), kumkumbuka na kumpenda, ni lipi hapo la bid'a?

4. Kumsifu Bwana Mtume (s.a.w.w.): Tunaposoma maisha yake, tunaambiwa kwamba, miongoni mwa maswahaba, walikuwako waliotunga mashairi ya kumsifu Bwana Mtume (s.a.w.w.) ambayo walikwenda nayo mbele zake na kumsomea. Bwana Mtume (s.a.w.w.) hakuwafukuza watu hao wala hakuwakataza, bali aliwasikiliza na kuyafurahia yote waliyomsomea. Kwa kitendo hicho kwa hivyo, Bwana Mtume (s.a.w.w.) alitufungulia mlango wa kumsifu. Tafauti ya pekee iliyoko baina ya maswahaba na sisi ni kwamba wao walimsifu machoni mwake, hali sisi tunamsifu akiwa hayuko na sisi kimwili. Sasa, kwa kitendo hiki, tunafanya jambo gani ambalo halikufanywa na maswahaba na kukubaliwa na mwenyewe Bwana Mtume (s.a.w.w.)?

Kama kufanya hivyo ni bid'a, basi sunna ni ipi?

Kwa leo tukomee hapa. Inshallah wiki ijayo tutaendelea na yaliyobaki.

ABDILAHI NASSIR

P.O. BOX 84603

MOMBASA

23 Rabiuth Thani, 1423

5 Julai, 2002

7

JAWABU KWA WAPINGA MAULIDI

MAKALA NO: (7)

MUANDISHI NI: SEHIKH ABILLAHI NAASIR

WANAVYOSEMA WAPINGA MAULIDI NA MAJIBU YETU

Wiki iliyopita tulidondoa baadhi ya mambo yanayofanywa maulidini ambayo, ama Qur'ani na / au Hadithi zimeyaamrisha, au zimeyapendekeza. Leo tunaendelea na yaliyobaki:

5. Kutoleana waadhi: Katika Qur'ani Tukufu (Sura 16:125) Mwenyezi Mungu anatuamrisha tulinganiane kwa hikima na mawaidha mema. Na vivyo hivyo ndivyo Bwana Mtume (s.a.w.w.) anavyotuhimiza katika Hadithi zake nyingi.

Jee, maulidini hatutoleani mawaidha na kulinganiana mema? Hayo nayo kama ni bid'a, sunna ni ipi?

6. Kumpenda Mtume (s.a.w.w.): Hadithi zake (s.a.w.w.) zatuhimiza tumpende, bali zinatueleza waziwazi kwamba hatuwi ni waumini mpaka tumpende yeye kuliko nafsi zetu, kuliko mali yetu na ahli zetu, bali kuliko watu wote.

Jee sifa zote zile anazosifiwa Mtume (s.a.w.w.) maulidini, furaha zote na nderemo zinazoonyeshwa maulidini, haziwi ni ushahidi wa mapenzi yetu kwa Mtume Muhammad (s.a.w.w.)? Mambo kama hayo hufanyiwa asiyependwa?

Kama kuonyesha mapenzi yetu kwa Mtume wetu ni bid'a, sunna ni ipi?

7. Kujumuika na kushikamana: Qur'ani Tukufu (Sura 3:103) inatuhimiza tushikamane na tusifarikiane. Na Mtume naye (s.a.w.w.) anatuhakikishia, katika Hadithi zake, kwamba popote ambapo tutajumuika kwa kheri -- na sidhani kuwa maulidi ni shari -- basi Malaika watatuzunguka, rehema za Mwenyezi Mungu zitufinike, na utulivu wa nyoyo utushukie.

Jee, tunapokusanyika maulidini, hatuyaoni hayo? Ule umoja na mshikamano unaopatikana maulidini, wa wafuasi wa madhihabi mbalimbali kusahau hitilafu zao na kuwa kitu kimoja, ni rehema ndogo?

8. Kutembeleana na kukirimiana: Bwana Mtume (s.a.w.w.), katika Hadithi zake, ametunasihi tuwe tukifanyiana hayo; na hayo huyapata kwa ukubwa siku za maulidi. Waislamu wa mtaa mmoja, au mji mmoja, au hata nchi moja -- kwa kuhudhuria sherehe za maulidi ya wenzi wao -- hupata fursa ya kutembeleana na kukirimiana. Kwa njia hii hujuana hali, wakasaidiana na kupanana (peana) moyo. Hilo huleta mapenzi na mshikamano baina yao. Na iwapo pale pasomwapo maulidi Waislamu ni wachache, kutembelewa kwao na ndugu zao wanaotoka sehemu nyengine huwatia moyo, na pia huwafanya wahishimiwe na wale jirani zao wasio Waislamu.

Katika hayo, ni lipi la bid'a, kama hapana la sunna?

9. Kutangaza Uislamu na kusilimisha wengine: Katika Qur'ani Tukufu (Sura 5:67) Mwenyezi Mungu anamwamrisha Mtume Wake (s.a.w.w.) awafikishie watu Ujumbe aliompa. Na katika khutba yake ya mwisho, Bwana Mtume (s.a.w.w.) alituamrisha sisi wafuasi wake tuufikishe Ujumbe huo kwa yule ambaye haujamfikia. Na hilo limepatikana -- na linaendelea kupatikana -- maulidini kwa ushahidi wa rikodi ya wengi waliosilimu baada ya kuhudhuria maulidini na kusikiliza kaswida na khutba zinazotolewa huko.

Jee, bid'a ni ipi hapo?

10. Kumkumbuka Mtume Muhammad (s.a.w.w.): Qur'ani Tukufu (Sura 41:34) inatwambia kuwa jema na ovu si sawa. Ukitaka kuliondoa ovu, liondoe kwa jema ndipo ovu litakapofutika. Na Mtume (s.a.w.w.) naye ametwambia vivyo hivyo. Hali kadhaalika wazee nao wanatwambia kwamba tukitaka kumpokonya mtoto wembe ili asijikate, tusimwache mikono mitupu maana ataurudia. Badali yake tumpe kitu chengine kisicho na madhara (k.m mpira) ashike. Kwa njia hii tutamwokoa na madhara.

Katika zama kama hizi zetu ambapo Waislamu kwa jumla, na watoto wao khaswa, wanayajua zaidi ya viongozi wasio Waislamu, bali hata ya walio maadui wa Uislamu, katika nyanja mbalimbali, na husherehekea mazazi yao -- ni lipi bora? Tuwaache waendelee vivyo hivyo? Au tuwaambie waache kufanya hivyo bila ya kuwawekea badali yake? Au tuwawekee badali iliyo nzuri (ya sherehe za mazazi ya Mtume (s.a.w.w.) na viongozi wengine wa Kiislamu) ili tuwaachishe hayo waliyoyashika? Jawabu hapo ninakuachia wewe, ndugu Mwislamu.

Mpaka hapa tumemaliza majibu yetu ya hujja zinazotolewa na wanaopinga maulidi; na kuwafikiwa ni kwa Mwenyezi Mungu. Inshallah wiki ijayo, kama tulivyoahidi katika makala yetu ya 9 Rabiuth Thani, 1423 / 21 Juni 2002, tutaanza kuyajibu ya Ahlu-Tawheed waliyoyasema katika makaratasi yao, "Uzushi na Shirk Ndani ya Barzanji na Vitabu Vyengine vya Maulidi".

ABDILAHI NASSIR

P.O. BOX 84603

MOMBASA

1 Jamaadal Uulaa, 1423

12 Julai, 2002

8

JAWABU KWA WAPINGA MAULIDI

MAKALA NO: (8)

MUANDISHI NI: SEHIKH ABILLAHI NAASIR

WANAVYOSEMA WAPINGA MAULIDI NA MAJIBU YETU

Kama tulivyoahidi wiki iliyopita, leo tunaanza kuwajibu Ahlu-Tawheed kwa waliyoyaandika katika makaratasi yao waliyoyapa jina la "Uzushi na Shirk Ndani ya Barzanji na Vitabu Vyengine vya Maulidi".

Katika makaratasi yao hayo, ndugu zetu hao wamenukuu baadhi ya maneno yaliyomo katika Barzanji na Burdah (vitabu viwili vinavyoeleza sifa za Mtume Muhammad s.a.w.w.) na kujaribu, kadri ya ujuzi na uweza wao, kuonyesha kwamba kusema maneno hayo ni shirki. Lakini, kabla ya kutoa majibu yetu, tuanze kwa kuyanukuu maneno yenyewe. Nayo ni mane yaliyotolewa katika Barzanji, na mawili katika Burdah.

Katika Barzanji wameyatoa yanayofuata:

1. "Na kama si yeye (Mtume s.a.w.) asingekuwa Alkhalilu (Ibrahim) na Adam. Na Musa (asingekuwepo) na Issa, bali hata Mulku Suleimani (usingekuwepo)."

2. "Ilisemekana alipotaka Mwenyezi Mungu, Mwenye Ezzi na Alietukuka, kumdhihirisha Mbora wa viumbe vyake, Muhammad, Rehma na Amani za Mwenyezi Mungu zimfikie. Akamuamrisha Jibril achukue Udongo wake (wa kumuumbia nao) kwenye mahali pa kaburi lake karimu".

3. "Alikuwa Mtume akikua mchana mmoja kama anavyokua mtoto mwengine kwa mwezi mzima kwa ajili ya kushughulikiwa na Mwenyezi Mungu".

4. "Akamwonyesha kwa haya macho ya kichwani (ya usoni) aliyomwonyesha. Nayo ni yeye mwenyewe Mwenyezi Mungu."

Na katika Burdah wameyatoa yanayofuata:

5. "Kama si yeye (Mtume s.a.w.w.) usingetoka ulimwengu (usingeumbwa)."

6. "Haukupata kunipiga vita Ulimwengu, nikataka nusra kwa Mtume, ila huipata tu."

Hayo ndiyo maneno waliyoyanukuu ndugu zetu wa Ahlu-Tawheed kuthubutisha kwamba, katika vitabu hivyo, muna shirki. Wakayaandamiza, pia, na hujja zao za kuyabatilisha hayo.

MAJIBU YETU :

Kwanza; tukumbuke kwamba tunalojadiliana si kuwa, katika vitabu vya maulidi, muna shirki au hamuna; la! Tunalojadiliana ni: maulidi ni bid'a au si bid'a; ni haramu au si haramu? Sisi, kwa upande wetu, katika makala yetu sabaa yaliyopita, kwa kujibu hujja zinazotolewa na wapinga maulidi, tumeonyesha kwamba maulidi si bid'a wala si haramu. Kwa hivyo sasa tunalolingojea kwa wapinga maulidi, wakiwamo Ahlu-Tawheed, ni majibu yao ya hujja tulizozitoa -- kiilimu na kimantiki, kama tulivyofanya sisi.

Pili; hata kama itakubaliwa kuwa hayo maneno waliyoyanukuu ni shirki -- na hilo hatulikubali kwa hujja tunayoitoa hapa chini -- hilo haliwi ni hujja ya kuharamishia maulidi au kuyasusia. La sawa kufanywa hapo ni kuyatoa hayo yanayoonekana ni shirki na / au kuyasahihisha; si kuzuia watu kuyasoma. Hivyo, kwa mfano, ndivyo alivyofanya marehemu Sheikh Abdulla Swaleh Farsy katika Wasila wa Nabahani. Yeye alipoona kwamba "Lawlaahu maa kunnaa walaa baaqiina" si sawa, hakuzuia watu, wala yeye hakuacha kuusoma. Alichofanya ni kukibadilisha kipande hicho na kukisoma alivyoona yeye ni sawa: "Lawlal ilaahu" Hakuutupa wasila wote, wala hakuzuia watu kuusoma kwa sababu tu muna kipande cha maneno asiyoyakubali.

Tatu; tunapoyataamali yote madondoo sita waliyoyanukuu Ahlu-Tawheed, ambayo nasi tumeyanukuu hapo juu, hakuna hata moja liwezalo kusemwa ni shirki kwa hujja ifuatayo:

Shirki ni kusema / kuamini kuwa Mwenyezi Mungu ana mwenziwe, au ana aliye sawa naye, au ana mfanowe, au ana anayetokana naye. Pia kusema / kuamini kuwa yuko muumbaji mwengine wa ulimwengu asiyekuwa Yeye, au muendeshaji (mudabbir) ulimwengu asiyekuwa Yeye, au mwenye haki ya kuweka sharia asiyekuwa Yeye, au anayelazimika kutwiiwa asiyekuwa Yeye, au kuna mtawala (haakim) asiyekuwa Yeye, au kuna mwenye haki ya kuabudiwa asiyekuwa Yeye.

Kwa kuwa hakuna hata moja, ya madondoo sita waliyoyanukuu Ahlu-Tawheed kutoka katika Barzanji na Burdah, linalosema hivyo, vipi basi mutakuwa muna shirki? Kama lipo, tunaomba watwambie ni dondoo lipi kati ya hayo waliyotutajia, na linaingia wapi katika hiyo taarifa ya shirki tuliyoieleza sisi hapo juu. Kama taarifa yetu imeacha mengine yaliyo shirki, basi tunaomba tukumbushwe. Kwa hakika haikuwa nia yangu kuingia katika masiala ya shirki kwa sababu hilo li nje ya maudhui yetu. Maudhui yetu ni maulidi ni bid'a au si bid'a; ni haramu au si haramu. Na hilo tushalijibu vya kutosha. Lakini, kwa kuwa wafuasi wa madhihabi ya wapinga maulidi hupenda kukibandika jina la bid'a au shirki kila wanachokipinga wao, nimeona japo kwa ufupi niwaeleze wasomaji wangu jamaa zetu hao hupotelea wapi katika kuielewa shirki ni nini, na si nini! Hilo, inshallah, tutalishughulikia wiki ijayo, kabla ya kuwajibu "Wakereketwa wa sunna Malindi".

ABDILAHI NASSIR

P.O. BOX 84603

MOMBASA

8 Jamaadal Uulaa, 1423

19 Julai, 2002

9

JAWABU KWA WAPINGA MAULIDI

MAKALA NO: (9)

MUANDISHI NI: SEHIKH ABILLAHI NAASIR

WANAVYOSEMA WAPINGA MAULIDI NA MAJIBU YETU

Wiki iliyopita tuliyataja maneno ambayo Ahlu-Tawheed wameyatoa katika Barzanji na Burdah ambayo, kwa maoni yao, ni shirki. Tukaahidi kuyajadili maoni hayo leo, baada ya kuieleza shirki ni nini.

Kwa taarifa tuliyoitoa sisi (na tumeomba tuelezwe kama tumeacha kitu katika taarifa hiyo), kati ya madondoo sita yaliyonukuliwa na ndugu zetu hao, matano yametushinda kuelewa vipi yaweza yakawa ni shirki. Kwa hivyo hatutashughulika nayo kwa leo mpaka hapo tutakapofafanuliwa inshallah. Tutakaloshughulika nalo leo ni moja tu lililobaki ambalo, kwa hujja walizozitoa kulipingia, tumeweza kulifahamu lililowafikirisha wao kuwa ni shirki. Nalo ni lile la Buswiri kusema katika Burdah: "Haukupata kunipiga vita Ulimwengu nikataka nusra kwa Mtume ila huipata tu."

Kulikosoa hilo, Ahlu-Tawheed wameitaja Sura 3:126 ambayo wameifasiri hivi: "Na msaada hautoki (kwa mwengine yoyote) isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu, Mwenye Nguvu na Mwenye hikima". Kwa kuitaja aya hii, kwa hivyo, tumeelewa kwamba ndugu zetu hao wameyaelewa maneno ya Buswiri hivi: "Kwa kuwa msaada (nasr) hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu, kuuomba kwa mtu mwengine yoyote asiyekuwa Mwenyezi Mungu, hata awe ni Mtume (s.a.w.w.), ni sawa na kumfanya mtu huyo ni Mwenyezi Mungu! Na kufanya hivyo ni shirki; kwa hivyo katika Burdah muna shirki!"

MAJIBU YETU :

Kwanza; katika tafsiri yao ya hiyo Sura 3:126 wameongeza maneno katika pinde, tuliyoyachapa kwa italiki, ambayo hayamo katika aya hiyo, wala hayaipunguzii maana lau yasingeongezwa.

Pili; kama maana ya "msaada hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu" ni kwamba haturuhusiwi kutafuta msaada kwa asiyekuwa Yeye, au asiyekuwa Yeye hana msaada wa kuutoa, basi ilikuwaje watu wa Madina wakaitwa answaar (wasaidizi)? Walimsaidia nani? Huyo aliyesaidiwa, aliukosa msaada wa Mwenyezi Mungu hata wakaingia kati wao? Na sisi Waislamu, pamoja na Mtume wetu (s.a.w.w.), tunamshirikisha Mwenyezi Mungu kwa kuwaita answaar watu wa Madina?

Tunaposoma Sura 3:81 tunaona jinsi Mwenyezi Mungu alivyochukua ahadi kwa Mitume Yake kwamba itamsaidia / itamnusuru (latansurunnahuu) Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Jee, kama "msaada hautoki (kwa mwengine yoyote) isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu," ilikuwaje hapo, Yeye Mwenyewe, akautaka kwa asiyekuwa Yeye? Jee, kwa kitendo hicho, Mwenyezi Mungu -- Mwenyezi Mungu apishe mbali! -- alikusudia kuifanya Mitume Yake ni miungu?

Katika Sura 7:157, kati ya sifa za waumini ambao "ndio wenye kufaulu", ni wale ambao wamemsaidia / wamemnusuru (wanaswaruuhu) Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Jee, kama "msaada hautoki (kwa mwengine yoyote) isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu", kwa nini akawaagiza waumini wamsaidie Mtume Wake? Kwa sifa hiyo hapo, ndio Mwenyezi Mungu amewafanya waumini kuwa ni miungu? Mwenyezi Mungu -- Mwenyezi Mungu apishe mbali -- hapo amefanya shirki?

Hali kadhaalika; tunaposoma Sura 28:15 tunaona jinsi jamaa yake Nabii Musa (a.s) "alivyomuomba msaada" (fastaghaathahuu) juu ya adui yake. Jee, Nabii Musa (a.s) alimrukia jamaa yake huyo, na kumwambia asilete shirki kwa kumuomba yeye msaada badali ya Mwenyezi Mungu? La! Alimsaidia; na siku ya pili (Sura 28:18) yule aliyeomba msaada jana (istanswarahuu) akamuomba tena! Jee, kama "msaada hautoki (kwa mwengine yoyote) isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu", kwa kutoa msaada wake huo, Nabii Musa (a.s) alikuwa Mwenyezi Mungu, au hakujua kuwa "msaada hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu"?

Kwa kutaja mifano hiyo hapo juu, sisi tusomao maulidi hatukusudii kukanusha yaliyomo katika aya iliyotajwa na wapinga maulidi, kuwa "msaada hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu"; hasha! Tunalokusudia ni kufahamisha kwamba: maneno yanapofanana, si lazima na maana yafanane (yawe mamoja). Kwa hivyo, msaada ambao Buswiri aliuomba kwa Bwana Mtume (s.a.w.w.), na sisi huukariri tunapoisoma hiyo Burdah, sio msaada ambao huombwa kwa Mwenyezi Mungu. Ni majina tu kufanana -- kama ulivyokuwa ule ambao Mwenyezi Mungu alimtakia Mtume Wake kwa Mitume mengine, na aliotutaka sisi waumini tumpatie Mtume Muhammad (s.a.w.w.), na ambao watu wa Madina walimpatia Bwana Mtume (s.a.w.w.) hata wakaitwa answaar (wasaidizi wake), na ule ambao Nabii Musa (a.s) alimpatia jamaa yake.

Msaada wa Mwenyezi Mungu unatokana na Yeye Mwenyewe; hakupawa na yoyote uweza huo wa kusaidia. Lakini wa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, akiwamo Mtume Muhammad (s.a.w.w.), si wake mwenyewe; ni wa kupawa (kuwezeshwa na Mwenyezi Mungu). Na hapo ndipo palipo na tafauti baina ya shirki ni nini, na si nini.

Ukiamini kwamba Mtume (s.a.w.w.) -- yeye mwenyewe, bila ya kupawa uweza huo na Mwenyezi Mungu -- aweza kusaidia; hiyo ni shirki. Na hilo silo alilokuwa akiliamini Buswiri, wala silo tunaloliamini sisi tusomao maulidi. Lakini ukiamini kuwa msaada uwezao kupawa na Mtume (s.a.w.w.) ni ule aliowezeshwa yeye na Mwenyezi Mungu; hiyo si shirki. Na hilo ndilo alilokusudia Buswiri katika Burdah, na ndilo tunaloliamini sisi tunaosoma maulidi. Kwa hivyo kubwa ambalo wapinga maulidi waweza kutwambia sisi ni kuwa Mtume (s.a.w.w.) hakuwa / hana uweza huo; kwa hivyo ni kazi bure kumuomba hivyo -- jambo ambalo hatulikubali kwa sababu ya hujja tulizonazo. Lakini hawawezi kutwambia ni shirki, kwa mifano mingi tuwezayo kuwatolea katika Qur'ani Tukufu.

Inshallah wiki ijayo tutaeleza kwa urefu ni wapi ambapo wapinga maulidi hupotea na kukosea kuielewa shirki. Nataraji baada ya hapo wataweza kuyaelewa yaliyomo katika Barzanji na Burdah.

ABDILAHI NASSIR

P.O. BOX 84603

MOMBASA

15 Jamaadal Uulaa, 1423

26 Julai, 2002

10

2

UCHUNGUZI JUU YA UWAHABI

KIASI CHENYE MAKOSA

Tunakwenda sambamba na mwandishi huyu wa Kiwahabi katika kitabu chake kisichokuwa na maana, na tunamuona anamkosoa Imam Ali ibn Abi-Talib [a] kwa njia ya kutaka kufahamu na kuuliza sababu za kufanya haraka kumuuzulu Muawiyah mara tu Imam Ali[a.s] alipotawalia (Ukhalifa) na anajiuliza anasema: Kwa nini, kwa nini? Bila shaka kilichompelekea kupinga ni kule kumlinganisha kwake Imam Ali[a.s] na watawala wenye kujali maslahi ambao hawafikiri isipokua maslahi yao binafsi na kuyatanguliza kuliko hukumu za sheria na wajibu aliowajibisha Mwenyezi Mungu, bali huupinda upande wa sheria kwa lengo la kulinda uongozi na utawala wao, basi kwa mujibu wao "lengo lao in kujisafishia wasiIa." Fikra hii potofu ndiyo iliyomfanya mwandishi huyo wa Kiwahabi ampinge kiongozi wa wachamungu Ali[a.s] kwa njia ya kuuliza na kutaka kufahamu. Naam, lau Imam Ali[a.s] angekuwa kama watawala wengine wanaojali maslahi yao, basi upinzani wa Wahabi huyu ungekuja hapa na angetakiwa awaache watu wapotofu na mafasid kama vile Muawiyah na mfano wake waendelee kuwatawala Waislamu kama zipendavyo nafsi zao za kishetani, lakini Imam Ali[a.s] siyo kiongozi wa aina hiyo ya watawala hao sivyo kabisa.

Kwa hakika ni kiongozi mwenye Ikhlas, kwani anasema Imam Ali[a.s] akimjibu Mughira ibn Shu'bah na walio kama Mughira "Mimi sitaki Mwenyezi Mungu anione ni mwenye kuwafanya wanaopotosha kuwa ni wasaidizi (wangu)".[14] Ewe msomaji mpendwa: Mpaka hapa tunafupisha maneno, na tunachokitarajia ni kwamba jibu hili la haraka tulilolileta limekuwekea wazi msimamo wa huyu Wahabi mwenye chuki dhidi ya kizazi cha Mtume Muhammad[s.a.w.w] na wafuasi wao na (na vile vile limekuwekea wazi) kufilisika kwake (Wahabi huyu) katika maarifa ya Dini na Itikadi za haki za Kiislamu na kukosea kwake na upotofu wake alioufanya kwa makusudi na riwaya zake za nongo. Nao wanachuoni wa dini na wanachuoni wa sheria ya haki watazishughulikia hujuma hizi mbaya za Kiwahabi, nasi tunataraji hivi karibuni apendapo Mwenyezi Mungu, litatolewa jawabu thabiti dhidi ya uzushi wa Wahabi huyu mpotofu mwenye kupotosha.

MWITO WA KUFANYIKA KONGAMANO LA KIISLAMU

Kwa hakika ni muhimu sana kufanyika kongamano la Kiislamu ambalo ndani yake yatatatuliwa Masail yenye Khitilafu kwa mujibu wa muongozo wa kielimu na Mantiq na dalili, kwani wakati huu wa sasa ziko khitilafu kubwa mbili ambazo ni Uwahabi na madhehebu mengine ya Kiislamu juu ya Tauhidi na shirki, basi Je, kwa lengo la kukurubiana pande hizi mbili si inafaa kufanya mkutano wa kielimu ambao Masail haya yataaridhiwa katika meza ya uchunguzi na uhakiki kwa lengo Ia kuondoa batili na kuithibitisha haki, kwani huenda ikachomoza nuru ya kuonyesha njia kwa wanaobabaika? Inabidi kongamano hili lifanyike kwa msingi wa kutatua tatizo na siyo propaganda tu, na lisichukuliwe kama vile ni jambo Ia propaganda ya Serikali fulani.

Na ili jambo hili lipate kukamilika kama inavyotakiwa, inapasa kuchunga sharti zifuatazo:

1. Mwito huo utolewe kwa wanafikra wa Kiislamu kutoka katika Madhehebu mbali mbali za Kiislamu ambao wanawakilisha Madhehebu hayo na wanafahamika khasa kuwa wao ni wanachuoni na ni wafikra wa dhehebu hilo (wanaloliwakilisha), na wasipelekewe mwito huu wanachuoni wa Pilato wa Saudia peke yao ambao wanapatikana India, Pakistani na Misri iliyodhulumiwa.

2. Na zaidi ya wawakilishi wa Madhehebu manne, ni lazima mwito huu utolewe kwa wanachuoni na wanafikra wa Shia Ithna-Asheriyyah na dhehebu la Zaydiyyah ili mkutano huo unenekane kwa muono wa pamoja na ujumla wa Waislamu wote.

3. Ni lazima utolewe uhuru kamili kwa wajumbe wa mkutano ili kila mmoja miongoni mwao aweze kujadili juu ya Masail yatakayokuwa yamearidhiwa kwenye uwanja (wa majadiliano), na awe na haki ya kuzitetea kwa uhuru fikra zake na itikadi zake, pia kongamano hilo lijiepushe na kila kitu kinachoharibu heshima ya wajumbe wake, miongoni mwa maneno ya matusi na dharau ambayo leo hii yameenea katika miji ya Saudia.

4. Na ni lazima idara inayoendesha kongamano isifungamane na upande wowote, na bora zaidi iwe imeundwa kutokana na Madh-hebu tofauti tofauti yanayoshiriki kwenye kongamano.

5. Utafiti wote unaofanyika kwenye kongamano usambazwe (kama ulivyo) bila ya mabadiliko yoyote ndani yake na utumwe kwenye vituo (vyuo) vya Elimu ulimwenguni ili wanaopenda kujua matokeo ya kongamano hilo wausome. Aina hii ya kongamano na kwa kuchunga sharti hizi, tunataraji Masail mengi mbali mbali yatatatuliwa, na kile kiini cha mafahamiano kitathibitika na maelewano baina ya Waislamu yatapatikana.

LENGO LA KITABU HIKI

Katika kitabu lilki tumejaribu kuchukua Masail ya msingi ambayo kuna hitilafu ndani yake baina ya Mawahabi na Madh-hebu mengine ya Kiislamu, na kuyatolea hukumu kwa mujibu wa Qur'an Tukufu na Sunna Tukufu ili tufahamu rai ya Uislamu katika Masail hayo. Na kitabu hiki siyo pekee ambacho tulichoandika kuhusu maudhui hizi, bali kimetanguliwa na vitabu vitatu na kila kimoja miongoni mwa hivyo kimebeba jukumu Ia kuchunguza na kuhakiki baadhi ya Masail haya, na vitabu hivyo ni:

1. Mafahimul-Qur'an: Na ndani yake kuna uchunguzi mpana juu ya Tauhidi katika ibada ndani ya juzuu ya kwanza ya kitabu hicho kutoka ukurasa wa 378 hadi 528, nayo ni mkusanyiko wa mihadhara iliyotolewa katika hauza ya elmu katika mji mtakatifu wa Qum, na akaiandika kwa kalamu Sheikh Jaafar al-Hadi na ikachapishwa nchini Iran na Lebanon.

2. At-Tawasul-Bil-Auliya: Ni uchunguzi unaohusu kujuzu kutawassal kwa Maimamu watakatifu (Amani iwashukie) na kutawassal kwa Mawalii wema wa Mwenyezi Mungu, na mas-ala haya ni miongoni mwa mas-ala muhimu ambayo Mawahabi wanaeneza Shub-ha (Utata) juu yake.

3. At-Tauhid Wash-Shirki Fil-Qur'anil-Karimu: Kwa hakika (ndani ya Kitabu hiki) nimejaribu kujihusisha na Mas-ail ya Tauhidi na shirki, na nimelitatua tatizo hili ambalo limekishughulisha kikundi hiki cha Mawahabi kwa muda wote wa karne mbili na nusu, na kimechapishwa katika nchi nyingi za ulimwengu.

Na mihadhara hii (iliyomo kitabuni humu) ni uchunguzi wa mara ya nne ambao tunautoa kwa ulimwengu wa Kiislamu, na tunawaita Mawahabi walioko Riyadhi na katika Haram mbili Tukufu na waandishi walioajiriwa na Mawahabi ambao wanaandika kwa Maslahi yao, waikubali haki wala usiwadanganye upinzani wa kijinga na wazinyenyekee dalili, na iwapo hawatakubali isipokuwa (kuendelea na) uadui na kupinga haki, basi sisi tunawapa changa moto ya kukijibu kitabu hiki kwa jawabu madhubuti linalokubalika, linalotegemea mantiki na siyo (jibu la) udanganyifu na uzushi. Na, Mawahabi wanalazimika kuwaacha huru Waislamu katika Haram mbili tukufu watende mambo yao matukufu ya dini, na wasiwakabili kwa uovu ndani ya Haram ya amani ya Mwenyezi Mungu na waache propaganda za Kiwahabi ambazo haziongezi chochote ndani ya Waislamu isipokuwa utengano, fitna na bughudha. "Bila shaka huu ni ukumbusho, basi yeyote atakaye na aishike njia kwenda kwa Mola wake". Jaafar Subhani

Chuo cha Elimu - Qum Tukufu

26 / Mfunguo Mosi /1406 A.H.

VIDOKEZO JUU YA MAISHA YA MUASISI WA UWAHABI

Madhehebu ya Kiwahabi yanahusishwa kwa Sheikh Muhammad bin Abdul-Wahabi kuwa ndiyo muanzilishi wake. Madhehebu ya Sheikh huyu yameitwa "Wahabiyya" kwa munasaba wa jina lababa yake aliyekuwa akiitwa "Abdul-Wahabi". Ama sababu zilizofanya Madhehebu ya Kiwahabi yasiitwe "Muhammadiyya" kwa munasaba wa jina la muanzilishi wake, ni kama wasemavyo baadhi ya Wanachuoni kwamba, palifanywa tahadhari ya kuepusha kufanana baina ya hao wafuasi wa Kiwahabi na Waislamu wengine ambao ni wafuasi wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (Muhammad bin Abdillahi).[15] Sheikh Muhammad bin Abdul-Wahab alizaliwa mwaka 1115 A.H. katika mji wa Uyainah ambao ni miongoni mwa miji ya Najdi; na mzazi wake alikuwa kadhi wa hapo Uyainah. Tangu utotoni, Muhammad bin Abdul-Wahab alikuwa na shauku sana ya kusoma vitabu vya tafsiri, hadithi na mambo ya ambaye alikuwa ni miongoni mwa wanachuoni wa Kihanbal. Na tangu akiwa kijana, Muhammad bin Abdul-Wahabi alikuwa akiyakosoa mambo mengi ya Dini waliyokuwa wakiyatenda watu wa Najdi.

Sheikh huyu hakutosheka na Najdi peke yake katika upinzani wake huo, bali alivuka mipaka hadi Madina alikokwenda wakati akitoka Hija na kuendelea kusambaza upinzani huo. Kwa hakika hapo Madina, alikuwa akiwakemea wata waliokuwa wakitawasal kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu [s.w.t] kwenye kaburi lake tukufu. Baadaye alirejea Najdi na hatimaye akaenda Basra kwa lengo la kwenda Shamu. Alipokuwa Basra alianza kuwakemea watu na kuwakataza wasitende mambo yao ya dini, wenyeji wa Basra walipoiona hali hii, wakamtimua na kumfukuzilia mbali kutoka katika mji wao. Muhammad bin Abdul-Wahabi akakimbia na kuelekea katika mji wa Az-Zubair. Wakati akiwa njiani kuelekea Az-Zubair, Muhammad bin Abdul-Wahabi alichoka sana kutokana na mwendo wasafari hiyo, hivyo basi joto kali la jua lilimsababishia kiu kali kiasi cha kukaribia kufa; (Afadhali angekufa). Kwa bahati mtu mmoja kutoka Az-Zubair alimuona akamhurumia hasa kwa kuwa mavazi aliyokuwa amevaa yalikuwa ni mavazi ya watu wa dini basi mtu huyo akamnywesha maji Muhammad bin Abdul-Wahab; na akampandisha kwenye kipando chake na kumfikisha mjini.

Makusudio ya Muhammad bin Abdul-Wahabi ilikuwa ni kwenda mpaka Shamu, lakini kutokana na kukosa kwake chakula na mali ya kuweza kumudu safari hiyo, alisafiri mpaka Al-Ahsaa; kisha akaenda Huraimala ambao ni mji katika miji ya Najdi, na huo ulikuwa ni mwaka 1139 A.H. Katika mwaka huo huo, baba yake alihama kutoka Uyainah akaenda Huraimala. Hapo Muhammad bin Abdul-Wahabi akaungana na mzazi wake na akaendelea kusoma kwake. Katika kipindi hicho hicho, yeye aliendelea kueneza upinzani wake dhidi ya ibada mbali mbali za kidini katika nchi ya Najdi, jambo ambalo lilisababisha machafuko na kutokuelewana baina yake na baba yake kwa upande mmoja, na baina yake na watu wa Najdi kwa upande wa pili. Hali hii ya vurugu na kutoelewana iliendelea hadi mwaka 1153 alipofariki baba yake.[16] Kufariki kwa baba yake kulimpa nafasi nzuri Muhammad bin Abdul-Wahabi kutangaza wazi wazi itikadi zake za pekee. Alitembea huku na kule kueneza Aqida yake potofu, akawa anawakemea watu kutenda matendo ya dini, na kuwataka wajiunge katika kundi lake na wawe chini ya uongozi wake. Baadhi ya watu walihadaika na mwenendo wake, na wengine walimpinga.

Pamoja na hali hii, mambo yake yalijulikana wazi kwa watu wa mji wa Huraimala, na baada ya muda Muhammad bin AbdulWahabi alifunga safari kurudi Uyainah mahala alipozaliwa. Wakati huu Athumani bin Hamad alikuwa ndiyo mtawala wa hapo Uyainah, na alimpokea Muhammad bin Abdul-Wahabi na akamkaribisha kwa wema. Muhammad bin Abdul-Wahabi na mtawala huyo wa Uyainah walifanya makubaliano ya kila mmoja kumlinda mwenzake; ili mmoja wao awe na nguvu za kisheria na mwingine awe na nguvu za utekelezaji wa maamuzi yanayoamuliwa.

Kwa hiyo basi mtawala wa Uyainah akawa anamsaidia Muhammad bin Abdul-Wahabi kutekeleza malengo yake kwa kutumia nguvu za kiutawala, naye Muhammad bin Abdul-Wahabi humsaidia mtawala huyo kwa kutoa fatwa zinazowataka watu wamtii mtawala huyo na kuzifuata amri zake. Habari zilimfikia mtawala wa Al-Ahsaa kwamba, Muhammad bin Abdul-Wahabi anawalingania watu kwenye rai zake na uzushi wake, na pia kwamba mtawala wa Uyainah ndiye anayempa nguvu ya kufanya hayo. Mtawala huyu wa Al-Ahsaa alimwandikia barua kiongozi wa Uyainah kumuonya kwa kumsaidia kwake Muhammad bin Abdul-Wahabi. Barua hiyo alipoisoma, akamwita Muhammad bin Abdul-Wahabi na kumfahamisha kuwa yeye hatomsaidia tena.

Muhammad bin Abdul-Wahabi akamwambia mtawala wa Uyainah, "Iau ungenisaidia katika mwito wangu huu, ungeitawala Najdi yote". Mtawala huyo alikataa rai hiyo na akamuamuni Muhammad bin Abdul-Wahabi aondoke hapo Uyainah. Hivyo basi Muhammad bin Abdul-Wahabi akafukuzwa kutoka Uyainah hali ya kuwa mwenye kufedheheka. Tukio hili la kufukuzwa kwa Muhammad bin Abdul-Wahabi lilitokea mwaka 1160 A.H. na aliondoka hapo Uyainah akaelekea Dir'iyyah, mji ambao ulikuwa mashuhuri miongoni mwa miji ya Najdi. Mtawala wa hapo alikuwa in Muhammad bin Saud ambaye ndiye babu mkuu wa kizazi cha Saud (wafalme wa Saudi Arabia). Muhammad bin Abdul-Wahabi alipofika hapo, akatembelewa na mtawala huyo na akakirimiwa vizuri na kuahidiwa kutendewa mema. Naye kwa upande wake alimpa bishara mtawala huyo kwamba, ataitawala miji yote ya Najdi. Hivyo ndivyo yalivyotimia maafikiano ya wawili hawa, katika kutekeleza maovu yao dhidi ya Uislamu.

Ukweli ulivyo kuhusu watu wa Dir'iyya ni kwamba, watu hawa walikuwa ni masikini mno mpaka kipindi alichofika Muhammad bin Abdul-Wahabi na kufanya mapatano ya kusaidiana baina yake na Muhammad bin Saud. Anasema Ibn Bishri An-Najdi kama alivyopokea kutoka kwake Al-Alusi: "Watu wa Dir'iyya zama hizo (kabla ya kufika huko Muhammad bin Abdul-Wahab) walikuwa katika dhiki na taabu ya maisha, kwa hakika nilipata kushuhudia dhiki yao ya maisha hapo mwanzoni, na kisha baadaye katika utawala wa Suud, niliwaona wakaazi wale wale wa Dir'iyya wakiwa na mali nyingi na silaha zilizorembeshwa kwa dhahabu na fedha. Pia nikawaona wakiwa na farasi wazuri, vyombo vizuri na mavazi ya fahari na mambo mengine ambayo ni katika kuonyesha kuwa hali yao ya utajiri sasa imekuwa bora kiasi cha kushindwa kutaja kila kitu kwa ubainifu. "Wakati fulani niliona katika kipindi cha mkusanyiko mkubwa wa watu wa Ad-Dir'iyya (siku ya soko) makundi ya wanaume wakiwa upande mmoja, na makundi ya wanawake yakiwa upande mwingine. Basi katika makundi haya niliona vitu mbali mbali ikiwemo dhahabu, fedha, silaha, ngamia, mbuzi, farasi na mavazi ya fahari pamoja na vitu vingine vingi visivyoweza kutajwa kutokana na wingi wake, isitoshe uwingi wa watu waliokuwepo hapo ulikuwa unatazamika hadi upeo wa macho.

Nami nilikuwa nazisikia sauti za wauzaji na wanunuzi zikivuma kama mvumo wa kundi Ia nyuki.[17] Sasa basi, utajiri huu mkubwa wa Ad-Dir'iyya umetokea wapi? Ibn Bishri An-Najdi hakufichua siri hii; lakini historia inaonyesha kuwa Muhammad bin Abdul-Wahab ndiye aliyekuwa akizipata mali hizo kwa kupitia mashambulizi yake ya kuvizia yeye na wafuasi wake dhidi ya miji ya Kiislamu ambayo ilikuwa ikipinga kukubaliana naye na kumtii. Hivyo basi, akawa anapora mali na milki ya miji hiyo na kuigawa kwa watu wa Ad-Dir'iyya. Katika kugawa mali alizozipora kutoka kwa waislamu waliokataa kumtii, Muhammad bin Abdul-Wahabi alikuwa akitumia njia ya pekee aliyojipangia, kwani ugawaji wake ulikuwa ni kwa namna apendavyo yeye. Wakati mwingine alikuwa akigawa mali hiyo baina ya watu wawili na watatu miongoni mwa wafuasi wake ijapokuwa mali hiyo ilikuwa nyingi. Ama mtawala wa Najdi yeye alikuwa akichukua fungu lake kwa ridhaa ya Muhammad Bin Abdul-Wahab mwenyewe.

Na katika mambo muhimu yanayoonyesha uasi wa Muhammad bin Abdul-Wahab, ni sera hii mbaya aliyowafanyia Waislamu waliokataa kutii matamanio yake na rai zake; akawa anawatendea nambo yanayostahiki kufanyiwa kafiri anayeupiga vita Uislamu. Bwana huyu alihalalisha mali za Waislamu ziporwe na heshima zao zivunjwe. Kwa kifupi, Muhammad bin Abdul-Wahabi alikuwa akilingania watu Tauhidi ya Mwenyezi Mungu, lakini Tauhidi aliyokuwa akiilingania yeye ilikuwa isiyo na maana sahihi; kwa sababu ilitokana naye mwenyewe, wala siyo ile Tauhidi inayolinganiwa katika Qur'an.

Ikawa yule anayekubali Tauhidi yake husalimika nafsi yake na mali yake, ama anayekataa basi huambiwa kuwa ni kafiri anayeupiga vita Uislamu, na kumwaga damu yake na kuchukua mali yake inatangazwa kuwa ni halali. Wafuasi wa Muhammad Abdul-Wahab wakawa wanazusha vita katika Najdi na nje ya Najdi, kama vile Yemen, Hijaz na sehemu za Syria na Iraq. Na kila mji waliyouteka, walikuwa wakiruhusu kufanya katika mji huo mambo yoyote wayapendayo; kiasi kwamba kila walipoweza kuiunganisha miji hiyo kwenye utawala wao waliiunganisha, na kama hawakuweza basi walitosheka na uporaji wa mali peke yake.[18]

Vile vile Muhammad ibn Abdul-Wahab alimuamuru kila aliyehadaika na wito wake huo wa Tauhidi potofu afike kwake na kula kiapo cha utii (Bai'ah); na yeyote atakayekataa ni lazima auawe na mali yake igawiwe. Na kwa sababu hii, aliwashambulia watu wa kijiji cha Al-Fusul kilicho pembezoni mwa Al-Ahsa, akawaua watu mia tatu na akapora mali zao. [19] [19] Ulipofika mwaka 1206 A.H. Muhammad ibn Abdul-Wahab alifariki dunia lakini wafuasi wake waliendeleza uzushi wake na upotovu wake. Na ilipokuwa mwaka 1216 Wahabi Amir Suud aliandaa jeshi kubwa lipatalo watu elfu ishirini, wakafanya mashambulizi ya kinyama katika mji mtukufu wa Karbala nchini Iraq. Mji wa Karbala ni mji mtukufu tangu hapo zamani mpaka sasa, na unao umaarufu mkubwa na mapenzi kwa waumini, na watu haukusudia kwa ajili ya ziyara kutoka sehemu mbali mbali na mataifa tofauti tofauti wakiwemo Wairan, Waturuki, Waarabu na wengineo.

Majeshi hayo ya Kiwahabi, yaliuzingira mji huu mtukufu na kufanya mauaji mengi na kupora mali, kuubomoa na kufanya kila aina ya uovu. Kwa hakika Mawahabi kwa kuishambulia Karbala tukufu walitenda jinai kubwa na walileta msiba usio mfano, kwani waliwaua watu wapatao elfu tano au zaidi, mpaka yasemekana waliwauwa watu wapatao elfu ishirini. Baada ya Amir Suud kumaliza mashambulizi ya kivita dhidi ya wakazi wa mji wa Karbala, alielekea kwenye Haram Tukufu ya Imam Husein bin Ali[a.s] , ambayo ilikuwa imejaa hazina mbali mbali nzuri na zawadi nyingi za thamani zilizotolewa na wafalme mbali mbali na Maamiri pamoja na watu wengine kwenye uwanja mtukufu wa Kaburi Ia Imam Husein[a.s] nazo akazipora.

Baada ya msiba huu unaoumiza roho, mji wa Karbala ulionekana wazi kuwa umekumbwa na huzuni kubwa na masikitiko kutokana na unyama uliofanywa na Mawahabi. Hali hii iliwatawanya washairi wengi wa Kiislamu watunge Mashairi ya kuomboleza msiba ulioufika mji huu Mtukufu wa Karbala.[20] Siyo tu kwamba Mawahabi walitosheka na shambulio hilo la kwanza dhidi ya mji wa Karbala na viunga vyake, bali waliendelea kufanya mashambulizi mara kwa mara karibu muda wa miaka kumi na miwili. Pia Mawahabi walikuwa wakiushambulia mji Mtukufu wa Najaf na kufanya uporaji, na kama tulivyokwisha sema, shambulio la mwanzo dhidi ya Karbala lilikuwa mwaka 1216 A.H.

Waandishi wa Kishia wameafikiana kwamba, tukio hilo Ia mashambulizi dhidi ya mji wa Najaf lilifanyika siku ya kumbukumbu ya Ghadir ambayo Mtume[s.a.w.w] alimbainisha Imam Ali bin Abi Talib kuwa ndiyo Khalifa wake baada ya kuondoka kwake yeye Mtume[s.a.w.w] . Ili kuifahamu kumbukumbu ya Ghadir, rejea: Kitabu cha Al-Ghadir cha Al-Aminiy, Juz. 1. Anasema Marhum Al-Allamah As-Sayyid Jawad Al-'Amili kuhusu mauaji yaliyofanywa na Mawahabi huko Karbala na Najaf: "Hakika Mwenyezi Mungu kwa hisani yake na fadhila zake pia kwa baraka za Mtume Muhammad na kizazi chake amejalia kutimia kwa Juzuu hii ya kitabu, "Miftah Al-Karamah" "usiku wa manane kuamkia tarehe tisa ya mwezi Mtukufu wa Ramadhani mwaka 1225 A.H. kwa mkono wa mwandishi wake..... (kazi hii ya kuandika kitabu hiki nimeifanya kutokana na ushawishi wa kimawazo pia kutokana na hali ya mambo kuharibika". Anaendelea kusema:

"Kwa hakika mabedui wenye imani za Kiwahabi kutoka Unaizah, (ambao wamekwisha toka katika Uislamu) waliuzingira mji mtukufu wa Najaf na kaburi la Imam Husein[a.s] katika Karbala, wakazifunga njia zote kisha wakawapora watu waliokuwa wakitoka kumzuru Imam Husein[a.s] katika ziyara ya nusu ya mwezi wa Shaaban, wakawaua watu wengi, na wengi waliouawa walikuwa Waajemi. Yawezekana idadi ya watu waliouawa ilikuwa mia moja na hamsini na pengine chini ya idadi hiyo kama inavyosemekana."[21]

Kwa ujumla, Tauhidi aliyokuwa akiilingania Muhammad ibn Abdul-Wahabi na kundi lake ilikuwa ni ile isemayo kwamba "Mwenyezi Mungu ana mwili wenye viungo na anapo mahala pake maalum (na walikuwa wanahalalisha damu na mali za wenye kupinga kauli yao hiyo)". Bwana Al-Alusi anasema kuhusu Tauhidi ya Mawahabi: "Mawahabi wanaziamini hadithi zisemwazo kuwa zimetoka kwa Mtume[s.a.w.w] kwamba, Mwenyezi Mungu hushuka hadi kwenye mbingu ya dunia kisha hauliza, "Je, kuna yeyote mwenye kutaka msamaha?"[22] .

Al-Alusi anaendelea kusema: "Mawahabi wanaitakidi pia kwamba, Mwenyezi Mungu atakuja siku ya Qiyama kama alivyosema katika Qur'an "Waja'a Rabbuka Wal Malaku Saffan Saffa", na wanaammi kwamba Mwenyezi Mungu hujisogeza kwa viumbe vyake namna apendavyo kama alivyosema katika Qur'an: "Nasi tuko karibu mno na binadamu kuliko mshipa wa shingo yake".[23] Katika kitabu cha Ibn Taymiyyah kiitwacho "Ar-Radd AlalAkhnaiy", kana ushahidi ulio wazi kwamba, yeye Ibn Taymiyyah alikuwa akiitakidi hadithi zilizopokelewa kuhusu fadhila za kumzuru Mtume[s.a.w.w] kuwa ni za uzushi, na kwamba anyeitakidi kuwa mjumbe wa Mwenyezi Mungu yu hai baada ya kufariki kwake kwa uhai kama ule wa zama alipokuwa duniani, basi mtu huyo atakuwa katenda dhambi kubwa. Na hivi ndivyo anavyoitakidi Muhammad ibn Abdul-Wahabi na wafuasi wake; lakini hawa wamezidi mno kuliko Ibn Taimiyyah katika upotovu na kuvuruga. Itikadi hizo mbovu za Kiwahabi zimekuwa ni sababu ya kuwafanya watu wanaotafiti juu ya dini ya Kiislamu kwa kupitia vitabu vya Mawahabi, wauone Uislamu kuwa ni Dini isiyo ya maendeleo na wala haiwezi kutegemewa kukidhi mahitaji ya maisha ya watu katika nyakati zote.

Mmarekani mmoja aitwaye "Lutrub Studard" anasema: 'Walisimama katika misingi hiyo watu wengi wanaoukosoa Uislamu, wakayafanya Madh-hebu ya Uwahabi kuwa ni ushahidi wa maneno yao wakasema, 'Hakika Uislamu kwa asili yake na mazingira yake, haukubali mabadiliko kulingana na wakati, wala haukubali maendeleo na mabadiliko ya hali, na Uislamu hauwezi kuwa tumaini katika maisha".[24]

Inapasa kusemwa kwamba wanachuoni wa Madh-hebu ya Hanbal tangu hapo mwanzo walimpinga Muhammad ibn Abdul Wahab na kupitisha uamuzi kuwa yeye amepotea, na kwamba hizo itikadi zake siyo sahihi. Na mtu wa kwanza kumpinga Muhammad ibn Abdul-Wahabi na kutangaza vita dhidi yake, alikuwa ni baba yake, kisha ndugu yake aliyekuwa akiitwa Sheikh Suleiman, na wawili hawa walikuwa ni wanachuoni wa Kihanbal. Ama huyu Sheikh Suleiman yeye aliandika kitabu cha kuzipinga itikadi za Muhammad ibn Abdul-Wahabi kiitwacho "As-Sawaiqul-llahiyyah Fi Araddi Al-Wahabiyyah". Ndani ya kitabu hicho amezipinga itikadi potofu na uzushi wa nduguye. Mufti wa Kis-Shafi'i katika Makka, Ash-Shaykh Zaini Dahlan, anasema kama ifuatavyo:- "Mzazi wa Muhammad ibn Abdul-Wahab ambaye ni Sheikh Abdul-Wahab, alikuwa ni mtu mcha Mungu miongoni mwa wanachuoni, naye Sheikh Suleiman ambaye ni ndugu wa Muhammad ibn Abdul-Wahab vile vile alikuwa miongoni mwa wanachuoni. Kwa kuwa Sheikh Abdul-Wahab na Sheikh Suleiman, toka hapo mwanzo walikuwa wakizifahamu fikra potofu za Muhammad ibn Abdul-Wahab hasa pale alipokuwa akiendelea na masomo yake huko Madina, walikuwa wakimlaumu na kuwatahadharisha watu kutokana naye." [25] .

Naye Abbas Al-'Aqqad Al-Misri anasema: "Mpinzani mkubwa wa Muhammad ibn Abdul-Wahab ni nduguye aliyekuwa akiitwa Sheikh Suleiman, ambaye ndiye mwandishi wa kitabu kiitwacho "As-Sawaiqul Ilahiyya". Sheikh Suleiman hakukubaliana kuwa nduguye (Muhammad ibn Abdul-Wahab) eti alikuwa amefikia daraja ya ijtihadi na akaweza kuifahamu Qur'an na Sunna. Na kwa maoni ya Sheikh Suleiman ni kwamba, zile bid'ah ambazo maimamu walikuwa wakiziona karne baada ya karne na hawamkufurishi mwenye kuzitenda, basi sisi hatuna haki ya kumkufurisha mtu kwa sababu ya hizo bid'ah wala hatuwezi kuhalalisha vita dhidi ya watu wanaotenda matendo hayo.

Anasema tena Sheikh Suleiman: "Mambo haya yalikuwepo sika nyingi hata kabla ya Imam Ahmad ibn Hanbal katika zama za Maimamu wa Kiislamu, na wenye kuyapinga waliyapinga miongoni mwa maimamu hao, na yaliendelea kuwepo mpaka yakaenea katika miji yote ya Kiislamu. Na matendo yote haya ambayo ninyi Mawahabi mnawakufurisha watu kwa kuyatenda, haikupokewa kutoka kwa Maimamu wa Waislamu kwamba, wao walimkufurisha mtu kwa ajili hiyo, wala hawakusema eti watendao matendo haya wameritadi, na wala maimamu hao hawakuamuru kuwapiga vita watendao mambo haya, wala hawakuiita miii ya Waislamu kuwa ni miji ya shirki na vita kama msemavyo ninyi; bali ninyi mmezidi mno kiasi cha kumkufurisha hata mtu asiyewakufurisha watu watendao haya japokuwa yeye mwenyewe hakuyatenda".[26]

Ni wazi kabisa kwamba, Muhammad ibn Abdul-Wahab siyo mtu wa mwanzo kutoa hizo rai zake na fikra zake azitoazo, bali yule aliyemtangulia tangu karne nyingi zilizopita ambaye ni Ibn Taymiyyah al-Harrani pamoja na mwanafunzi wake aitwaye Ibnul-Qayyim Al-Jauziyyah, na wengineo kama hawa, fikra za wote hawa hazikuanzisha madhehebu kama alivyozusha jambo hilo mwana wa Abdul Wahab.