TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NANE Juzuu 8

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NANE0%

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NANE Mwandishi:
: HASANI MWALUPA
Kundi: tafsiri ya Qurani

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NANE

Mwandishi: Sheikh Muhammad Jawad Mughniyya
: HASANI MWALUPA
Kundi:

Matembeleo: 12065
Pakua: 2507


Maelezo zaidi:

Juzuu 1 Juzuu 2 Juzuu 3 Juzuu 4 Juzuu 5 Juzuu 6 Juzuu 7 Juzuu 8 Juzuu 12 Juzuu 13 Juzuu 14 Juzuu 15 Juzuu 16 Juzuu 17 Juzuu 18 Juzuu 19 Juzuu 20 Juzuu 21 Juzuu 22 Juzuu 23 Juzuu 24
Tafuta ndani ya kitabu
  • Anza
  • Iliyopita
  • 17 /
  • Inayofuata
  • Mwisho
  •  
  • Pakua HTML
  • Pakua Word
  • Pakua PDF
  • Matembeleo: 12065 / Pakua: 2507
Kiwango Kiwango Kiwango
TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NANE

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASIF JUZUU YA NANE Juzuu 8

Mwandishi:
Swahili

3

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA NANE

فَمَن يُرِدِ اللَّـهُ أَن يَهْدِيَهُ يَشْرَحْ صَدْرَهُ لِلْإِسْلَامِ ۖ وَمَن يُرِدْ أَن يُضِلَّهُ يَجْعَلْ صَدْرَهُ ضَيِّقًا حَرَجًا كَأَنَّمَا يَصَّعَّدُ فِي السَّمَاءِ ۚ كَذَٰلِكَ يَجْعَلُ اللَّـهُ الرِّجْسَ عَلَى الَّذِينَ لَا يُؤْمِنُونَ ﴿١٢٥﴾

125.Basi yule ambaye Mwenyezi Mungu anataka kumwongoza humfungulia kifua chake Uislam; na yule anayetaka apotee hufanya kifua chake kina dhiki kimebana, Kama kwamba anapanda mbinguni. Namna hii anajaalia Mwenyezi Mungu adhabu juu ya wale wasioamini.

وَهَـٰذَا صِرَاطُ رَبِّكَ مُسْتَقِيمًا ۗ قَدْ فَصَّلْنَا الْآيَاتِ لِقَوْمٍ يَذَّكَّرُونَ ﴿١٢٦﴾

126.Na huu (Uislamu) ndio njia ya Mola wako iliyonyooka. Hakika tumezipambanua ishara kwa watu wenye kukumbuka.

لَهُمْ دَارُ السَّلَامِ عِندَ رَبِّهِمْ ۖ وَهُوَ وَلِيُّهُم بِمَا كَانُوا يَعْمَلُونَ ﴿١٢٧﴾

127.Watapata nyumba ya salama kwa Mola wao naye ndiye walii wao, kwa sababu ya yale waliyokuwa wakiyatenda.

HUMFUNGULIA KIFUA CHAKE UISLAM

Aya 125 – 127

MAANA

Basi yule ambaye Mwenyezi Mungu anataka kumwongoza humfungulia kifua chake Uislam; na yule anayetaka apotee hufanya kifua chake kinadhiki kimebana.

Anasema Razi: “Wameshikilia masahibu zetu -yaani Sunni Ashaira - Aya hii katika kubainisha kuwa upotevu na uongofu unatoka kwa Mwenyezi Mungu.” Ama masahibu zetu sisi- Shia - wanasema lau ingelikuwa upotevu na uongofu unatoka kwa Mwenyezi Mungu, basi kusingelikuwa na taklifu zozote na ingebatilika hisabu na malipo. Kwa sababu yeye Mwenyezi Mungu Mtukufu ni mwadilifu, hawezi kufanya jambo na kisha amhisabu mwingine kwalo. Itakuwaje hivyo na hali yeye ndiye aliyesema:

﴿ وَلَا تَزِرُ وَازِرَةٌ وِزْرَ أُخْرَىٰ﴾

“Wala mbebaji hatabeba mzigo wa mwingine” (6:164)

Ama Aya hii tuliyonayo haifahamishi madai ya Razi na masahibu zake; wa haikuja kubainisha chimbuko la upotevu na uongofu, au kwamba unatoka kwa Mwenyezi Mungu au mwinginewe; isipokuwa imekuja kubainisha kuwa watu ni makundi mawili:

Kundi la kwanza, ni wale ambao vifua vyao vitakunjukia haki, wataitumia na kuitegemea, kwa sababu ya mwamko wao, kujiepusha kwao na malengo ya kiutu na kujikomboa na kuiga na hawaa. Hao ndio wanaokusudiwa na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿ الَّذِينَ يَسْتَمِعُونَ الْقَوْلَ فَيَتَّبِعُونَ أَحْسَنَهُ أُولَـٰئِكَ الَّذِينَ هَدَاهُمُ اللَّـهُ وَأُولَـٰئِكَ هُمْ أُولُو الْأَلْبَابِ﴾

“Ambao husikia maneno wakafuata yaliyo mazuri yao, Hao ndio aliowaongowa Mwenyezi Mungu na hao ndio wenye akili” (39: 18)

Alipojua Mwenyezi Mungu (s.w.t) kheri kutoka katika kundi hili aliwazidishia uongofu na akawasaidia kwa tawfiki yake, akasema:

﴿ وَيَزِيدُ اللَّـهُ الَّذِينَ اهْتَدَوْا هُدًى﴾

“Na Mwenyezi Mungu huwazidishia uowongofu wale walioongoka…” (19:76).

Akasema tena:

﴿ وَالَّذِينَ اهْتَدَوْا زَادَهُمْ هُدًى وَآتَاهُمْ تَقْوَاهُمْ﴾

“Na wale wanaofuata uongofu anawazidishia uongofu na huwapa takua yao.” (47:17).

Vilevile mwalimu humshughulikia na kumshujaisha mwanafunzi wake atakapojua kuwa ni mwerevu na mchangamfu.

Kundi la pili: Ni wale ambao vifua vyao haviikunjukii haki kwa ujinga wao na kuwa finyu fikra zao, au kwa kuwa haki inapingana na manufaa yao na faida zao au desturi zao na takilidi zao. Hawa ndio waliokusudiwa na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

﴿ فَوَيْلٌ لِّلْقَاسِيَةِ قُلُوبُهُم مِّن ذِكْرِ اللَّـهِ﴾

“Basi ole wao wale wenye nyoyo ngumu kumkumbuka Mwenyezi Mungu …” (39:22)

Na kauli yake:

﴿ مَا يَأْتِيهِم مِّن ذِكْرٍ مِّن رَّبِّهِم مُّحْدَثٍ إِلَّا اسْتَمَعُوهُ وَهُمْ يَلْعَبُونَ﴾

“Hayawafikii mawaidha mapya kutoka kwa Mola wao ila huyasikiza, na hali wanafanya mchezo” (21:2)

Na pia kauli yake:

﴿ وَلَوْ عَلِمَ اللَّـهُ فِيهِمْ خَيْرًا لَّأَسْمَعَهُمْ وَلَوْ أَسْمَعَهُمْ لَتَوَلَّوا وَّهُم مُّعْرِضُونَ﴾

“Na Mwenyezi Mungu angelijaalia wema wowote kwao angeliwasikilizisha, na lau angeliwasikilizisha wangelikengeuka wakapuuza” (8:23)

Kwa hiyo Mwenyezi Mungu (s.w.t) anaachana na mja na kumwacha ajitegemee mwenyewe, ikiwa haoni kheri yoyote kwake; kama ambavyo mwalimu anampuuza mwanafunzi wake baada ya kukata tamaa na kufaulu kwake. Angalia Juz.5 (4:88).

Kama kwamba anapanda mbinguni.

Zamani watu walikuwa wakipigia mfano wa mtu aliyelemewa kwa kupanda mbinguni, ambapo hakuna wasila wa kufika huko kwa hali yoyote. Mfananisho katika Aya unaafikiana na wakati ilipoteremka. Makusudio yake ni kwamba kundi la watu, ambalo ni kundi la pili tulilolielezea, linapata dhiki na uzito wakikalifishwa kufuata haki, sawa na kuamrishwa kupanda mbinguni.

Namna hii anajaalia Mwenyezi Mungu adhabu juu ya wale wasioamini.

Neno Rijsi hapa lina maana ya adhabu. Maana ni kuwa wale wanaoona dhiki na tabu kufuata haki katika dunia, vilevile kesho wataingia katika adhabu ambayo ni kali na kubwa kuliko kufuata haki.

﴿ وَقَالُوا لَا تَنفِرُوا فِي الْحَرِّ قُلْ نَارُ جَهَنَّمَ أَشَدُّ حَرًّا﴾

“…. Wakasema msiende katika joto hili. Sema: Moto wa Jahanamu una joto zaidi …” (9:81)

Na huu (Uislamu) ndio njia ya Mola wako iliyonyooka.

Huu, ni ishara ya Uislam ambao hukunjua nyoyo za wale wanaosikiliza kauli wakafuata mazuri yake. Na Uislamu ndio njia isiyo kombo.

Hakika tumezipambanua ishara kwa watu wenye kukumbuka.

Yaani, tumesimamisha dalili na hoja zilizo wazi zenye kutosheleza, juu ya kuswihi Uislamu na ukweli wake katika Qur’an na Aya zake. Kwa hoja hizo watanufaika wale ambao wanajua dalili za haki na kuzitumia.

Watapata nyumba ya salama kwa Mola wao.

Watakaokaa katika nyumba hii ya Mwenyezi Mungu hawatapatwa na uovu wowote wala hawatahuzunika, kwa sababu Mwenyezi Mungu ndiye anayewatunza naye ndiye walii wao kwa sababu ya yale waliyokuwa wakiyatenda miongoni mwa mambo ya kheri na twaa.

وَيَوْمَ يَحْشُرُهُمْ جَمِيعًا يَا مَعْشَرَ الْجِنِّ قَدِ اسْتَكْثَرْتُم مِّنَ الْإِنسِ ۖ وَقَالَ أَوْلِيَاؤُهُم مِّنَ الْإِنسِ رَبَّنَا اسْتَمْتَعَ بَعْضُنَا بِبَعْضٍ وَبَلَغْنَا أَجَلَنَا الَّذِي أَجَّلْتَ لَنَا ۚ قَالَ النَّارُ مَثْوَاكُمْ خَالِدِينَ فِيهَا إِلَّا مَا شَاءَ اللَّـهُ ۗ إِنَّ رَبَّكَ حَكِيمٌ عَلِيمٌ ﴿١٢٨﴾

128.Na siku atakapowakusanya wote, (awaambie): Enyi makundi ya majini! Hakika nyinyi mmechukua wafuasi wengi katika watu, Na marafiki wao katika watu waseme: Mola wetu tulinufaishana sisi na wao, na tumefikia muda wetu uliotuwekea. Atasema: Moto ndio makazi yenu, mtadumu humo, ila apende Mwenyezi Mungu, Hakika Mola wako ndiye mwenye hekima, Mjuzi.

وَكَذَٰلِكَ نُوَلِّي بَعْضَ الظَّالِمِينَ بَعْضًا بِمَا كَانُوا يَكْسِبُونَ ﴿١٢٩﴾

129.Na kama hivi tunawatia mapenzi baadhi, wao kwa wao, kwa sababu ya yale waliyokuwa wakiyachuma.

يَا مَعْشَرَ الْجِنِّ وَالْإِنسِ أَلَمْ يَأْتِكُمْ رُسُلٌ مِّنكُمْ يَقُصُّونَ عَلَيْكُمْ آيَاتِي وَيُنذِرُونَكُمْ لِقَاءَ يَوْمِكُمْ هَـٰذَا ۚ قَالُوا شَهِدْنَا عَلَىٰ أَنفُسِنَا ۖ وَغَرَّتْهُمُ الْحَيَاةُ الدُّنْيَا وَشَهِدُوا عَلَىٰ أَنفُسِهِمْ أَنَّهُمْ كَانُوا كَافِرِينَ ﴿١٣٠﴾

130.Enyi makundi ya majini na watu! Je, hawakuwafikia Mitume miongoni mwenu kuwasomea Aya zangu na kuwaonya kukutana na siku yenu hii? Watasema: Tumeshuhudia juu ya nafsi zetu, Na yaliwadanganya maisha ya dunia, Nao watajishuhudia wenyewe kwamba wao walikuwa Makafiri.

ذَٰلِكَ أَن لَّمْ يَكُن رَّبُّكَ مُهْلِكَ الْقُرَىٰ بِظُلْمٍ وَأَهْلُهَا غَافِلُونَ ﴿١٣١﴾

131.Hayo ni kwa sababu ya kuwa Mola wako hakuwa ni mwenye kuiangamiza miji kwa dhulma na hali wenyewe wameghafilika.

وَلِكُلٍّ دَرَجَاتٌ مِّمَّا عَمِلُوا ۚ وَمَا رَبُّكَ بِغَافِلٍ عَمَّا يَعْمَلُونَ ﴿١٣٢﴾

132.Na wote wana daraja mbali mbali kutokana na yale waliyoyatenda. Na Mola wako si mwenye kughafilika na yale wanayoyatenda.

SIKU ATAKAPOWAKUSANYA WOTE

Aya 128 – 132

MAANA

Na siku atakapowakusanya wote, yaani majini na watu, na awaambie:Enyi makundi ya majini! Hakika nyinyi mmechukua wafuasi wengi katika watu. Yaani kuwapoteza na kuwahadaa.

Na marafiki wao katika watu waseme; yaani wanadamu ambao wamemtawalisha shetani na kumtii, watasema kumwambia Mwenyezi Mungu:Mola wetu! Tulinufaishana sisi na wao . Yaani walinufaisha watu na watu wao wakawanufaisha majini. Razi amebainisha wajihi wa kunufaishana huko kwa kusema: “Watu walikuwa wakiwatii majini, kwa hiyo majini wakawa kama viongozi, Huku ndiko kunufaika majini. Ama kunufaika watu, ni kuwa majini walikuwa wakiwafahamisha watu aina za matamanio na kuwafanyia sahali”

Na tumefikia muda wetu uliotuwekea.

Bado maneno yanaendelea ya watu waliowatii majini, Maana ni kuwa kunufaishana kwetu sisi kwa sisi kulikuwa kwa muda maalum na wakati uliopangwa – nao ni siku ile tulipouacha uhai wa dunia, Sasa tuko mbele yako tukikiri dhambi zetu, basi tuhukumu unavyotaka.

Atasema: Moto ndio makazi yenu, mtadumu humo, ila apende Mwenyezi Mungu.

Hii ndiyo hukumu ya sawa na malipo yenye kulingana.

Hakika Mola wako ndiye mwenye hekima, Mjuzi.

Hupitisha hukumu yake kwenye misingi ya hekima na ujuzi.

Na kama hivi tunawatia mapenzi baadhi wao kwa wao, kwa sababu ya yale waliyokuwa wakiyachuma.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) alipotaja katika Aya iliyotangulia (127) kuwa Yeye ndiye walii wa waumini, hapa anataja kuwa makafiri katika majini na watu baadhi yao ni marafiki wa wengine kwa sababu wao wanashirikiana katika kufuru na dhuluma, na siku ya Kiyama watakuwa washirika katika adhabu vilevile.

Enyi makundi ya majini na watu! Je, hawakuwafikia Mitume mion- goni mwenu kuwasomea Aya zangu na kuwaonya kukutana na siku yenu hii?

Swali hili : atalielekeza kesho Mwenyezi Mungu (s.w.t) kwa waovu katika majini na watu; nalo ni kulaumu na kukemea; sio kuwa Mwenyezi Mungu anataka kujua. Kwa sababu Mwenyezi Mungu anajua na wao wanajua kuwa Mwenyezi Mungu amewatumia Mitume watoaji bishara na waonyaji.

﴿ وَإِن مِّنْ أُمَّةٍ إِلَّا خَلَا فِيهَا نَذِيرٌ﴾

“Na hakuna umma wowote ila alipita humo muonyaji” (35:24)

Watasema: Tumeshuhudia juu ya nafsi zetu.

Kwa vile hakuna nafasi ya kukanusha hapa, Na mahali pengine aliwapa nafasi wakakadhibisha, Wakasema: “Wallahi, Mola wetu! Hatukuwa washirikina” kama ilivyoelezwa katika Aya 23 ya Sura hii.

Na yaliwadanganya maisha ya dunia.

Kwa sababu dunia haikuficha chochote katika mawaidha yake na mageuzi yake.

Nao watajishuhudia wenyewe kwamba wao walikuwa makafiri.

Kwanza Mwenyezi Mungu (s.w.t) ametaja kuwa wao watasema: Tumeshuhudia juu ya nafsi zetu, kisha akafuatishia kwa kusema kuwa wao watajishuhudia wenyewe.

Makusudio ya msisitizo huu ni makaripio ya ukafiri na maasia. Kwa sababu mwenye kujaribu kufanya dhambi akiwa na yakini kwamba yeye atalazimika kukiri, basi ataacha, ikiwa ana akili.

Hayo ni kwa sababu ya kuwa Mola wako hakuwa ni mwenye kuiangamiza miji kwa dhulma na hali wenyewe wameghafilika.

Hayo, ni hayo ya kupeleka Mitume. Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu ni mwadilifu, hamdhulumu yeyote wala hamwadhibu ila baada ya kutuma Mitume watakaoamrisha mema na kukataza maovu. Kama mja hakuamri- ka na akakoma, basi ataambiwa na Mtume yatakayompata ikiwa hatatubu na kuacha. Akiendelea ataadhibiwa na Mwenyezi Mungu yale anayostahiki.

Na wote wana daraja mbalimbali kutokana na yale waliyoyatenda.

Waovu wana daraja kulingana na dhara zao, kunyonya jasho la wananchi na kutupa mabomu ya Atomic kwa maelfu ya watu. Na wema nao wana daraja kulingana na matendo yao, kuanzia mamkuzi mpaka kufa shahid katika njia ya haki na maslahi ya umma.

Na Mola wako si mwenye kughafilika na yale wanayoyatenda.

Kila kitu kimesajiliwa, kiwe kikubwa au kidogo, kizuri au kibaya. Si vibaya kurudia yale tuliyoyaeleza mara kwa mara, kwamba sisi tunaamini kiujumla kuweko majini, kwa sababu wahyi umethibtisha hilo na akili hailikanushi; sawa na kuhusu Malaika. Ama kuhusu ufafanuzi wao bado uko kwa Mwenyezi Mungu Mjuzi wa ghaibu.

4

TAFSIRI YA QURANI AL-KAASHIF JUZUU YA NANE

وَرَبُّكَ الْغَنِيُّ ذُو الرَّحْمَةِ ۚ إِن يَشَأْ يُذْهِبْكُمْ وَيَسْتَخْلِفْ مِن بَعْدِكُم مَّا يَشَاءُ كَمَا أَنشَأَكُم مِّن ذُرِّيَّةِ قَوْمٍ آخَرِينَ ﴿١٣٣﴾

133.Na Mola wako ndiye Mkwasi, mwenye rehema, Akipenda atawaaondoa, na kuweka wengine awapendao baada yenu. Kama alivyowaanzisha kutokana na uzao wa watu wengine.

إِنَّ مَا تُوعَدُونَ لَآتٍ ۖ وَمَا أَنتُم بِمُعْجِزِينَ ﴿١٣٤﴾

134.Hakika mnayoahidiwa yatafika tu. Wala hamtaweza (kuepuka)

قُلْ يَا قَوْمِ اعْمَلُوا عَلَىٰ مَكَانَتِكُمْ إِنِّي عَامِلٌ ۖ فَسَوْفَ تَعْلَمُونَ مَن تَكُونُ لَهُ عَاقِبَةُ الدَّارِ ۗ إِنَّهُ لَا يُفْلِحُ الظَّالِمُونَ ﴿١٣٥﴾

135.Sema: Enyi watu wangu! Fanyeni vile muwezavyo; na mimi nafanya. Mtakujajua ni nani atakuwa na makazi mema mwishoni, Hakika madhalimu hawafaulu.

NA MOLA WAKO NDIYE MKWASI

Aya 133 – 135

MAANA

Na Mola wako ndiye mkwasi, mwenye rehema.

Baada ya Mwenyezi Mungu kutaja kwamba atawahisabu watu kulingana na matendo yao. Ameashiria kuwa yeye ni mkwasi (mwenye kujitosheleza), hawahitajii viumbe.

Haimnufaishi twaa ya mwenye kumtii, wala hayamdhuru maasi ya mwenye kuasi; na kwamba ulimwengu wote una haja ya rehema yake; Kwa sababu, yeye ndiye sababu ya kwanza ya kupatikana huo ulimwengu.

Akipenda atawaaondoa kwa sababu ni Mkwasi, hawahitajii,na kuweka wengine awapendao baada yenu awabadili wengine wawe watiifu zaidi kuliko nyinyi. Lakini amewaacha na kuwapa muda kutokana na fadhila na ukarimu kutoka kwake.

Kama alivyowaanzisha kutokana na uzao wa watu wengine.

Yaani kama ambavyo imekuwa wepesi kwake kuwaleta nyinyi kutokana na kizazi kilichopita, vilevile ni wepesi kwake kuleta kizazi kipya kutokana na nyinyi na wengineo.

Makusudio ya Aya hii ni kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu anawaonya makafiri, wenye inadi, na maangamivu, kama ilivyokuwa kwa kaumu ya Nuh(a.s) , A’d na Thamud.

Hakika mnayoahidiwa yatafika tu.

Baada ya Mwenyezi Mungu kuwahofisha na adhabu ya dunia, sasa anawahofisha na Kiyama na adhabu yake; kwamba Kiyama kitakuja bila ya shaka yoyote, wala hapana pa kukikimbia ila kwake yeye tu, peke yake.

Sema: Enyi watu wangu! Fanyeni vile muwezavyo; na mimi nafanya. Mtakujajua ni nani atakuwa na makazi mema mwishoni.

Baada ya Mtume(s.a.w.w) kuwalingania kwenye Uislamu waarabu wa ujahiliya na wakaitikia mwito wake walioitikia na kupinga waliopinga, Mwenyezi Mungu Mtukufu alimwamrisha kuwaambia wenye inadi: Kuweni kama mlivyo na mimi ninafanya kulingana na uongozi wa Mola wangu.

Baada ya muda mtajua mwisho mwema utakuwa wa nani; sawa na kumwambia yule anayepinga nasaha zako: Haya endelea tu utaona!

Hakika madhalimu hawafaulu.

Wale wanaojidhulumu wenyewe au wengineo kwa uadui. Lau angefaulu dhalimu, basi mwadilifu angelikuwa na hali mbaya kuliko dhalimu. Na maneno ya msimamo wa usawa yangelikuwa ni misamiati ya unafiki na ria.

وَجَعَلُوا لِلَّـهِ مِمَّا ذَرَأَ مِنَ الْحَرْثِ وَالْأَنْعَامِ نَصِيبًا فَقَالُوا هَـٰذَا لِلَّـهِ بِزَعْمِهِمْ وَهَـٰذَا لِشُرَكَائِنَا ۖ فَمَا كَانَ لِشُرَكَائِهِمْ فَلَا يَصِلُ إِلَى اللَّـهِ ۖ وَمَا كَانَ لِلَّـهِ فَهُوَ يَصِلُ إِلَىٰ شُرَكَائِهِمْ ۗ سَاءَ مَا يَحْكُمُونَ ﴿١٣٦﴾

136.Na wamemfanyia sehemu Mwenyezi Mungu katika mimea aliyoiumba na katika wanyama na kusema: hii ni ya Mwenyezi Mungu, kwa madai yao, na hii ni ya wale tunaowashirikisha. Basi vile walivyokusudia wale wanaowashirikisha, havifiki kwa Mwenyezi Mungu, na vilivyokuwa vya Mwenyezi Mungu huwafikia wanaowashirikisha, Ni mabaya kabisa wanayoyahukumu.

وَكَذَٰلِكَ زَيَّنَ لِكَثِيرٍ مِّنَ الْمُشْرِكِينَ قَتْلَ أَوْلَادِهِمْ شُرَكَاؤُهُمْ لِيُرْدُوهُمْ وَلِيَلْبِسُوا عَلَيْهِمْ دِينَهُمْ ۖ وَلَوْ شَاءَ اللَّـهُ مَا فَعَلُوهُ ۖ فَذَرْهُمْ وَمَا يَفْتَرُونَ ﴿١٣٧﴾

137.Namna hivi wanaowashrik- isha wamewapambia wengi katika makafiri kuwaua watoto wao. Ili kuwaangamiza na kuwavu- rugia dini yao. Na kama Mwenyezi Mungu angependa wasingalifanya hayo. Basi waache na haya wanayoyazua.

وَقَالُوا هَـٰذِهِ أَنْعَامٌ وَحَرْثٌ حِجْرٌ لَّا يَطْعَمُهَا إِلَّا مَن نَّشَاءُ بِزَعْمِهِمْ وَأَنْعَامٌ حُرِّمَتْ ظُهُورُهَا وَأَنْعَامٌ لَّا يَذْكُرُونَ اسْمَ اللَّـهِ عَلَيْهَا افْتِرَاءً عَلَيْهِ ۚ سَيَجْزِيهِم بِمَا كَانُوا يَفْتَرُونَ ﴿١٣٨﴾

138.Na husema: Wanyama hawa na mimea hii ni mwiko, hawatokula ila wale tuwapendao - kwa madai yao (tu). Na wanyama wengine imeharamishwa migongo yao, Na wanyama wengine hawalitaji jina la Mwenyezi Mungu juu yao. Wanamzulia tu. Atawapa kwa hayo wanayomzulia.

وَقَالُوا مَا فِي بُطُونِ هَـٰذِهِ الْأَنْعَامِ خَالِصَةٌ لِّذُكُورِنَا وَمُحَرَّمٌ عَلَىٰ أَزْوَاجِنَا ۖ وَإِن يَكُن مَّيْتَةً فَهُمْ فِيهِ شُرَكَاءُ ۚ سَيَجْزِيهِمْ وَصْفَهُمْ ۚ إِنَّهُ حَكِيمٌ عَلِيمٌ ﴿١٣٩﴾

139.Na husema: waliomo matumboni mwa wanyama hawa ni kwa ajili ya wanaume wetu tu, na wameharamishwa kwa wake zetu. Lakini ikiwa ni nyamafu hushirikiana. Atawalipa kwa maelezo yao. Hakika Yeye ni mwenye hekima, Mjuzi

قَدْ خَسِرَ الَّذِينَ قَتَلُوا أَوْلَادَهُمْ سَفَهًا بِغَيْرِ عِلْمٍ وَحَرَّمُوا مَا رَزَقَهُمُ اللَّـهُ افْتِرَاءً عَلَى اللَّـهِ ۚ قَدْ ضَلُّوا وَمَا كَانُوا مُهْتَدِينَ ﴿١٤٠﴾

140.Hakika wamehasirika wale waliowaua watoto wao kwa upumbavu bila ya elimu, Na wakaharamisha alivyowaruzuku Mwenyezi Mungu Kwa kumzulia Mwenyezi Mungu, Hakika wamepotea wala hawakuwa wenye kuongoka.

HUSEMA: HII NI SEHEMU YA MWENYEZI MUNGU

Aya 136 – 140

MAANA

Na wamemfanyia sehemu Mwenyezi Mungu katika mimea aliyoiumba na katika wanyama na kusema: hii ni ya Mwenyezi Mungu, kwa madai yao, na hii ni ya wale tunaowashirikisha. Basi vile walivyokusudia wale wanaowashirikisha, havifiki kwa Mwenyezi Mungu, na vilivyokuwa vya Mwenyezi Mungu huwafikia wanaowashirikisha, Ni mabaya kabisa wanayoyahukumu.

Dhamiri katika ‘wamemfanyia’ inawarudia washirikina wa kiarabu.

Maana ni kuwa Mwenyezi Mungu (s.w.t) baada ya kubatilisha itikadi ya washirikina, katika Aya zilizotangulia, kwa mantiki ya kiakili na kimaumbile, katika Aya hizi anaonyesha baadhi ya vile ambavyo washirikina walikuwa wakivitenga katika mali zao na watoto wao.

Aya hii tuliyonayo inaonyesha hali zao katika utajiri wao wa mali ambao ni kilimo na mifugo. Walikuwa, kama inavyoelezwa katika vitabu vya tafsiri, wakitenga sehemu katika mimea yao na mifugo kwa ajili ya Mungu na kuitoa kwa watoto na maskini. Na hutenga sehemu kwa ajili ya masana- mu yao, na kuitoa kwa watunzaji na walinzi wa masanamu.

Walikuwa wakijitahidi kuzidisha fungu la masanamu, kuliko la Mwenyezi Mungu, ili litosheleze. Kwa sababu Mwenyezi Mungu ni tajiri na masanamu ni mafakiri. Ikiwa kitu walichokifanya ni cha Mwenyezi Mungu kinachanganyika na kile walichokifanya cha masanamu, basi hukiachia masanamu. Na ikiwa kile walichokifanya ni cha masanamu kinachanganyika na kile walichokifanya ni cha Mwenyezi Mungu, hukirudisha kwa masanamu. Vilevile wakikumbwa na ukame walikuwa wakila fungu la Mwenyezi Mungu na kuacha fungu la masanamu.

Huu ni ufafanuzi wazi wa“Ni mabaya kabisa wanayoyahukumu” katika kuyatanguliza masanamu yao kuliko Mwenyezi Mungu Mtukufu.

Namna hivi wanaowashirikisha wamewapambia wengi katika makafiri kuwaua watoto wao.

Yametangulia maelezo kuwa maana ya wanaowashirikisha katika Aya iliyopita kuwa ni masanamu. Ama katika Aya hii inakusudia makuhani na walinzi wa masanamu kulingana na hali ilivyo. Kwa sababu masanamu hayatambui wala hayasemi, basi yatawezeje kuwapambia na kuwahadaa. Maana ni kuwa washirikina kama waliyopiga mafungu mali zao kwa Mwenyezi Mungu na masanamu, vilevile makuhani na watunzaji wamewapambia kuwaua watoto wao.

Unaweza kuuliza : Matumizi ya washirikina katika mali zao na watoto wao, kwa namna iliyotangulia, yalikuwa ni kwa kutokana na desturi ya wakati wa ujahiliya. Inajulikana kuwa desturi huwekwa na watu. Mmoja wao alikuwa anaweza kuua mwanawe kwa kuogopa ufukara, au akimzika binti yake kwa kuogopa aibu; kama ilivyonasibishwa kwa Qais bin Asim aliyeigwa kwa ujinga. Sasa kuna wajihi gani katika kulinasibisha hilo kwa masanamu au wanaosimamia masanamu?

Jibu : Ni kweli kuwa matumizi ya washirikina yalitokana na desturi, lakini Makuhani na viongozi wao walipendekeza na kuipamba desturi hii, nao ndio wasemaji rasmi wa masanamu, kwa hiyo ikafaa kunasibishwa kwenye masanamu.

Ili kuwaangamiza na kuwavurugia dini yao.

Yaani Makuhani waliwapambia washirikina amali zao, ikawa natija ya kupambia huku ni kuangamia washirikina na kupotea kwao na haki na dini iliyonyooka.

Na kama Mwenyezi Mungu angependa wasingalifanya hayo.

Yaani kama Mwenyezi Mungu angelitaka kuwazuia hilo kwa nguvu wasingelifanya ubaya huo kwa mali zao na watoto wao, lakini amewaacha kama walivoyo baada ya kuwabainishia njia ya kheri na shari.

Basi waache na haya wanayoyazua ya kutegemeza kwa Mwenyezi Mungu yale wanayoyahalalisha na kuyaharamisha.

Amri ya kuwaacha na uzushi wao, imekuja kwa kuwakemea na kuwapa kiaga washirikina na sio kwa njia yake na uhakika wake; kama vile ilivyo amri katika kauli yake Mwenyezi Mungu:

﴿ اعْمَلُوا مَا شِئْتُمْ إِنَّهُ بِمَا تَعْمَلُونَ بَصِيرٌ﴾

“Fanyeni mpendavyo, hakika yeye anayaona myafanyayo.” (41:40)

Baada ya hapo Mwenyezi Mungu anataja katika Aya inayofuatia kwamba washirikina waligawanya mavuno yao na mifugo yao mafungu matatu:

1. Fungu la kwanza:Na husema: Wanyama hawa na mimea hii ni mwiko, hawatokula ila wale tuwapendao - kwa madai yao (tu) . Yaani washirikina walikuwa wakigawa sehemu ya mazao na mifugo na kukataza kutumiwa ila kwa wanaowachagua. Mwenyezi Mungu (s.w.t.) hakubainisha hao waliochaguliwa na washirikina. Lakini baadhi ya wafasiri wamesema, ni makuhani na watumishi wa masanamu. Wengine wakasema ni wanaume tu, sio wanawake.

2. Fungu la pili:Na wanyama wengine imeharamishwa migongo yao, hawapandwi wala kubebeshwa mizigo. Rejea maelezo katika Juz.7 (5:103).

3. Fungu la tatu:Na wanyama wengine hawalitaji jina la Mwenyezi Mungu juu yao wakati wa kuchinja, bali wanataja majina ya waungu wao.

Umetangulia ufafanuzi katika kusafiri Sura hii, Aya ya 121, kuwa wao wamemnasibishia Mwenyezi Mungu kugawanya huku kwa uwongo na uzushi na Mwenyezi Mungu atawaadhibu.

Na husema: waliomo matumboni mwa wanyama hawa ni kwa ajili ya wanaume wetu tu, na wameharamishwa kwa wake zetu. Lakini ikiwa ni nyamafu hushirikiana. Atawalipa kwa maelezo yao. Hakika yeye ni mwenye hekima, Mjuzi.

Razi amesema: “Hii ni aina ya nne katika mambo yao maovu. Walikuwa wakisema katika mimba za Bahira na Saiba: “atakayezaliwa hai basi atahusu wanaume tu, hawali wanawake, na atakayezaliwa maiti basi watashirkiana kumla wanaume na wanawake.”Watalipwa maelezo yao.

Na makusudio ya kiaga cha kuwa.Hakika yeye ni mwenye hekima, Mjuzi, ni makemeo yawe kwenye hekima na kwa mujibu wa inavyostahiki.”

Hakika wamehasirika wale waliowaua watoto wao kwa upumbavu bila ya elimu.

Kuna upumbavu gani zaidi ya mzazi kumchinja mwanawe kwa mkono wake au kumzika mzima. Kauli yake Mwenyezi Mungu bila ya elimu ni kusisitiza upumbavu wao. Ama hasara yao katika dunia ni kule kuua watoto wao na ufisadi wa maisha yao ya kijamii. Na hasara yao katika akhera ndiyo nzito na chungu.

Na wakaharamisha alivyowaruzuku Mwenyezi Mungu katika wanyama na mazao ambayo wamedai kuwa ni mwiko.

Kwa kumzulia Mwenyezi Mungu .

Kwa sababu kuharamisha kunatokana na wao na wala sio kutoka kwake Mwenyezi Mungu.

Hakika wamepotea wala hawakuwa wenye kuongoka kwenye kheri yoyote na uwongofu.

Razi anasema: “Mwenyezi Mungu ametaja mambo saba na kila moja kati hayo ni sababu tosha ya kupatikana shutuma. Nayo ni: Kupata hasara, upumbavu, ujinga, kuharamisha aliyoyahalalisha Mwenyezi Mungu, kumzulia Mungu, upotevu na kuacha kuongoka.”

Kisha akaendelea kusema Razi: “Imethibiti kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu amewashutumu wanaowaua watoto na kuharamisha aliyohalalisha Mwenyezi Mungu Mtukufu, kwa sifa hizi saba zenye kuwajibisha aina kubwa na ya mwisho ya shutuma, na huo ni ufasaha wa hali ya juu.”

Nasi tunamwambia Razi: Ikiwa Mwenyezi Mungu amewashutumu kwa upotevu kuwa ndiyo aina kubwa na ya mwisho ya shutuma, sasa vipi wewe unadai kuwa Mwenyezi Mungu ndiye aliyewapoteza? Ni mantiki gani yanayosema kuwa inafaa asiye na hatia kuadhibiwa na kushutumiwa kwa kitendo ambacho amekifanya yule anayeshutumu na kuadhibu?

Hayo Razi ameyasema mara kadhaa katika tafsir yake Al-Kabir, miongoni mwayo ni yale aliyoyasema karibuni katika kufasiri Aya 125 ya Sura hii.

وَهُوَ الَّذِي أَنشَأَ جَنَّاتٍ مَّعْرُوشَاتٍ وَغَيْرَ مَعْرُوشَاتٍ وَالنَّخْلَ وَالزَّرْعَ مُخْتَلِفًا أُكُلُهُ وَالزَّيْتُونَ وَالرُّمَّانَ مُتَشَابِهًا وَغَيْرَ مُتَشَابِهٍ ۚ كُلُوا مِن ثَمَرِهِ إِذَا أَثْمَرَ وَآتُوا حَقَّهُ يَوْمَ حَصَادِهِ ۖ وَلَا تُسْرِفُوا ۚ إِنَّهُ لَا يُحِبُّ الْمُسْرِفِينَ ﴿١٤١﴾

141.Naye ndiye aliyeumba bustani zenye kutambaa na zisizotambaa na mitende na mimea yenye kutofautiana uliwaji wake. Na mizaituni na mikomamanga. Inayofanana na isiyofanana, Kuleni matunda yake inapozaa, Na toeni haki yake siku ya kuvunwa kwake, Wala msifanye ufujaji, hakika Yeye hawapendi wafujaji.

وَمِنَ الْأَنْعَامِ حَمُولَةً وَفَرْشًا ۚ كُلُوا مِمَّا رَزَقَكُمُ اللَّـهُ وَلَا تَتَّبِعُوا خُطُوَاتِ الشَّيْطَانِ ۚ إِنَّهُ لَكُمْ عَدُوٌّ مُّبِينٌ ﴿١٤٢﴾

142.Na katika wanyama wale wabebao na wa kutoa matandiko. Kuleni katika alivyowaruzuku Mwenyezi Mungu, wala msifuate nyayo za Shetani; hakika yeye ni adui yenu dhahiri.

ثَمَانِيَةَ أَزْوَاجٍ ۖ مِّنَ الضَّأْنِ اثْنَيْنِ وَمِنَ الْمَعْزِ اثْنَيْنِ ۗ قُلْ آلذَّكَرَيْنِ حَرَّمَ أَمِ الْأُنثَيَيْنِ أَمَّا اشْتَمَلَتْ عَلَيْهِ أَرْحَامُ الْأُنثَيَيْنِ ۖ نَبِّئُونِي بِعِلْمٍ إِن كُنتُمْ صَادِقِينَ ﴿١٤٣﴾

143.Namna nane za madume na majike: wawili katika kondoo dume na jike na wawili katika mbuzi dume na jike. Sema je, ameharamisha madume mawili au majike mawili, au waliomo matumboni mwa majike mawili, niambieni kwa ilimu ikiwa nyinyi mnasema kweli.

وَمِنَ الْإِبِلِ اثْنَيْنِ وَمِنَ الْبَقَرِ اثْنَيْنِ ۗ قُلْ آلذَّكَرَيْنِ حَرَّمَ أَمِ الْأُنثَيَيْنِ أَمَّا اشْتَمَلَتْ عَلَيْهِ أَرْحَامُ الْأُنثَيَيْنِ ۖ أَمْ كُنتُمْ شُهَدَاءَ إِذْ وَصَّاكُمُ اللَّـهُ بِهَـٰذَا ۚ فَمَنْ أَظْلَمُ مِمَّنِ افْتَرَىٰ عَلَى اللَّـهِ كَذِبًا لِّيُضِلَّ النَّاسَ بِغَيْرِ عِلْمٍ ۗ إِنَّ اللَّـهَ لَا يَهْدِي الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ ﴿١٤٤﴾

144.Na wawili katika ngamia na wawili katika ng’ombe, Sema je, ameharamisha madume mawili au majike mawili, au waliomo matumboni mwa majike mawili? Au nyinyi mlikuweko Mwenyezi Mungu alipowausieni haya? Basi ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule anayemzulia Mwenyezi Mungu uwongo ili kuwapoteza watu bila ya ilimu? Hakika Mwenyezi Mungu hawaongozi watu madhalimu.

KULENI MATUNDA YAKE

Aya 141 – 144

MAANA

Baada ya Mwenyezi Mungu (s.w.t) kubainisha katika Aya zilizotangulia, waliyoharamisha katika kilimo na mifugo kwa uzushi, amebainisha katika Aya hizi kwamba yeye ameumba mimea na wanyama binadmau anufaike nayo.

Anasema Mtukufu wa Wasemaji:

Naye ndiye aliyeumba bustani zenye kutambaa inayowekwa matawi yake katika chanjana zisizotambaa na mitende na mimea inaungana na Bustani katika upande wa kuunganisha mahsus kutoka ujumla.

Yenye kutofautiana uliwaji wake.

Nafaka ziko aina nyingi na kila moja ina aina yake, na kila aina ina ladha yake. Matunda nayo yako aina kwa aina; yenye rangi tofauti, ladha na hata harufu, vilevile mboga.

Na mizaituni na mikomamanga.

Hiyo pia inaungana na bustani.

Inayofanana na isiyofanana.

Matunda ya mikomamanga yanafanana, lakini kuna yaliyo tamu na yaliyo ugwadu. Vilevile matunda ya jamii ya malimau na mizaituni; kuna mazuri na mabaya.

Kuleni matunda yake inapozaa.

Kwa sababu imeumbwa kwa ajili yenu.

Na toeni haki yake siku ya kuvunwa kwake.

Imesemekana kuwa makusudio ya haki yake ni Zaka. Wengine wakasema kuwa ni sadaka ya Sunna. Lakini, kauli zote mbili ni kinyume na dhahiri.

Linalokuja haraka kwenye akili ni kukusanywa na wala yasiachwe yakaharibika na kupotea.

Wala msifanye ufujaji, hakika Yeye hawapendi wafujaji.

Ufujaji (Israf) ni kupetuka kiwango, na Mwenyezi Mungu amelikataza hilo: ni sawa iwe ni kutumia mtu mwenyewe, au kumpa mwingine.

Na katika wanyama wale wabebao na wa kutoa matandiko.

Yaani ameumba katika wanyama wanaowabeba nyinyi na kubeba mizigo yenu; kama vile ngamia. Na wale mnaowachinja na kunufaika kwa nyama yake manyoya na sufi zake.

Kuleni katika alivyowaruzuku Mwenyezi Mungu,

kama vile wanyama hawa na wengineo na mshukuru neema zake.

Wala msifuate nyayo za Shetani , kwa kuhalalisha aliyoyaharamisha Mwenyezi Mungu, na kuharamisha aliyoyahalalisha, na pia kufanya ubadhirifu.

Hakika yeye ni adui yenu dhahiri .

Anawaamrisha uovu na kusema kwa Mwenyezi Mungu msiyoyajua.

Namna nane za madume na majike: wawili katika kondoo dume na jike na wawili katika mbuzi dume na jike. Sema je, ameharamisha madume mawili ya kondoo na mbuziau majike mawili , ya kondoo na mbuzi?Au waliomo matumboni mwa majike mawili ya kondoo na mbuzi?

Niambieni kwa ilimu ikiwa nyinyi mnasema kweli sio kwa hawa za nafsi na kufuata mnavyoambiwa tu, kwa sababu kuharamisha kunahitajia dalili mkato; sasa je, iko wapi?

Na wawili katika ngamia na wawili katika ng’ombe, Sema je, ameharamisha madume mawili au majike mawili, au waliomo matumboni mwa majike mawili? Au nyinyi mlikuweko Mwenyezi Mungu alipowausieni haya?

Walidai kwamba Mwenyezi Mungu ndiye aliyewaharamishia waliowa- haramisha katika wanyama na mimea. Ndipo akawaambia kuwa jambo halithibitiki ila kwa mojawapo ya hali mbili. Ama kwa kuona au kwa kushuhudia shahidi mkweli. Na nyinyi hamkupata hukumu ya uharamu kutoka kwa Mwenyezi Mungu moja kwa moja au kupitia kwa Mtume wake; basi mmezitoa wapi hukumu hizi?

Basi ni nani dhalimu mkubwa kuliko yule anayemzulia Mwenyezi Mungu uwongo?

Ikiwa hamkuona, wala hakuna ushahidi wowote, basi nyinyi mtakuwa wazushi. Na mzushi ni dhalimu mwenye dhambi. Bali nyinyi ni madhalimu kuliko dhalimu yeyote, kwa sababu mnamzulia Mwenyezi Mungu uwongo.

Ili kuwapoteza watu bila ya ilimu.

Akiwazuia kufuata njia ya Mwenyezi Mungu na wakati huo huo anadai kuwa yeye ni kiongozi wa dini ya Mwenyezi Mungu; kama walivyo masheikh wengi siku hizi.

Hakika Mwenyezi Mungu hawaongozi watu madhalimu.

Kwa sababu wao wamekata uhusiano na Mwenyezi Mungu. Isitoshe wameharamisha aliyoyahalalisha na kuhalalisha aliyoyaharamisha.