Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

MJADALA KUHUSU MWANZO WA UUMBAJI

0 Voti 00.0 / 5

BISMILLAH AR-RAHMANI AR-RAHIIM.

KWA JINS LS MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEM.

MJADALA KUHUSU MWANZO WA UUMBAJI
Kutokana na hisia aliyoumbwa nayo kila mwanadamu,ni wazi kwamba hisia hii humpeleka Mwanadamu huyu kutaka kujua sababu ya kutokea au kuwepo kwa kila kitu akionacho mbele yake.Kamwe huwa hafikiria kuwa huenda vitu hivyo vimetokea au kudhihiri hivi hivi tu (vyenyewe) pasina sababu yoyote au chanzo chochote kilichopelekea kutokea kwa vitu hivyo. Kwa ibara nyingine tunasema kwamba:Mwanadamu haoni kuwa vitu hivyo vimedhihirika kiajali au kighafla.Mfano:Dereva ambaye gari lake husimama ghafla hushuka kutoka kwenye gari na kuanza kukagua na kutazama sehemu anayodhani kuwa inaweza kuwa na hitilafu ambayo imepelekea kusimama ghafla kwa gari lake.Huwezi kuamini kuwa gari lake ambalo liko katika hali nzuri ya kuendelea na mwendo linaweza kusimama ghafla bila ya kuwepo sababu yoyote ile iliyopelekea lisimame ghafla.! Anapotaka kuliendesha gari gari hilo hutumia vifaa vilivyowekwa kwenye gari hilo na kamwe hawezi kutegemea bahati nasibu.

Mfano mwingine ni huu kwamba:Mwanadamu anapohisi njaa,huanza kuwaza juu ya chakula chochote kile kinachoweza kumuondolea njaa hiyo kama vile mkate n.k Anapohisi kiu huanza kutafuta maji ili kukata kiu yake.Anahisi baridi huanza kuona umuhimu wa nguo za baridi au akihisi joto basi huanza kuona umuhimu wa nguo za joto,yaani kiufupi haridhiki na kukaa akitegemea kwamba matatizo hayo yataondoka yenyewe kwa bahati nasibu bali anajishughulisha ili kujaribu kutatua jambo hilo alilokumbana nalo.

Mfano mwingine ni huu hapa kwamba mtu anayetaka kujenga jengo fulani,bila shaka huanza kutafuta vifaa vya ujenzi kama vile simenti,matofari ,mchanga,kokoto,minondo nakadhalika,kasha hutafuta mafundi na wafanyakazi.Kamwe huwa hatarajii kuwa nyumba yake anayoifikiria kuijenga itajijenga yenyewe tu kighafla ghafla au kibahati nasibu.!

Mfano mwingine ni kwamba Milima ,Misitu na Bahari pana (kama vile bahari ya Hindi au Atlantic) vyote vimekuwepo hapa duniani sambamba na Mwanadamu.Wanadamu wamekuwa wakiliona Jua,Mwezi na Nyota zinazong'ara angani huku zikiwa katika njia zilizopangiwa ziwe.Lkini pamoja na hayo yote ,utakuta wanasayansi ulimwengini daima wamekuwa wakizijadili sababu na vyanzo vilivyopelekea kuwepo viumbe hivi yaani milima,bahari,misitu,nyota,mwezi na jua) vya kustaajabisha.Na wanafanya uchunguzi kwa kina pasina kuchoka.Kamwe hawasemi kuwa kwamba wamekuwa wakiviona viumbe hivyo katika hali ile ile ya mwanzo tangu mwanzo wa maisha yao na kwamba viumbe hivyo au vitu hivyo vimedhihiri vyenyewe.

Hivyo utakuta kwamba hisia kama hiyo ya kujiuliza ,sababu na chanzo cha vitu mbali mbali anavyoviona mwanadamu mbele yake,humfanya mwanadamu kuanza kuvichunguza viumbe hivyo vilivyomo ulimwenguni kama vilivyo na mpangilio wake wa kushangaza.!Umilikaji wa hisia kama hizi kimaumbile humpelekea mwanadamu kujiuliza swali kama hili:

Je,Ulimwengu huu mkubwa ambao una viumbe lukuki vyenye uhusiano na vyenye kuwa pamoja bila ya mvurugano huenda kweli umedhihiri (yaani ulimwengu) hivi hivi wenyewe au umesababishwa na jambo fulani? Je,kuna uwezo na Elimu isiyokuwa na mwisho inayouongoza Ulimwengu huu wa ajabu unaofata sheria maalum zilizowekwa kote ulimwenguni na zinazokielekea kila kitu katika lengo lake kililopangiwa? au anajiuliza je, ulimwengu huu umepatikana tu hivi hivi kiajari au kighafla ghafla tu ukashtukia umesha kuwepo au kibahati nasibu?

Hivyo utakuta kila mwanadamu ana hisia kama hizi za kujiuliza na kutaka kujua chanzo cha vitu anavyoviona mbele yake, na kamwe hakubali kusema ati vitu hivyo vimekuwepo kuwepo tu vyenyewe pasina sababu,iliyofifanya kuwepo,kwani fikra kama hii haingii akilini, bali akili inamwambia mwanadamu kwamba:Vitu hivi unavyoviona mbele yako,vina chanzo au vina sababu, basi hapo ndipo utakapomuona mwanadamu anaanza kufanya utafiti na uchunguzi wa kina ili kujua sababu iliyopelekea kuwepo vitu hivyo, au ili kujua imekuwa kuwaje vikawepo!.

Usikose kufuatilia sehemu ya pili ijayo kuhusiana na Imani.

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini