Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

UMOJA WA WAISLAMU

0 Voti 00.0 / 5

BISMILLAHIR-RAHMAANIR-RAHIIM

UMOJA WA WAISLAMU

Ayatullah Ali Taskhiri, Katibu Mkuu wa Taasisi ya Kimataifa ya Kukurubisha pamoja Madhehebu ya Kiislamu katika mazungumzo yake na Shirika la Habari la Fars amebainisha malengo na shughuli za taasisi hiyo katika kukabiliana na vitendo vya uchochezi na mgawanyiko dhidi ya Waislamu.

Amesema Taasisi ya Kukurubisha pamoja Mahdhebu ya Kiislamu imekuwa na nafasi muhimu katika kunyanyua uelewa wa Waislamu na kwamba ili kufikia lengo hilo taasisi hiyo imetuma jumbe mbalimbali katika vikao vya kimataifa na pia katika nchi tofauti kwa madhumuni ya kuondoa sutafahumu na shubha za kidini.

Katibu Mkuu wa Taasisi ya Kukurubisha pamoja Madhehebu ya Kiislamu amesema, kuongezeka kwa uelewa katika ulimwengu wa Kiislamu kumekuwa na nafasi muhimu katika kuleta umoja na mshikamano miongoni mwa Waislamu na kwamba hilo ni moja ya malengo muhimu ya taasisi hiyo. Ayatullah Muhammad Ali Taskhiri amesema kuwa juhudi kubwa zimefanywa na zingali zinafanywa na mabeberu wa dunia kwa lengo la kuharibia jina la Uislamu na Ushia na hasa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran.

Akizungumzia juhudi ambazo zinafanywa na Taasisi kwa madhumuni ya kukabiliana na uchochezi na siasa za mifarakano za maadui, Katibu Mkuu wa Taasisi ya Kukurubisha pamoja Madhehebu ya Kiislamu amesema kwamba juhudi nyingine ambazo zinafanywa na taasisi hiyo kwa lengo la kueneza Uislamu na kuleta umoja na mshikamano miongoni mwa Waislamu ni kuchapisha mamia ya vitabu vya kueneza mafundisho ya Kiislamu na kufichua njama za maadui wa Uislamu katika ulimwengu wa Kiislamu.

Huku akiashiria umuhimu wa kuandaliwa kikao cha kimatifa cha umoja wa Kiislamu mjini Tehran, Ayatullah Taskhiri amesema vikao hivyo ni njia muhimu ya kunyanyua uelewa katika ulimwengu wa Kiislamu kwa ajili ya kupambana na fikra potofu za kukabiliana na Ushia, Iran Mapinduzi ya Kiislamu na kuwafahamisha walimwengu malengo na ujumbe wa mapinduzi hayo.

Ayatullah Taskhiri amesisitiza kuwa shughuli nyingi za Taasisi ya Kukurubisha ni za kiutamaduni. Amesema, jukumu jingine la taasisi hiyo ni kupatanisha na kujaribu kutatua tofauti za kisiasa zinazojitokeza kati ya nchi za Kiislamu. Akizungumzia njia za kuepusha hitilafu za ndani na nje ya nchi kupitia shughuli za taasisi hiyo, Taskhiri amesema kuhusiana na suala la ndani kuwa Taasisi imekuwa ikitekeleza mipango ya kuimarisha umoja na mshikamamo miongoni mwa Washia na Wasunni wa Iran kupitia vikao mbalimbali.

Ama kuhusu sula la nje ya nchi, imekuwa ikiimarisha muamko na uelewa wa Waislamu waliopotoshwa na propaganda za maadui ili waweze kupata kureje kwenye njia sahihi. Ayatullah Taskhiri amesema kuwa sehemu kubwa ya shughuli za Taasisi ya Kukurubisha pamoja Madhehebu ya Kiislamu ni kuleta umoja na mshikamno miongoni mwa Waislamu katika Ulimwengu wa Kiislamu na kupunguza matatizo yaliyopo kwa lengo la kuwakurubisha pamoja wafuasi wa madhebu mbalimbali ya Kiislamu.

MWISHO

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini