Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

SHAABANI

0 Voti 00.0 / 5

BISMILLAHIR-RAHMAANIR-RAHIIM

MWEZI SHAABANI

Na huu ni mwezi wa Mtume wako bwana wa Mitume wako. (kwa mnasaba wa kuingia mwezi mtukuf wa shaaban)

Hakika mwezi mtukufu wa Shaaban ni mwezi mtukufu na mkubwa nao ni mwezi wa Mtume wetu Muhammad (s.a.w.w) kwani yeye alisema: 

شهر شعبان شهري رحم الله من أعانني على شهري

Mwezi wa Shaabani ni mwezi wangu Mwenyezi Mungu amrehemu mwenye kunisaidia juu ya mwezi wangu huu).

FADHILA ZA MWEZI WASHAABAN

Kuna habari zilizo pokelewa kutoka kwa Mtume mkarimu (s.a.w.w) na pia kutoka kwa maimamu waongofu (a.s) zijulishazo kuwa ubora wa mwezi huu mtukufu na mkubwa ni nyingi  sana na malipo ndani ya mwezi huu ni mara dufu, kwa hakika imekuja na kupolekewa habari kutoka kwa ibnu Abbas ya kuwa amesema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) wakati maswahaba wake walipo kuwa wakizungumzia fadhila za mwezi wa Shaaban mbele yake: Ni mwezi mtukufu, nao ni mwezi wangu, na wabebaji wa Arshi ya Mwenyezi Mungu wanautukuza na wanafahamu haki ya mwezi huu, nao ni mwezi ambao huzidishwa ndani yake riziki za waumini kama ulivyo mwezi wa Ramadhan, na pepo hupambwa ndani ya mwezi huu, …nao ni mwezi ambao kufanya  matendo ndani yake hulipwa mara dufu, jema moja hulipwa kwa wema sabini, na kosa huanguka na kusamehewa, na madhambi hughufiriwa, na mema hukubaliwa, na Mwenye nguvu mwenyezi Mungu alie takasika Huwaelewa ndani ya mwezi huu waja wake, na huwaangali wafungaji  wa mwezi huu na wasimamji kwa ajili ya ibada, na kujifakharisha nao kwa wabebaji wa Arshi)[1].

Na amesema (s.a.w.w): (Shaaban ni mwezi wenye kutwaharisha, na Ramadhani ni mwezi wenye kufuta madhambi, ……na Ndani ya mwezi wa Shaaban huinuliwa matendo ya waja)[2].

SABABU YA KUITWA SHAABAN

Imekuja na kuelezwa katika maana ya neno Shaaban kauli nyingi  sana. Na kati ya kauli hizo ni yale yaliyo semwa na Ibnu mandhuur katika lisaanul-arab juzu ya kwanza:(Kwa hakika umeitwa kwa jina la Shaaban kwa sababu umedhihiri na kuwa kati ya mwezi wa Ramadhani na Rajabu, na wingi wake ni Shaabaanaati, na Shaabaini, na Shaaban: Ni kizazi kitokanacho na Hamdan, Kilitoka katika vizazi vya Yemen, Na kwenye kizazi hichi hunasibishwa Aamir As-sha’abiy, na imesemekana: Shaaba ni jabali lililoko kwenye nchi ya Yemea, nalo ni lenye mapango au mabonde mawili).

Na muandishi wa Al-munjid fi llugha amesema: (umeitwa kwa jina hilo kutokana na waarabu kutawanyika na kusambaa ndani ya mwezi huo katika kutafuta maji).

Ama yaliyo kuja kutoka kwa mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) ni kauli yake isemayo: (Kwa hakika umeitwa kwa jina la Shaaban kwa sababu ndani ya mwezi huo hutawanyika riziki za waumini)[3].

Na amesema (s.a.w.w) (Kwa hakika umeitwa kwa jina la Shaaban kwa sababu hudhihiri ndni yake kheri nyingi kwa ajili ya Ramadhan)[4].

FADHILA ZA MATENDO YA MWEZI WA SHAABAN

Imekuja katika Tafsiri ya Imam Hasan Askariy (a.s) kuhusiana na matendo ya mwezi mtukufu wa Shaaban riwaya ifuatayo:

(Na kwa hakika Amirul-muuminiin (a.s) alipita kwa kaumu fulani kati ya waislaam waliojumuika mahala pamoja, ndani yake kukiwa hakuna Muhajiriina wala answari, nao wakiwa wameketi katika baadhi ya misikiti. Katika siku ya kwanza ya mwezi wa Shaaban, mara akawasikia wakizungumza kuhusiana na suala la usiku wa Qadri, na mambo mengine kati ya mambo waliyo tofautiana kwayo watu, na sauti zao zikiwa zimepaa juu, na ubishani na majadiliano kuwa makali kati yao, mara Mtume (a.s) akasimama na kutoa salam na wao kumpatia nafasi, na wakaanza kumuuliza kuhusu sababu ya kukaa kwake kati yao, nae hakujumuika nao, kisha akasema kuwambia na kuwaita:

Enyi watu wenye kuzungumzia mambo yasiyo wahusu,  na hakuwa  akiwajibu-hadi akafikia kusema (a.s)-Enyi wazuaji wa bidaa, hii ni siku ya mwanzo ya mwezi mtukufu wa Shaaban, mola wetu ameuita kwa jina la Shaaban,  kutokana na kutawanyika na kudhihiri ndani yake kheri nyingi, hakika Mola wenu amefungua ndani ya mwezi huu milango ya pepo, na akakutandazieni na kukuonyesheni ndani yake majumba yake ya kifakhari na kheri zake zilizo nyingi ndani ya mwezi huu, na kwa thamani ndogo na kwa mambo mepesi, basi nunueni vitu hivyo, na Iblisi alie laaniwa akakutangazieni na kukuanikieni, kundi la shari zake na mabalaa yake, kwa hivyo nyinyi si vinginevyo bali nyinyi mnazidi kudidimia katika uovu na upotevu, na mnazidi kushikamana na matawi ya ibilisi, na mkijitenga na kujiweka mbali na matawi ya kheri, iliyo funguliwa milango yake kwa ajili yenu, Na huu ni mwezi mtukufu wa Shaaban na kheri zake zilizo nyingi:

Swala, Funga, Zaka, Kuamrisha mema na kukataza Mabaya, na kuwatendea wema wazazi wawili, na watu wa karibu, majirani na kusuluhisha kati ya watu walio gombana, na kutoa sadaka kwa mafukara na masikini, mnajilazimisha kufanya mambo yaliyo ondolewa kwenu, na mambo mliyo zuiliwa kuyazungumzia, kwani kufichua na kupembua siri za Mwenyezi Mungu, ambazo mwenye kuzipembua na kuzikashifu atakuwa ni iongoni mwa watu walio angamia, ama kwa hakika nyinyi lau kama mnge simama juu ya yale mliyo andaliwa na Mola wetu alie takasika, kwa ajili ya watiifu kati ya waja wake katika siku hii, basi msinge pata muda wa kujishughulisha na haya myafanyayo, na munge anza kufanya yale mliyo amrishwa kuyafanya, wakasema: Ewe amiril-muuminiin, ni mambo yapi aliyo yaandaa Mwenyezi Mungu katika siku hii kwa ajili ya waja wenye kumtii yeye? Amirul-muuminiin (a.s) Akasema:

Sinta kuhadithieni isipokuwa niliyo yasikia kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w)- hadi akafikia kusema-kisha Mtume wa Mwenyezi Mungu akasema: Ninaapa kwa haki ya yule alie nituma kwa haki kama mtume, hakika Iblisi inapofika siku ya kwanza ya mwezi wa Shaaban, hutawanya majeshi yake katika pembe zote za ardhi na kona zake, anawambia: jitahidini kuwavutia baadhi ya waja wa Mwenyezi Mungu kwenu katika siku hii, na hakika Mwenyezi Mungu alie takasika, amewatawanya malaika katika pembe zote za ardhi na kona zake, anasema kuwambia: watieni uimara waja wangu na waongozeni, na wote watapata saada kupitia kwenu isipokuwa atakae kataa, na kupetuka na kufanya jeuri, hakika huyo atakuwa katika kikundi cha iblisi na wanajeshi wake, hakika Mwenyezi Mungu alie takasika inapofika siku ya kwanza ya mwezi wa Shaaban, huamrisha milango ya pepo ifunguliwe, na huuamrisha mti wa Tuuba uchomoze matawi yake juu ya dunia hii, kisha mnadi wa Mola wetu alie takasika huita:

Enyi waja wa Mwenyezi Mungu, Haya hapa matawi ya mti wa Tuuba…, basi shikamaneni nayo yatakuinueni hadi peponi, na haya hapa matawi ya mti wa Zaquum basi jihadharini na matawi hayo yasikupelekeni kwenye moto wa jahiim, Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w): Ninaapa kwa haki ya yule ambae amenituma kwa haki kama Mtume, hakika mwenye kuuendea mlango wa mambo ya kheri na mema katika siku hii, hakika atakuwa ameshika tawi moja wapo katika ya matawi ya mti wa Tuuba, basi litampeleka na kumfikisha peponi, na mwenye kushikilia mlango wa shari katika siku hii, basi atakuwa ameshikilia tawi moja wapo kati ya matawi ya mti wa Zaquum, nalo litampeleka hadi Motoni, kisha Mtume ( s.a.w.w) akasema:

Mwenye kujitolea na kusali kwa ajili ya Mwenyezi Mungu katika siku hii, kwa hakika atakuwa ameshikilia tawi moja wapo kati ya matawa hayo, na mwenye kufunga katika siku hii, atakuwa ameshikilia tawi moja wapo, na mwenye kutoa sadaka katika siku hii, atakuwa ameshikilia tawi katika mti huo, na mwenye kutoa msamaha kutokana na dhuluma aliyo fanyiwa atakuwa ameshikilia tawi moja wapo katika mti huo, na mwenye kusuluhisha kati ya mtu na mkewe, au kati ya mzazi na mwanawe, au watu wake wa karibu na jamaa zake, au kati ya jirani wa kiume na kike, au kati ya watu wawili wasio ndugu, kwa hakika atakuwa ameshikilia tawi moja katika mti huo, na mwenye kumpunguzia deni mtu asie weza kulipa deni lake au kuliangusha deni hilo, atakuwa ameshikilia tawi moja kati ya matawi ya mti huo, na mwenye kuangalia hesabu zake, na kuona deni la muda mrefu ambalo mwenye nalo amelikatia tamaa na kulilipa deni hilo, kwa hakika atakuwa ameshikamana na tawi moja katika mti huo, na mwenye kumchukua yatima kwa ajili ya malezi, atakuwa ameshikilia tawi moja katika mti huo, na mwenye kumzuwia mwenda wazimu kumfanyia uchokozi muumini, atakuwa ameshikilia tawi moja katika mti huo, na mwenye kusoma Qur’an yote ndani ya mwezi huu au kiasi fulani cha Qur’an, kwa hakika atakuwa ameshikilia tawi moja wapo katika mti huo, na mwenye kukaa na kumtaja Mwenyezi Mungu na neema zake na kumshukuru juu ya neema hizo, kwa hakika atakuwa ameshikilia tawi moja wapo katika mti huo, na mwenye kumtembelea mgonjwa, kwa hakika atakuwa ameshikilia tawi moja katika mti huo, na mwenye kuwafanyia wema wazazi wake au mmoja wapo katika siku hii, kwa hakika atakuwa ameshikilia tawi moja wapo katika mti huo, na yule ambae alikuwa amewakasirisha kabla ya siku hii wazazi wake na akawaridhisha katika siku hii, kwa hakika atakuwa ameshikilia tawi moja wapo katika mti huo, na mwenye kusindikiza jeneza atakuwa ameshikilia tawi moja wapo katika mti huo, na mwenye kumlewaza katika ziku hii mtu alie patwa na msiba kwa hakika atakuwa ameshikilia tawi moja wapo katika mti huo, na vilevile mwenye kufanya jambo lolote kati ya milango mingine ya kheri katika siku hii, kwa hakika atakuwa ameshikilia tawi moja wapo katika mti huo, kisha Mtume (s.a.w.w) akataja milango ya shari, na aliyo yaona kati ya hali za mti wa Tuuba, na mti wa Zaquum, na mapigano ya malaika na mashetani-hadi akafikia kusema mwishoni mwa maneno yake-hivi kweli hamuitukuzi siku hii ya mwezi wa Shaaban, baada ya kuutukuza kwenu mwezi wa shaaban, Ni wangapi watapata saada katika mwezi huu, na niwangapi watakuwa waovu wa kupitukia katika mwezi huu? Basi kuweni  watu wema na wenye saada katika mwezi huu na wala msiwe waovu)[5].

MIONGONI MWA MATENDO YA MWEZI MTUKUFU WA SHAABAN  NI HAYA YAFUATAYO:

1-FUNGA:

Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w): (Mwenye kufunga siku ya juma tatu na Alkhamisi ya mwezi wa Shaaban Mwenyezi Mungu mtukufu atamuwekea fungu lake, na mwenye kufunga siku ya juma tatu na Al-khamisi ya mwezi wa Shaaban atakidhiwa haja ishirini katika haja za kidunia, na haja ishirini kati ya haja za Akhera[6].

Na imepokelewa kutoka kwa Amiril-muuminiin (a.s) ya kuwa amesema: Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w):(Kila Al-khamisi ya mwezi wa Shaaban mbingu hupambika, na malaika husema ewe Mola wetu msamehe mfungaji wa mwezi huu, na wajibu dua zao (hadi akafikia kusema) na mwenye kufunga kwenye mwezi huu siku moja Mwenyezi Mungu huuharamisha mwili wake kuingia Motoni)[7].

Na Mtume (s.a.w.w) aliulizwa kuhusiana na funga katika mwezi wa Rajab akasema: (Iko wapi funga ya Rajabu ukiilinganisha na Shaaban)[8].

Na amesema kiongozi wetu Amiril-muminiin (a.s): (Mwenye kufunga mwezi wa Shaaban kutokana na mapenzi yake kwa Mtume (s.a.w.w) na kwa ajili ya kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu alie takasika basi Mwenyezi Mungu atampenda na kumkaribisha kwenye ukarimu wake siku ya kiama na atamuwajibishia pepo )[9].

Na Imamu wetu Abu Jaafar Al-baaqir (a.s) akasema: (Hakika funga ya mwezi wa Shaaban ni funga ya manabii, na ni funga ya wafuasi wa mitume, basi mwenye kufunga mwezi wa shaaban kwa hakika atakuwa amefikiwa na wito wa Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) kutokana na kauli yake, Mwenyezi Mungu amrehemu mwenye kunisaidia juu ya mwezi wangu huu)[10].

Na Abu Abdillahi As-swadiq (a.s) akasema: (Mwenye kufunga siku moja ya mwezi wa Shaaban ataingia peponi) na (Mwenye kufunga siku tatu katika mwezi wa Shaaban atawajibikiwa na pepo, na Mtume (s.a.w.w) atakuwa muombezi wake siku ya kiama)[11].

Na imekuja kutoka kwa Hasan bin Ali bin Shuubah Al-harraniy katika kitabu chake (Tuhaful-ukuul) kutoka kwa (Imam Ridhaa (a.s) katika barua yake kuelekea kwa Maamun amesema: (Na funga ya mwezi wa Shaaban ni jambo jema nayo ni sunna) ([12]).

2- KUFANYA ISTIGHFARI

Hilo litatimia kwa kusema kila siku mara sabini: (Astaghfiru llah wa’as’aluhut-tawbah) na (Astaghfirullah alladhi laa ilaha illa huwar-rahmanir-rahiim, al-hayyil-qayyum wa atuubu ilaihi).

Na tunafaidika kutoka kwenye habari hii kuwa dua  na nyuradi zilizo kuwa bora zaidi katika mwezi huu mtukufu ni kuomba istighfari.

Amesema Imamu Ridhaa (a.s): (Mwenye kumuomba Mwenyezi Mungu istighfari katika mwezi wa Shaaban mara sabini, Mwenyezi Maungu atamsamehe madhambi yake, hata kama yatakuwa ni kiasi cha idadi ya nyota)[13].

3- KUTOA SADAKA

Kiasi kiwezekacho hata kama ni kipande chatende.

Aliulizwa Imam Swaadiq (a.s): Ewe mtoto wa Mtume wa Mwenyezi Mungu! ni tendo gani bora kati ya matendo yafanywayo katika mwezi wa Shaaban? Akasema: (Ni kutoa sadaka na kufanya istighfari, na mwenye kutoa sadaka katika mwezi wa Shaaban Mwenyezi Mungu mtukufu atailea kama ambavyo mmoja wenu aleavyo mtoto wake hadi aweze kulipwa siku ya kiama na imekua kubwa na kuwa  kama mlima wa Uhud)[14].

4-KUSOMA TAHLIIL (YAANI: LAA ILAHA ILLA LLAH)

Na atafanya tahliil katika siku zote za mwezi mara elfu moja:

(لا إله إلا الله ولا نعبد إلا إيّاه مخلصين له الدين ولو كره المشركون)   

5-KUSALI RAKAA MBILI

Kila siku ya Al-khamisi ya mwezi mtukufu wa Shaaban.

Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w): (Mwenye kusali rakaa mbili katika mwezi huu: akisoma katika kila rakaa Suuratul-fatiha na Qul-huwallahu ahad) mara mia moja na akitoa na kumsalimia Mtume (s.a.w.w) mara mia moja Mwenyezi mungu atamkidhia haja zake zote kati ya mambo yake ya dini yake na  dunia)[15].

6-KUSOMA SWALAWAAT ILIYO POKELEWA KUTOKA KWA IMAMU WETU ZAINUL-ABIDIIN (A.S)

Kila mchana kati ya siku za mwezi wa Shaaban na katika usiku wa nusu ya mwezi huo na swalawat hiyo ni hii ifuatayo:

(بسم الله الرحمن الرحيم، اللهم صلّ على محمد وآل محمد شجرة النبوة وموضع الرسالة ومختلف الملائكة ومعدن العلم وأهل بيت الوحي و...).

7-KUSOMA MUNAAJAATI ULIO POKELEWA KUTOKA KWA AMIRIL-MUUMINIIN (A.S)

Na ulio maarufu kwa jina la (Al-munajaatish-shaabaniyyah na matni yake imo kwenye vitabu vya dua.

MATENDO YA USIKU WA NUSU YA MWEZI WA SHAABAN

Muumini mpenzi fahamu ya kuwa usiku wa nusu wa mwezi wa Shaaban ni usiku mtukufu na wenye cheo kikubwa, na Imam Baaqir (a.s) aliulizwa kuhusu usiku huu na akasema:

«هي أفضل ليلة بعد ليلة القدر، فيها يمنح الله العباد فضله، ويغفر لهم بمنّه، فاجتهدوا في القربة الى الله فيها، فانها ليلة آلى الله على نفسه ألّا يردّ سائلاً فيها ما لم يسأل معصية، وإنها الليلة التي جعلها الله لنا أهل البيت بإزاء ما جعل ليلة القدر لنبيّنا صلى الله عليه وآله فاجتهدوا في الدعاء والثناء على الله...»

(Ni usiku bora baada ya usiku wa Lailatul-qadri, ndani ya usiku huu Mwenyezi Mungu huwapa waja wake fadhila zake, na huwasamehe madhambi yao kwa fadhila zake, basi jitahidini kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu katika usiku huu, hakika ni usiku ambao Mwenyezi Mungu amejiandikia katika nafsi yake ya kuwa hatoacha kumjibu muombaji maadamu hajaomba maasi ndani ya usiku huo, na kwamba ni usiku ambao alituwekea sisi Ahlul-baiti badala ya aliyo yaweka katika usiku wa lailatul-qadri kwa ajili ya Mtume wetu (s.a.w.w) basi jitahidini kwa dua na kumsifu Mwenyezi Mungu…)[16].

Na katika usiku huu wenye baraka ndimo kulipo tokea mazazi matukufu ya mawlaana Baqiyyahtullahil-aadham Al-mahdiy mwenye kungojewa (Mwenyezi Mungu mtukufu aharakishe faraja yake tukufu) na ni sunna katika usiku huu kufanya mambo hafuatayo:

1-Ghusli: Amesema Imam Swaadiq (a.s):

«صوموا شعبان واغتسلوا ليلة النصف منه، ذلك تخفيف من ربكم ورحمة»

(Fungeni mwezi wa Shaaban na Muoge katika usikuwa wa nusu ya mwezi huo, hiyo ni takhfifu kutoka kwa Mola wenu na rehma)[17].

2-Kuuhuisha kwa ibada: Hadi asubuhi kwa kusali na kufanya ibada zingine na kumtaja au kumdhikiri Mwenyezi Mungu na kuomba istighfari na kusoma Qur’an na mengineyo kati ya matendo ambayo humkaribisha mja kwa Mwenyezi Mungu alie takasika, na imepokelewa kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) ya kuwa amesema:  Nilikuwa nimelala usiku wa nusu wa mwezi wa shaaban, mara nikajiwa na Jibrilu (a.s) akasema: Ewe Muhammad je unalala katika usiku huu?

Nikasema: Ewe Jibrilu ni usiku gani huu? Akasema: Huu ni usiku wa nusu ya mwezi wa shaaban, simama Ewe Muhammad. Akaniamsha kisha akanichukua hadi Baqii kisha akaniambia: Inua kichwa chako hakika usiku huu hufunguliwa ndani yake milango ya mbingu, na kufunguliwa ndani yake milango ya rehma, mlango wa ridhwaan, mlango wa maghfira, mlango wa fadhila, na mlango wa Tawba, na…. Ewe Muhammad! Mwenye kuuhuisha usuku huu kwa kufanya tasbihi na Tahlili na takbiri na kwa kusoma dua na kusali na kusoma na kusali sala za sunna na kufanya istighfari basi atakuwa na pepo yenye cheo kikubwa na mahala pa kupumzika, na Mwenyezi Mungu atamsamehe madhambi yake yaliyo tangulia na yatakayo fuatia)[18].  

3- Kusoma ziyara ya mawlana baba wa watu huru wote Imam Husein (a.s).

Amesema Imam Swaadiq (a.s): (Mwenye kupenda kupeana mkono na manabii laki mbili  na manabii elfu ishirini basi alizuru kaburi la Husein bin Ali (a.s) katika nusu ya mwezi wa shaaban, hakika roho za manabii humuomba idhini Mwenyezi Mungu kwenda kumfanyia ziara nae kuwapa idhini) [19].

Na imepokelewa kutoka kwake (a.s): Mwenye kumzuru Husein usiku wa nusu ya mwezi wa shaaban Mwenyezi Mungu atamghufiria mtu huyo madhambi yake yaliyo tangulia na yatakayo fuatia)[20].

4- kusoma Dua ya kumaili bin Ziyaad: Na dua hiyo ni miongoni mwa dua kubwa sana na tukufu za muwlaana Amiril-muuminiin (a.s).

5-Kusoma Duaul-ahad (dua ya ahadi) iliyo pokelewa kutoka kwa maulana Abi Abdillahi As-swaadiq (a.s).

Na kuna matendo mengine mengi ambayo ni sunna kuyatekeleza katika mwezi huu wenye fadhila yametajwa kwenye vitabu vya dua na ziyara basi mwenye kutaka na arejee.

KUMBU KUMBU ZA MWEZI WA SHAABAN

SIKU YA TATU:

Kuzaliwa maulana baba wa watu huru Imam Husein Shahiid rehama za Mwenyezi Mungu na amani ziwe juu yake, mwaka 4 hijiria.

SIKU YA NNE:

Kuzaliwa mnyweshelezaji wa watu wenye kiu wa Karbalaa, Qamar bani Haashim, Sayyidina Abil-fadhlil-abbas juu yake rehma na amani, mwaka 27 hijiria.

SIKU YA TANO:

Kuzaliwa kwa Zainul-aabidiin na bwana wa wenye kusujudu Imam Ali bin Husein juu yake rehma na amani, mwka 38 hijiria.

SIKU YA KUMI NA MOJA:

Kuzaliwa kwa mtu amfananae Mtume mtukufu (s.a.w.w) kwa maumbile na tabia, bwana wetu Ali Akbar juu yake rehma na amani.

SIKU YA KUMI NA TANO:

Kuzaliwa kwa muokozi wa viumbe, na matarajio ya wanyonge, na atakae ondoa shida na matatizo, walii mtukufu wa Mwenyezi Mungu, Qaaimu Aali Muhammad maulana Imam mahdiy mwenye kungojewa (Mwenyezi Mungu aharakishe kudhihiri kwake kutukufu, mwaka 255 hijiria.

Kama ambavyo siku ya kwanza inaangukia: Kufariki kwa Shekh Muhammad Husein An-najafiy muandishi wa kitabu Jawaahiril-kalaam, mwaka 1266 hijiria.

SIKU YA ISHIRINI:

Kufariki kwa Sayyid Muhammad Al-muusawiy Al-shiraziy alie mashuhuri kwa jina la Sultanil-waaidhiin (Mwenyezi Mungu autukuze utajo wake) muandishi wa kitabu maarufu (Layaali biishawar), mwaka 1319 hijira.

SIKU YA ISHIRINI NA NNE:

Kufariki kwa Mujaddidil-kabiir, Sayyid Miirza Muhammad Hasan Al-shiraziy (Mwenyezi Mungu autukuze utajo wake), msimamizi wa mapinduzi ya Tumbaku, mwka 1312 hijiria.

Na mwisho:

Tuna muomba Mwenyezi Mungu alie takasika atukubalie hiki kidogo tulicho kitekeleza, na awawafikishe waumini wa kiume na kike katika mwezi huu mtukufu, mwezi wa Mtume mtukufu (s.a.w.w), kuweza kutekeleza yale yaletayo maridhio yake alie takasika, na atuneemeshe kwa uokovu na ushindi mkubwa kwa kudhihiri walii wake mtukufu maulana Imam mahdiy mwenye kungojewa  (Mwenyezi aharakishe faraji yake tukufu), hakika yeye ndie walii wa tawfiki zote. Waswalla llahu alaa Muhammad wa Aalihi twahiriin.

[1]-Al-aamal cha Swaduuq.

[2] -Mustadraku wasaailu shia Juzu 7 Abwaabu swaumul-mandub Babu Istihbabul-istighfar wa…..fii shaaban ukurasa 544 chapa ya Muassasah Aalul-baiti liihyaait-turaath chapa ya kwanza 1407 hijiria.

[3] -Al-amaal cha Swaduuq.

[4] -Tafsiri Majmaul-bayaan ya Twabarasiy juzu 5.

[5]-Mustadraku wasaailu shia juzu 7 chapa ya Muassasatu Aalul-baiti li’ihyaai turaath, Abwaabus-swaumu al-manduub baabu istihbaabul-istighfari wa… fii shaaban ukurasa 542.

[6] -Wasaailu shia kitaabus-swaumu Abuwaabus-swaumul-manduub Istihbaabu swaumu shaaban ukurasa 366 Daru ihyaau turaathil-arabiy chapa ya nne 1219 hijira.

[7]-Chanzo kilicho tangulia.

[8]- Chanzo kilicho tangulia.

[9]-Chanzo hichohicho.

[10]-Chanzo kilicho tangulia.

[11]-Chanzo kilicho tangulia.

[12]-Tuhaful-ukuul baabu kalimaatul-imam Ridhaa (a.s).

[13]-Mustadraku Safiinatul-buhaar cha Namaaziy – juzu 5 414.

[14]-Iqbalul-aamal cha Sayyid ibnu Twaawus juzu 3 294.

[15]-Wasailu shia chapa ya Aalul baiti juzu 8 104.

[16]-Aamali cha Tuusiy ukurasa 297.

[17]-Wasaailu shia juzu 3 335.

[18]-iqbalul-aamal juzu 3 320.

[19]-Wasaailu shia kitabul-haji ab’waabul-mirzaar baabu ziyaarul-Husein (a.s) fii nisfi min shaaban.

[20]-Chanzo kilicho tangulia.

MWISHO

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini