Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

HUKUMU ZA KIISLAMU

0 Voti 00.0 / 5

BISMILAHI RAHMANI RAHIYMI

KWA JINA LA MWENYEEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU

 HUKUMU ZA KIISLAMU

KUJA KWA HUKUMU ZA KIISLAMU KIJUMLA JUMALA

Dini ya kiislamu imeelezea sheria za hukumu za kiislamu kijumla jamala, ambapo hakuna dini yoyote iliyoelezea na kufafanua kwa upana sheria zinazohusiana na dini hiyo.

Dini ya kiislamu imezigawa hukumu na sheria za kiislamu katika masuala yanayohusiana na sheria za ibada (yaani mja na Mola wake, na katika masuala yanayohusiana na sheria za mja kwa mja, pindi watu watakapozifuata sheria na kanuni hizo zilizoelezewa katika dini ya kiislamu kwa hakika watapata saada ya maisha ya dunia na ya akhera.

Katika kanuni na sheria za dini ya kiislamu imeelezewa kwamba kufanya ibada humfanya mwanaadamu aishi katika maisha ya utulivu, na kumfanya awe thabiti katika kukuza uhusiano wake na Mola wake, ambapo hii humpelekea mwanaadamu huyo kuipa nguvu na kuitakasa nafsi yake. kufanya ibada za wajibu au za sunna na kusoma nyuradi wakati wa sala au wakati mwengine wowote humfanya mwanaadamu aitakase nafsi yake na kuwa karibu na Mola wake, na imetiliwa mkazo zaidi iwapo ibada hizo zitafanywa katika sehemu takatifu humfanya mwanaadamu afikie katika ukamilifu katika jamii.

Neno (), ambalo lina maana ya kutakasa linamaanisha kwamba hadafu na dhumuni la kufanya ibada ni kuitakasa nafsi ya mwanaadamu, ambapo katika surat-Shamsi Aya ya 9 tunasoma:-

قَدْ اَفْلَحَ مَن زَكَّاهَا[1]

Maana ya Aya hiyo ni kama hivi ifuatavyo:-

Bila ya shaka amefaulu aliyeitakasa (nafsi yake).

 Mwanaadamu pindi anapokaa na kufikiri kwa makini kuhusu kuwepo kwake hujihisi kuwa kuna mtu bora zaidi ulimwenguni mwenye nguvu ambaye ameumba vitu vyote anavyovishuhudia, na wakati huo basi huhisi kuwa yeye sio kitu chochote, bali yule mtu ambaye ni mwenye nguvu za kila kitu ndiye anayemuongoza, mwanaadamu huyo anapogunduwa udhaifu wake huo hutafuta njia itakayoweza kumfikisha katika ukamilifu na kuizingatia pamoja na kuikuza nafsi yake ili ifikie katika ukamilifu, na kwa sababu hiyo basi hufanya jitihada ili kufikia katika ukamilifu, na huomba maghafira kwa Mola wake kwa makosa aliyoyafanya, na hicho ni kitu kitakachomfanya mwanaadamu huyo ajifahamu yeye ni nani na inamuwajibikia kufanya nini.

Kila dini ina mtindo wake mahasusi wa kufanya ibada ambazo hupelekea kuitakasa nafsi ya mwanaadamu, katika dini za Hindu, Zartushtiy na dini nyengine wana ibada zao ama inaeleweka wazi kuwa ibada zinazofanywa katika dini hizo zimechanganyika kwa uharibifu na uzushi.

Tukiwachilia mbali masuala hayo ya ibada ambayo yanajenga uhusiano baina ya mja na Mola wake, kuna nyanja nyengine ambayo inaelezea kanuni na sheria zinazojenga uhusiano baina ya mja na mja, kimsingi sheria na kanuni zilizomo katika dini ya kiislamu – ambazo zimekusanya nyanja zote za maisha ya wanaadamu katika jamii ndio sheria pekee zilizoweza kuwaletea wanaadamu ukamilifu katika maisha yao ya dunia na akhera.

Tunayathibitisha hayo kwa kuzingatia surat Al-Imrani Aya ya 19 Allah

(s.w) anasema:-

إِنَّ الدِّينَ عِندَ اللهِ الإِسْلاَمُ وَمَا اخْتَلَفَ الَّذِينَ اُوْتُواْ الْكِتَابَ إِلاَّ مِن بَعْدِ مَا جَاءهُمُ الْعِلْمُ بَغْياً بَيْنَهُمْ وَمَن يَكْفُرْ بِآيَاتِ اللهِ فَإِنَّ اللهِ سَرِيعُ الْحِسَابِ[2]

Maana ya Aya hiyo ni kama ifuatavyo:-

Bila ya shaka dini (ya haki) mbele ya Mwenyeezi Mungu ni Uislamu. Na waliopewa kitabu (Mayahudi na Manasara) hawakuhitilafiana ila baada ya kuwajia ilimu. (Wakikhitilafiana) kwa sababu ya uhasidi uliokuwa baina yao. Na anayezikataa Aya za Mwenyeezi Mungu (mara moja Mwenyeezi Mungu atamuadhibu huko Akhera), na Mwenyeezi Mungu ni mwepesi wa kuhisabu.

Na katika sura hiyo hiyo Aya ya 85 anasema:-

وَمَن يَبْتَغِ غَيْرَ الإِسْلاَمِ دِيناً فَلَن يُقْبَلَ مِنْهُ وَهُوَ فِى الآخِرَةِ مِنَ الْخَاسِرِينَ[3]

Na anayetaka dini isiyokuwa ya kiislamu, basi haitakubaliwa kwake. Naye Akhera atakuwa katika wenye khasara (kubwa kabisa).

[1] surat-Shamsi Aya ya 9

[2] surat Al-Imrani Aya ya 19

[3] surat Al-Imrani Aya ya 85

MWISHO

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini