Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

HEKIMA ZA ALLAH (S.W) KWA WENYE KUFUATA HAKI

0 Voti 00.0 / 5

 

BISMILAHI RAHMANI RAHIYMI

KWA JINA LA MWENYEEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU

HEKIMA ZA MWENYEEZI MUNGU KWA WENYE KUFUATA HAKI.

Ijapokuwa milki na hekima za Mwenyeezi Mungu katika dunia ni jambo lililowazi kabisa kwa wale ambao wanatafuta haki, lakini siku ya kiama watu wote watajua na kuelewa uhakika huo.

Kama vile ambavyo tunaona katika dunia kuwa baadhi ya watu hukumbwa na adhabu kali ya Mwenyeezi Mungu, na wakati huo basi hufahamu hekima zake Allah (s.w),kuhusiana na maelezo hayo Allah (s.w) anasema:-

وَلاَ يَزَالُ الَّذِينَ كَفَرُوا فِى مِرْيَةٍ مِّنْهُ حَتَّي تَاْتِيَهُمُ السَّاعَةُ بَغْتَةً اَوْ يَاْتِيَهُمْ عَذَابُ يَوْمٍ عَقِيمٍ  . الْمُلْكُ يَوْمَئِذٍ لِّلَّهِ يَحْكُمُ بَيْنَهُمْ فَالَّذِينَ آمَنُوا وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ فِى جَنَّاتِ النَّعِيمِ[1]

Na walio kufuru hawatoacha kuwa katika wasiwasi kwa hilo mpaka Saa iwafikie ghafla, au iwafikie adhabu ya Siku Tasa. Ufalme wote siku hiyo utakuwa wa Mwenyezi Mungu. Atahukumu baina yao. Basi walio amini na wakatenda mema watakuwa katika Bustani zenye neema.

Siku ya Kiama hekima ya Mwenyeezi Mungu itadhihirika kwa uwazi kabisa kiasi ya kwamba hakuna mtu mwenye haki au atakayeweza kuzungumza bila ya idhini ya Mola wake.Kama tunavyosoma katika Qur-ani:-

رَبِّ السَّمَاوَاتِ وَالاَرْضِ وَمَا بَيْنَهُمَا الرحْمَنِ لاَ يَمْلِكُونَ مِنْهُ خِطَاباً . يَوْمَ يَقُومُ الرُّوحُ وَالْمَلاَئِكَةُ صَفّاً لاَّ يَتَكَلَّمُونَ إِلاَّ مَنْ اَذِنَ لَهُ الرحْمَنُ وَقَالَ صَوَاباً[2]

Mola Mlezi wa mbingu na ardhi na vilio baina yao, Arrahman, Mwingi wa rehema; hawamiliki usemi mbele yake! .Siku atakapo simama Roho na Malaika kwa safu. Hawatasema ila Mwingi wa rehema aliye mruhusu, na atasema yaliyo sawa tu.

Waislamu kwa kusoma Aya hii mara kwa mara Usiku na mchana, watazingatia uhakika huo kuwa Mwenyeezi Mungu ndiye Mwenye kufanya yote siku ya Kiama. Aya hiyo ni hii ifuatayo:-

مٰلِكِ يَوْمِ الدِّينِ[3]

Mwenye Kumiliki Siku ya Malipo.

HUKUMU ZISIZO MPAKA ZA MWENYEEZI MUNGU NA HUKUMU ZA KITAGHUTI.

Watu wengi wanaomuabudu Mwenyeezi Mungu wanaweza kujiwa au kujiuliza Suala hili:-

Kuna uwiano gani baina ya milki na hukumu ya uhakika isiyo mpaka ya Mwenyeezi Mungu na hukumu ya kitaluti?.

Na kwa upande mwengine mahakimu wengi wanaohukumu kidhalimu wameyaeneza malumbano hayo miongoni mwa watu, na kusema kuwa mtu yoyote anayeingia katika hukuma na kuwahukumu watu katika jamii, mtu huyo ameingia katika serikali hiyo kutokana na mapendeleo yake Allah (s.w). Na hakuna mtu yoyote mwenye haki ya kupingana na hukuma au serikali hiyo.

Ili kulijibu suala hilo ni lazima tuelewe kuwa kuna tofauti miongoni mwa mapendeleo ya kimaumbile ya Mwenyeezi Mungu  na yale ya kisheria. Mwenyeezi Mungu kutokana na mapendeleo yake ya kimaumbile,ameifanya dunia kuwa ni mahala pa mitihani , na matatizo kwa waja wake, ili waja hao kwa kutumia sehemu waliyoko katika jamii au sababu nyenginezo wanaweza kufikia katika madhumuni yao.

Ama mapendeleo ya kisheria ya Mwenyeezi Mungu yanawafanya wanaadamu kuchagua njia sahihi, na kufanya jitihada katika kufanya uadilifu. Kwa hiyo milki na hukuma zote za wanaadamu zinatokana na mapendeleo yake Yeye Allah (s.w). kama inavyosema Qur-ani takatifu:-

قُلِ اللهُمَّ مَالِكَ الْمُلْكِ تُؤْتِى الْمُلْكَ مَن تَشَاء وَتَنزِعُ الْمُلْكَ مِمَّن تَشَاء وَتُعِزُّ مَن تَشَاء وَتُذِلُّ مَن تَشَاء بِيَدِكَ الْخَيْرُ إِنَّكَ عَلـٰيَ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ[4]

Sema: Ewe Mwenyezi Mungu uliye miliki ufalme wote! Wewe humpa ufalme umtakaye, na humwondolea ufalme umtakaye, na humtukuza umtakaye, na humuangusha umtakaye. Kheri yote iko mikononi mwako. Hakika Wewe ni Muweza wa kila kitu.

Kwa hiyo pindi itakapokuwa milki na hukuma hizo zinaendeshwa kwa haki na uadilifu, basi zitakuwa zimeendeshwa kwa mapendeleo ya kisheria ya Mwenyeezi Mungu, na watu hao watafaidika kwa kusaidiwa na Mwenyeezi Mungu katika dunia, na kupata thawabu za siku ya Kiama.

Katika Qur-ani takatifu tunashuhudia kauli ya Nabii Yussuf (a.s) pale aliposema:-

رَبِّ قَدْ آتَيْتَنِى مِنَ الْمُلْكِ وَعَلَّمْتَنِى مِن تَاْوِيلِ الاَحَادِيثِ فَاطِرَ السَّمَاوَاتِ وَالاَرْضِ اَنتَ وَلِيِّى فِى الدُّنُيَا وَالآخِرَةِ تَوَفَّنِى مُسْلِماً وَاَلْحِقْنِى بِالصَّالِحِينَ[5]

Ewe Mola wangu Mlezi! Hakika umenipa utawala, na umenifunza tafsiri ya mambo. Ewe Muumba wa mbingu na ardhi! Wewe ndiye Mlinzi wangu katika dunia na Akhera. Nifishe hali ya kuwa ni Muislamu na nichanganyishe na watendao mema.

Ama pindi itakapokuwa milki na hukuma zinaendeshwa kinyume na dasturi za Mwenyeezi Mungu, basi zitakuwa zinakhitilafiana na mapendeleo ya kisheria ya Mwenyeezi Mungu, hukuma kama hizo katika utamaduni wa kiislamu huitwa hukuma za Kitaluti, na watu wanaohukumu hukuma kama hizo watadhalilika na kupata adhabu kali za Mwenyeezi Mungu, kama alivyosema Allah (s.w) kumwambia Nemrud:-

اَلَمْ تَرَ إِلَي الَّذِى حَآجَّ إِبْرَاهِيمَ فِى رِبِّهِ اَنْ آتَاهُ اللّهُ الْمُلْكَ إِذْ قَالَ إِبْرَاهِيمُ رَبِّيَ الَّذِى يُحْيِـي وَيُمِيتُ قَالَ اَنَا اُحْيِـي وَاُمِيتُ قَالَ إِبْرَاهِيمُ فَإِنَّ اللّهَ يَاْتِى بِالشَّمْسِ مِنَ الْمَشْرِقِ فَاْتِ بِهَا مِنَ الْمَغْرِبِ فَبُهِتَ الَّذِى كَفَرَ وَاللّهُ لاَ يَهْدِى الْقَوْمَ الظَّالِمِينَ[6]

Hukumwona yule aliye hojiana na Ibrahim juu ya Mola wake Mlezi kwa sababu Mwenyezi Mungu alimpa ufalme? Ibrahim alipo sema: Mola wangu ni yule ambaye huhuisha na kufisha. Yeye akasema:

Mimi pia nahuisha na kufisha. Ibrahim akasema: Mwenyezi Mungu hulichomozesha jua mashariki, basi wewe lichomozeshe magharibi. Akafedheheka yule aliye kufuru; na Mwenyezi Mungu hawaongoi watu madhaalimu.

*katika zama za Nabii Ibrahimu (a.s) alikuweko mfalme jabari ambaye alidai Uungu, na raia zake wakamuabudu, alipokuja Nabii ibrahimu (a.s) kufundisha dini ya haki kuwa huyo si mungu, alimwambia Nabii Ibrahimu (a.s):-

“Kwani huyo Mungu wa haki hufanya nini?” akamwambia “Huhuisha na hufisha”. Akajitia pambani – kufanya kama kwamba hakufahamu muradi au maelezo ya Nabii Ibrahimu – akamwambia .”

na mimi pia nafanya kazi hii. Nitazame ninavyoifanya. Pale pale akaamrisha waletwe watu wawili waliostahiki kuuawa, akaamrisha auawe mmoja katika hao na mmoja asamehewe. Yakafanywa hayo.

 Akamwambia Nabii Ibrahimu “umeonaje? Si nimehuisha na nimefisha?.

Nabii Ibrahimu alipomuona anajitia pambani alimpa jambo ambalo hawezi kulitilia pambani; akamwambia habari hii ya kutolesha Mwenyeezi Mungu jua Mashariki… Yeye alitoleshe Magharibi kama yeye ni Mungu pia. Hapo akatahayari asijue la kutenda wala la kunena.

Natija tunayoipata katika maelezo hayo ni kwamba, ijapokuwa nidhamu ya dunia inatokana na mapendeleo ya kimaumbile ya Mwenyeezi Mungu, na kuwepo kwa hukuma za kitaluti, lakini watu wote wanawajibika kuikubali hukuma ya Mwenyeezi Mungu katika nidhamu ya kisheria, na Mwenyeezi Mungu anawataka waja wake kuwafuata wajembe wake ambao amewaleta, na kujiepusha na hukuma za kitaluti,kama tunavyosoma ndani ya Qur-ani:-

وَلَقَدْ بَعَثْنَا فِى كُلِّ اُمَّةٍ رَّسُولاً اَنِ اعْبُدُواْ اللّهَ وَاجْتَنِبُواْ الطَّاغُوتَ فَمِنْهُم مَّنْ هَدَي اللّهُ وَمِنْهُم مَّنْ حَقَّتْ عَلَيْهِ الضَّلالَةُ فَسِيرُواْ فِى الاَرْضِ فَانظُرُواْ كَيْفَ كَانَ عَاقِبَةُ الْمُكَذِّبِينَ[7]

Na kwa hakika kwa kila umma tuliutumia Mtume kwamba: Muabuduni Mwenyezi Mungu, na muepukeni Shetani. Basi kati yao wapo alio waongoa Mwenyezi Mungu. Na kati yao wapo ambao ulio wathibitikia upotovu. Basi tembeeni katika ardhi, muangalie ulikuwaje mwisho wa wanao kanusha.

Maelezo kwa ufupi kuhusiana na somo lililopita.

* Neno milki lina maana ya kuwa na Qudra na uwezo wa mali. Na vile kuwa na uwezo katika kuhukumu katika mambo. Na neno hukuma lina maana ya kuwa na nguvu au uwezo wa kuzuilia mambo.

* Viumbe vyote ulimwenguni vinaonyesha utukufu, milki, hekima na hukuma zake Allah (s.w).

* kubadilika kwa baadhi ya vitu au mambo, na kuletwa miujiza ni dalili tosha inayothibitisha hekima isiyo mpaka ya Mwenyeezi Mungu katika nidhamu ya kimaumbile.

*Kuteremshwa Mitume yote na Mola mmoja mtakatifu, ni dalili tosha inayothibitisha milki na hekima isiyo mpaka ya Mwenyeezi Mungu.

* Milki na ufalme wa viumbe vyote duniani utadhihirika kwa watu wote siku ya Kiama.

* Hakuna uwiano wowote baina ya hukuma ya Mwenyeezi Mungu na hukuma ya kitaluti, kwa sababu mapendeleo ya kimaumbile ya Mwenyeezi Mungu yanaonyesha kwamba Mwenyeezi Mungu ameijaalia dunia kuwa ni mahala pa mitihani na matatizo kwa waja wake.

Masuala:

1 .Maalik (mfalme) na Hakim ni watu gani?

2. Qur-ani kariym katika aya ya 22 ya surat Saba vipi inathibitisha na kutoa dalili ya ufalme usio mpaka wa Mwenyeezi Mungu?.

3. Vipi miujiza inathibitisha na kutoa dalili ya milki isiyo mpaka ya Mwenyeezi Mungu?.

4. Vipi ufalme wa Mwenyeezi Mungu unathibitisha hekima na hukuma za Mwenyeezi Mungu katika mambo ya kisheria?.

5. Vipi Qur-ani Kariym inathibitisha hekima za Mwenyeezi Mungu katika nidhamu ya siku ya Kiama?.

6. Hukuma ya kitaluti ni hukuma gani na ina maana gani?.

7. Kuna uwiano gani baina ya hukuma isiyo mpaka ya Mwenyeezi Mungu na hukuma ya kitaluti?.

[1] Surat hajj Aya ya 55-56

[2] Surat Nabaa Aya ya 37, 38

[3] Surat Alfaatiha Aya ya 3

[4] Surat Al-Imrani Aya ya 26

[5] Surat Yussuf Aya ya 101

[6] Suratul Baqarah Aya ya 258

[7] Surat Nahli Aya ya 36

MWISHO

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini