Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

FAIDA ZA KUTOWEKA IMAMU MUOKOZI NO.1

0 Voti 00.0 / 5

BISMILAHI RAHMANI RAHIYMI

KWA JINA LA MWENYEEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU

FAIDA ZA KUTOWEKA IMAMU MUOKOZI NO.1

Kutoweka kwa Imam kunaleta faida gani katika dunia?.

Ni zaidi ya miaka mia sasa walimwengu wamekutwa na msiba wa kutomuona Imam. Na kwa upande wa Waislamu imekuwa ni msiba mkubwa zaidi kwani hawakumuona Imam wao na kufaidika na neema za mtu huyo.

Hivi kupotea Imam machoni mwa watu kunaleta faida gani kwa watu na jamii kwa ujumla? Baadhi ya watu wanasema kwa nini Imam Mahdiy (a.s) asingelizaliwa karibu na wakati wa kudhuhuru kwake ili wafuasi wake wakaondokana na msiba huu waliokuwa nao sasa?. Suala kama hilo linajitokeza katika akili za watu kwa sababu watu bado hawajawa na elimu ya kumfahamu Imam Mahdiy, na hakuna mtu anayeijuwa dalili ya kutoweka Imam Mahdiy isipokuwa Allah (s.w), hivi kuwepo Imam Mahdiy kunaleta faida na baraka katika dunia nzima, Waislamu wote, au kwa wafuasi wa madhehebu ya Mashia tu?.

IMAM NI MSINGI WA KUWEPO KWA DUNIA.

Kwa mtizamo wa wafuasi wa madhehebu ya Kishia, wanasema kwamba kutokana na elimu ya dini Imam ni neema moja wapo aliyoleta Mwenyeezi Mungu kwa ajili ya viumbe wake wote,na yeye ndiye kiongozi wa dunia nzima, katika watu, majini, wanyama, miti, mimea n.k. Mmoja katika wafuasi wa Imam Sadiq aliuliza suala:- Ewe Imam wangu hivi dunia inaweza kubakia bila ya kuwa na Imam? Imam akasema:- "Ikiwa dunia itabakia bila ya kuwa na Imam dini na watu wote watabagaranyika na kutawanyika" Imam ndiye mwenye kupeleka ujumbe kwa walimwengu wote duniani, na ndiye mwenye kuwaongoza watu katika njia ya haki, neema na rehma zote ambazo Allah (s.w) anawateremshia waja wake ni kutokana na kuwepo kwake, kwani Mwenyeezi Mungu mwanzo aliwateremsha Mitume na baadae Maimamu ili kuwaongoza watu katika njia iliyo haki, kwa kuthibitisha kauli hii nakariri maelezo ya mmoja wa Maimamu ya kwamba, neema zote anazoteremsha Mwenyeezi Mungu kwa waja wake, ikiwa neema kubwa au ndogo ni kwa sababu ya kuwepo Maimamu. Ili kuthibitisha hayo na tuangalie dua hii ifuatayo ijulikanayo kwa jina la (Ziyarati jaamia kabiyra), dua hiyo inasema hivi:- Enyi Maimamu Mwenyeezi Mungu ameanza kuumba dunia kwa sababu yenu nyinyi, na utafika mwisho wa dunia kwa sababu yenu nyinyi, ananyesha mvua na kuleta baraka kwa viumbe wake kwa sababu yenu nyinyi, kaumba mbingu na ardhi na kuzizuilia zisianguke kwa sababu ya utukufu wenu nyinyi.

Kwa hiyo faida za kuwepo Imamu sio lazima tumshuhudie kwa macho, ila kutokuwepo kwake pia kuna umuhimu mkubwa na kunaleta faida katika viumbe wote duniani. Na Mwenyeezi Mungu ndiye aliyetaka kuumba kiumbe kitukufu kama hicho, kwani Mola ana nguvu za kila kitu na za kufanya kila kitu, na hafanyi kitu ila kina hekima ndani yake.

Mmoja katika wafuasi wa Imam aliuliza suala kuhusu vipi binaadamu anaweza kufaidika na Imamu hali ya kuwa haonekani machoni mwa watu? Imam akamjibu kwa kusema:-Kufaidika na mimi wakati nitakapotoweka ni kama kufaidika na jua wakati linapoangaza na kutoa nuru.

Katika sehemu hii na tuangalie kumfananisha Imam na jua na kutoweka kwake kunaleta athari gani?

Jua ni lenye kuzunguka katika sayari yake peke yake, na kuzunguka kwa jua kunasababisha kutoa muangaza, ambao muangaza huo una faida nyingi katika maisha ya mwanaadamu. basi katika maelezo ya hapo juu tumefahamu kwamba kwa kuwepo jua binaadamu anafaidika na mengi katika maisha yake.

Sasa natuangalie kwa kuwepo Imam duniani vipi mwanaadamu anaweza kufaidika?. Dunia imebakia kutokana na utukufu na baraka alizokuwa nazo, na mbigu na ardhi zimejengeka kutokana na kuwepo kwake.

Jua siku zote ni lenye kutoa nuru yenye kutosheleza, na walimwengu wanafaidika kutokana na nuru hiyo.

Basi kwa kuwepo Imam Mahdiy Allah (s.w) anatushushia rizki na neema, (neema za duniani na neema za akhera).

Basi kama jua litapatwa dunia itakuwa katika hali ya kiza na hakuna mtu atakayesubutu hata kutoka nje, na walimwengu hawatoweza tena kuishi katika dunia. Na kama Imam Mahdiy hatakuwepo dunia itajaa mabalaa na misuko suko na binaadamu hawataweza tena kuishi duniani.

Sheikh Mufiyd katika barua yake anasema hivi:- "Sisi hatutakuacha hata siku moja peke yako, na wala hatutakusahau, kwani bila ya kuwepo wewe dunia ingelikuwa imejaa mabalaa na matatizo, na maadui wa kiislamu wangelituondoa kabisa katika dunia.

MWISHO

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini