Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini

KUANZIA NDOA HADI KUWA WAZAZI (SEHEMU YA NANE) B

0 Voti 00.0 / 5

KUANZIA NDOA HADI KUWA WAZAZI (SEHEMU YA NANE) B
MLANGO WA 8: BAADA YA KUJIFUNGUA
MUENDELEZO WA MAKALA ILIYOPITA
NI NINI KINACHOPASA KICHINJWE

Ni kawaida miongoni mwa ulamaa kwamba Aqiqah iwe ni kondoo, ngamia au mbuzi, na kwamba Aqiqah kwa ajili ya mvulana inapaswa iwe mnyama dume na Aqiqah kwa ajili ya msichana iwe mnyama jike.

Kama ni ngamia, anapaswa awe na umri wa miaka mitano. Kama ni mbuzi inapaswa awe na umri wa mwaka mmoja zaidi ya huo, kama ni kondoo, anapaswa awe angalau na umri miezi sita au zaidi na ni bora kama mwezi wa saba utakuwa umetimia.

Korodani zake zisikatwe na pia ni bora kama hazitapondwa vile vile. Pembe zake zisivunjwe (kiasi kwamba akatoa damu) na masikio yake yasikatwe. Asiwe mwembamba aliyekonda sana, wala asiwe kipofu, wala asiwe kilema sana kiasi kwamba kutembea kunakuwa ni kugumu juu yake.

Hata hivyo, ni muhimu kutambua kwamba, kama ilivyosimuliwa kutoka kwa Imam as-Sadiq (a.s.), Aqiqah sio sawa na kafara (qurbaani) ambayo ina shuruti kali kwa ajili ya mnyama anayetolewa kafara.

Kwa hiyo, kama haiwezekani kutekeleza shuruti hizo hapo juu, kondoo yoyote yule ni sawa, ingawa aliyenenepa ni bora zaidi.
DUA WAKATI WA AQIQAH

Wakati1 wa kumchinja mnyama kwa ajili ya Aqiqah, du’a zifuatazo zinapasa kusomwa:

1. Mwishoni mwa du’a hii, mtu lazima ataje jina lake na jina la baba yake [kwa mfano, kama jina la baba ni Taahir na jina la baba yake ni Abdullah utasema, Taahir ibn (mwana wa) Abdullah] Dua hii inaanza na Aya za 78 na 79 za Suratul-An’am zikufuatiwa na Aya za 162 na 163 za Suratul-An’am hiyo hiyo:

“Enyi watu wangu! mimi simo katika hayo mnayoyashirikisha (na Allah). Mimi nimeuelekeza uso wangu kwa yule aliyeziumba mbingu na ardhi, hali ya kuwa nimewacha dini za upotovu, mimi si miongoni mwa washirikina. Hakika swala yangu na ibada zangu na uzima wangu na kufa kwangu, ni kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, Mola wa ulimwengu wote. Hana mshirika, na hayo ndiyo niliyoamrishwa, na mimi ni wa kwanza wa waliojisalimisha (kwa Mwenyezi Mungu). Ewe Allah! kwa hakika mnyama huyu anatoka Kwako na anarudi Kwako kwa Jina la Allah na Yeye Allah ni Mkubwa kuliko maelezo yoyote yanayoweza kutajwa juu Yake. Ewe Allah! shusha rehma na amani juu ya Muhammad na kizazi chake Muhammad na ikubali hii kutoka kwa (jina lako na jina la baba yako).”

2. Dua ifuatayo pia lazima isomwe wakati mnyama anapokuwa anachinjwa (mtoto huyo akiwa ni mvulana ama msichana).

“Kwa jina la Allah, na kwake Allah, na sifa zote ni zake Mwenyezi Mungu pekee, na Allah ni Mkubwa kuliko maelezo yoyote yanayoweza kuelezwa juu Yake. Kwa imani kamili kwake Allah na mapenzi kwa Mtume wa Allah (s.a.w.w.) na wana shukurani juu ya riziki ya Allah (s.w.t.). na kinga iliyotolewa kwa amri ya Allah na utambuzi kamili na mazingatio juu ya neema Zake juu yetu sisi Ahlil-Bayt.”

Kama mtoto ni mvulana, basi du’a ifuatayo pia inapaswa isomwe:

“Ewe Mungu! Umetuzawadia sisi mtoto mwanaume na Wewe unajua vizuri zaidi ni nini ulichotuzawadia sisi, na kurejea Kwako ni kile tuna- chokifanya sisi - hivyo basi ridhia kutoka (kafara) hili kutoka kwetu juu ya mila (sunnah) Yako na sunnah ya Mtume Wako, (rehma na amani juu yake na juu ya kizazi chake) na utuweke mbali na Shetani aliyelaaniwa. Kwa ajili Yako damu (ya mnyama huyu) imemwagwa, na Wewe huna mshirika na sifa zote njema ni Allah pekee, Mola wa ulimwengu wote.”

3. Dua ifuatayo pia ni lazima isomwe katika wakati wa kumchinja mnya- ma. Pale mtu atakapofikia mabano ya pembe, atataja jina la mtoto huyo na lile la baba yake [kwa mfano, kama jina la mtoto ni Jabir na jina la baba ni Kumayl, basi utasema: Jabir ibn Kumayl] na kisha uendelee na sehemu ya du’a iliyobakia. Maelezo ya kwanza ya du’a hii ni kwa sababa ya mtoto mvulana, du’a ya pili ni iwapo kama mtoto ni wa kike.

“Kwa jina la Allah na kwa Allah, Aqiqah hii (uchinjaji wa mnyama) ni kwa ajili ya [Jina la mtoto na jina la kwanza la baba yake]. Nyama yake badala ya nyama ya mtoto; damu yake badala ya damu yake mtoto; mifupa yake badala ya mifupa ya mtoto vyote vinatolewa Kwako. Ee Allah! ikubali hii kwa ajili kile ambacho kwacho mtoto huyu atakingwa na kuhifadhiwa, kwa jina la kizazi cha Muhammad, rehma na amani ya Allah iwe juu yake na juu ya kizazi chake.

“Kwa jina la Allah na kwa Allah, Aqiqah hii (uchinjaji wa mnyama) ni kwa ajili ya [Jina la mtoto na jina la kwanza la baba yake]. Nyama yake badala ya nyama ya mtoto; damu yake badala ya damu yake mtoto; mifupa yake badala ya mifupa ya mtoto vyote vinatolewa Kwako. Ee Allah! ikubali hii kwa ajili kile ambacho kwacho mtoto huyu atakingwa na kuhifadhiwa, kwa jina la kizazi cha Muhammad, rehma na amani ya Allah iwe juu yake na juu ya kizazi chake.”
JINSI GANI ITAKAVYOGAWANYWA?

Inashauriwa kwamba mifupa hiyo isije ikavunjwa; bali inapaswa kuten- ganishwa kwenye maungio yake. Ni bora vile vile kwamba nyama hiyo igawanywe ikiwa imepikwa (kwa angalau na maji na chumvi tu) na ngozi yake kutolewa kama sadaka.

Inapendekezwa kwamba miguu na mapaja ya aqiqah (hii inaweza kuh- esabiwa kama moja ya tatu au moja ya nne ya kondoo huyo kutegemeana na namna ya ugawaji) lazima itolewe kwa mkunga (au daktari) yule aliye- saidia wakati wa kujifungua na iliyobakia itolewe kwa watu iliwe kama sadaka. Ikiwa mkunga au daktari huyo ni Myahudi, basi thamani ya robo ya kondoo huyo lazima itolewe (kumpa yeye badala ya nyama).

Kama mtoto huyo alizaliwa bila ya mkunga au daktari, basi inapasa kutole- wa kwa mama ambaye anaweza kuigawa kwa yeyote anayemtaka yeye; ni lazima yeye aitoe kwa waislamu angalau kumi hivi, na kama anaweza kuigawa kwa wengi zaidi ni bora. Sio lazima kwamba nyama hiyo itolewe kwa masikini tu; hata hivyo, ni bora zaidi kwamba inatolewa kwa wachamungu na masikini.

Inashauriwa kwamba huyo baba na mama (na wale ambao wanawatege- mea wao, kama vile watoto wao na wazazi) wao hawali kutoka kwenye nyama iliyopikwa ya Aqiqah, na hii imesisitizwa hasa kwa mama.
NAMNA INAYOPENDEKEZWA YA KUMPONGEZA MTU WAKATI WA KUZALIWA KWA MTOTO

Inasimuliwa kutoka kwa Imam as-Sadiq (a.s.) kwamba alimpongeza mtu mmoja kwa mtoto ambaye Mwenyezi Mungu alikuwa amembariki naye kwa namna ifuatayo (kumekuwa na simulizi nyingi za namna hiyo kutoka kwa Imam Hasan (a.s.) vilevile): 2

“Mwenyezi Mungu akuruzuku na shukurani juu ya alichokujaalia, na akibariki kile alichokujaalia nacho, na amfanye afikie umri wa balekhe, na akujaalie na uadilifu wake mtoto huyu.”3
KUMPATIA MTOTO JINA
UMUHIMU WA KUMPA MTOTO JINA

Imesimuliwa kutoka kwa Imam al-Kadhim (a.s.) kwamba wema wa kwanza ambao baba anaweza kuufanya kwa ajili ya mwanawe ni kumpatia jina 4 zuri.

Ni haki ya mtoto kwamba wazazi wake wampatie jina zuri na kumtunza na kumtendea wema.5 Katika riwaya nyingine, imesimuliwa kwamba miongoni mwa haki za mtoto ni pamoja na jina bora, kumfundisha kuandika na kumuozesha wakati anapofikia umri wa utu uzima (balekhe).6
WAKATI GANI WA KUMPA MTOTO JINA

Inasimuliwa kutoka wa Imam Ali (a.s.): “Mtoto anapaswa kupewa jina wakati akiwa bado yuko tumboni, na kama hakupewa jina na mimba ikaporomoka, katika Siku ya Kiyama atakuja kumuuliza baba yake, “Kwa nini hukunipatia jina?” Mtukufu Mtume alimpatia jina Muhsin, mtoto wa Hadhrat Fatimah wakati akiwa yuko tumboni, na Muhsin huyu ni yule mtoto ambaye, baada ya kufariki kwa Mtukufu Mtume, yeye alikuwa bado yuko tumboni wakati Umar alipomfanya kuwa (afe) Shahidi.”

Imesimuliwa kutoka kwa Maimam (a.s.) kwamba: “Mtoto wa kiume haz- aliwi kwetu sisi, Ahlul-Bayt, isipokuwa kwamba anaitwa Muhammad kwa siku saba, na halafu kama ikihitajika, jina hilo linaweza kubadilishwa au kuondolewa.”7

Imeelezwa ndani ya Fiqh al-Ridhaa kwamba weka jina (yaani, tangaza jina hilo kwa wengine) mnamo siku ya saba.
MAJINA YANAYOPENDEKEZWA

Kumwita mtoto kwa majina ya Ahlul-Bayt (a.s.) ni tangazo la wazi la mapenzi na urafiki kwao, na dini sio chochote bali ni mapenzi na urafiki wa Ahlul-Bayt (a.s.) kama Allah (s.w.t.). anavyoelezea ndani ya Qur’ani Tukufu, katika ile Surat al-Imraan; 3:31:

إِنْ كُنْتُمْ تُحِبُّونَ اللَّهَ فَاتَّبِعُونِي يُحْبِبْكُمُ اللَّهُ وَيَغْفِرْ لَكُمْ ذُنُوبَكُمْ ۗ وَاللَّهُ غَفُورٌ رَحِيمٌ {31}

“Sema: Ikiwa ninyi mnampenda Mwenyezi Mungu, basi nifuateni mimi Mwenyezi Mungu atawapenda …...” (Al-Imraan; 3:31).

Imesimuliwa kutoka kwa Imam al-Baqir (a.s.) kwamba majina yanayofaa zaidi kwa ajili ya mtoto ni yale ambayo yanaashiria utumwa kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu kama vile Abdullah (mtumwa wa Allah), na majina bora zaidi kwa mtoto ni yale ya Mitume.

Mtukufu Mtume (s.a.w.w.) amesema kwamba yeyote aliye na watoto wanne na akawa hajamuita yoyote kati yao kwa jina langu, huyo amenionea mimi.8

Inasimuliwa kutoka kwa Mtukufu Mtume (s.a.w.w.): “Katika nyumba ambamo majina ya baadhi ya watu wake ni yale ya mitume (a.s.), neema za nyumba hiyo hazitatoweka kamwe.9

Katika riwaya nyingine, imesimuliwa kutoka kwa Imam al-Kadhim (a.s.) kwamba umasikini na ufukara kamwe havitaingia kwenye nyumba ambamo jina la Muhammad, au Ahmad, au Ali, au Hasan, au Husein, au Ja’far, au Talib, au Abdullah, au Fatimah linapatikana.10

Imesimuliwa kutoka kwa Imam Husein (a.s.); “Kama ningekuwa na watoto mia moja, ningependelea kuwaita wote kwa jina la Ali.”11

Imesimuliwa kwamba mtu mmoja alikwenda kwa Mtukufu Mtume (s.a.w.w.) na akauliza: “Ametujia (amezaliwa) mtoto wa kiume kwetu, je nimuite jina gani?” Mtukufu Mtume (s.a.w.w.) alijibu akasema: “Muite yeye jina bora kabisa katika majina niliyonayo mimi, nalo ni Hamza.”

Imesimuliwa kutoka kwa Jabir ambaye amesema: Nilikwenda kwenye nyumba ya mtu mmoja nikiwa pamoja na Imam al-Baqir na mtoto mmoja akatoka nje yake. Imam akamuuliza: “Unaitwa nani?” Yeye akajibu akase- ma. “Ninaitwa Muhammad.” Imam akamuuliza: “Ni lipi jina la cheo (kuniyah) chako?” Yeye akajibu: “Ni Abu Ali.” Imam akasema; “Wewe umejitoa kwenye ngome ya Shetani. Kwa kweli, kila wakati Shetani anapomsikia mtu akiitwa Ya Muhammad! au Ya Ali! anatoweka zake na wakati anaposikia mtu akiitwa kwa jina la maadui zetu, yeye anafurahia na anajifaharisha katika hilo.”

Katika hadithi nyingine, inasimuliwa kwamba mtu mmoja alikuja kwake Imam as-Sadiq (a.s.) na akasema kwamba Mwenyezi Mungu Mtukufu alikuwa amemjaalia mtoto mwanaume, Imam akampongeza, na akasema, “Wewe umempatia jina gani? Yeye akajibu, “Nimemwita Muhammad.” Imam akageuzia kichwa chake kuangalia chini ardhini na akawa anaendelea kurudia jina hilo Muhammad mpaka uso wake karibu uguse ardhi.

Kisha akasema, “Maisha yangu, watoto wangu, wake zangu, baba yangu, mama yangu na watu wote wa dunia hii watolewe kafara kwa ajili ya Mtukufu Mtume (s.a.w.w.). Kwa sababu umempa jina lililobarikiwa kiasi hicho, basi usije ukamtukana na usiwe unampiga na usimkaribie kwa ubaya. Na ulijue hili kwamba hakuna nyumba ambamo hili jana la Muhammad linapatikana bali kwamba kila siku nyumba hiyo inafanywa kuwa tukufu na safi halisi.”

Katika riwaya nyingine inasimuliwa kwamba mtu anapaswa kumheshimu binti ambaye jina lake ni Fatimah na asiwe anamtukana yeye na kamwe asimpige.”

Majina ya kivyeo ya Hadhrat Fatimah (a.s.) yanaweza kutumika kwa maji- na ya mabinti:

Mubaraka: Aliyebarikiwa.
Tahira: Aliyetakasika.
Zakiyya: Mwenye hekima.
Radhiya: Aliyetosheka.
Mardhiyya: Aliyeridhiwa na Mwenyezi Mungu Mtukufu
Siddiqah: Aliye mkweli.
Muhaddathah: Ambaye Malaika wanazungumza naye.
Muhaddithah: Anayesimulia hadithi za Mtume (s.a.w.w.).
Zahrah: Mwenye nuru.
MAJINA AMBAYO HAYAPENDEKEZWI KUTUMIKA

Katika riwaya kadhaa imesimuliwa kwamba Mtukufu Mtume (s.a.w.w.) amekataza kumwita mtoto kwa majina yafuatayo: Haakim, Hakim, Khalid na Maalik.

Na amesema kwamba majina mabaya sana kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu ni Harith, Maalik na Khalid. Na pale jina linapokuwa ni Muhammad, amekataza vyeo (kuniyah) vinne: Abu Isa, Abul Hakim, Abu Malik na Abul-Qasim, kwani vyote, majina na vyeo havikubaliki kwa Mtume (s.a.w.w.).

Katika riwaya moja, imesimuliwa kwamba mtu anapaswa kutomwita mtoto Yaasiin, kwani hilo ni makhususia kwa Mtukufu Mtume (s.a.w.w.) pekee.

REJEA:

    1. Halliyatul Muttaqin, Uk. 125-127
    2. Kitabu, ‘A Mother’s Prayer’
    3. Hilliyatul-Muttaqin, Uk. 127
    4. al-Kafi, Jz. 6, Uk. 17
    5. Hilliyatul-Muttaqin, Uk. 128-130
    6. Mustadrakul-Wasa’il, Jz. 15, Uk.128, hadithi ya 17748
    7. Mustadrakul-Wasa’il, Jz. 15, Uk.166, hadithi ya 17876
    8. al-Kafi, Jz. 6, Uk. 18, hadithi ya 4
    9. Tahdhib al-Balaghah, Jz. 7, Uk. 438, hadithi ya 11
    10. Mustadrakul-Wasa’il, Jz. 15, 129, hadithi ya 17751
    11. al-Kafi, Jz. 6, Uk. 19, hadithi ya 8
    12. al-Kafi, Jz. 6, Uk. 19, hadithi ya 7

ITAENDELEA KATIKA MAKALA IJAYO

Toa maoni yako

Maoni ya watumiaji

Hakuna maoni
*
*

Site ya Al-Imaamaini Al-Hassanaini (A.S) ya usambazaji wa utamaduni wa Kiislamu na mafunzo ya Kidini